Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Fanyeni Hivi kwa Kunikumbuka Mimi’

‘Fanyeni Hivi kwa Kunikumbuka Mimi’

“Baada ya kutoa shukrani, akaumega [mkate] na kusema: ‘Huu unamaanisha mwili wangu ambao ni kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.’”1 KOR. 11:24.

1, 2. Huenda mitume walikuwa wakifikiria nini kuhusu safari ya kwenda Yerusalemu?

‘MWEZI mchanga unaonekana waziwazi kwa sababu hakuna mawingu. Bila shaka, walinzi wa Yerusalemu waliuona mwezi huo jana jioni. Baada tu ya Sanhedrini kujua hilo, inatangaza kuanza kwa mwezi mpya wa Nisani. Kisha, watu wanapata habari hizo kupitia wajumbe au mioto inayowashwa kotekote kama ishara. Ni wazi kwamba Yesu anajitayarisha kwenda Yerusalemu ili afike kabla ya Pasaka.’

2 Huenda mitume waliokuwa na Yesu huko Perea (ng’ambo ya Yordani) katika safari yake ya mwisho kuelekea Yerusalemu walikuwa wakifikiria safari hiyo. (Mt. 19:1; 20:17, 29; Marko 10:1, 32, 46) Mara tu baada ya siku ya kwanza ya mwezi wa Kiyahudi wa Nisani kujulikana, Pasaka ingefanywa siku 13 baadaye, yaani, Nisani 14, baada ya jua kutua.

3. Kwa nini Wakristo wanapendezwa na tarehe ya Pasaka?

3 Tarehe ya Mlo wa Jioni wa Bwana itakuwa Aprili 14, 2014, baada ya jua kutua. Tarehe hiyo inalingana na tarehe ambayo Pasaka ilifanywa. Itakuwa siku ya pekee kwa Wakristo wa kweli na watu wanaopendezwa. Kwa nini? Kwa sababu ya yale tunayosoma katika 1 Wakorintho 11:23-25: “Yesu katika ule usiku aliokuwa akienda kutolewa alichukua mkate na, baada ya kutoa shukrani, akaumega na kusema: ‘Huu unamaanisha mwili wangu ambao ni kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.’ Akafanya vivyo hivyo kuhusu kile kikombe.”

4. (a) Tunaweza kujiuliza maswali gani kuhusu Ukumbusho? (b) Tunajuaje tarehe ya Ukumbusho kila mwaka? (Tazama sanduku lenye kichwa  “Ukumbusho wa Mwaka wa 2014.”)

4 Bila shaka, utahudhuria tukio hilo ambalo Yesu aliwaagiza wafuasi wake wakumbuke kila mwaka. Kabla ya siku hiyo, jiulize hivi: ‘Nitajitayarishaje kwa ajili ya Ukumbusho? Ni mifano gani itakayotumika? Ni utaratibu gani utakaofuatwa katika tukio hilo? Tukio hilo  na mifano itakayotumiwa ina maana gani kwangu?’

MKATE NA DIVAI

5. Yesu aliwaambia mitume wafanye matayarisho gani kwa ajili ya Pasaka yake ya mwisho pamoja nao?

5 Yesu alipowaambia mitume wake watayarishe chumba kwa ajili ya mlo wa Pasaka, hakusema lolote kuhusu mapambo ya pekee; badala yake, inaelekea kwamba alitaka tu chumba kilicho safi, kinachofaa, na chenye nafasi ya kutosha. (Soma Marko 14:12-16.) Walipaswa pia kutayarisha vitu fulani, kutia ndani mkate usiotiwa chachu na divai nyekundu. Baada ya kumaliza mlo wa Pasaka, Yesu alizungumza kuhusu mkate usiotiwa chachu na divai nyekundu.

6. (a) Baada ya mlo wa Pasaka, Yesu alisema nini kuhusu mkate? (b) Ni mkate wa aina gani unaotumiwa katika Ukumbusho?

