Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Rafiki Yetu Mkubwa Zaidi

Yehova Ni Rafiki Yetu Mkubwa Zaidi

“[Abrahamu] akaitwa ‘rafiki ya Yehova.’” YAK. 2:23.

1. Kwa kuwa tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, tuna uwezo gani?

KUNA msemo kwamba “mwana humwiga baba.” Kwa kweli, watoto wengi hufanana sana na wazazi wao kwa sababu mtoto hurithi chembe za urithi kutoka kwa mama na baba. Yehova, Baba yetu wa mbinguni ndiye Mpaji wa uhai. (Zab. 36:9) Na tukiwa watoto wake wa kibinadamu, tunafanana naye kwa kiasi fulani. Kwa kuwa tumeumbwa kwa mfano wake, tuna uwezo wa kufikiria na kufanya maamuzi, kusitawisha na kudumisha urafiki.—Mwa. 1:26.

2. Urafiki wetu na Yehova unategemea nini?

2 Yehova anaweza kuwa Rafiki yetu mkubwa zaidi. Urafiki huo unategemea upendo ambao Mungu anatuonyesha na imani yetu kumwelekea yeye na Mwana wake. Yesu alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Kuna mifano mingi ya watu waliokuwa marafiki wa karibu wa Yehova. Acheni tuchunguze mifano miwili.

“ABRAHAMU RAFIKI YANGU”

3, 4. Tofauti na wazao wake, Abrahamu aliuonaje urafiki wake pamoja na Yehova?

3 Yehova alisema hivi kumhusu Abrahamu, mzee wa ukoo na  babu ya Waisraeli: “Abrahamu rafiki yangu.” (Isa. 41:8) Andiko la 2 Mambo ya Nyakati 20:7 linamtaja Abrahamu kuwa rafiki ya Mungu. Urafiki huo wa kudumu kati ya mwanamume huyo mwaminifu na Muumba wake ulitegemea nini? Ulitegemea imani ya Abrahamu.—Mwa.15:6; soma Yakobo 2:21-23.

4 Mwanzoni, Yehova alikuwa Baba na Rafiki ya wazao wa Abrahamu ambao baadaye walikuwa taifa la kale la Israeli. Hata hivyo, inasikitisha kwamba walipoteza urafiki wao pamoja na Mungu. Kwa nini? Kwa sababu hawakuendelea kuamini ahadi za Yehova.

5, 6. (a) Yehova amekuwaje Rafiki yako? (b) Ni maswali gani tunayopaswa kufikiria?

5 Kadiri unavyojifunza mambo mengi zaidi kumhusu Yehova, ndivyo imani na upendo wako kumwelekea utakavyoongezeka. Fikiria mwanzoni ulipojifunza kwamba Mungu ni halisi, na anaweza kuwa rafiki yako wa karibu. Ulijifunza pia kwamba sote tumezaliwa katika dhambi kwa sababu ya kutotii kwa Adamu. Ulijifunza kwamba wanadamu wote wametengwa na Mungu. (Kol. 1:21) Kisha ukajifunza kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anapendezwa nasi na hayuko mbali. Tulipojifunza kwamba Mungu aliandaa dhabihu ya fidia ya Yesu, tulionyesha imani katika uandalizi huo na kuanza kusitawisha urafiki pamoja na Mungu.

6 Tunapokumbuka wakati huo, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, urafiki wangu pamoja na Mungu unazidi kukua? Je, ninamtumaini na kumpenda zaidi Rafiki yangu mpendwa, Yehova, kadiri siku zinavyopita?’ Gideoni pia alikuwa rafiki wa karibu wa Yehova. Acheni sasa tuchunguze mfano wake mzuri na kumwiga.

“YEHOVA NI AMANI”

7-9. (a) Gideoni aliona jambo gani la kushangaza, na matokeo yalikuwa nini? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 21.) (b) Tunawezaje kuwa marafiki wa Yehova?

