Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shangilieni kwa Sababu ya Ndoa ya Mwana-Kondoo!

Shangilieni kwa Sababu ya Ndoa ya Mwana-Kondoo!

 

“Acheni tushangilie na kuwa wenye shangwe mno . . . kwa sababu ndoa ya Mwana-Kondoo imefika.”UFU. 19:7.

1, 2. (a) Ni arusi ya nani itakayoleta shangwe mbinguni? (b) Ni maswali gani yanayotokea?

INACHUKUA muda kutayarisha arusi. Lakini tutazungumzia arusi ya pekee sana, arusi ya mfalme. Hebu wazia jambo hili! Imekuwa ikitayarishwa kwa miaka 2,000 hivi. Sasa wakati unakaribia haraka wa Bwana-Arusi kuungana na bibi arusi wake. Hivi karibuni, makao ya Mfalme huyo yatajaa nyimbo za shangwe, na umati ulio mbinguni utaimba hivi: “Msifuni Yah, kwa sababu Yehova Mungu wetu, Mweza-Yote, ameanza kutawala akiwa mfalme. Acheni tushangilie na kuwa wenye shangwe mno, na tumpe yeye utukufu, kwa sababu ndoa ya Mwana-Kondoo imefika na mke wake amejitayarisha.”Ufu. 19:6, 7.

2 Yesu Kristo ndiye “Mwana-Kondoo” atakayefunga ndoa itakayoleta shangwe mbinguni. (Yoh. 1:29) Amevaa mavazi gani ya arusi? Bibi-arusi ni nani? Amejitayarishaje kwa ajili ya ndoa? Arusi itafanywa wakati gani? Ndoa hiyo italeta shangwe mbinguni, lakini je, wale wanaotumaini kuishi milele duniani watashiriki katika shangwe hiyo? Tutazungumzia maswali hayo tunapoendelea kuchunguza Zaburi ya 45 tukiwa na hamu kubwa.

 ‘MAVAZI YAKE YANA MANUKATO’

3, 4. (a) Biblia inasema nini kuhusu mavazi ya Bwana-arusi? Ni nini kinachomletea shangwe zaidi? (b) Ni nani “binti za wafalme” na ‘waandamani wa malkia’ wanaoshangilia pamoja na Bwana-Arusi?

3 Soma Zaburi 45:8, 9Bwana-Arusi, Yesu Kristo, anavaa mavazi ya arusi ya kifalme yanayong’aa. Kwa kufaa, mavazi yake yana harufu yenye kuvutia kama ya “manukato bora zaidi,” kama vile manemane na kida. Manukato hayo yalikuwa kati ya vitu vilivyotumiwa kutengenezea mafuta matakatifu yaliyotumiwa katika Israeli.—Kut.—30:23-25.

4 Nyimbo zinazoimbwa mbinguni katika makao ya kifalme ya Bwana-Arusi zinamfanya awe na shangwe zaidi kadiri ndoa yake inavyokaribia. ‘Waandamani wa malkia,’ sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Mungu, inayotia ndani “binti za wafalme,” yaani, malaika watakatifu, wanashangilia pia. Inasisimua kama nini kusikia sauti zikitangaza hivi mbinguni: “Acheni tushangilie na kuwa wenye shangwe mno . . . kwa sababu ndoa ya Mwana-Kondoo imefika”!

BIBI-ARUSI YUKO TAYARI KWA AJILI YA ARUSI

5. Ni nani “mke wa Mwana-Kondoo”?

5 Soma Zaburi 45:10, 11. Tunajua Bwana-Arusi, lakini bibi-arusi ni nani? Bibi-arusi huyo ni washiriki wa kutaniko linaloongozwa na Yesu Kristo. (Soma Waefeso 5:23, 24.) Watashiriki katika Ufalme wa Kimasihi wa Kristo. (Luka 12:32) Wakristo hao 144,000 waliotiwa mafuta kwa roho ‘wanaendelea kumfuata Mwana-Kondoo popote anapoenda.’ (Ufu. 14:1-4) Wanakuwa “mke wa Mwana-Kondoo” na kukaa pamoja naye katika makao yake mbinguni.—Ufu. 21:9; Yoh. 14:2, 3.

6. Kwa nini watiwa-mafuta wanaitwa “binti ya mfalme,” na kwa nini wanaambiwa ‘wawasahau watu wao’?

6 Bibi-arusi huyo haitwi tu “binti” bali pia “binti ya mfalme.” (Zab. 45:13) Ni “mfalme” gani huyo? Wakristo watiwa-mafuta wanafanywa kuwa “watoto” wa Yehova. (Rom. 8:15-17) Kwa kuwa watiwa-mafuta watakuwa bibi-arusi mbinguni, wanaagizwa hivi: “Uwasahau watu wako na nyumba ya [kimwili ya] baba yako.” Wanapaswa kukaza akili zao “juu ya mambo yaliyo juu, si juu ya mambo yaliyo duniani.”—Kol. 3:1-4.

