Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Siku Hii Itakuwa Ukumbusho Kwenu”

“Siku Hii Itakuwa Ukumbusho Kwenu”

“Siku hii itakuwa ukumbusho kwenu, nanyi mtaisherehekea ikiwa sherehe kwa Yehova.”KUT. 12:14.

1, 2. Wakristo wote wanapaswa kupendezwa na sherehe gani, na kwa nini?

NI SIKU gani muhimu unayokumbuka kwa urahisi? Huenda mtu aliyefunga ndoa akasema: “Siku ya harusi.” Wengine hukumbuka tukio fulani la kihistoria kama vile siku ambayo nchi yao ilipata uhuru. Lakini je, unajua sherehe ya kitaifa ambayo imeadhimishwa kwa miaka zaidi ya 3,500?

2 Ni sherehe ya Pasaka. Ilikuwa sherehe ya kukumbuka kukombolewa kwa taifa la kale la Israeli kutoka utumwani huko Misri. Tukio hilo linapaswa kuwa muhimu kwako. Kwa nini? Kwa sababu linahusiana na mambo fulani muhimu maishani mwako. Hata hivyo, huenda ukasema: ‘Wayahudi ndio wanaosherehekea Pasaka, lakini mimi si Myahudi. Inanihusuje?’ Maneno haya muhimu yanajibu swali hilo: “Kristo pasaka yetu ametolewa dhabihu.” (1 Kor. 5:7) Ili tuelewe vizuri umuhimu wa maneno hayo ya kweli, tunahitaji kuijua Pasaka ya Wayahudi na kuona jinsi inavyohusiana na amri fulani waliyopewa Wakristo wote.

KWA NINI WAISRAELI WALISHEREHEKEA PASAKA?

3, 4. Ni nini kilichotukia kabla ya Pasaka ya kwanza?

3 Ulimwenguni pote, mamilioni ya watu wasio Wayahudi wanajua kwa kadiri fulani kilichotukia kabla ya Pasaka ya kwanza. Huenda walisoma kitabu cha Biblia cha Kutoka, walisimuliwa au kuona sinema inayohusu tukio hilo.

4 Baada ya Waisraeli kuwa watumwa kwa miaka mingi huko Misri, Yehova alimtuma Musa na Haruni ndugu yake, wakamwambie Farao awaachilie huru watu Wake. Mtawala huyo wa Misri mwenye kiburi alikataa kuwaruhusu Waisraeli waende zao, hivyo Yehova akaipiga nchi ya Misri kwa mfululizo wa mapigo yenye kuangamiza. Mwishowe, Mungu alileta pigo la kumi lililoua wazaliwa wote wa kwanza Wamisri, na  hivyo Farao akawaacha Waisraeli waende zao.—Kut. 1:11; 3:9, 10; 5:1, 2; 11:1, 5.

5. Waisraeli walipaswa kujitayarishaje ili waachiliwe huru? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 17.)

5 Hata hivyo, Waisraeli walipaswa kufanya nini kabla ya kuachiliwa huru? Ulikuwa wakati wa majira ya kuchipua ya mwaka wa 1513 K.W.K., katika mwezi wa Kiebrania wa Abibu, uliokuja kuitwa Nisani, wakati ambapo saa za mchana hulingana kwa urefu na saa za usiku. * Mungu alisema kwamba katika siku ya kumi ya mwezi huo, Waisraeli walipaswa kuanza kujitayarisha kufanya mambo fulani Nisani 14. Siku hiyo ilianza jua lilipotua kwa kuwa kulingana na Waebrania, siku ilianza na kwisha jua lilipotua. Katika Nisani 14, kila familia ilipaswa kuchinja kondoo dume (au mbuzi), kuchukua sehemu ya damu na kuipaka juu ya miimo ya mlango na sehemu ya juu ya mlango wa nyumba. (Kut. 12:3-7, 22, 23) Kila familia ilipaswa kumla mwana-kondoo aliyechomwa kwa moto, mboga, na mkate usiotiwa chachu. Malaika wa Mungu angepita katikati ya nchi na kumchinja kila mzaliwa wa kwanza wa Misri, lakini Waisraeli waliotii wangelindwa, kisha Farao angewaruhusu waende zao.—Kut. 12:8-13, 29-32.

