Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Usitikiswe Upesi Kutoka Kwenye Kufikiri Kwako’!

‘Usitikiswe Upesi Kutoka Kwenye Kufikiri Kwako’!

“Akina ndugu, . . . tunawaomba ninyi msitikiswe upesi kutoka kwenye kufikiri kwenu.”2 THE. 2:1, 2.

1, 2. Kwa nini udanganyifu umeenea sana leo, nao huenezwaje? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

HILA, ulaghai, na udanganyifu ni mambo ya kawaida sana katika mfumo huu wa mambo. Hilo halipaswi kutushangaza kwa sababu Biblia inasema wazi kwamba Shetani Ibilisi ana uzoefu katika kudanganya, na ndiye mtawala wa mfumo huu. (1 Tim. 2:14; 1 Yoh. 5:19) Tunapokaribia mwisho wa mfumo huu mwovu, hasira ya Shetani inaongezeka kwa sababu ana ‘kipindi kifupi tu cha wakati.’ (Ufu. 12:12) Kwa hiyo, tunatarajia wale wanaomfuata Ibilisi wawe wenye hila zaidi na kujaribu kuwadanganya hasa waabudu wa kweli.

2 Nyakati nyingine, vyombo vya habari hueneza uwongo wa wazi na habari zenye kupotosha kuhusu watumishi wa Yehova na mafundisho yao. Magazeti, televisheni, na Intaneti hutumiwa kueneza mambo hayo yasiyo ya kweli. Na watu fulani wasiojua ukweli huamini uwongo huo na kuvurugika.

3. Ni nini kinachoweza kutusaidia kutodanganywa?

3 Neno la Mungu ambalo ni “lenye faida . . . kwa kunyoosha mambo” hutusaidia kujilinda dhidi ya mbinu hiyo inayotumiwa na adui yetu kutuvunja moyo. (2 Tim. 3:16) Mambo yaliyoandikwa na mtume Paulo yanapaswa kutufundisha kwamba baadhi ya Wakristo katika karne ya kwanza huko Thesalonike walidanganywa na kukubali mambo yasiyo ya kweli. Aliwahimiza ‘wasitikiswe upesi kutoka kwenye kufikiri kwao.’ (2 The. 2:1, 2) Tunajifunza nini kutokana na himizo hilo lenye upendo alilotoa Paulo, na tunawezaje kulitumia leo?

MAONYO YA WAKATI UNAOFAA

4. Wakristo wa Thesalonike walipewa onyo gani kuhusu kuja kwa “siku ya Yehova,” na sisi huonywa kwa njia gani?

4 Katika barua yake ya kwanza kwa kutaniko la  Thesalonike, Paulo aliwaonya kuhusu kuja kwa “siku ya Yehova.” Hakutaka ndugu zake wawe gizani na kutojitayarisha. Badala yake, wakiwa “wana wa nuru,” aliwahimiza ‘wakae macho na kutunza akili zao.’ (Soma 1 Wathesalonike 5:1-6.) Leo, tunangojea uharibifu wa Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo. Huo utakuwa mwanzo wa siku kuu ya Yehova. Leo, tunaelewa vizuri zaidi jinsi Yehova atakavyotimiza kusudi lake. Kupitia kutaniko, tunapokea pia kwa ukawaida na kwa wakati unaofaa vikumbusho vinavyotusaidia kutunza akili zetu. Kutii maonyo hayo yanayotolewa tena na tena kunaweza kuimarisha azimio letu la kumtolea Mungu ‘utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zetu za kufikiri.’—Rom. 12:1.

Paulo aliwaandikia Wakristo barua zenye maonyo ya wakati unaofaa (Tazama fungu la 4 na 5)

5, 6. (a) Paulo alizungumzia nini katika barua yake ya pili kwa Wathesalonike? (b) Hivi karibuni Mungu atamtumia Yesu kufanya nini? Tunapaswa kujiuliza maswali gani?