7 Mwamuzi Gideoni alimtumikia Yehova taifa la Israeli lilipokuwa na msukosuko baada ya kuingia katika Nchi ya Ahadi. Kitabu cha Waamuzi sura ya 6 kinasema kwamba malaika wa Yehova alimtembelea Gideoni huko Ofra. Wakati huo, taifa jirani la Midiani lilitisha Israeli. Kwa hiyo, Gideoni alipura ngano katika shinikizo la divai, mahali ambapo angeweza kuificha kwa haraka nafaka hiyo yenye thamani, badala ya kufanya hivyo kwenye uwanja wa kupuria. Gideoni alishangaa malaika alipomtokea na kumwita ‘shujaa mwenye nguvu.’ Ndipo Gideoni akamuuliza ikiwa Yehova aliyewakomboa Waisraeli kutoka Misri, angewasaidia tena pindi hiyo. Akiongea kwa niaba ya Muumba, malaika huyo alimhakikishia Gideoni kwamba Yehova alikuwa pamoja naye.

8 Gideoni akauliza ikiwa kwa kweli angeweza ‘kuwaokoa Israeli kutoka katika mkono wa Midiani.’ Alijibiwa hivi moja kwa moja: “Kwa sababu nitakuwa pamoja nawe,” akasema Yehova, “utapiga Midiani kama mtu mmoja.” (Amu. 6:11-16) Akiwa na shaka, Gideoni aliomba ishara. Mazungumzo hayo yanaonyesha wazi kwamba Gideoni alimwona Yehova kuwa halisi.

9 Jambo lililotokea baada ya hapo liliimarisha imani ya Gideoni na kumfanya amkaribie Mungu zaidi. Gideoni alitayarisha chakula na kumpa malaika huyo. Gideoni alipoona chakula kikiteketea kimuujiza baada ya malaika huyo kunyoosha fimbo yake na kukigusa, alitambua kwamba kwa kweli malaika huyo alimwakilisha Yehova. Gideoni aliogopa na kusema hivi: “Ole wangu, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, kwa sababu nimeona malaika wa Yehova uso kwa uso!” (Amu. 6:17-22) Lakini je, tukio hilo lilimtenganisha Gideoni na Mungu wake? La hasha! Lilimfanya amkaribie zaidi Yehova. Gideoni alimjua Yehova vizuri sana hivi kwamba akawa na amani pamoja na Mungu. Jina la madhabahu ambayo Gideoni alijenga  mahali hapo, “Yehova-shalomu,” linathibitisha jambo hilo. Jina hilo linamaanisha “Yehova Ni Amani.” (Soma Waamuzi 6:23, 24.) Tunapotafakari kuhusu mambo ambayo Yehova anatufanyia kila siku, tunatambua kwamba yeye ni Rafiki wa kweli. Kusali kwa Mungu kwa ukawaida hutusaidia kuwa na amani zaidi na kuimarisha urafiki wetu pamoja naye.

NI NANI ATAKAYEKUWA ‘MGENI KATIKA HEMA LA YEHOVA’?

10. Kulingana na Zaburi 15:3, 5, Yehova anataka tufanye nini ili tuwe marafiki wake?

10 Hata hivyo, ili Yehova awe Rafiki yetu, ni lazima tutimize masharti fulani. Kama ilivyoandikwa katika Zaburi ya 15, Daudi alitaja katika wimbo mambo tunayopaswa kufanya ili tuwe ‘wageni katika hema la Yehova,’ yaani, marafiki wa Mungu. (Zab. 15:1) Acheni tuchunguze matakwa mawili, yaani, kuepuka uchongezi na kutenda kwa unyoofu katika shughuli zetu zote. Kuhusiana na mambo hayo, Daudi alisema hivi kuhusu mgeni katika hema la Yehova: ‘Hachongei kwa ulimi wake, wala hachukui rushwa dhidi ya mtu asiye na hatia.’—Zab. 15:3, 5.

11. Kwa nini tunapaswa kuepuka kumchongea mtu yeyote?

11 Katika zaburi nyingine, Daudi alionya hivi: “Linda ulimi wako na yaliyo mabaya.” (Zab. 34:13) Kutotii shauri hilo lililoongozwa na roho takatifu kunaweza kututenga mbali na Baba yetu wa mbinguni ambaye ni mwadilifu. Kwa kweli, uchongezi ni tabia ya Shetani, adui mkubwa wa Yehova. Jina “Ibilisi” linatokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “mchongezi.” Kuwa waangalifu kuhusu maneno tunayosema kuhusu wengine hutusaidia kuendelea kuwa karibu na Yehova. Tunapaswa hasa kuwa waangalifu kuhusu mtazamo wetu kuelekea wanaume waliowekwa rasmi kutanikoni.—Soma Waebrania 13:17; Yuda 8.

