Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vifanye Vikumbusho vya Yehova Kuwa Furaha ya Moyo Wako

Vifanye Vikumbusho vya Yehova Kuwa Furaha ya Moyo Wako

“Nimevichukua vikumbusho vyako kuwa ni urithi mpaka wakati usio na kipimo.”ZAB. 119:111.

1. (a) Wanadamu huitikiaje wanaposhauriwa, na kwa nini? (b) Kiburi kinaweza kuathirije mtazamo wa mtu anaposhauriwa?

WANADAMU huitikia mashauri kwa njia tofauti-tofauti. Huenda wakakubali haraka wanaposhauriwa na mtu mwenye mamlaka, lakini wakakataa mara moja shauri kutoka kwa mtu wa rika lao au asiye na mamlaka. Pia, wanadamu huitikia nidhamu na himizo kwa njia zinazotofautiana kabisa. Huenda baadhi yao wakahuzunika, wakasikitika, au kuaibika, lakini huenda wengine wakachochewa kutumia mashauri hayo. Kwa nini wanaitikia kwa njia tofauti? Sababu moja ni kiburi. Kwa kweli, roho ya majivuno inaweza kumpofusha mtu akili na kumfanya akatae mashauri, na hivyo kukosa kufaidika na maagizo yenye thamani.Met. 16:18.

2. Kwa nini Wakristo wa kweli wanathamini mashauri ya Neno la Mungu?

2 Hata hivyo, Wakristo wa kweli wanathamini mashauri yanayofaa, hasa yanapotegemea Neno la Mungu. Vikumbusho vya Yehova vinatusaidia kuwa na ufahamu, vinatufundisha na kutusaidia kuepuka mitego kama vile kufuatilia vitu vya kimwili, mwenendo mpotovu wa kingono, ulevi, na matumizi mabaya ya dawa za kulevya. (Met. 20:1; 2 Kor. 7:1; 1 The. 4:3-5; 1 Tim. 6:6-11) Zaidi ya hayo, tunafurahia “hali nzuri ya moyo” inayotokana na kutii vikumbusho vya Mungu.Isa. 65:14.

3. Ni mtazamo gani wa mtunga-zaburi tunaopaswa kuiga?

3 Ili kulinda uhusiano wetu wenye thamani pamoja na Baba yetu wa mbinguni, tunapaswa kuendelea kufuata mwongozo wa Yehova wenye hekima maishani mwetu. Ni vizuri kuwa na mtazamo kama wa  mtunga-zaburi aliyeandika hivi: “Nimevichukua vikumbusho vyako kuwa ni urithi mpaka wakati usio na kipimo, kwa maana hivyo ni furaha ya moyo wangu.” (Zab. 119:111) Je, tunapendezwa na amri za Yehova kama mtunga-zaburi au nyakati nyingine tunaziona kuwa mzigo? Hata kama pindi fulani hatupendezwi na shauri tunalopewa, hatupaswi kukata tamaa. Tunaweza kujifunza kutegemea kabisa hekima ya Mungu iliyo bora! Acheni tufikirie njia tatu za kufanya hivyo.

MTEGEMEE YEHOVA KUPITIA SALA

4. Daudi aliendelea kufanya nini maishani mwake?

4 Ingawa Mfalme Daudi alikabili hali mbalimbali maishani mwake, aliendelea kumtegemea kabisa Muumba wake. Alisema hivi: “Kwako wewe, Ee Yehova, naiinua nafsi yangu. Ee Mungu wangu, nimekutegemea wewe.” (Zab. 25:1, 2) Ni nini kilichomsaidia Daudi kumtegemea kabisa Baba yake wa mbinguni?

5, 6. Neno la Mungu linaonyesha nini kuhusu uhusiano ambao Daudi alikuwa nao na Yehova?

5 Watu wengi husali kwa Mungu wanapokabili tu hali ngumu. Ungehisije ikiwa rafiki au ndugu yako angezungumza nawe tu anapohitaji pesa au msaada fulani? Huenda baada ya muda ungeanza kutilia shaka nia yake ya kukutafuta. Lakini Daudi hakuomba tu msaada. Uhusiano wake na Yehova ulionyesha kwamba alikuwa na imani na alimpenda Mungu wake maishani mwake, katika hali nzuri au mbaya.Zab. 40:8.

