Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Aliwalinda Katika Vivuli vya Milima

Yehova Aliwalinda Katika Vivuli vya Milima

MWANAMKE mmoja anapotoka nje asubuhi, anapata kifurushi mlangoni pake. Anakichukua na kuangalia huku na huku, lakini haoni mtu yeyote. Bila shaka, mtu fulani alikileta usiku. Anakichukua, anakifungua kidogo na kurudi haraka nyumbani kwa sababu kina machapisho ya Biblia yaliyopigwa marufuku! Anakikumbatia kifurushi hicho na kumshukuru Yehova kimya-kimya kwa sababu ya chakula hicho cha kiroho chenye thamani.

Hilo lilikuwa jambo la kawaida nchini Ujerumani katika miaka ya 1930. Baada ya Wanazi kuanza kutawala katika mwaka wa 1933, kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipigwa marufuku katika maeneo mengi nchini humo. “Tulisadiki kwamba amri hiyo ya wanadamu haingeweza kuzuia kazi ya kuhubiri kumhusu Yehova na kutangaza jina lake,” akasema Richard Rudolph aliye na umri wa miaka zaidi ya 100. * “Tuliyahitaji sana machapisho ya Biblia kwa ajili ya funzo na huduma. Lakini yalikuwa yamepigwa marufuku, hivyo hayakupatikana kwa urahisi. Hatukujua jinsi ambavyo kazi yetu ingesonga mbele.” Baada ya muda, Richard aliombwa asaidie kusambaza machapisho hayo kwa njia isiyo ya kawaida. Kazi hiyo ingefanywa katika vivuli vya milima.—Amu. 9:36.

TULITUMIA VIJIA VYA WAFANYABIASHARA WA MAGENDO

Ukielekea juu kufuata mto Elbe (au, Labe) utafika kwenye Milima ya Giant (Krkonoše) iliyo kwenye mpaka wa Jamhuri ya Cheki na Poland. Ingawa milima hiyo ina urefu wa mita 1,600 hivi, imeitwa kisiwa cha aktiki kilicho katikati ya bara la Ulaya. Kwa miezi sita, sehemu zilizoinuka za milima hiyo hufunikwa na theluji yenye kina cha mita 3 hivi. Wale wasiojua kwamba hali ya hewa hubadilika-badilika wanaweza kunaswa na ukungu mzito unaofunika kwa ghafla vilele vya milima hiyo.

Kwa karne nyingi, safu hiyo ya milima imetumiwa kama mpaka kati ya mikoa, falme, na mataifa. Haikuwa rahisi kwa askari kulinda eneo hilo hatari,  hivyo zamani lilitumiwa na watu walioingiza bidhaa za magendo. Katika miaka ya 1930, Milima ya Giant ilipotumiwa kutenganisha Chekoslovakia na Ujerumani, Mashahidi wenye bidii walianza kutumia vijia vilivyotumiwa zamani na wafanyabiashara wa magendo. Kwa kusudi gani? Ili kusafirisha machapisho muhimu sana ya Biblia. Young Richard alikuwa mmoja wa Mashahidi hao.

Ndugu na dada waliovalia kama wapanda-milima walibeba machapisho na kuvuka Milima ya Giant hadi Ujerumani

SAFARI HATARI ZA “KUPANDA MILIMA”

Richard anakumbuka hivi: “Wakati wa miisho-juma, tulivalia kama wapanda-milima na kuelekea milimani tukiwa vijana saba au zaidi.” “Ilituchukua saa tatu hivi kuvuka milima hiyo kutoka Ujerumani ili kufika eneo la watalii la Špindlerův Mlýn,” kilomita 16.5 hivi nchini Cheki. Wakati huo, Wajerumani wengi waliishi katika eneo hilo. Mmoja wao alikuwa mkulima aliyekubali kuwasaidia akina ndugu. Akitumia gari la kukokotwa na farasi lililowasafirisha watalii, alibeba masanduku ya machapisho kutoka mji mdogo uliokuwa karibu, mahali ambapo yaliletwa kwa gari-moshi kutoka Prague. Alipeleka machapisho hayo katika shamba lake na kuyaficha katika ghala la nyasi kavu ili ndugu waje na kuyapeleka nchini Ujerumani.

Richard anaendelea kusema hivi: “Tulipofika katika shamba hilo, tulibeba machapisho hayo kwa mifuko mikubwa inayobebwa mgongoni. Kila mmoja wetu alibeba kilogramu 50 hivi.” Ili wasikamatwe, walianza safari yao jioni, wakatembea usiku na kufika nyumbani alfajiri. Ernst Wiesner, aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko nchini Ujerumani wakati huo alieleza baadhi ya mbinu walizotumia ili wasikamatwe: “Ndugu wawili walitangulia na walipokutana na mtu yeyote, walitoa ishara haraka kwa kutumia tochi zao. Ndugu waliokuwa wakiwafuata kwa umbali wa mita 100 hivi wakiwa wamebeba machapisho walipoona ishara hiyo walijificha vichakani mpaka ndugu hao waliporudi na kutoa ishara tofauti. Ishara hiyo ilibadilishwa kila juma.” Hata hivyo, walikabili hatari nyingine mbali na hatari ya kukamatwa na askari Wajerumani wenye mavazi ya bluu.