12, 13. (a) Kwa nini tunapaswa kuwa wanyoofu katika mambo yote? (b) Unyoofu wetu unaweza kuwa na matokeo gani kwa wengine?

12 Unyoofu ni sifa nyingine inayowatambulisha watumishi wa Yehova, na ni kinyume kabisa na kuwatendea wengine isivyo haki. Mtume Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kusali kwa ajili yetu, kwa maana sisi tuna uhakika kwamba tuna dhamiri nyoofu, kwa kuwa tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Ebr. 13:18) Kwa sababu tumeazimia ‘kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote,’ tunaepuka kuwatendea isivyo haki ndugu zetu Wakristo ili kujifaidi wenyewe. Kwa mfano, ikiwa tumewaajiri, tunahakikisha kwamba tunawatendea kwa haki na kuwalipa kama tulivyokubaliana. Tukiwa Wakristo, tunawatendea kwa unyoofu wafanyakazi wetu na watu wengine. Na ikiwa tumeajiriwa na Mkristo mwenzetu, hatupaswi kutumia vibaya nafasi hiyo na kudai atutendee kwa njia ya pekee.

13 Mara nyingi, tunasikia kuhusu watu wanaowasifu Mashahidi wa Yehova. Kwa mfano, mkurugenzi wa kampuni kubwa ya ujenzi alitambua kwamba Mashahidi wa Yehova hutimiza ahadi zao. Alisema hivi: “Sikuzote ninyi hutimiza ahadi zenu.” (Zab. 15:4) Mwenendo kama huo hutusaidia kudumisha urafiki wetu pamoja na Yehova. Isitoshe, mwenendo huo unamletea sifa Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo.

WASAIDIE WENGINE WAWE MARAFIKI WA YEHOVA

Tunawasaidia wengine kuwa marafiki wa Yehova (Tazama fungu la 14, 15)

14, 15. Tunawezaje kuwasaidia wale tunaokutana nao katika huduma yetu kuwa marafiki wa Yehova?

14 Ingawa huenda watu tunaokutana nao katika huduma yetu wanaamini kwamba kuna Mungu, wengi wao hawamwoni kuwa Rafiki yao mkubwa. Tunawezaje kuwasaidia? Fikiria maagizo ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake 70 alipowatuma wawili-wawili kwenda kuhubiri: “Popote pale  mtakapoingia katika nyumba kwanza semeni, ‘Nyumba hii na iwe na amani.’ Na ikiwa rafiki wa amani yumo, amani yenu itakaa juu yake. Lakini ikiwa hayumo, itawarudia ninyi.” (Luka 10:5, 6) Tunaweza kufanya watu wavutiwe na kweli tukiwa na mtazamo wa kirafiki. Tukifanya hivyo, hata watu wanaotupinga wanaweza kuacha kutuchukia na huenda wakatusikiliza pindi nyingine.

15 Tunapokutana na watu wanaofuata kwa dhati dini ya uwongo au desturi zisizopatana na Maandiko, tunaonyesha urafiki na kudumisha amani. Tunawakaribisha kwa uchangamfu kwenye mikutano yetu wale wanaotaka kujifunza mengi zaidi kumhusu Mungu tunayemwabudu kwa sababu wametamaushwa na hali za ulimwengu. Tunaweza kutumia mifano mingi mizuri katika makala zenye kichwa “Biblia Inabadili Maisha.”

KUFANYA KAZI NA RAFIKI YETU MKUBWA ZAIDI

16. Tunawezaje kuwa rafiki na “wafanyakazi wenzi” wa Yehova?

16 Mara nyingi, watu wanaofanya kazi pamoja husitawisha urafiki wa karibu. Watu wote waliojiweka wakfu kwa Yehova wana pendeleo la kuwa rafiki zake na ‘wafanyakazi wenzake.’ (Soma 1 Wakorintho 3:9.) Kwa kweli, tunapofanya kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, tunaelewa zaidi sifa zenye kustaajabisha za Baba yetu wa mbinguni. Tunaona jinsi roho yake takatifu inavyotusaidia kuhubiri habari njema.