6 Fikiria maneno haya ya Daudi ya kumsifu na kumshukuru Yehova: “Ee Yehova Bwana wetu, jina lako ni lenye utukufu kama nini katika dunia yote, wewe ambaye utukufu wako unasimuliwa juu ya mbingu!” (Zab. 8:1) Je, unaona uhusiano wa karibu ambao Daudi alikuwa nao pamoja na Baba yake wa mbinguni? Daudi alichochewa kumtukuza Yehova “mchana kutwa” kwa sababu alithamini fahari na ukuu Wake.Zab. 35:28.

7. Tunafaidikaje tunapomkaribia Mungu kupitia sala?

7 Kama Daudi, tunahitaji kumtegemea Yehova kwa kuwasiliana naye kwa ukawaida. Biblia inasema hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:8) Kumkaribia Mungu kupitia sala ni njia muhimu ya kupata roho takatifu.Soma 1 Yohana 3:22.

8. Kwa nini tunapaswa kuepuka kurudia maneno yaleyale tunaposali?

8 Je, wewe hurudia maneno yaleyale unaposali? Ikiwa ndivyo, kabla ya kusali, tumia wakati fulani kufikiria kile unachotaka kusema. Je, rafiki au mtu wetu wa ukoo atafurahia ikiwa tunarudia maneno yaleyale tunapozungumza naye? Huenda akaacha kutusikiliza. Bila shaka, Yehova hawezi kamwe kuacha kusikiliza sala ya kutoka moyoni ya mmoja wa watumishi wake washikamanifu. Hata hivyo, ni jambo la busara kuepuka kuwasiliana naye kidesturi tu.

9, 10. (a) Tunaweza kutaja nini katika sala zetu? (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia kusali kutoka moyoni?

9 Bila shaka, ikiwa tunataka kumkaribia Mungu, sala zetu hazipaswi kuwa za kijuujuu tu. Kadiri tunavyomwambia Yehova mambo yaliyo moyoni mwetu ndivyo tunavyozidi kumkaribia na kumtegemea. Lakini tunahitaji kutaja mambo gani katika sala zetu? Neno la Mungu linajibu hivi: “Katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.” (Flp. 4:6) Kwa kweli, tunapaswa kusali kuhusu kila jambo linaloathiri uhusiano wetu na Mungu au maisha yetu tukiwa watumishi wake.

10 Tunajifunza mengi tunapochunguza sala za wanaume na wanawake waaminifu zilizoandikwa katika Biblia. (1 Sam. 1:10, 11;  Mdo. 4:24-31) Kitabu cha Zaburi kina nyimbo na sala za kutoka moyoni zilizotolewa kwa Yehova. Sala na nyimbo hizo zinaonyesha hisia mbalimbali za wanadamu kama vile mahangaiko na shangwe. Kuchanganua sala hizo za watumishi washikamanifu kunaweza kutusaidia kusali kwa Yehova kwa njia inayofaa.

TAFAKARI KUHUSU VIKUMBUSHO VYA MUNGU

11. Kwa nini tunahitaji kutafakari kuhusu mashauri ya Mungu?

11 Daudi alitangaza hivi: “Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, humfanya asiye na uzoefu awe na hekima.” (Zab. 19:7) Hata ikiwa hatuna uzoefu, tunaweza kupata hekima kwa kutii amri za Mungu. Hata hivyo, ili tufaidike kikamili na mashauri fulani ya Kimaandiko tunahitaji kutafakari. Kutafakari kunaweza pia kutusaidia kuendelea kuwa watimilifu tunapokabili mkazo shuleni au kazini, kutatusaidia kushikilia viwango vya Mungu kuhusu damu, kudumisha msimamo wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote, na kufuata kanuni za Biblia kuhusu mavazi na kujipamba. Kuwa na maoni kama ya Mungu kuhusu mambo hayo kutatusaidia kuwa tayari kukabiliana na matatizo. Kisha tunaweza kuazimia mioyoni mwetu jambo tutakalofanya tatizo likitokea. Kufikiria na kujitayarisha mapema kwa njia hiyo kutatusaidia kuepuka maumivu ya moyo.Met. 15:28.

12. Tunaweza kuvitii vikumbusho vya Mungu tukitafakari juu ya nini?

12 Tunapoendelea kusubiri Mungu atimize ahadi zake, je, mwenendo wetu unaonyesha kwamba tunaendelea kukesha kiroho? Kwa mfano, je, tunaamini kabisa kwamba hivi karibuni Babiloni Mkubwa ataharibiwa? Je, bado tunaziona baraka za wakati ujao, kama vile uzima wa milele katika dunia paradiso, kuwa halisi kama tulivyoziona tulipoanza kujifunza? Je, bado tunaendelea kuhubiri kwa bidii badala ya kutanguliza mambo ya kibinafsi maishani? Vipi kuhusu tumaini la ufufuo, kutakaswa kwa jina la Yehova, na kutetewa kwa enzi yake kuu? Je, mambo hayo bado ni muhimu kwetu? Kutafakari kuhusu maswali hayo huenda kukatusaidia kutenda kama mtunga-zaburi alivyosema, yaani, kuvifanya ‘vikumbusho vya Mungu kuwa urithi mpaka wakati usio na kipimo.’Zab. 119:111.