7. (a) Kristo amekuwa akimtayarishaje bibi-arusi wake? (b) Bibi-arusi anamwonaje Bwana-Arusi?

7 Kwa karne nyingi, Kristo amekuwa akimtayarisha bibi-arusi wake kwa ajili ya arusi itakayofanywa mbinguni wakati ujao. Mtume Paulo alieleza kwamba Kristo ‘alilipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake, ili alitakase, akilisafisha na kuliosha kwa maji kwa njia ya neno, ili kujipa mwenyewe kutaniko likiwa na fahari, likiwa bila doa au kunyanzi au lolote la mambo hayo, bali ili liwe takatifu na bila dosari.’ (Efe. 5:25-27) Paulo aliwaambia hivi Wakristo watiwa-mafuta katika jiji la kale la Korintho: “Nina wivu juu yenu kwa wivu wa kimungu, kwa maana mimi binafsi niliwachumbia ninyi mume mmoja ili niwatoe mkiwa bikira safi kiadili kwa Kristo.” (2 Kor. 11:2) Bwana-Arusi ambaye ni Mfalme Yesu Kristo, anathamini “urembo” wa kiroho wa bibi-arusi wake. Naye bibi-arusi anamwona kuwa “bwana” wake na ‘kumwinamia’ kwa sababu atakuwa mume wake.

BIBI-ARUSI ‘APELEKWA KWA MFALME’

8. Kwa nini inafaa kusema kwamba bibi-arusi ana “utukufu wote”?

8 Soma Zaburi 45:13, 14a. Biblia inasema kwamba bibi-arusi ana “utukufu wote” kwa ajili ya arusi yake ya kifalme. Katika andiko la Ufunuo 21:2, bibi-arusi analinganishwa na jiji, Yerusalemu Jipya, na ‘amepambwa kwa ajili ya mume wake.’ Jiji  hilo la kimbingu lina “utukufu wa Mungu” na linang’aa, “kama jiwe la thamani zaidi, kama jiwe la yaspi lenye kung’aa kwa uangavu kama fuwele.” (Ufu. 21:10, 11) Kitabu cha Ufunuo kinafafanua vizuri sana mng’ao wa Yerusalemu Jipya. (Ufu. 21:18-21) Si ajabu kwamba mtunga-zaburi anataja kwamba bibi-arusi ana “utukufu wote”! Bila shaka, ndoa hiyo ya kifalme itafanyiwa mbinguni.

9. Bibi-arusi atapelekwa kwa “mfalme” gani, na amevaa mavazi ya aina gani?

9 Bibi-arusi analetwa kwa Bwana-Arusi, yaani, Mfalme wa Kimasihi. Amekuwa akimtayarisha bibi-arusi kwa ‘kumsafisha na kumwosha kwa maji kwa njia ya neno.’ Bibi-arusi ni ‘mtakatifu na hana dosari.’ (Efe. 5:26, 27) Ni lazima bibi-arusi avae pia mavazi yanayofaa pindi hiyo. Na hivyo ndivyo alivyovaa! “Mavazi yake yamepambwa kwa dhahabu,” na “atapelekwa kwa mfalme akiwa na mavazi yaliyofumwa.” Kwa ajili ya ndoa ya Mwana-Kondoo, “amepewa ruhusa ya kupambwa kitani bora, changavu, safi, kwa maana hicho kitani bora humaanisha matendo ya uadilifu ya watakatifu.”—Ufu. 19:8.

‘NDOA IMEFIKA’

10. Ndoa ya Mwana-Kondoo itafanywa wakati gani?

10 Soma Ufunuo 19:7. Ndoa ya Mwana-Kondoo itafanywa wakati gani? Ingawa “mke wake amejitayarisha” kwa ajili ya ndoa, maneno yafuatayo hayahusu arusi yenyewe. Badala yake, yanaonyesha waziwazi sehemu ya mwisho ya dhiki kuu. (Ufu. 19:11-21) Je, hilo linamaanisha kwamba ndoa hiyo itafanywa kabla ya Bwana-Arusi Mfalme kukamilisha ushindi wake? Hapana. Maono ya kitabu cha Ufunuo hayafuatani kulingana na wakati. Katika Zaburi ya 45, arusi ya mfalme inafanywa baada ya Mfalme Yesu Kristo kujifunga upanga wake na ‘kuendelea mpaka anapofanikiwa’ juu ya adui zake.—Zab. 45:3, 4.