6 Mtume Mathayo aliyehudhuria mwadhimisho huo aliandika hivi baadaye: “Yesu alichukua mkate na, baada ya kutoa baraka, akaumega, akawapa wanafunzi, akasema: ‘Chukueni, mle.’” (Mt. 26:26) Sawa tu na mkate uliotumiwa katika Pasaka, “mkate” huo haukutiwa chachu. (Kut. 12:8; Kum. 16:3) Mkate huo ulitengenezwa kwa unga wa ngano na maji bila kutiwa chachu au kikolezo chochote, kama vile chumvi. Mkate huo haukuumuka au kuvimba kwa sababu haukuwa na chachu. Ungekuwa mkavu na rahisi kuvunjika. Kabla ya Ukumbusho, wazee wa kutaniko wanaweza kumwomba ndugu au dada atayarishe mkate huo kwa unga wa ngano na maji, na kuuoka kwenye sufuria iliyopakwa mafuta kidogo sana. (Ikiwa unga wa ngano haupatikani, mkate huo unaweza kutengenezwa kwa unga wa mchele, shayiri, mahindi, au nafaka kama hizo.) Au mnaweza kutumia mkate wa Wayahudi usiotiwa chachu (matzoth) ambao hauna kimea (malt), mayai, au vitunguu.

7. Yesu alizungumza kuhusu divai ya aina gani? Ni divai ya aina gani inayoweza kutumiwa leo katika Ukumbusho?

7 Mathayo aliendelea kusema hivi: “[Yesu] akachukua kikombe na, akiisha kushukuru, akawapa, akisema: ‘Kinyweeni, ninyi nyote.’” (Mt. 26:27, 28) Yesu alichukua kikombe chenye divai nyekundu. (Kwa kuwa mavuno ya zabibu yalikuwa tayari yamepita, ni wazi kwamba hayakuwa maji ya  matunda ya zabibu.) Ijapokuwa divai haikutumiwa katika mlo wa kwanza nchini Misri, Yesu hakupinga matumizi ya divai katika Pasaka. Hata alitumia kiasi fulani cha divai katika Mlo wa Jioni wa Bwana. Hivyo, Wakristo hutumia divai katika Ukumbusho. Kwa kuwa damu ya Yesu haikuhitaji kuongezwa thamani au nguvu, divai inayotumiwa haipaswi kuwa na brandi au vikolezo vyovyote. Divai nyekundu isiyo na vikolezo vyovyote inapaswa kutumiwa, iwe imetengenezwa nyumbani au kiwandani, kama vile Rocamar, Burgundy, au Cabernet.

MAANA YA MKATE NA DIVAI

8. Kwa nini Wakristo wanapendezwa kujua maana ya mkate na divai?

8 Mtume Paulo alisema wazi kwamba Wakristo pia wanapaswa kukumbuka Mlo wa Jioni wa Bwana si mitume tu. Aliwaandikia hivi waamini wenzake katika jiji la Korintho: “Nilipokea kutoka kwa Bwana kile nilichowapa ninyi pia, kwamba Bwana Yesu . . . alichukua mkate na, baada ya kutoa shukrani, akaumega na kusema: ‘Huu unamaanisha mwili wangu ambao ni kwa ajili yenu. Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.’” (1 Kor. 11:23, 24) Kwa hiyo, Wakristo leo hukumbuka tukio hilo la pekee kila mwaka na wanapendezwa kujua maana ya mkate na divai.

9. Baadhi ya watu wana maoni gani yasiyo sahihi kuhusu mkate aliotumia Yesu?

9 Baadhi ya wanadini wanaamini kwamba Yesu aliposema: ‘Huu ni mwili wangu,’ mkate ulibadilika kimuujiza na kuwa mwili wake halisi. Hata hivyo, jambo hilo si kweli. * Mwili huo, yaani, Yesu mwenyewe alikuwa mbele ya mitume wake waaminifu, na mkate usiotiwa chachu ambao wangekula ulikuwa pia mbele yao. Ni wazi kwamba Yesu alikuwa akiongea kwa kutumia mfano kama alivyofanya mara nyingi.—Yoh. 2:19-21; 4:13, 14; 10:7; 15:1.

10. Ni nini kinachofananishwa na mkate unaotumiwa katika Mlo wa Jioni wa Bwana?

 10 Mkate huo ambao mitume wangeula ulimaanisha mwili wa Yesu. Mwili gani? Zamani, watumishi wa Mungu walifikiri kwamba kwa kuwa Yesu alivunja mkate lakini hakuna mfupa wake uliovunjwa, basi mkate ulimaanisha “mwili wa Kristo,” yaani, kutaniko la watiwa-mafuta. (Efe. 4:12; Rom. 12:4, 5; 1 Kor. 10:16, 17; 12:27) Hata hivyo, baada ya kufanya utafiti na kuchunguza Maandiko, walielewa kwamba mkate unafananisha mwili wa kibinadamu wa Yesu aliotayarishiwa. Yesu “aliteseka katika mwili,” na hata alitundikwa mtini. Kwa hiyo, katika Mlo wa Jioni wa Bwana, mkate unafananisha mwili wa kibinadamu wa Yesu ‘aliochukulia dhambi zetu.’—1 Pet. 2:21-24; 4:1; Yoh. 19:33-36; Ebr. 10:5-7.