17. Chakula cha kiroho kinachotolewa katika makusanyiko yetu kinaonyeshaje kwamba Yehova ni Rafiki yetu?

17 Kadiri tunavyoshiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi, ndivyo tunavyomkaribia zaidi Yehova. Kwa mfano, tunaona jinsi Yehova anavyotulinda dhidi ya wapinzani. Fikiria mambo yaliyotokea miaka michache iliyopita. Je, si wazi kwamba Yehova anatuongoza? Tunafurahia sana chakula kingi kizuri cha kiroho tunachoendelea kupata. Makusanyiko yetu yanaonyesha kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anajua vizuri matatizo na mahitaji yetu. Familia fulani iliyohudhuria kusanyiko la wilaya ilionyesha uthamini kwa kuandika hivi: “Kusanyiko hilo liligusa sana mioyo yetu. Tuliona kwamba Yehova anampenda sana kila mmoja wetu na anataka tufanikiwe.” Baada ya kuhudhuria kusanyiko la wilaya la pekee nchini Ireland, wenzi fulani wa ndoa kutoka Ujerumani walithamini sana jinsi walivyokaribishwa kwa uchangamfu na kutunzwa. Walisema hivi: “Tunamshukuru sana Yehova na Mfalme wake Yesu Kristo. Wameturuhusu kujiunga na taifa hili lenye umoja. Hatusemi tu kwamba tuna umoja, tunaufurahia kila siku. Mambo tuliyojionea katika kusanyiko la wilaya la pekee  huko Dublin yatatukumbusha daima pendeleo letu lenye thamani la kumtumikia Mungu wetu mkuu pamoja nanyi nyote.”

MARAFIKI HUWASILIANA

18. Tunaweza kujiuliza maswali gani kuhusu jinsi tunavyowasiliana na Yehova?

18 Mawasiliano mazuri huimarisha urafiki. Kwa sababu ya maendeleo ya kiteknolojia na mawasiliano, watu wengi huwasiliana kupitia vituo vya mawasiliano na simu. Lakini, je, unawasiliana mara nyingi kadiri gani na Yehova, Rafiki yako mkubwa zaidi? Yeye ni “Msikiaji wa sala.” (Zab. 65:2) Lakini tunazungumza naye mara nyingi kadiri gani?

19. Tuna msaada gani ikiwa ni vigumu kwetu kumweleza Baba yetu wa mbinguni jinsi tunavyohisi moyoni mwetu?

19 Huenda isiwe rahisi kwa watumishi fulani wa Mungu kumweleza hisia zilizo moyoni mwao. Hata hivyo, Yehova anataka tufanye hivyo tunaposali. (Zab. 119:145; Omb. 3:41) Tunaweza kupata msaada ikiwa ni vigumu kueleza yaliyo moyoni mwetu. Paulo aliwaandikia hivi Wakristo waliokuwa Roma: “Lile tatizo kuhusu tunalohitaji kusali hatujui, lakini roho yenyewe hutuombea pamoja na kuugua kusikotamkwa. Lakini yeye ambaye huichunguza mioyo anajua ni nini maana ya roho, kwa sababu inaomba kupatana na Mungu kwa ajili ya watakatifu.” (Rom. 8:26, 27) Kutafakari maneno yaliyo katika vitabu vya Biblia kama vile Ayubu, Zaburi, na Methali kutatusaidia kumweleza Yehova hisia zetu za moyoni.

20, 21. Maneno ya Paulo katika Wafilipi 4:6, 7 yanatufariji jinsi gani?

20 Tunapokabili hali ngumu, acheni tutii shauri hili liliongozwa na roho la Paulo kwa Wafilipi: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu.” Bila shaka, tukiwasiliana waziwazi kwa njia hiyo na Rafiki yetu mkubwa zaidi tutapata faraja na kitulizo kama Paulo alivyosema: “Amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Flp. 4:6, 7) Sikuzote na tuthamini pendeleo kubwa sana la kuwa na “amani ya Mungu” ambayo kwa kweli inalinda mioyo na nguvu zetu za akili.

Sala huimarishaje urafiki wetu pamoja na Mungu? (Tazama fungu la 21)

21 Sala hutusaidia kusitawisha urafiki pamoja na Yehova. Basi, ‘tusali bila kuacha.’ (1 The. 5:17) Funzo hili na liimarishe uhusiano wetu wenye thamani pamoja na Mungu na azimio letu la kufuata viwango vyake vya uadilifu. Na tutumie wakati kutafakari baraka tunazofurahia kwa sababu Yehova kwa kweli ni Baba yetu, Mungu wetu, na Rafiki yetu.