11. Kristo atakamilisha ushindi wake kwa mfuatano gani wa matukio?

11 Kwa hiyo, tunaweza kusema kwamba matukio hayo yatafuatana hivi: Kwanza, “kahaba mkubwa” atahukumiwa, yaani, Babiloni Mkubwa, ile milki ya ulimwenguni ya dini ya uwongo. (Ufu. 17:1, 5, 16, 17; 19:1, 2) Kisha, Kristo atatekeleza hukumu za Mungu juu ya sehemu inayobaki ya mfumo mwovu wa Shetani duniani kwa kuiharibu kwenye Har–Magedoni, “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.” (Ufu. 16:14-16; 19:19-21) Mwishowe, Mfalme huyo Shujaa atakamilisha ushindi wake kwa kumtupa Shetani na roho wake waovu ndani ya abiso, ambamo watakuwa katika hali ya kutotenda kama ya wafu.—Ufu. 20:1-3.

12, 13. (a) Ndoa ya Mwana-Kondoo itafanywa wakati gani? (b) Ni nani watakaoshangilia mbinguni kwa sababu ya ndoa ya Mwana-Kondoo?

12 Wakristo watiwa-mafuta wanapokufa wakati wa kuwapo kwa Kristo, wanafufuliwa na kwenda kuishi mbinguni. Muda fulani baada ya uharibifu wa Babiloni Mkubwa, Yesu atawakusanya washiriki wote wanaobaki wa jamii ya bibi-arusi ili wawe pamoja naye. (1 The. 4:16, 17) Kwa hiyo, kabla ya vita vya Har–Magedoni, washiriki wote wa “bibi-arusi” watakuwa mbinguni. Baada ya vita hivyo, ndoa ya Mwana-Kondoo inaweza kufanywa. Utakuwa wakati wa shangwe kama nini! Andiko la Ufunuo 19:9 linasema hivi: “Wenye furaha ni wale walioalikwa kwenye mlo wa jioni wa ndoa ya Mwana-Kondoo.” Washiriki 144,000 wa jamii ya bibi-arusi watakuwa wenye furaha kwelikweli. Naye Bwana-Arusi Mfalme atashangilia kuwa na wafalme wenzake ‘wakila na kunywa kwa njia ya mfano mezani pake katika ufalme wake.’ (Luka 22:18, 28-30) Hata hivyo, si Bwana-Arusi na bibi-arusi peke yao  watakaoshangilia kwa sababu ya ndoa ya Mwana-Kondoo.

13 Kama tulivyoona mwanzoni, umati ulio mbinguni unaimba hivi kwa umoja: “Acheni tushangilie na kuwa wenye shangwe mno, na tumpe yeye [Yehova] utukufu, kwa sababu ndoa ya Mwana-Kondoo imefika na mke wake amejitayarisha.” (Ufu. 19:6, 7) Namna gani kuhusu watumishi wa Yehova duniani? Je, watashangilia pia?

‘WATAPELEKWA KWA SHANGWE’

14. Ni nani ‘mabikira walio katika msafara’ wa bibi-arusi wanaotajwa katika Zaburi ya 45?

14 Soma Zaburi 45:12, 14b, 15. Nabii Zekaria alitabiri kwamba siku za mwisho, watu wa mataifa watashirikiana kwa shangwe na washiriki waliobaki wa taifa la kiroho la Israeli. Aliandika hivi: ‘Katika siku hizo watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa watashika, ndiyo, wataushika upindo wa nguo ya mtu aliye Myahudi, wakisema: “Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia ya kuwa Mungu yupo pamoja nanyi.”’ (Zek. 8:23) Katika Zaburi 45:12, ‘watu hao kumi’ wa mfano wanaitwa “binti Tiro” na “walio matajiri kati ya watu.” Wanawapelekea zawadi watiwa-mafuta ambao wangali duniani, ‘wakiutuliza uso wao,’ yaani, wanatafuta kibali chao na kuomba msaada wa kiroho. Kuanzia mwaka wa 1935, mamilioni ya watu wamewaruhusu watiwa-mafuta hao ‘wawalete kwenye uadilifu.’ (Dan. 12:3) Watu hao washikamanifu wanaoandamana na Wakristo watiwa-mafuta wamesafisha maisha yao na kuwa mabikira wa kiroho. ‘Mabikira walio katika msafara’ wa bibi-arusi wamejiweka wakfu kwa Yehova na wamethibitika kuwa raia waaminifu wa Bwana-Arusi Mfalme.

