Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 KUTOKA KATIKA HIFADHI YETU YA VITU VYA KALE

Mfalme Alifurahi Sana!

Mfalme Alifurahi Sana!

ILIKUWA Agosti 1936 katika kiwanja cha Makao ya Mfalme wa Swaziland. Wakitumia gari lenye vipaaza-sauti, Robert na George Nisbet walikuwa wamemaliza tu kucheza rekodi za muziki na hotuba zilizorekodiwa za Ndugu J. F. Rutherford. Mfalme Sobhuza wa Pili alifurahi sana. George anaeleza hivi: “Tulishindwa la kufanya Mfalme alipotaka kununua mashine ya kuchezea rekodi, rekodi zenyewe, na kipaaza-sauti cha habari za Ufalme!”

Robert alimwomba msamaha na kumwambia kwamba vitu hivyo haviuzwi. Kwa nini? Kwa sababu vifaa hivyo ni mali ya mtu fulani. Mfalme alitaka kumjua mtu huyo.

Robert akamjibu, “Vitu hivyo ni vya Mfalme mwingine.” Kisha Sobhuza akataka kumjua Mfalme huyo. Robert akamwambia: “Ni Yesu Kristo, Mfalme wa Ufalme wa Mungu.”

Sobhuza akasema hivi kwa heshima kubwa: “Naam, yeye ni Mfalme mkuu. Nisingependa kuchukua chochote kilicho chake.”

Robert aandika hivi: ‘Nilivutiwa sana na utu wa chifu huyo mkuu, Mfalme Sobhuza. Alizungumza Kiingereza kwa ufasaha bila kujigamba au kuwa na kiburi, naye alikuwa mnyoofu na mwenye urafiki. Nilikaa naye ofisini mwake kwa dakika 45 hivi George alipokuwa nje akicheza rekodi za muziki.

Robert aendelea kusema hivi: ‘Baadaye siku hiyo, tulitembelea shule kuu ya nchi hiyo na kupata mambo yaliyoonwa yenye kusisimua sana. Tulimhubiria mwalimu mkuu, naye alikuwa tayari kutusikiliza. Tulipotaja kuhusu kinanda na kwamba tungependa kujitolea kucheza rekodi kwa ajili ya shule nzima, mwalimu huyo alifurahi sana na kuwakusanya wanafunzi mia moja hivi ili waketi kwenye nyasi na kusikiliza. Tulielezwa kuwa shule hiyo inafundisha wavulana masomo ya kilimo, kutunza bustani, useremala, ujenzi, Kiingereza, na hesabu; wasichana nao walifundishwa jinsi ya kuwauguza wagonjwa, kazi za nyumbani, na nyingine muhimu.’ Nyanya ya Mfalme Sobhuza ndiye aliyeanzisha shule hiyo. *

Wanafunzi wa shule ya sekondari waliosikiliza hotuba ya watu wote huko Swaziland mwaka wa 1936

Tangu mwaka wa 1933, Mfalme Sobhuza aliwasikiliza kwa furaha mapainia waliotembelea Makao ya Mfalme. Pindi moja, hata aliwakusanya askari 100 waliokuwa wakimlinda ili  wasikilize ujumbe wa Ufalme uliorekodiwa. Alijiandikisha ili apokee magazeti yetu na alikubali machapisho tuliyompelekea. Baada ya muda mfupi, Mfalme huyo alikuwa na maktaba ya kitheokrasi yenye vitabu vingi! Isitoshe, aliitunza licha ya kwamba machapisho yetu yalikuwa yamepigwa marufuku na serikali ya wakoloni ya Uingereza wakati wa vita vya pili vya ulimwengu.

Mfalme Sobhuza wa Pili aliendelea kuwakaribisha Mashahidi kwenye Makao ya Kifalme huko Lobamba, na hata aliwaita viongozi wa kidini kuja kusikiliza hotuba za Biblia zilizotolewa na Mashahidi. Shahidi wa eneo hilo anayeitwa Helvie Mashazi alipokuwa akizungumzia Mathayo sura ya 23, baadhi ya viongozi hao wa kidini walisimama kwa ghadhabu na kujaribu kumlazimisha aketi chini. Lakini Mfalme aliingilia kati na kumwambia Ndugu Mashazi aendelee. Isitoshe, Mfalme aliwaambia wasikilizaji waandike maandiko yote ya Biblia yaliyotajwa katika hotuba hiyo!

Pindi nyingine baada ya kusikiliza hotuba iliyotolewa na ndugu aliyekuwa painia, viongozi wanne wa kidini waliokuwapo waligeuza na kufunika kola zao za kidini na kusema hivi: “Sisi si viongozi wa kidini tena bali kuanzia sasa, sisi ni Mashahidi wa Yehova.” Kisha, walimuuliza painia huyo ikiwa ana vitabu kama alivyo navyo Mfalme.

Kuanzia miaka ya 1930 hadi alipokufa mwaka wa 1982, Mfalme huyo aliwaheshimu Mashahidi wa Yehova na hakuruhusu wateswe kwa sababu ya kutoshiriki desturi za Waswazi. Kwa hiyo, Mashahidi walikuwa na sababu nzuri ya kumshukuru, na waliomboleza alipokufa.

Mwanzoni mwa mwaka wa 2013, kulikuwa na watangazaji wa Ufalme zaidi ya 3,000 huko Swaziland. Katika nchi hiyo yenye idadi ya watu zaidi ya milioni moja, kila mhubiri anapaswa kuwahubiria watu 384. Kuna makutaniko 90 yenye mapainia 260 wenye bidii, na watu 7,496 walihudhuria Ukumbusho katika mwaka wa 2012. Ni wazi kwamba kuna tumaini la kupata ongezeko zaidi. Bila shaka, msingi thabiti uliwekwa katika ziara hizo za kwanza huko Swaziland miaka ya 1930.—Kutoka katika hifadhi yetu ya vitu vya kale nchini Afrika Kusini.

^ fu. 8 The Golden Age, la Kiingereza, Juni 30, 1937, ukurasa wa 629.