Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usemi Wako​—Je, Unamaanisha “Ndiyo na pia Siyo”?

Usemi Wako​—Je, Unamaanisha “Ndiyo na pia Siyo”?

Fikiria hali hii: Mzee aliye mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali amepanga kuhubiri na ndugu kijana Jumapili asubuhi. Lakini mzee huyo anapigiwa simu ya dharura asubuhi na ndugu ambaye mke wake amehusika katika aksidenti na kupelekwa hospitalini. Anamwomba mzee huyo amsaidie kupata daktari atakayemtibu mke wake bila kumtia damu. Kwa hiyo, mzee huyo anavunja mpango wa kuhubiri pamoja na yule ndugu kijana ili aisaidie kwa upendo familia iliyopatwa na dharura.

Wazia hali hii nyingine: Mama asiye na mume anaalikwa pamoja na watoto wake wawili kuwatembelea wenzi fulani wa ndoa katika kutaniko lao jioni. Watoto wake wanafurahi sana anapowaambia kuhusu mwaliko huo. Wanatazamia kwa hamu jioni hiyo. Hata hivyo, kabla ya siku hiyo, wenzi hao wa ndoa wanamjulisha mama huyo kwamba jambo fulani lisilotazamiwa limetokea na hivyo wamevunja mpango huo. Baadaye, mama huyo anapata habari kwamba baada ya kuwaalika, wenzi hao wa ndoa walivunja mpango huo kwa sababu walialikwa na kukubali mwaliko wa kuwatembelea rafiki zao jioni hiyohiyo.

Bila shaka, tukiwa Wakristo tunapaswa kutimiza ahadi zetu. Hatupaswi kamwe kusema “Ndiyo na pia Siyo.” (2 Kor. 1:18) Hata hivyo, hali hutofautiana kama mifano hiyo miwili inavyoonyesha. Pindi nyingine tunalazimika kuvunja mipango tuliyofanya. Pindi moja, mtume Paulo alijikuta katika hali kama hiyo.

PAULO ASHTAKIWA KUWA MTU ASIYE NA MSIMAMO

Mwaka wa 55 W.K., Paulo alipokuwa Efeso wakati wa safari yake ya tatu ya umishonari, alikusudia kuvuka Bahari ya Aegea hadi Korintho na kusafiri hadi Makedonia. Alipokuwa akirudi Yerusalemu, alipanga kutembelea kutaniko la Korintho kwa mara ya pili ili achukue zawadi yao ya fadhili kwa ajili ya ndugu waliokuwa Yerusalemu. (1 Kor. 16:3) Jambo hilo linatajwa katika andiko la 2 Wakorintho 1:15 na 16 linalosema hivi: “Nikiwa na uhakika huu, nilikuwa nikikusudia hapo mbeleni kuja kwenu, ili muwe na pindi ya pili ya kuwa na shangwe, nami niende Makedonia baada ya kukaa kidogo kwenu, na kurudi kutoka Makedonia kuja kwenu nanyi mnisindikize kwenda Yudea.”

Inaonekana kwamba katika barua iliyotangulia, Paulo aliwajulisha ndugu Wakorintho kuhusu mpango wake. (1 Kor. 5:9) Hata  hivyo, muda mfupi tu baada ya kuandika barua hiyo, Paulo alijulishwa na nyumba ya Kloe kwamba kulikuwa na magombano makali katika kutaniko. (1 Kor. 1:10, 11) Paulo aliamua kubadili mpango wake wa awali, na kuandika barua ya Kwanza kwa Wakorintho. Katika barua hiyo, Paulo aliwarekebisha na kuwapa mashauri ya upendo. Alitaja pia kwamba amebadili safari yake. Angeenda Makedonia kwanza kisha Korintho.​—1 Kor. 16:5, 6. *

Inaonekana kwamba ndugu wa Korintho walipopokea barua yake, baadhi ya ‘mitume waliojiona kuwa bora sana’ katika kutaniko hilo walidai kwamba Paulo hana msimamo, yaani, hatimizi ahadi zake. Akijitetea, Paulo aliuliza hivi: “Basi, nilipokuwa nikikusudia hivyo, je, nilifanya mambo kijuujuu? Au mambo yale ninayokusudia, je, mimi nayakusudia kulingana na mwili, ili kwamba niseme ‘Ndiyo, Ndiyo’ na ‘Siyo, Siyo’?”​—2 Kor. 1:17; 11:5.

Huenda tukauliza hivi: Chini ya hali hizo, je, ni kweli kwamba mtume Paulo ‘alifanya mambo kijuujuu’? La hasha! Neno lililotafsiriwa “kijuujuu” linamaanisha mtu asiye na msimamo, asiyetegemeka, na asiyetimiza ahadi zake. Paulo aliuliza hivi: “Je, mimi nayakusudia kulingana na mwili?” Swali hilo lilipaswa kuwasaidia Wakristo wa Korintho kuelewa kwamba Paulo hakubadili mipango yake eti kwa sababu hakutegemeka.

