Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fanya Maamuzi ya Kibinafsi kwa Hekima

Fanya Maamuzi ya Kibinafsi kwa Hekima

“Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe.”MET. 3:5.

1, 2. Una maoni gani kuhusu kufanya maamuzi, unahisije kuhusu maamuzi fulani uliyofanya?

MAAMUZI! Maamuzi! Kila siku tunafanya maamuzi mengi. Unahisije kuhusu maamuzi unayopaswa kufanya kila siku? Watu fulani hupenda kujiamulia kila jambo. Wanasisitiza kwamba wana haki ya kujifanyia maamuzi, na wanachukia kufanyiwa maamuzi na wengine. Hata hivyo, wengine huogopa kufanya maamuzi mazito zaidi maishani. Watu fulani hutafuta mashauri katika vitabu vya miongozo au kutoka kwa washauri na huenda wakatumia pesa nyingi kutafuta mashauri wanayohitaji.

2 Wengi wetu tunaogopa kufanya maamuzi na hatutaki kutafuta mashauri. Tunatambua kwamba hatuna haki ya kufanya maamuzi fulani na hatuwezi kufanya lolote kuhusiana na hilo; lakini kuna maamuzi mengi ya kibinafsi tunayoweza kufanya. (Gal. 6:5) Hata hivyo, huenda tukakubali kwamba baadhi ya maamuzi tunayofanya si ya hekima au hayana faida.

3. Tuna miongozo gani kuhusu kufanya maamuzi, lakini tunakabili tatizo gani?

3 Tukiwa watumishi wa Yehova, tunafurahi kwamba ametupa miongozo iliyo wazi kuhusu mambo mengi muhimu maishani mwetu. Tunajua kwamba tukifuata miongozo hiyo, tunaweza kufanya maamuzi yatakayompendeza Yehova na kutunufaisha. Hata hivyo, huenda tukakabili hali na mambo yasiyotajwa waziwazi katika Neno la Mungu. Basi, tutajuaje jambo tunalopaswa kufanya? Kwa mfano, tunajua kwamba hatupaswi kuiba. (Efe. 4:28) Lakini kuiba kunahusisha nini? Je, kunategemea thamani ya kitu kilichoibiwa, nia, au jambo lingine? Tutaamuaje jambo la kufanya inapohusu mambo ambayo wengine wanasema kwamba hayatajwi waziwazi katika Biblia? Ni nini kinachoweza kutuongoza?

 UWE NA UTIMAMU WA AKILI

4. Huenda tulipokea ushauri gani tulipotaka kufanya uamuzi fulani?

4 Tunaposema kwamba tunataka kufanya uamuzi fulani muhimu, huenda Mkristo mwenzetu akatuambia kwamba tunahitaji kuwa na utimamu wa akili. Bila shaka, huo ni ushauri mzuri. Biblia inatuonya hivi kuhusu kuchukua hatua haraka-haraka: “Kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huuelekea uhitaji.” (Met. 21:5) Lakini ni nini maana ya kuwa na utimamu wa akili? Je, inamaanisha kutumia wakati mwingi kutafakari ili tufanye uamuzi mzuri? Ingawa mambo hayo yote yanaweza kutusaidia kufanya uamuzi mzuri, kuwa na akili timamu kunahusisha mengi zaidi.Rom. 12:3; 1 Pet. 4:7.

5. Kwa nini hatuna akili kamilifu?

5 Ni kweli kwamba hakuna yeyote kati yetu aliyezaliwa akiwa na akili kamilifu. Kwa nini? Kwa sababu sote huzaliwa katika dhambi na hivyo hatuwezi kuwa na mwili au akili kamilifu. (Zab. 51:5; Rom. 3:23) Isitoshe, wengi wetu tulikuwa ‘tumepofushwa’ akili na Shetani; hatukumjua Yehova na viwango vyake vya uadilifu. (2 Kor. 4:4; Tito 3:3) Hivyo, tukifanya maamuzi kwa kutegemea tu mambo tunayofikiri ni mazuri na yanafaa, huenda tukajidanganya, hata kama tutatumia wakati mwingi kutafakari kuhusu jambo hilo.Met. 14:12.