5 Paulo aliwaandikia Wakristo Wathesalonike barua ya pili muda mfupi baada ya kuwatumia barua ya kwanza. Katika barua hiyo ya pili, alionya kuhusu dhiki inayokuja wakati Bwana Yesu atakapotekeleza hukumu ya Mungu juu ya “wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema.” (2 The. 1:6-8) Sura ya pili ya barua hiyo inafunua kwamba baadhi ya watu katika kutaniko hilo ‘walisisimuka’ kuhusu siku ya Yehova na kuamini kwamba ilikuwa karibu sana. (Soma 2 Wathesalonike 2:1, 2.) Wakristo hao wa mapema hawakuelewa kikamili jinsi ambavyo Yehova angetimiza kusudi lake, ndiyo sababu Paulo alikiri hivi baadaye kuhusu unabii: “Tuna ujuzi wa sehemu tu nasi tunatoa unabii kwa sehemu tu; lakini wakati kile kilicho kamili kitakapofika, kile kilicho kwa sehemu tu kitaondolewa mbali.” (1 Kor. 13:9, 10) Hata hivyo, maonyo yaliyoongozwa na roho na kuandikwa na Paulo, mtume Petro, na ndugu wengine waaminifu watiwa-mafuta yangewasaidia kudumisha imani yao.

6 Paulo aliongozwa na roho takatifu kunyoosha mambo aliposema kwamba uasi-imani mkubwa na “yule mtu wa uasi-sheria” angetokea kabla ya siku ya Yehova. *  Kisha, kwa wakati wake, Bwana Yesu ‘atawafanya kuwa si kitu’ wote waliodanganywa. Mtume Paulo alisema kwamba watahukumiwa kwa sababu “hawakukubali kuipenda ile kweli.” (2 The. 2:3, 8-10) Tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Ninaipenda kweli kwa kadiri gani? Je, uelewaji wangu unapatana na uelewaji wa sasa unaofunuliwa katika gazeti hili na machapisho mengine yanayotegemea Biblia yanayotayarishwa kwa ajili ya kutaniko la ulimwenguni pote la watu wa Mungu?’

CHAGUA MARAFIKI WAKO KWA HEKIMA

7, 8. (a) Wakristo walikabili hatari gani katika karne ya kwanza? (b) Wakristo wa kweli leo wanakabili hatari gani kubwa?

7 Kwa kweli, Wakristo wangekabili hatari nyingine mbali na hatari ya waasi-imani na mafundisho yao. Paulo alimwandikia Timotheo kwamba “kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.” Mtume Paulo alisema kwamba “kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Tim. 6:10) Wakristo wangekabili pia hatari ya “matendo ya mwili.”—Gal. 5:19-21.

8 Hata hivyo, unaweza kuelewa kwa nini Paulo aliwaonya vikali Wathesalonike kuhusu hatari kubwa ya wale aliowaita “mitume wa uwongo.” Baadhi yao walisema “mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (2 Kor. 11:4, 13; Mdo. 20:30) Baadaye, Yesu alilipongeza kutaniko la Efeso kwa sababu ‘halikuvumilia watu wabaya.’ Waefeso hao ‘waliwajaribu’ watu ambao kwa kweli walikuwa mitume wa uwongo, yaani, wasema-uwongo. (Ufu. 2:2) Katika barua yake ya pili kwa Wathesalonike, Paulo alitoa himizo hili: “Sasa tunawapa ninyi maagizo, akina ndugu, katika jina la Bwana Yesu Kristo, mjiepushe na kila ndugu anayetembea bila utaratibu.” Kisha akataja waziwazi Wakristo ambao ‘hawakutaka kufanya kazi.’ (2 The. 3:6, 10) Ikiwa Wakristo hao walionwa kuwa wasio na utaratibu, ni wazi kwamba ilikuwa muhimu hata zaidi kuwaepuka watu walioanza kuwa waasi-imani! Naam, Wakristo walipaswa kuepuka kushirikiana na waasi-imani kwa sababu walikuwa hatari sana na ndivyo ilivyo leo pia.—Met. 13:20.

9. Kwa nini tunapaswa kumwepuka mtu yeyote anayeanza kukisia-kisia au kuchambua-chambua mambo?

9 Kwa kuwa tunakaribia mwanzo wa dhiki kuu na mwisho wa mfumo huu mwovu, maonyo yaliyoandikwa kwa mwongozo wa roho katika karne ya kwanza ni muhimu zaidi leo. Bila shaka hatutaki ‘kukosa kusudi’ la fadhili zisizostahiliwa za Yehova na kukosa uzima wa milele tulioahidiwa, iwe mbinguni au duniani. (2 Kor. 6:1) Tunapaswa kumwepuka kabisa mtu yeyote anayehudhuria mikutano ya kutaniko na kujaribu kutushawishi kukisia-kisia au kuchambua-chambua mambo.—2 The. 3:13-15.