13. Kwa nini Wakristo wa karne ya kwanza hawakuelewa mambo fulani? Toa mfano.

13 Huenda baadhi ya mambo yaliyotajwa katika Biblia yasieleweke kikamili sasa kwa kuwa wakati wa Yehova wa kuyafunua haujafika. Yesu aliwaambia mitume wake tena na tena kwamba ilikuwa lazima ateseke na kisha kuuawa. (Soma Mathayo 12:40; 16:21.) Hata hivyo, mitume hawakuelewa alichomaanisha. Walielewa jambo hilo baada ya Yesu kufa na kufufuliwa. Wakati huo, aliwatokea baadhi ya wanafunzi wake akiwa amejivika mwili wa kibinadamu na ‘kufungua akili zao ili wafahamu maana ya Maandiko.’ (Luka 24:44-46; Mdo. 1:3) Vilevile, baada tu ya roho takatifu kumiminwa juu ya wafuasi wa Kristo wakati wa Pentekoste ya 33 W.K., ndipo walipojua kwamba Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala mbinguni.Mdo. 1:6-8.

14. Mwanzoni mwa karne ya 20, ndugu wengi waliweka mfano gani mzuri licha ya kwamba hawakuelewa vizuri kuhusu siku za mwisho?

14 Vivyo hivyo, mwanzoni mwa karne ya 20 Wakristo wa kweli walikuwa na matarajio yasiyo sahihi kuhusu “siku za mwisho.” (2 Tim. 3:1) Kwa mfano, baadhi yao walifikiri kwamba wangechukuliwa na kwenda mbinguni mwaka wa 1914. Matumaini yao yalipokosa kutimia wakati huo, walichunguza tena Maandiko kwa bidii na kutambua kwamba kazi kubwa ya kuhubiri  ilihitaji kufanywa. (Marko 13:10) Hivyo, katika mwaka wa 1922, J. F. Rutherford, aliyeongoza katika kazi ya kuhubiri, aliwaambia hivi wale waliohudhuria kusanyiko la kimataifa huko Cedar, Point, Ohio, Marekani: “Tazameni, Mfalme anatawala! Ninyi ndio mawakili wa kumtangaza. Kwa hiyo, mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Tangu wakati huo na kuendelea, kazi ya kutangaza “habari njema ya ufalme” inawatambulisha watumishi wa Yehova.Mt. 4:23; 24:14.

15. Tunafaidikaje tunapotafakari jinsi ambavyo Mungu amekuwa akishughulika na watu wake?

15 Tunapotafakari jinsi ambavyo Yehova amekuwa akishughulika na watu wake, zamani na sasa, tunakuwa na uhakika zaidi kwamba atatimiza mapenzi na makusudi yake wakati ujao. Wakati huohuo, vikumbusho vya Mungu vinatusaidia kuendelea kukumbuka na kuthamini unabii utakaotimizwa wakati ujao. Tunaweza kuwa na hakika kwamba kufanya hivyo kutatusaidia kutegemea ahadi zake.

MTEGEMEE YEHOVA KUPITIA MATENDO YA IBADA

16. Tunapata baraka gani tunapoendelea kuwa wenye bidii katika huduma?

16 Mungu wetu, Yehova, ni Mungu mwenye nguvu, Mungu anayetenda. Mtunga-zaburi aliuliza hivi: “Ni nani aliye na nguvu kama wewe, Ee Yah?” Kisha akaongezea hivi: “Mkono wako una nguvu, mkono wako wa kuume umeinuliwa.” (Zab. 89:8, 13) Kwa hiyo, Yehova anathamini na kubariki jitihada zetu za kuunga mkono masilahi ya Ufalme. Anahakikisha kwamba watumishi wake, wanaume na wanawake, vijana na wazee, hawakai tu na kula “mkate wa uvivu.” (Met. 31:27) Tunamwiga Muumba wetu kwa kuwa na mengi ya kufanya katika utendaji wa kitheokrasi. Tunapomtumikia Mungu kwa moyo wote tunapata  thawabu, na Yehova anafurahi na kubariki huduma yetu.Soma Zaburi 62:12.