6. Ni nini kitakachotusaidia kusitawisha utimamu wa akili?

6 Yehova, Baba yetu wa mbinguni ni mkamilifu kwa kila njia, tofauti na wanadamu wasio wakamilifu. (Kum. 32:4) Tunafurahi kwamba anatufundisha kufanya upya akili yetu na kusitawisha utimamu wa akili. (Soma 2 Timotheo 1:7.) Tukiwa Wakristo, tunahitaji kuchanganua mambo kwa busara na kutenda inavyofaa. Ni lazima tudhibiti fikira na hisia zetu na kuiga njia ya Yehova ya kufikiri, kuhisi, na kutenda.

7, 8. Simulia kisa kinachoonyesha kwamba mtu anaweza kufanya uamuzi mzuri licha ya mikazo au hali ngumu.

7 Fikiria mfano ufuatao. Ili waendelee kufanya kazi na kupata pesa, baadhi ya wazazi wanaohamia nchi nyingine huwapeleka watoto wao wachanga kuishi na kutunzwa na watu wao wa ukoo. * Mwanamke mmoja anayeishi katika nchi ya kigeni alijifungua mtoto mvulana mwenye afya. Wakati huo, alianza kujifunza Biblia na kufanya maendeleo ya kiroho. Marafiki na watu wa ukoo walianza kumshinikiza mwanamke huyo na mume wake wampeleke mtoto kwa wazazi wao. Hata hivyo, alipokuwa akijifunza Biblia alitambua kwamba Mungu amempa jukumu la kumlea mtoto wake. (Zab. 127:3; Efe. 6:4) Je, angefuata desturi inayokubaliwa na wengi, au angefuata mambo aliyokuwa akijifunza katika Biblia licha ya matatizo ya kifedha na dhihaka za watu? Kama ni wewe ungefanya nini?

8 Mwanamke huyo aliyekuwa na mkazo mwingi, alimweleza Yehova alivyohisi na kumwomba msaada. Baada ya kuzungumza na mwalimu wake wa Biblia na washiriki wengine wa kutaniko kuhusu hali yake, alianza kuelewa maoni ya Yehova kuhusu jambo hilo. Pia, alifikiria jinsi watoto wachanga wanavyoathiriwa kihisia wanapotenganishwa na wazazi wao. Baada ya kufikiria sababu za Kimaandiko, aliona kwamba halikuwa jambo linalofaa kumpeleka mtoto wake mbali. Mume wake aliona jinsi washiriki wa kutaniko walivyojitolea kuwasaidia na jinsi  mtoto wao alivyokuwa mwenye furaha na afya nzuri. Alikubali kujifunza Biblia na kuanza kuhudhuria mikutano na mke wake.

9, 10. Kuwa na utimamu wa akili kunamaanisha nini, na tutaupataje?

9 Hicho ni kisa kimoja tu, lakini kinaonyesha kwamba kuwa na utimamu wa akili hakumaanishi kufuata tu mambo ambayo sisi au wengine wanafikiri au kuhisi kwamba yanafaa. Akili na moyo wetu usio mkamilifu ni kama saa inayozunguka haraka sana au polepole sana. Tunaweza kutumbukia katika matatizo makubwa tukiongozwa na saa hiyo. (Yer. 17:9) Tunahitaji kutumia viwango vya Mungu vyenye kutegemeka kuzoeza akili na moyo wetu.Soma Isaya 55:8, 9.

10 Kwa kufaa, Biblia inatushauri hivi: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” (Met. 3:5, 6) Angalia maneno “usitegemee uelewaji wako mwenyewe.” Yanafuatwa na maneno “mtambue [Yehova].” Yeye peke yake Ndiye aliye na akili kamilifu. Hivyo, kila mara tunapohitaji kufanya uamuzi tunahitaji kuchunguza maoni ya Mungu katika Biblia. Kisha tufanye uamuzi tukitegemea Biblia. Huo ni utimamu wa akili, yaani, kuiga njia ya Yehova ya kufikiri.