Paulo alipinga vikali shtaka hilo alipoandika hivi: “Lakini Mungu anaweza kutegemewa ili neno letu kwenu lisiwe ni Ndiyo na pia Siyo.” (2 Kor. 1:18) Bila shaka, Paulo alibadili mipango yake kwa sababu aliwahangaikia sana ndugu na dada zake katika Korintho. Andiko la 2 Wakorintho 1:23 linasema kwamba alibadili mipango yake ya awali ya kwenda Korintho kwa sababu ‘aliwahurumia.’ Kwa kweli, aliwapa nafasi ya kurekebisha mambo kabla ya kukutana nao. Kama alivyotarajia, Paulo akiwa angali Makedonia alijulishwa na Tito kwamba barua aliyowaandikia iliwachochea kuonyesha huzuni na toba, jambo lililomletea shangwe nyingi.​—2 Kor. 6:11; 7:5-7.

“AMINA” INAYOSEMWA KWA MUNGU

Huenda shtaka la kwamba Paulo hakuwa na msimamo lilimaanisha kwamba kwa kuwa hangetimiza ahadi zake katika maisha ya kila siku basi hangeweza kutegemeka katika kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, Paulo aliwakumbusha Wakorintho kwamba aliwahubiria kumhusu Yesu Kristo. “Mwana wa Mungu, Kristo Yesu, aliyehubiriwa katikati yenu kupitia sisi, yaani, kupitia mimi na Silvano na Timotheo, hakuwa Ndiyo na pia Siyo, bali Ndiyo imekuwa Ndiyo kuhusiana naye.” (2 Kor. 1:19) Je, Yesu Kristo, ambaye Paulo alimwiga hakutegemeka kwa njia yoyote? Hapana! Katika maisha na huduma yake yote, Yesu alisema kweli sikuzote. (Yoh. 14:6; 18:37) Ikiwa ujumbe ambao Yesu alihubiri ulikuwa wa kweli kabisa na wenye kutegemeka, basi kazi ya kuhubiri ya mtume Paulo ilikuwa yenye kutegemeka pia kwa kuwa alihubiri ujumbe huohuo.

Bila shaka, Yehova ndiye “Mungu wa ukweli.” (Zab. 31:5) Maneno haya aliyoandika Paulo yanaonyesha hivyo: “Hata ahadi za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa Ndiyo kwa njia yake,” yaani, kwa njia ya Kristo. Utimilifu kamili wa Yesu akiwa duniani uliondoa shaka yoyote kuhusu ahadi za Yehova. Paulo anaendelea kusema hivi: “Kwa hiyo kupitia yeye [Yesu] pia ‘Amina’ husemwa kwa Mungu kwa ajili ya utukufu kupitia sisi.” (2 Kor. 1:20) Yesu mwenyewe ndiye “Amina,” au uhakikisho wa kwamba kila ahadi anayotoa Yehova Mungu itatimia!

Yehova na Yesu husema kweli sikuzote, vivyo hivyo, sikuzote Paulo alimaanisha alichosema. (2 Kor. 1:19) Yeye hakuwa mtu asiye na  msimamo aliyetoa ahadi “kulingana na mwili.” (2 Kor. 1:17) Badala yake, ‘alitembea kwa roho.’ (Gal. 5:16) Aliwajali sana watu aliposhughulika nao. Ndiyo yake ilimaanisha Ndiyo!

JE, NDIYO YAKO INAMAANISHA NDIYO?

Siku hizi, ni kawaida kwa watu wasioishi kupatana na kanuni za Biblia kutoa ahadi na kutozitimiza tatizo dogo linapotokea au wanapopata jambo bora zaidi. Inapohusu biashara, wengi husema “ndiyo” lakini haimaanishi “ndiyo,” hata kama wamefanya mkataba na kuandikiana. Watu wengi hawaoni ndoa kuwa makubaliano ya kudumu kati ya watu wawili. Badala yake, idadi kubwa sana ya talaka inaonyesha kwamba wengi wanaiona ndoa kuwa muungano wa kijuu-juu tu unaoweza kuvunjwa kwa urahisi.​—2 Tim. 3:1, 2.

Namna gani wewe? Je, Ndiyo yako inamaanisha Ndiyo? Kama tulivyoona mwanzoni mwa makala hii, huenda ukalazimika kuvunja ahadi nyakati fulani kwa sababu ya hali zisizoepukika bali si kwa sababu huna msimamo. Lakini ukiwa Mkristo, unapoweka mkataba au kutoa ahadi, kwa kweli unapaswa kujitahidi kadiri unavyoweza ili kutimiza ahadi hiyo. (Zab. 15:4; Mt. 5:37) Ukifanya hivyo, utajulikana kuwa mtu mwenye kutegemeka, anayetimiza ahadi zake na kusema kweli sikuzote. (Efe. 4:15, 25; Yak. 5:12) Watu wanapotambua kwamba unategemeka katika mambo ya kawaida, watakuwa tayari zaidi kukusikiliza unapowaambia kweli kuhusu Ufalme wa Mungu. Hivyo, acheni tuhakikishe kwamba Ndiyo yetu kwa kweli inamaanisha Ndiyo!

^ fu. 7 Muda mfupi baada ya kuandika 1 Wakorintho, Paulo kwa kweli alienda Makedonia akipitia Troa. Aliandika 2 Wakorintho akiwa Makedonia. (2 Kor. 2:12; 7:5) Baadaye, alitembelea kutaniko la Korintho.