6. Watu wa Mungu walipaswa kuendelea kuionaje Pasaka?

6 Hivyo ndivyo ilivyotukia, na Waisraeli walipaswa kuendelea kukumbuka ukombozi wao. Mungu aliwaambia hivi: “Siku hii itakuwa ukumbusho kwenu, nanyi mtaisherehekea ikiwa sherehe kwa Yehova katika vizazi vyenu vyote. Nanyi mtaisherehekea kama sheria mpaka wakati usio na kipimo.” Mwadhimisho huo uliofanywa siku ya 14 ulifuatiwa na sherehe ya siku saba. Nisani 14 ndiyo iliyokuwa siku ya Pasaka, lakini siku zote nane za sherehe hiyo ziliitwa pia Pasaka. (Kut. 12:14-17; Luka 22:1; Yoh. 18:28; 19:14) Pasaka ilikuwa mojawapo ya sherehe rasmi (“sikukuu,” Union Version) ambazo Wayahudi walipaswa kusherehekea kila mwaka.—2 Nya. 8:13.

7. Yesu alianzisha nini wakati wa Pasaka ya mwisho halali?

7 Yesu na mitume wake walisherehekea Pasaka kila mwaka kwa sababu walikuwa Wayahudi na hivyo walikuwa chini ya Sheria ya Musa. (Mt. 26:17-19) Mara ya mwisho waliposherehekea Pasaka, Yesu alianzisha mwadhimisho mpya ambao wafuasi wake wangekumbuka kila mwaka, yaani, Mlo wa Jioni wa Bwana. Lakini walipaswa kuuadhimisha siku gani?

MLO WA JIONI WA BWANA UNGEADHIMISHWA SIKU GANI?

8. Ni maswali gani tunayoweza kuuliza kuhusu Pasaka na Mlo wa Jioni wa Bwana?

8 Kwa kuwa Yesu alianzisha Mlo wa Jioni wa Bwana baada tu ya Pasaka hiyo ya mwisho, mwadhimisho huo mpya ulifanywa katika siku ambayo Pasaka ilikuwa ikisherehekewa. Hata hivyo, huenda umeona kwamba tarehe ya Pasaka ya Kiyahudi katika kalenda za leo inatofautiana kwa siku moja au zaidi na tarehe tunayoadhimisha kifo cha Kristo. Kwa nini? Kwa njia fulani, ni kwa sababu ya amri ambayo Mungu aliwapa Waisraeli. Baada ya kusema kwamba “kutaniko zima la kusanyiko la Israeli litamchinja” mwana-kondoo, Musa alitaja wakati hususa wa kumchinja mwana-kondoo huyo siku ya Nisani 14.—Soma Kutoka 12:5, 6.

9. Kulingana na Kutoka 12:6, mwana-kondoo wa Pasaka alipaswa kuchinjwa wakati gani? (Tazama pia sanduku  “Ni Wakati Gani wa Siku?”)

9 Kulingana na kitabu kimoja (The Pentateuch and Haftorahs), andiko la Kutoka  12:6 linasema kwamba mwana-kondoo alipaswa kuchinjwa “katikati ya zile jioni mbili.” Tafsiri fulani za Biblia hutumia maneno hayohayo. Tafsiri nyingine, kama vile Tanakh ya Kiyahudi hutafsiri maneno hayo kuwa “saa za jioni.” Tafsiri nyingine husema “wakati wa jioni,” “giza linapoanza kuingia,” au “jua linapotua.” Kwa hiyo, mwana-kondoo alipaswa kuchinjwa baada ya jua kutua lakini kabla ya giza kuingia, mwanzo wa Nisani 14.