15. ‘Mabikira walio katika msafara’ wamefanyaje kazi pamoja na washiriki wa jamii ya bibi-arusi ambao bado wako duniani?

 15 Washiriki wanaobaki wa jamii ya bibi-arusi wanawashukuru hasa ‘mabikira walio katika msafara’ huo kwa sababu wanawasaidia kwa bidii kuhubiri “hii habari njema ya ufalme” katika dunia yote inayokaliwa. (Mt. 24:14) “Roho na bibi-arusi huendelea kusema: ‘Njoo!’” nao wale wanaosikia wanasema: “Njoo!” (Ufu. 22:17) Naam, “kondoo wengine” waliwasikia washiriki wa jamii iliyotiwa mafuta ya bibi-arusi wakisema “Njoo!” nao wamejiunga na bibi-arusi katika kuwaambia wakaaji wa dunia, “Njoo!”—Yoh. 10:16.

16. Yehova amewapa kondoo wengine pendeleo gani?

16 Watiwa-mafuta ambao wangali duniani wanawapenda waandamani wao na wanafurahi kujua kwamba Yehova, Baba ya Bwana-Arusi, amewapa kondoo wengine walio duniani pendeleo la kushangilia pamoja nao kwa sababu ya ndoa ya kimbingu ya Mwana-Kondoo. Ilitabiriwa kwamba ‘mabikira hao walio katika msafara’ wa bibi-arusi “watapelekwa kwa furaha na shangwe.” Naam, kondoo wengine, wanaotumaini kuishi milele duniani, watajiunga na ulimwengu mzima katika kushangilia wakati ndoa ya Mwana-Kondoo itakapofanywa mbinguni. Kwa kufaa, kitabu cha Ufunuo kinasema kwamba washiriki wa “umati mkubwa” “wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo.” Wanamtolea Yehova utumishi mtakatifu katika ua wa kidunia wa hekalu lake la kiroho.—Ufu. 7:9, 15.

Ndoa ya Mwana-Kondoo huwaletea shangwe ‘mabikira walio katika msafara’ wa bibi-arusi

“MAHALI PA MABABU ZAKO PATACHUKULIWA NA WANA WAKO”

17, 18. Ndoa ya Mwana-Kondoo inazaaje matunda? Kristo atakuwa baba ya nani wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja?

17 Soma Zaburi 45:16. ‘Mabikira walio katika msafara’ wa bibi-arusi wa kimbingu wa Kristo, watashangilia zaidi wanapoona ndoa hiyo ikizaa matunda katika ulimwengu mpya. Bwana-Arusi Mfalme ataielekezea dunia fikira na kuwafufua “mababu” zake duniani, ambao watakuwa “wana” wake duniani. (Yoh. 5:25-29; Ebr. 11:35) Atachagua kutoka miongoni mwao “wakuu katika dunia yote.” Bila shaka, Kristo atawaweka rasmi baadhi ya wazee waaminifu leo kuongoza katika ulimwengu mpya.—Isa. 32:1.

18 Wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja, Kristo atakuwa baba ya wengine pia. Kwa kweli, wakaaji wote wa dunia watapata uzima wa milele kwa sababu ya kuonyesha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. (Yoh. 3:16) Hivyo, anakuwa ‘Baba yao wa Milele.’—Isa. 9:6, 7.

WACHOCHEWA ‘KULITANGAZA JINA LAKE’

19, 20. Matukio yenye kusisimua yanayotajwa katika Zaburi ya 45 yanawahusuje Wakristo wote wa kweli leo?

19 Soma Zaburi 45:1, 17. Kwa kweli, matukio yaliyoandikwa katika Zaburi ya 45 yanawahusu Wakristo wote. Watiwa-mafuta ambao wangali duniani wanasisimuka kwa sababu wanatumaini kuungana hivi karibuni mbinguni na ndugu zao na pia Bwana-arusi wao. Kondoo wengine wanachochewa kujinyenyekeza zaidi kwa Mfalme wao mtukufu na wanathamini pendeleo la kushirikiana na washiriki wa bibi-arusi wake ambao wangali duniani. Baada ya ndoa yao, Kristo na Wafalme wenzake watawaletea wakaaji wa dunia baraka nyingi sana.—Ufu. 7:17; 21:1-4.

20 Tunapotazamia “jambo jema” litimizwe kumhusu Mfalme wa Kimasihi, je, hatuchochewi ‘kulitangaza jina lake’? Na tuwe miongoni mwa wale ‘watakaomsifu Mfalme milele na milele.’