“MWENDELEE KUYASHIKA MAPOKEO”

10. Wakristo wa Thesalonike walihimizwa washike sana mapokeo gani?

10 Paulo aliwahimiza ndugu zake wa Thesalonike ‘wasimame imara’ na kuyashika sana mapokeo waliyofundishwa. (Soma 2 Wathesalonike 2:15.) Ni “mapokeo” gani waliyofundishwa? Bila shaka, si mapokeo ya dini ya uwongo yanayoenezwa kana kwamba ni mafundisho ya Biblia yenye thamani. Badala yake, Paulo alikuwa akirejelea mafundisho ambayo yeye na wengine walipokea kutoka kwa Yesu na mambo ambayo mtume huyo aliandika  kwa mwongozo wa Mungu, mambo ambayo sasa ni sehemu ya Maandiko yaliyoongozwa na roho takatifu. Paulo aliwapongeza ndugu zake katika kutaniko la Korintho kwa sababu ‘katika mambo yote walimkumbuka na kuyashika sana mapokeo kama alivyowapa wao.’ (1 Kor. 11:2) Mafundisho hayo yalitokana na chanzo chenye kutegemeka na kwa kweli yaliaminika.

11. Huenda Wakristo fulani wakaathiriwa na uwongo kwa njia zipi?

11 Paulo alipowaandikia Waebrania, alitaja njia mbili ambazo Mkristo anaweza kupoteza imani yake na kushindwa kusimama imara. (Soma Waebrania 2:1; 3:12.) Alitaja ‘kupeperushwa’ na ‘kujiondoa.’ Mashua hupeperushwa au kusukumwa na upepo polepole kutoka ufuoni. Kisha, hatua kwa hatua inasonga mbali zaidi. Hata hivyo, mashua inaweza kwenda mbali na ufuo ikisukumwa na mtu kimakusudi. Mifano hiyo inaonyesha jinsi Wakristo fulani wanavyodanganywa na kuruhusu uhakika wao katika kweli udhoofike.

12. Ni mambo gani yanayoweza kuharibu hali yetu ya kiroho leo?

12 Huenda ndivyo Wathesalonike fulani walivyodanganywa. Namna gani leo? Kuna mambo mengi yanayopoteza muda. Fikiria saa nyingi wanazotumia watu kuwasiliana katika vituo vya kijamii, kusoma na kujibu ujumbe wa kielektroniki, na kufuatilia mapendezi ya kibinafsi au michezo. Mkristo anaweza kukengeushwa na hivyo kupunguza bidii yake akifuatilia lolote kati ya mambo hayo. Matokeo yatakuwa nini? Huenda akaacha kusali kutoka moyoni, kujifunza Neno la Mungu, kuhudhuria mikutano, na kuacha kuhubiri habari njema. Tutafanya nini ili tusitikiswe upesi kutoka kwenye kufikiri kwetu?

KUJILINDA ILI TUSITIKISWE

13. Kama ilivyotabiriwa, watu wengi wana mtazamo gani? Tutafanya nini ili imani yetu isidhoofishwe?

13 Bila shaka, tunahitaji kuendelea kuzingatia kwamba mwisho wa ulimwengu huu unakaribia na kutambua hatari ya kushirikiana na watu wasiokubali kwamba hizi ni “siku za mwisho.” Mtume Petro aliandika hivi kuhusu kipindi hiki: “Watakuja wadhihaki na dhihaka zao, wakiendelea kulingana na tamaa zao wenyewe na kusema: ‘Huku kuwapo kwake kulikoahidiwa kuko wapi? Kwani, tangu siku mababu zetu walipolala katika kifo, mambo yote yanaendelea sawasawa kama tangu mwanzo wa uumbaji.’” (2 Pet. 3:3, 4) Kusoma kila siku na kujifunza kwa ukawaida Neno la Mungu kutatusaidia kuzingatia kwamba tunaishi katika “siku za mwisho.” Uasi-imani uliotabiriwa ulianza miaka mingi iliyopita na bado unaendelea. “Mtu wa uasi-sheria” yupo, naye anaendelea kuwapinga watumishi wa Mungu. Kwa hiyo, tunahitaji kuendelea kukaa macho na kuzingatia kwamba siku ya Yehova inakaribia.—Sef. 1:7.