10. Watu fulani husema mwana-kondoo alichinjwa wakati gani, lakini hilo linatokeza swali gani?

10 Baadaye, Wayahudi fulani walifikiri kwamba ingechukua saa nyingi kuchinja wana-kondoo wote walioletwa hekaluni. Kwa hiyo, walielewa kwamba andiko la Kutoka 12:6 lilimaanisha mwisho wa Nisani 14, yaani, kuanzia jua linapoanza kushuka (baada ya saa sita mchana) hadi mwisho wa siku jua linapotua. Ikiwa ilimaanisha hivyo, basi mlo wa Pasaka ungeliwa wakati gani? Profesa Jonathan Klawans, mtaalamu wa dini ya kale ya Kiyahudi aliandika hivi: “Siku mpya huanza jua linapotua, hivyo dhabihu inatolewa siku ya 14 lakini mlo na sherehe ya Pasaka hufanywa siku ya 15, ingawa kitabu cha Kutoka hakitaji jambo hilo waziwazi.” Pia aliandika hivi: “Maandishi ya Marabi . . . hayasemi lolote kuhusu utaratibu uliofuatwa katika mlo wa Pasaka [Seder] kabla ya Hekalu kuharibiwa” mwaka wa 70 W.K.—Italiki ni zetu.

11. (a) Yesu alikabili hali gani siku ya Pasaka ya 33 W.K.? (b) Kwa nini Nisani 15 mwaka wa 33 W.K. iliitwa Sabato “kuu”? (Tazama maelezo ya chini.)

11 Hivyo, tuna sababu ya kuuliza hivi: Pasaka ya mwaka wa 33 W.K. ilifanywa siku gani? Mnamo Nisani 13, siku ilipokaribia ambayo ‘mnyama wa pasaka alipaswa kutolewa dhabihu,’ Kristo aliwaambia hivi Petro na Yohana: “Nendeni mkatutayarishie pasaka ili tule.” (Luka 22:7, 8) ‘Mwishowe, saa ikafika’ ya mlo wa Pasaka, baada ya jua kutua mnamo Nisani 14, ilikuwa Alhamisi jioni. Yesu alikula mlo huo pamoja na mitume wake, kisha akaanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana. (Luka 22:14, 15) Usiku huo, alikamatwa na kushtakiwa. Yesu alitundikwa mtini karibu saa sita mchana Nisani 14, naye akafa siku hiyohiyo alasiri. (Yoh. 19:14) Hivyo, ‘Kristo pasaka yetu akatolewa dhabihu’ siku ileile ambayo mwana-kondoo wa Pasaka alichinjwa. (1 Kor. 5:7; 11:23; Mt. 26:2) Yesu alizikwa mwishoni mwa siku hiyo ya Kiyahudi, kabla ya Nisani 15 kuanza. *Law. 23:5-7; Luka 23:54.

 UKUMBUSHO WENYE MAANA KWAKO

12, 13. Watoto Wayahudi walishiriki jinsi gani katika sherehe ya Pasaka?

12 Acheni tufikirie tena kilichotukia Misri. Musa alisema kwamba watu wa Mungu wangeendelea kusherehekea Pasaka; ilipaswa kuwa sharti “mpaka wakati usio na kipimo.” Wakati wa sherehe hiyo ya kila mwaka, watoto waliwauliza wazazi wao maana ya tukio hilo. (Soma Kutoka 12:24-27; Kum. 6:20-23) Kwa hiyo, Pasaka ingekuwa “ukumbusho” hata kwa watoto.—Kut. 12:14.

13 Akina baba wangewafundisha watoto wao mambo muhimu na kuyakazia kizazi baada ya kizazi. Kwa mfano, waliwafundisha kwamba Yehova angewalinda waabudu wake. Watoto walifundishwa kwamba Yehova si mungu wa kuwaziwa tu na asiyeeleweka. Yehova ni Mungu halisi aliye hai, anayewajali na kuwalinda watu wake. Alithibitisha hilo “alipowaletea Wamisri pigo” na kuwalinda wazaliwa wa kwanza wa Israeli. Hakuwaangamiza wazaliwa wa kwanza wa Israeli.