ZOEZA NGUVU ZAKO ZA UFAHAMU

11. Ni nini siri ya kujifunza kufanya maamuzi ya hekima?

11 Si rahisi kujifunza kufanya maamuzi ya hekima na kuyatekeleza. Hilo linaweza kuwa jambo gumu hasa kwa watu wapya katika kweli au wale wanaofanya maendeleo ili kufikia ukomavu wa kiroho. Hata hivyo, watoto hao wachanga kiroho, kama wanavyoitwa katika Biblia, wanaweza kufanya maendeleo. Fikiria jinsi mtoto mchanga anavyojifunza kutembea bila kuanguka. Kwa kawaida, siri ni kupiga hatua ndogo-ndogo. Hivyo ndivyo mtoto mchanga kiroho anavyoweza kujifunza hatua kwa hatua kufanya maamuzi ya hekima. Kumbuka mtume Paulo alisema kwamba watu wakomavu ni wale ambao “kwa kutumia, nguvu zao za ufahamu  zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” Maneno “kwa kutumia” na “zimezoezwa” yanaonyesha hali ya kuendelea kujitahidi bila kuacha, na hivyo ndivyo wapya wanavyohitaji kufanya.Soma Waebrania 5:13, 14.

Tunapofanya maamuzi yanayofaa katika mambo madogo, tunazoeza nguvu zetu za ufahamu (Tazama fungu la 11)

12. Tunawezaje kusitawisha uwezo wa kufanya maamuzi kwa hekima?

12 Kama ilivyotajwa mwanzoni, hatuna budi kufanya maamuzi mengi kila siku, iwe ni madogo au makubwa. Uchunguzi fulani ulionyesha kwamba karibu nusu ya mambo tunayotenda yanategemea mazoea tu. Kwa mfano, huenda kila asubuhi unachagua nguo utakazovaa. Huenda usitumie muda mwingi kufanya hivyo hasa ikiwa una haraka. Lakini ukiwa mtumishi wa Yehova ni muhimu kufikiria ikiwa nguo hizo zinafaa. (2 Kor. 6:3, 4) Unaponunua nguo, huenda ukapendezwa na mitindo ya kisasa, lakini unapaswa kufikiria pia gharama yake na ikiwa ni zenye kiasi. Kufanya maamuzi yanayofaa kuhusiana na mambo hayo kutazoeza nguvu zetu za ufahamu, ambazo zinaweza kutusaidia kufanya maamuzi mazito yanayofaa.Luka 16:10; 1 Kor. 10:31.

SITAWISHA TAMAA YA KUFANYA YALIYO SAWA

13. Tunahitaji nini ili tufanikiwe kutekeleza maamuzi yetu?

13 Tunajua kwamba ni rahisi kufanya uamuzi unaofaa, lakini si rahisi kushikamana nao na kuutekeleza. Kwa mfano, baadhi ya watu wanaotaka kuacha kuvuta sigara hawajafanikiwa kuacha kwa sababu hawajaazimia. Wanahitaji kuazimia kutekeleza uamuzi wao. Watu fulani husema kwamba tunaweza kuimarisha tamaa hiyo kama tunavyoimarisha misuli ya mwili. Kadiri tunavyoitumia au kuizoeza ndivyo inavyoimarika zaidi. Tusipoitumia au kuizoeza kwa ukawaida, itadhoofika. Basi tunawezaje kusitawisha na kuimarisha tamaa au azimio la kushikamana na kutekeleza maamuzi yetu? Tunahitaji kumtegemea Yehova ili atusaidie.Soma Wafilipi 2:13.

14. Paulo alipataje nguvu za kufanya jambo alilopaswa kufanya?

14 Paulo alijifunza jambo hilo maishani. Pindi moja aliomboleza hivi: “Nina uwezo wa kutaka, bali uwezo wa kufanya yaliyo mazuri haupo.” Alijua jambo alilotaka kufanya au alilopaswa kufanya, lakini nyakati nyingine jambo fulani lilimzuia kufanya hivyo. Alikiri hivi: “Kwa kweli naipenda sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini mimi naona ndani ya viungo vyangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo ndani ya viungo vyangu.” Je, hakuwa na tumaini lolote? Hapana. Alisema hivi: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Rom. 7:18, 22-25) Pia, aliandika hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”Flp. 4:13.