Kujitayarisha vizuri na kushiriki katika huduma kunaweza kutusaidia kuepuka kutikiswa upesi kutoka kwenye kufikiri kwetu (Tazama fungu la 14 na 15)

14. Kuhubiri kwa bidii hutulinda jinsi gani?

14 Mambo yaliyoonwa yanathibitisha kwamba kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa ukawaida kunatusaidia sana kukaa macho na kutotikiswa kutoka kwenye kufikiri kwetu. Kwa hiyo, Kristo Yesu, Kichwa cha kutaniko, alipowaamuru wafuasi wake wafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote na kuwafundisha kushika mambo yote aliyofundisha, alikuwa akiwapa mashauri ambayo yangewalinda. (Mt. 28:19, 20) Tunatii amri yake tunapohubiri kwa bidii. Je, unafikiri kwamba ndugu zako wa Thesalonike walihubiri na kufundisha kidesturi tu ili kutimiza wajibu? Kumbuka alichowaambia Paulo:  “Msiuzime moto wa roho. Msiyatendee kwa dharau maneno ya unabii.” (1 The. 5:19, 20) Tunajifunza na kuwafundisha wengine unabii wenye kusisimua kama nini!

15. Ni mambo gani muhimu tunayoweza kuzungumzia katika ibada ya familia?

15 Kwa kweli, tungependa kusaidia familia zetu kuwa na ustadi katika utumishi wa shambani. Ndugu na dada wengi wameona kwamba njia moja ya kufanya hivyo ni kutumia muda fulani wa ibada yao ya familia ili kufanya mazoezi ya kuhubiri. Mnaweza kuzungumzia jinsi washiriki wa familia yenu wanavyoweza kuwarudia watu waliopendezwa. Watazungumzia nini wanapowarudia watu hao? Ni habari gani zitakazowavutia zaidi? Ni wakati gani unaofaa zaidi wa kuwarudia? Familia nyingi hutumia pia muda fulani wa ibada yao ya familia kutayarisha mikutano ili wajue mambo yatakayozungumziwa mikutanoni. Je, mnaweza kujitahidi zaidi kutayarisha ili mshiriki katika mikutano? Kushiriki katika mikutano kutaimarisha imani yenu na kuwasaidia kutotikiswa kutoka kwenye kufikiri kwenu. (Zab. 35:18) Naam, ibada ya familia itawalinda ili msikisie-kisie mambo na kuwa na shaka.

16. Ni nini kinachowachochea Wakristo watiwa-mafuta kudumisha uwezo wao wa kufikiri?

16 Tukifikiria jinsi ambavyo Yehova amewabariki watu wake kwa miaka mingi kwa kuwasaidia kuelewa vizuri zaidi unabii wa Biblia, tutathamini thawabu nzuri sana ya wakati ujao. Watiwa-mafuta wana tumaini la kuungana na Kristo mbinguni. Tumaini hilo linawachochea sana kudumisha uwezo wao wa kufikiri. Bila shaka, tunaweza kuwaambia hivi kama Paulo alivyowaandikia Wathesalonike: “Sisi tuna wajibu wa kumshukuru Mungu sikuzote kwa ajili yenu, akina ndugu mnaopendwa na Yehova, kwa sababu Mungu aliwachagua ninyi . . . kwa kuwatakasa ninyi kwa roho na kwa imani yenu katika kweli.”—2 The. 2:13.

17. Andiko la 2 Wathesalonike 3:1-5 linakutia moyo jinsi gani?

17 Na wale wanaotazamia kupata uzima wa milele duniani wanapaswa pia kujitahidi ili wasitikiswe upesi kutoka kwenye kufikiri kwao. Ikiwa una tumaini la kuishi milele duniani, fikiria kwa uzito jinsi Paulo alivyowatia moyo kwa upendo watiwa-mafuta wenzake huko Thesalonike. (Soma 2 Wathesalonike 3:1-5.) Kila mmoja wetu anapaswa kuthamini sana maneno hayo ya upendo. Naam, barua za Paulo kwa Wathesalonike zina maonyo muhimu sana kuhusu mambo ya kukisiwa-kisiwa na mawazo yenye kutiliwa shaka. Tunathamini sana maonyo hayo tukiwa Wakristo kwa kuwa tunaishi katika siku za mwisho kabisa.

^ fu. 6 Kama tunavyosoma katika Matendo 20:29 na 30, Paulo alisema kwamba ‘watu wangesimama kutoka katika makutaniko ya Kikristo na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.’ Historia inathibitisha kwamba baada ya muda kulikuwa na tofauti kubwa kati ya makasisi na watu wa kawaida. Kufikia karne ya tatu W.K., makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walidhihirisha wazi kwamba walikuwa yule “mtu wa uasi-sheria.”—Tazama Mnara wa Mlinzi, Februari 1, 1990, ukurasa wa 10-14.