14. Wazazi Wakristo wanaweza kutumia simulizi la Pasaka kuwasaidia watoto wao wathamini nini?

14 Kila mwaka, wazazi Wakristo hawawaambii wana na binti zao maana ya Pasaka. Hata hivyo, je, unawafundisha watoto wako kwamba Mungu huwalinda watu wake? Je, watoto wako wanaona kwamba unasadiki kabisa kuwa Yehova bado huwalinda kikweli watu wake? (Zab. 27:11; Isa. 12:2) Je, unafanya hivyo kupitia mazungumzo wanayofurahia au ni kana kwamba unawatolea hotuba? Jitahidi kuifundisha familia yako jambo hilo ili ikue kiroho.

Utawafundisha nini watoto wako mnapozungumzia Pasaka? (Tazama fungu la 14)

15, 16. Masimulizi kuhusu Pasaka na Kutoka yanaweza kutumiwa kukazia nini kumhusu Yehova?

15 Jambo lingine tunalojifunza kutokana na Pasaka ni kwamba Yehova anaweza kuwalinda watu wake na pia kuwakomboa. Alifanya hivyo ‘alipowatoa Misri.’ Alifanyaje hivyo? Alitumia nguzo ya wingu na ya moto kuwaongoza. Wakatembea juu ya sakafu ya Bahari Nyekundu huku maji yakiwa kama ukuta upande wa kushoto na kulia. Walipofika upande wa pili, waliona bahari ikilifunika jeshi la Misri. Baada ya Waisraeli kukombolewa waliimba hivi: “Acheni nimwimbie Yehova . . . Farasi na mpandaji wake amewatupa baharini. Nguvu zangu na uwezo wangu ni Yah, kwa maana yeye ndiye wokovu wangu.”—Kut. 13:14, 21, 22; 15:1, 2; Zab. 136:11-15.

16 Je, unawasaidia watoto wako kumtegemea Yehova akiwa Mkombozi? Je, mazungumzo yako na maamuzi unayofanya yanawasadikishia kwamba unaamini hivyo? Mnaweza kuzungumzia Kutoka sura ya 12-15 kwenye Ibada ya Familia na kukazia jinsi Yehova alivyowakomboa watu wake. Unaweza pia kukazia jambo hilo pindi nyingine mnapozungumzia Matendo 7:30-36 au Danieli 3:16-18, 26-28. Naam, vijana na wazee wanapaswa kusadiki kwamba Yehova hakuwa Mkombozi nyakati za kale tu. Atatukomboa wakati ujao kama alivyowakomboa  watu wake katika siku za Musa.—Soma 1 Wathesalonike 1:9, 10.

JAMBO TUNALOPASWA KUKUMBUKA

17, 18. Kufikiria jinsi damu ilivyotumiwa Pasaka ilipoanzishwa kunapaswa kutukumbusha nini?

17 Wakristo wa kweli hawasherehekei Pasaka ya Kiyahudi. Sherehe hiyo ilikuwa sehemu ya Sheria ya Musa, na hatuko chini ya Sheria hiyo. (Rom. 10:4; Kol. 2:13-16) Hata hivyo, tunakumbuka kwa uthamini kifo cha Mwana wa Mungu. Lakini kuna mambo fulani katika sherehe ya Pasaka iliyoanzishwa huko Misri yaliyo na maana kwetu.

18 Damu ya mwana-kondoo iliyopakwa juu ya miimo na sehemu ya juu ya mlango iliokoa uhai. Leo, hatumtolei Mungu dhabihu za wanyama siku ya Pasaka au siku nyingine yoyote. Lakini kuna dhabihu bora zaidi inayoweza kuokoa uhai milele. Mtume Paulo aliandika kuhusu “kutaniko la wazaliwa wa kwanza ambao wameandikishwa mbinguni.” Uhai wa Wakristo hao watiwa-mafuta utaokolewa na “damu ya kunyunyiza,” yaani, damu ya Yesu. (Ebr. 12:23, 24) Wakristo wanaotumaini kuishi milele duniani wanategemea damu hiyohiyo ili waokolewe. Wanapaswa kujikumbusha kwa ukawaida uhakikisho huu: “Kwa njia yake tuna kuachiliwa huru kwa njia ya fidia kupitia damu ya huyo, ndiyo, msamaha wa makosa yetu, kulingana na utajiri wa fadhili zake zisizostahiliwa.”—Efe. 1:7.

