Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Chakula Changu Ni Kufanya Mapenzi ya Mungu’

‘Chakula Changu Ni Kufanya Mapenzi ya Mungu’

Ni nini kinachokufurahisha sana? Je, ni mahusiano ya kibinadamu kama vile ndoa, kuwa na familia, au kusitawisha urafiki? Yawezekana kwamba wewe hufurahia kushiriki mlo pamoja na wapendwa wako. Hata hivyo, ukiwa mtumishi wa Yehova, je, si ni kweli kwamba kufanya mapenzi ya Mungu, kujifunza Neno lake, na kuhubiri habari njema ni mambo yanayothawabisha zaidi?

Mfalme Daudi wa taifa la kale la Israeli aliimba hivi akimsifu Muumba: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” (Zab. 40:8) Licha ya magumu na mikazo aliyokabili maishani, Daudi alipendezwa kikweli kufanya mapenzi ya Mungu. Bila shaka, Daudi hakuwa mwabudu pekee wa Yehova aliyefurahia kumtumikia Mungu wa kweli.

Mtume Paulo alitumia maneno ya Zaburi 40:8 kumrejelea Masihi, au Kristo. Aliandika hivi: “Wakati yeye [Yesu] anapokuja katika ulimwengu anasema: ‘“Dhabihu na toleo wewe hukutaka, bali ulinitayarishia mwili. Hukukubali matoleo mazima ya kuteketezwa na toleo la dhambi.” Ndipo nikasema, “Tazama! Nimekuja (katika kitabu cha kukunjwa imeandikwa juu yangu) ili kufanya mapenzi yako, Ee Mungu.”’”—Ebr. 10:5-7.

Alipokuwa duniani, Yesu alifurahia kutazama uumbaji, kuwa pamoja na marafiki, na kula chakula pamoja na wengine. (Mt. 6:26-29; Yoh. 2:1, 2; 12:1, 2) Hata hivyo, alihangaikia na kupendezwa kufanya mapenzi ya Baba yake wa mbinguni. Kwa kweli, Yesu alisema: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yoh. 4:34; 6:38) Wanafunzi wa Yesu walijifunza kutoka kwa Bwana wao siri ya kupata furaha ya kweli. Kwa hiari, waliwahubiria wengine ujumbe wa Ufalme kwa hamu na shangwe kubwa.—Luka 10:1, 8, 9, 17.

“NENDENI MKAFANYE WANAFUNZI”

Yesu aliwaamuru hivi wafuasi wake: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20) Ili tutimize mgawo huo, tunahitaji kuwahubiria watu popote wanapoweza kupatikana, kuwarudia wale wanaopendezwa, na kujifunza Biblia pamoja nao. Kufanya kazi hiyo kunaweza kutuletea shangwe kubwa sana.

Upendo hutuchochea kuendelea kuhubiri hata watu wasipopendezwa na ujumbe wetu

 Iwe watu wanapendezwa au hawapendezwi na ujumbe wetu, tunaweza kupata shangwe katika huduma yetu tukiwa na mtazamo unaofaa. Kwa nini tunaendelea kutangaza habari njema hata kama watu hawapendezwi au wanapuuza ujumbe wetu? Kwa sababu tunatambua kwamba tunaposhiriki katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu na jirani. Kwa kweli, uhai wetu na wa jirani zetu umo hatarini. (Eze. 3:17-21; 1 Tim. 4:16) Acheni tufikirie mambo fulani ambayo yamewasaidia wengi wa wafanyakazi wenzetu kudumisha au kuchochea upya bidii yao wanapohubiri katika maeneo magumu.

TUMIA KILA FURSA

Mara nyingi, tunapotumia maswali yanayofaa katika huduma tunapata matokeo mazuri. Asubuhi moja, Amalia alimwona mwanamume fulani akisoma gazeti katika bustani. Alimkaribia na kumuuliza ikiwa amesoma habari yoyote njema. Mwanamume huyo aliposema kwamba hajaona habari njema, Amalia alisema, “Nimekuletea habari njema ya Ufalme wa Mungu.” Hilo lilichochea upendezi wa mwanamume huyo, akakubali funzo la Biblia. Kwa kweli, Amalia alianzisha mafunzo matatu ya Biblia katika bustani hiyo.

Janice amefanya mahali pake pa kazi kuwa eneo lake la kuhubiri. Mlinzi mmoja na mfanyakazi mwenzake walipopendezwa na makala iliyochapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, Janice aliahidi kuwaletea magazeti hayo kwa ukawaida. Alimwahidi pia mfanyakazi mwenzake aliyefurahia sana kusoma habari mbalimbali zilizozungumziwa katika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Hilo lilifanya mfanyakazi mwingine aombe magazeti hayo. Janice anasema hivi: “Yehova amenibariki sana!” Mwishowe, alipata watu 11 aliowapelekea magazeti kwa ukawaida kazini.

UWE NA MTAZAMO UNAOFAA

Mwangalizi anayesafiri alipendekeza kwamba katika huduma ya nyumba kwa nyumba, wahubiri wasimalizie mazungumzo kwa kuwaambia tu wenye nyumba kwamba watarudi siku nyingine. Badala yake, wanaweza kuuliza hivi: “Je, ungependa nikuonyeshe jinsi unavyoweza kujifunza Biblia?” au, “Ungependa nirudi siku gani na saa ngapi ili tuendelee na mazungumzo yetu?” Mwangalizi huyo anayesafiri alisema kwamba kwa kutumia njia hiyo, akina ndugu na dada katika kutaniko moja alilotembelea, walianzisha mafunzo 44 ya Biblia katika muda wa juma moja.

Tunaweza kupata matokeo mazuri sana tukiwarudia wenye nyumba haraka iwezekanavyo, hata baada ya siku chache tu. Kwa nini? Kwa sababu tunapofanya hivyo tunaonyesha kwamba tunataka kikweli kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu kuielewa Biblia. Mwanamke mmoja alipoulizwa kwa nini alikubali kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, alisema hivi: “Nilianza kujifunza kwa sababu  walipendezwa nami kikweli na kunionyesha upendo.”

Unaweza kumuuliza hivi mwenye nyumba: “Je, ungependa nikuonyeshe jinsi unavyoweza kujifunza Biblia?”

Muda mfupi baada ya kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia, Madaí aliongoza mafunzo 15 ya Biblia na akawapa wahubiri wengine mafunzo matano. Watu wengi aliokuwa akijifunza nao Biblia walianza kuhudhuria mikutano yetu kwa ukawaida. Ni nini kilichomsaidia Madaí kuanzisha mafunzo mengi ya Biblia? Shule hiyo ilimsaidia kuona umuhimu wa kurudi tena na tena hadi anapowapata wale waliopendezwa mwanzoni. Shahidi mwingine ambaye amesaidia wengi kujifunza kweli za Biblia anasema hivi: “Nimejifunza kwamba ili kuwasaidia watu wanaotaka kumjua Yehova, ni muhimu kutochoka kufanya ziara za kurudia.”

Kuwarudia wenye nyumba haraka iwezekanavyo huonyesha kwamba tunataka kikweli kuwasaidia wanaotaka kuielewa Biblia

Ni lazima tujitahidi kabisa ili kufanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia. Hata hivyo, tunapojitahidi tunapata thawabu nyingi sana. Tukifanya yote tuwezayo katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme, tunaweza kuwasaidia wengine “kupata ujuzi sahihi wa kweli” na kuokolewa. (1 Tim. 2:3, 4) Hilo litatuletea uradhi na furaha isiyo na kifani.