11, 12. (a) Yesu alisema nini kuhusu divai? (b) Divai inayotumiwa katika Mlo wa Jioni wa Bwana inafananisha nini?

11 Jambo hilo linatusaidia kuelewa alichosema Yesu kuhusu divai. Tunasoma hivi: “Akafanya vivyo hivyo kuhusu kile kikombe pia, baada ya yeye kula mlo wa jioni, akisema: ‘Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu.’” (1 Kor. 11:25) Tafsiri nyingi za Biblia zinatumia maneno haya yaliyo katika tafsiri ya neno kwa neno ya Robert Young: “Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu.” (Italiki ni zetu.) Je, kikombe halisi ambacho Yesu alikuwa nacho kilikuwa agano jipya? Hapana. Neno “kikombe,” lilimaanisha divai iliyokuwa ndani ya kikombe hicho. Yesu alisema divai ilimaanisha au kufananisha nini? Damu yake iliyomwagwa.

12 Tunasoma maneno haya ya Yesu katika Injili ya Marko: “Hii inamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi.” (Marko 14:24) Kwa kweli, damu ya Yesu ‘ingemwagwa kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi.’ (Mt. 26:28) Hivyo, kwa kufaa, divai nyekundu inafananisha damu halisi ya Yesu. Kwa damu hiyo, tunaachiliwa huru kupitia dhabihu, yaani, “msamaha wa makosa yetu.”—Soma Waefeso 1:7.

Mitume walikunywa divai iliyofananisha damu ya Yesu ya agano (Tazama fungu la 11 na 12)

KUKUMBUKA KIFO CHA KRISTO

13. Mwadhimisho wa kila mwaka wa Ukumbusho wa kifo cha Kristo hufanywaje?

13 Ikiwa ni mara yako ya kwanza kuhudhuria Ukumbusho pamoja na Mashahidi wa Yehova, utarajie nini? Bila shaka, mkutano huo utafanywa mahali safi panapofaa ili wahudhuriaji wote wafurahie. Huenda jumba likapambwa kwa njia ya kawaida tu, hivyo, hutakengeushwa na mapambo yanayopita kiasi au shamra-shamra za karamu. Mzee anayestahili atatumia Biblia kueleza kuhusu Ukumbusho kwa njia ya heshima na iliyo wazi. Atawasaidia wote kuthamini alichotufanyia Kristo. Alikufa akiwa fidia ili tuishi. (Soma Waroma 5:8-10.) Msemaji atafafanua matumaini mawili tofauti ya Wakristo yanayotajwa katika Biblia.

14. Ni matumaini gani yanayozungumziwa katika hotuba ya Ukumbusho?

14 Kikundi kidogo cha wafuasi wa Kristo kina tumaini la kutawala na Kristo mbinguni, na mitume waaminifu walikuwa na tumaini hilo. (Luka 12:32; 22:19, 20; Ufu. 14:1) Lakini Wakristo wengi washikamanifu wanaomtumikia Mungu katika siku zetu wanatumaini kuishi milele katika dunia paradiso. Kisha, mapenzi ya Mungu yatatendeka duniani kama ilivyo mbinguni, jambo ambalo Wakristo wamekuwa wakisali kwa muda mrefu kulihusu. (Mt. 6:10) Maandiko yanaeleza vizuri kuhusu hali nzuri sana watakazofurahia kwa umilele wote.—Isa. 11:6-9; 35:5, 6; 65:21-23.

15, 16. Mkate hutumiwa namna gani katika Mlo wa Jioni wa Bwana?

15 Mwishoni mwa hotuba, msemaji atataja kwamba wakati umefika wa kufanya kama Yesu alivyowaagiza mitume wake wafanye. Kama ilivyotajwa mwanzoni,  mifano miwili itatumiwa, yaani, mkate usiotiwa chachu na divai nyekundu. Huenda mifano hiyo ikawekwa mezani karibu na msemaji. Msemaji atazungumzia simulizi la Biblia linaloonyesha mambo ambayo Yesu alisema na kufanya alipoanzisha mwadhimisho huo. Kwa mfano, tunasoma hivi katika simulizi la Mathayo: “Yesu alichukua mkate na, baada ya kutoa baraka, akaumega, akawapa wanafunzi, akasema: ‘Chukueni, mle. Huu unamaanisha mwili wangu.’” (Mt. 26:26) Yesu aliumega mkate huo usiotiwa chachu na kuwapa mitume waliokuwa kando yake. Katika ukumbusho utakaofanywa Aprili 14, utaona vipande vichache vya mikate isiyotiwa chachu vikiwa kwenye sahani.