15. Kufanya au kutofanya uamuzi kunaweza kuwa na matokeo gani kwa wanaohusika?

15 Ni wazi kwamba ili kumpendeza Mungu, ni lazima tuchukue hatua inayofaa. Kumbuka maneno haya ambayo Eliya aliwaambia waabudu wa Baali na Waisraeli waasi-imani kwenye Mlima Karmeli: “Mtayumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti mpaka wakati gani? Ikiwa Yehova ndiye Mungu wa kweli, mfuateni yeye; lakini ikiwa ni Baali, mfuateni yeye.” (1 Fal. 18:21) Wana wa Israeli walijua walilopaswa kufanya, lakini walikuwa ‘wakiyumba-yumba’ badala ya kufanya uamuzi. Lakini Yoshua aliweka mfano mzuri alipowaambia hivi Waisraeli  miaka mingi mapema: “Ikiwa mnaona ni vibaya machoni penu kumtumikia Yehova, jichagulieni leo yule mtakayemtumikia . . . Lakini mimi na nyumba yangu, tutamtumikia Yehova.” (Yos. 24:15) Alipata baraka gani kwa sababu ya azimio lake? Yoshua na wale walioshikamana naye walipata baraka ya kuingia katika Nchi ya Ahadi, “nchi inayotiririka maziwa na asali.”Yos. 5:6.

FANYA MAAMUZI YA HEKIMA NAWE UTABARIKIWA

16, 17. Simulia kisa kinachoonyesha faida za kufanya maamuzi kupatana na mapenzi ya Mungu.

16 Fikiria kisa kifuatacho. Ndugu aliyebatizwa karibuni ameoa, naye ana watoto watatu wadogo. Siku moja, mfanyakazi mwenzake alimpendekezea ndugu huyo wahamie katika kampuni nyingine ambayo ingewalipa mshahara mkubwa zaidi. Ndugu yetu alifikiria na kusali kuhusu jambo hilo. Alikubali kazi aliyo nayo sasa yenye mshahara mdogo kwa kuwa alitaka kupata wakati wa kuhudhuria mikutano na kuhubiri na familia yake mwisho-juma. Hivyo, aliona kwamba ikiwa angekubali kazi hiyo mpya ratiba yake ingebadilika. Wewe ungefanya nini?

17 Ndugu huyo alifikia mkataa kwamba faida za kiroho anazopata ni muhimu kuliko mshahara mnono, hivyo akakataa kazi hiyo mpya. Je, unafikiri alijutia uamuzi huo? Hapana. Aliona kwamba baraka za kiroho zingemnufaisha yeye na familia yake kuliko mshahara mnono. Yeye na mke wake walifurahi sana binti yao mkubwa mwenye umri wa miaka kumi alipowaambia kwamba aliwapenda, aliwapenda ndugu na dada kutanikoni, na alimpenda sana Yehova. Alisema kwamba alitaka kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Bila shaka, alithamini sana mfano mzuri wa baba yake katika kutanguliza ibada ya Yehova maishani.

Fanya maamuzi ya hekima na ufurahie kushirikiana na watu wa Mungu (Tazama fungu la 18)

18. Kwa nini ni muhimu tufanye maamuzi ya hekima kila siku?

18 Yesu Kristo, yule Musa Mkuu Zaidi, amekuwa akiwaongoza waabudu wa kweli wa Yehova kwa miaka mingi katika ulimwengu wa Shetani ulio kama nyika. Yesu, yule Yoshua Mkuu Zaidi, yuko tayari kukomesha mfumo huu mwovu na kuwaongoza wafuasi wake kuingia katika ulimwengu mpya wa uadilifu ulioahidiwa na Mungu. (2 Pet. 3:13) Kwa hiyo, huu si wakati wa kurudia njia yetu ya zamani ya kufikiri, tabia, viwango, na malengo tuliyokuwa nayo. Badala yake, huu ni wakati wa kufahamu waziwazi zaidi mapenzi ya Mungu. (Rom. 12:2; 2 Kor. 13:5) Fanya maamuzi ya hekima kila siku ili Mungu akubariki milele.Soma Waebrania 10:38, 39.

^ fu. 7 Baadhi yao huwachukua watoto hao ili kuwaonyesha marafiki na watu wa ukoo kwamba wana wajukuu.