Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumia Ile Kanuni Bora Katika Huduma Yako

Tumia Ile Kanuni Bora Katika Huduma Yako

“Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.”—MT. 7:12.

1. Je, itikio la watu katika huduma linaweza kuathiriwa na jinsi tunavyowatendea? Toa mfano. (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

MIAKA michache iliyopita, wenzi fulani wa ndoa Mashahidi nchini Fiji walikuwa wakishiriki katika kampeni ya kuwaalika watu kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Walipokuwa wakiongea na mwanamke mmoja nje ya nyumba yake, mvua ilianza kunyesha. Ndugu alimpa mwanamke huyo mwavuli, kisha yeye na mke wake wakajifunika mwavuli mmoja. Wenzi hao walifurahi sana mwanamke huyo alipohudhuria Ukumbusho. Alikiri kwamba ingawa hakukumbuka mambo ambayo Mashahidi hao walisema walipomtembelea, alivutiwa sana na jinsi walivyomtendea hivi kwamba akaamua kuhudhuria Ukumbusho. Kwa nini? Kwa sababu wenzi hao walitumia ile ambayo mara nyingi huitwa Kanuni Bora.

2. Ile Kanuni Bora ni nini, na tutaitumiaje?

2 Ile Kanuni Bora ni nini? Ni lile shauri alilotoa Yesu aliposema hivi: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mt. 7:12) Tutaitumiaje kanuni hiyo? Kwa kuchukua hatua mbili. Kwanza, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Kama ningekuwa katika hali yake, ningependa nitendewe jinsi gani?’ Kisha, tunahitaji kujitahidi  kadiri tuwezavyo kuelewa hali yake.—1 Kor. 10:24.

3, 4. (a) Kwa nini tunapaswa kutumia ile Kanuni Bora hata tunaposhughulika na watu ambao si waamini wenzetu? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Mara nyingi sisi hutumia ile Kanuni Bora tunaposhughulika na waamini wenzetu. Lakini Yesu hakusema kwamba tunapaswa kutumia kanuni hiyo tunaposhughulika na waamini wenzetu tu. Alitaja Kanuni hiyo Bora alipokuwa akizungumzia jinsi tunavyopaswa kuwatendea watu kwa ujumla, hata adui zetu. (Soma Luka 6:27, 28, 31, 35.) Ikiwa tunapaswa kutumia Kanuni Bora tunaposhughulika na adui zetu, je, hatupaswi kufanya hivyo hata zaidi tunapowahubiria wengine, hasa ‘wale wote walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele’?—Mdo. 13:48.

4 Sasa, tutazungumzia maswali manne tunayohitaji kujiuliza tunapohubiri: Ninahubiria nani? Ninawahubiria wakiwa wapi? Ni wakati gani mzuri wa kuwahubiria watu? Nitatumia utangulizi gani? Kama tutakavyoona, maswali hayo yanaweza kutusaidia kujali hisia za wale tunaowahubiria na hivyo kubadili mazungumzo yetu ili yapatane na hali zao.—1 Kor. 9:19-23.

NINAHUBIRIA NANI?

5. Tunaweza kujiuliza maswali gani?

5 Kwa kawaida, sisi huzungumza na mtu mmoja-mmoja katika huduma yetu. Kila mtu amelelewa katika mazingira tofauti na anakabili matatizo tofauti. (2 Nya. 6:29) Unapomhubiria mtu habari njema, jiulize hivi: ‘Ikiwa mimi ndiye ninayehubiriwa, ningependa mtu huyo awe na maoni gani kunihusu? Je, ningefurahi ikiwa angeniona kuwa jirani tu? Au je, ningependa anifahamu vizuri kibinafsi?’ Kufikiria maswali kama hayo kunaweza kutukumbusha kwamba tunapaswa kumtendea kila mwenye nyumba kulingana na hali yake.

6, 7. Tunapaswa kufanya nini tukikutana na mtu anayeonekana kuwa na hasira?

6 Hakuna anayependa kuitwa “mtu mbaya.” Kwa mfano: Tukiwa Wakristo, tunajitahidi kadiri tunavyoweza ili kufuata shauri la Biblia kwa kusema ‘maneno yenye neema sikuzote.’ (Kol. 4:6) Hata hivyo, kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, pindi nyingine tunasema maneno tunayojutia baadaye. (Yak. 3:2) Tukiongea kwa njia isiyo ya fadhili, labda kwa sababu ya mkazo fulani, hatungependa mtu aseme kwamba “tunawadharau” au “hatuwajali wengine.” Tunatarajia kwamba ataelewa hali yetu. Je, hatupaswi kuwaonyesha wengine ufikirio kwa njia hiyohiyo?

7 Ukimhubiria mtu anayeonekana kuwa na hasira, jaribu kuelewa kwa nini anahisi hivyo. Je, inawezekana kwamba ana hasira kwa sababu ya mkazo shuleni au kazini? Je, ana tatizo kubwa la kiafya? Katika visa vingi, wenye nyumba waliokuwa na hasira waliitikia vizuri baadaye kwa sababu watu wa Yehova waliwatendea kwa heshima na upole.—Met. 15:1; 1 Pet. 3:15.