Richard anakumbuka hivi: “Jioni moja nilichelewa kutoka kazini, hivyo nikachelewa kuondoka pamoja na ndugu waliokuwa wakielekea upande wa Cheki. Kulikuwa na giza na ukungu, na nilitetemeka nilipokuwa  nikitembea katika mvua. Nilipotea katika vichaka vya misonobari kwa saa kadhaa. Wapanda-milima wengi wamekufa kwa sababu ya hali hizo. Nilikutana na ndugu hao walipokuwa wakirudi alfajiri.”

Kwa miaka mitatu hivi, kikundi hicho kidogo cha ndugu wenye ujasiri kilielekea milimani kila juma. Wakati wa majira ya baridi kali, walivaa viatu maalumu au kutumia vigari vinavyoteleza kwenye theluji ili kusafirisha machapisho hayo yenye thamani. Mara kwa mara, vikundi vya ndugu 20 hivi vilivuka mpaka wakati wa mchana, wakifuata vijia vilivyotumiwa na wapanda-milima. Ndugu hao waliandamana na dada kadhaa ili kuonyesha kwamba walikuwa wapanda-milima tu. Baadhi ya dada hao walitangulia na kurusha kofia zao hewani walipoona hatari yoyote.

Safari ya kuvuka Milima ya Giant ilikuwa hatari sana kwa sababu ya theluji

Ilikuwaje walipofikisha machapisho baada ya kusafiri usiku kucha? Mipango ilifanywa ili kuhakikisha kwamba yamegawanywa haraka. Jinsi gani? Machapisho yalipakiwa kama sabuni na kupelekwa kwenye kituo cha magari-moshi cha Hirschberg. Vifurushi hivyo vilisafirishwa sehemu mbalimbali za Ujerumani, kisha kwa busara, ndugu na dada walivipeleka kwa waamini wenzao kama ilivyotajwa mwanzoni. Mpango huo wa kugawanya machapisho kwa siri uliwahusisha watu wengi hivi kwamba matokeo yangekuwa mabaya sana ikiwa mmoja wao angekamatwa. Kwa kweli, siku moja wenye mamlaka waligundua mpango huo.

Katika mwaka wa 1936, depo ya machapisho iligunduliwa karibu na mji wa Berlin. Vifurushi vitatu vilivyotumwa kutoka Hirschberg na mtu asiyejulikana viligunduliwa katika depo hiyo. Baada ya kuchunguza mwandiko uliokuwa kwenye kifurushi hicho, polisi walimkamata mtu aliyehusika sana katika kusafirisha kisiri machapisho hayo nchini. Muda mfupi baadaye, Richard Rudolph pamoja na mshukiwa mwingine walikamatwa. Ndugu hao walikubali kuwa na hatia, hivyo wengine waliendelea kwa muda fulani na safari hizo zilizokuwa hatari hata zaidi.

TUNAYOJIFUNZA

Machapisho ya Biblia yaliyobebwa mgongoni na akina ndugu kupitia Milima ya Giant yalikuwa muhimu sana kwa Mashahidi nchini Ujerumani. Hata hivyo, hawakutumia njia hiyo tu kupitishia machapisho. Walitumia njia nyingine ili kuvuka mpaka hadi mwaka wa 1939 majeshi ya Ujerumani yalipoingia Chekoslovakia. Mashahidi katika nchi nyingine zinazopakana na Ujerumani, kama vile Ufaransa, Uholanzi, na Uswisi, walihatarisha uhai wao ili kusafirisha chakula cha kiroho kwa waamini wenzao waliokuwa wakiteswa.

Wengi wetu leo tunaweza kupata machapisho ya Biblia kwa wingi na kwa njia mbalimbali. Iwe unapata machapisho mapya katika Jumba la Ufalme au kupitia Tovuti ya jw.org, kwa nini usitafakari kuhusu kazi iliyofanywa ili upate machapisho hayo? Huenda haikuwa chini ya hali ngumu kama vile kuvuka milima iliyofunikwa na theluji wakati wa usiku, lakini bila shaka waamini wenzako wengi wamejitolea kufanya kazi ngumu bila ubinafsi ili upate machapisho hayo.

^ fu. 3 Alitumikia katika Kutaniko la Hirschberg huko Silesia. Mji wa Hirschberg unaoitwa sasa Jelenia Góra uko kusini-magharibi mwa Poland.