19. Kutayarishwa kwa mwana-kondoo wa Pasaka huimarishaje uhakika wetu katika unabii?

19 Mwana-kondoo alipochinjwa kwa ajili ya mlo wa Pasaka, Waisraeli hawakupaswa kuvunja mfupa wake wowote. (Kut. 12:46; Hes. 9:11, 12) Namna gani “Mwana-Kondoo wa Mungu” aliyekuja kutoa fidia? (Yoh. 1:29) Alitundikwa mtini katikati ya wahalifu wawili. Wayahudi walimwomba Pilato aagize mifupa ya wanaume hao waliotundikwa ivunjwe. Hilo lingefanya wafe haraka na hivyo kuondolewa juu ya miti kabla ya Nisani 15, siku ya Sabato kuu. Askari-jeshi walivunja miguu ya wahalifu wawili waliotundikwa, “lakini walipokuja kwa Yesu, kwa kuwa waliona kwamba tayari alikuwa amekufa, hawakuivunja miguu yake.” (Yoh. 19:31-34) Vivyo hivyo, mwana-kondoo wa Pasaka hakuvunjwa miguu. Kwa njia hiyo, mwana-kondoo huyo alikuwa “kivuli” cha jambo ambalo lingetukia Nisani 14, mwaka wa 33 W.K. (Ebr. 10:1) Isitoshe, mambo hayo yalitimiza Zaburi 34:20, na hilo linapaswa kuimarisha uhakika wetu katika unabii.

20. Kuna tofauti gani kubwa kati ya Pasaka na Mlo wa Jioni wa Bwana?

20 Hata hivyo, kuna tofauti kati ya Pasaka na Mlo wa Jioni wa Bwana. Tofauti hizo zinaonyesha kwamba Pasaka ambayo Wayahudi walisherehekea haikuwa kivuli cha mambo ambayo Kristo aliwaambia wafuasi wake wafanye ili kukumbuka kifo chake. Huko Misri, Waisraeli walikula nyama ya mwana-kondoo lakini hawakunywa damu yake. Yesu hakuwaagiza wanafunzi wake wafanye hivyo. Alisema kwamba wale watakaotawala “katika Ufalme wa Mungu” wanapaswa kula mkate na kunywa divai ambayo ni mifano ya nyama yake na damu yake. Tutazungumzia jambo hilo kwa undani zaidi katika makala inayofuata.—Marko 14:22-25.

21. Tunafaidikaje kwa kujifunza kuhusu Pasaka?

21 Hakuna shaka yoyote kwamba Pasaka ilikuwa sherehe muhimu sana Mungu aliposhughulika na Waisraeli, na kila mmoja wetu anajifunza mambo muhimu kutokana nayo. Hivyo, Pasaka ilipaswa ‘kuwa ukumbusho’ kwa Wayahudi wala si kwa Wakristo, hata hivyo, tukiwa Wakristo tunapaswa kuijua na kuthamini mambo muhimu tunayojifunza kwa sababu ni sehemu ya ‘Andiko lote lililoongozwa na roho ya Mungu.’—2 Tim. 3:16.

^ fu. 5 Mwezi wa kwanza wa kalenda ya Kiyahudi uliitwa Abibu, lakini baadaye uliitwa Nisani Wayahudi waliporudi kutoka uhamishoni. Katika makala hii, tutauita mwezi huo Nisani.

^ fu. 11 Jua lilipotua, Nisani 15 ilianza, na hivyo mwaka huo, Sabato ya kawaida ya kila juma (Jumamosi) iliangukia siku ya kwanza ya Sherehe ya Keki Zisizo na Chachu, ambayo sikuzote ilikuwa sabato. Kwa kuwa Sabato zote mbili zilifanywa siku moja, ilikuwa Sabato “kuu.”—Soma Yohana 19:31, 42.