16 Sahani za kutosha zitatumiwa ili mikate hiyo ipitishwe kwa wahudhuriaji wote kwa muda mfupi iwezekanavyo. Jambo hilo halitafanywa kwa kufuata utaratibu fulani wa kipekee. Sala fupi itatolewa kisha sahani zitapitishwa kwa mpangilio na njia inayofaa. Watu wachache watakula mkate (au huenda yeyote asile) kama tu ilivyokuwa katika makutaniko mengi mwaka wa 2013.

17. Maagizo ya Yesu kuhusu divai yanafuatwa jinsi gani wakati wa Ukumbusho?

17 Baada ya hilo, msemaji atakazia fikira maneno haya ya Mathayo: “[Yesu] akachukua kikombe na, akiisha kushukuru, akawapa, akisema: ‘Kinyweeni, ninyi nyote; kwa maana hii inamaanisha “damu yangu ya agano,” ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi.’” (Mt. 26:27, 28) Kulingana na kielelezo hicho, sala nyingine itatolewa kisha ‘vikombe’ vyenye divai nyekundu vitapitishwa kwa kila mtu aliyehudhuria.

18. Kwa nini ni muhimu kuhudhuria Ukumbusho licha ya kwamba ni watu wachache au hakuna yeyote atakayekula mkate na kunywa divai?

18 Kwa heshima, wahudhuriaji wengi hawali mkate wala kunywa divai inapopitishwa kwa kuwa Yesu alisema kwamba wanaopaswa kufanya hivyo ni wale tu watakaotawala pamoja naye katika Ufalme wa mbinguni. (Soma Luka 22:28-30; 2 Tim. 4:18) Wahudhuriaji wengine wote hawali mkate na kunywa divai lakini wanaonyesha heshima kwa kuhudhuria Ukumbusho. Hata hivyo, wanapohudhuria Mlo wa Jioni wa Bwana wanaonyesha kwamba wanathamini sana dhabihu ya Yesu. Wakati wa Ukumbusho, wanatafakari kuhusu baraka watakazopata kwa sababu ya dhabihu ya fidia ya Yesu. Wana tumaini la kuwa miongoni mwa “umati mkubwa” utakaookoka “dhiki kuu” inayokuja. Waabudu hao watakuwa “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.”—Ufu. 7:9, 14-17.

19. Unaweza kufanya nini ili kujitayarisha na kufaidika na Mlo wa Jioni wa Bwana?

19 Mashahidi wa Yehova duniani pote hujitayarisha kwa ajili ya mkutano huo wa pekee. Majuma kadhaa mapema, tutawaalika watu wengi iwezekanavyo ili wahudhurie. Isitoshe, siku ya Ukumbusho inapokaribia, wengi wetu tutasoma masimulizi ya Biblia kuhusu mambo aliyofanya Yesu na mambo mengine yaliyotukia siku hiyo mwaka wa 33 W.K. Tunahitaji kufanya mipango ili tusikose kuhudhuria mwadhimisho huo. Ni vizuri kufika mapema kabla ya wimbo na sala ili tuwakaribishe wageni na kufaidika na programu nzima. Sisi sote, yaani, washiriki wa kutaniko na wageni, tutafaidika sana tukifungua Biblia na kusoma Maandiko yanayofafanuliwa na msemaji. Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba tunapohudhuria Ukumbusho tunaonyesha kwamba tunathamini kutoka moyoni dhabihu ya Yesu na tunatii amri hii aliyotoa: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.”—1 Kor. 11:24.

^ fu. 9 Msomi Mjerumani Heinrich Meyer anasema hivi: “Kwa kuwa . . . mwili wa Yesu haukuwa umevunjwa (bado alikuwa hai), na bado damu Yake haikuwa imemwagwa, hakuna mgeni yeyote [mitume] angefikiri . . . kwamba walikuwa wakila na kunywa kihalisi mwili na damu halisi ya Bwana, [kwa hiyo] Yesu Mwenyewe hakukusudia maneno Yake rahisi yaeleweke isivyofaa.”