17, 18. Kwa nini tunaweza kusema kwamba matendo ya imani yanatusaidia kutegemea maagizo ya Yehova? Toa mfano.

17 Matendo ya imani yanatusaidiaje kumtegemea Yehova? Fikiria simulizi la Kimaandiko linaloonyesha jinsi Waisraeli walivyoingia katika Nchi ya Ahadi. Yehova aliwaagiza makuhani waliobeba sanduku la agano waingie ndani ya Mto Yordani. Hata hivyo, watu walipokuwa wakikaribia, waliona kwamba mto umefurika baada ya mvua kunyesha. Waisraeli wangefanya nini? Je, wangepiga kambi kwenye ukingo wa mto na kusubiri kwa majuma kadhaa au zaidi mpaka maji yapungue? Hapana, walimtegemea Yehova kikamili na kufuata maagizo yake. Matokeo yakawa nini? Simulizi hilo linasema hivi: “Mara tu nyayo za miguu ya makuhani zilipogusa maji, maji ya mto yakaacha kutiririka, . . . na makuhani wakasimama katikati ya bonde kavu la mto karibu na Yeriko huku wengine wote wakivuka.” (Yos. 3:12-17, Contemporary English Version) Hebu wazia jinsi walivyotiwa moyo walipoona maji hayo yenye nguvu yakiwa yamesimamishwa! Kwa kweli, imani ya Waisraeli katika Yehova iliimarishwa kwa sababu walitegemea maagizo yake.

Je, utamtegemea Yehova kama watu Wake walivyofanya katika siku za Yoshua? (Tazama fungu la 17 na 18)

18 Ni kweli kwamba leo Yehova hafanyi miujiza kwa ajili ya watu wake, lakini anawabariki kwa sababu ya matendo yao ya imani. Nguvu ya utendaji ya Mungu inawawezesha kutimiza kazi waliyopewa ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme ulimwenguni pote. Pia, Kristo Yesu aliyefufuliwa, ambaye ni Shahidi mkuu zaidi wa Yehova, aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba angewategemeza wanapofanya kazi hiyo muhimu. Aliwaambia hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote . . . Mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20) Mashahidi wengi ambao huenda waliogopa au kukosa ujasiri wanaweza kusema kwamba roho takatifu ya Mungu imewapa ujasiri wa kuzungumza na watu wasiowajua katika huduma ya shambani.Soma Zaburi 119:46; 2 Wakorintho 4:7.

19. Tuna uhakika gani licha ya udhaifu wetu?

19 Baadhi ya ndugu na dada hawawezi kutimiza mengi kwa sababu ya ugonjwa au kuzeeka. Hata hivyo, wanaweza kuwa na hakika kwamba “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote” anaelewa hali za kila Mkristo wa kweli. (2 Kor. 1:3) Anathamini yote tunayofanya ili kuunga mkono masilahi ya Ufalme. Sote tunahitaji kukumbuka kwamba nafsi zetu zinahifadhiwa hai kwa msingi tu wa imani yetu katika fidia ya Kristo, huku tukifanya yote tunayoweza kulingana na hali zetu.Ebr. 10:39.

20, 21. Tunaonyesha kwa njia zipi kwamba tunamtegemea Yehova?

20 Ibada yetu inahusisha kutumia wakati, nguvu, na mali zetu kikamili zaidi iwezekanavyo. Kwa kweli, tungependa ‘kufanya kazi ya mweneza-injili’ kwa moyo wetu wote. (2 Tim. 4:5) Ukweli ni kwamba tunafurahia kufanya hivyo kwa kuwa tunawasaidia wengine “kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Ni wazi kwamba tunatajirika kiroho tunapomheshimu na kumsifu Yehova. (Met. 10:22) Na hilo linatusaidia kumtegemea kikamili kabisa Muumba wetu.Rom. 8:35-39.

21 Kama tulivyoona, ni lazima tujitahidi ili kutegemea mwongozo wenye hekima wa Yehova. Kwa hiyo, jitahidi kadiri uwezavyo kumtegemea Yehova kupitia sala. Tafakari jinsi Yehova alivyotimiza mapenzi yake zamani na jinsi atakavyofanya hivyo wakati ujao. Endelea kumtegemea Yehova kupitia matendo ya ibada. Kwa kweli, vikumbusho vya Yehova vitadumu milele. Wewe pia unaweza kuishi milele!