8. Kwa nini hatupaswi kusita kuwahubiria “watu wa namna zote” ujumbe wa Ufalme?

8 Katika huduma yetu, tunakutana na watu wenye hali na malezi mbalimbali. Kwa mfano, katika miaka michache tu iliyopita, masimulizi zaidi ya 60 yamechapishwa katika makala za Mnara wa Mlinzi zenye kichwa: “Biblia Inabadili Maisha.” Baadhi ya watu wanaosimuliwa katika makala hizo walikuwa wezi, walevi, majambazi, au waraibu wa dawa za kulevya. Wengine walikuwa wanasiasa, viongozi wa kidini, au watu waliofuatilia kazi  ya kimwili maishani. Baadhi yao waliishi maisha mapotovu. Hata hivyo, wote walisikia habari njema, wakakubali kujifunza Biblia, wakabadilika, na kukubali kweli. Kwa hiyo, hatupaswi kamwe kufikiri kwamba watu fulani hawawezi kukubali ujumbe wa Ufalme. (Soma 1 Wakorintho 6:9-11.) Badala yake, tunatambua kwamba “watu wa namna zote” wanaweza kukubali habari njema.—1 Kor. 9:22.

NINAWAHUBIRIA WAKIWA WAPI?

9. Kwa nini tunapaswa kuheshimu nyumba za watu?

9 Tunawahubiria watu wakiwa wapi? Mara nyingi, tunawatembelea nyumbani mwao. (Mt. 10:11-13) Kwa kawaida, tunathamini watu wanapoheshimu nyumba na mali yetu. Tunapenda kuishi mahali salama penye faragha. Tunapaswa kuwaheshimu vivyo hivyo jirani zetu. Kwa hiyo, tunapohubiri nyumba kwa nyumba, ni vizuri kuheshimu nyumba zao.Mdo. 5:42.

10. Tunawezaje kuepuka kuwaudhi watu tunapohubiri?

10 Katika ulimwengu wa leo uliojaa uhalifu, wenye nyumba wengi huwa na wasiwasi wanapoona watu wasiowajua. (2 Tim. 3:1-5) Hatupaswi kuwafanya wawe na wasiwasi zaidi. Kwa mfano, wazia kwamba tunagonga mlango wa nyumba fulani. Ikiwa hakuna anayejibu, tunaweza kushawishiwa kuchungulia dirishani au kuzunguka-zunguka nyumba hiyo tukimtafuta mwenye nyumba. Je, mwenye nyumba ataudhika ukifanya hivyo? Jirani zake watafikiria nini? Ni kweli kwamba tunapaswa kuhubiri eneo letu kikamili. (Mdo. 10:42) Tuna hamu ya kueneza habari njema, na hilo ni jambo linalofaa. (Rom. 1:14, 15) Hata hivyo, kwa hekima tunaepuka kufanya jambo lolote linaloweza kuwaudhi watu isivyo lazima katika eneo tunalohubiri. Mtume Paulo aliandika hivi: “Sisi hatutoi sababu yoyote ya kukwaza kwa njia yoyote, ili huduma yetu isilaumiwe.” (2 Kor. 6:3) Tunapoheshimu mali na nyumba za watu katika eneo letu, huenda mwenendo wetu ukawachochea watu wakubali kweli.—Soma 1 Petro 2:12.

Sikuzote na tuheshimu mali na faragha ya wenye nyumba (Tazama fungu la 10)

NI WAKATI GANI MZURI WA KUWAHUBIRIA WATU?

11. Kwa nini tunathamini watu wanapoheshimu ratiba yetu?

11 Tukiwa Wakristo, wengi wetu tuna shughuli nyingi. Ili tutimize wajibu wetu, tunaamua mambo ya kutanguliza na kupanga ratiba yetu kwa makini. (Efe. 5:16; Flp. 1:10) Jambo fulani linapovuruga ratiba yetu, huenda tukavunjika moyo. Kwa hiyo, tunathamini wengine wanapoheshimu ratiba yetu na kuonyesha usawaziko kwa kutotumia muda mwingi wanapotutembelea. Tutaonyeshaje kwamba tunazingatia ile Kanuni Bora kwa kuwaheshimu wale tunaohubiria?

12. Tutajuaje wakati mzuri zaidi wa kuwahubiria watu katika eneo letu?

12 Tunapaswa kujitahidi kujua wakati unaofaa zaidi wa kuwatembelea wenye nyumba. Kwa kawaida, watu hupatikana wakati gani katika eneo letu? Ni wakati gani ambao inaelekea wataitikia vizuri? Ni vyema tubadili ratiba yetu ili ipatane na hali zao. Katika nchi fulani, wahubiri hupata matokeo mazuri zaidi wanapohubiri nyumba kwa nyumba wakati wa alasiri au jioni. Ikiwa ndivyo ilivyo katika eneo lenu, je, unaweza kupanga kuhubiri nyumba kwa nyumba wakati huo? (Soma 1 Wakorintho 10:24.) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatubariki tukijidhabihu kwa njia yoyote ili kuhubiri wakati unaowafaa zaidi wenye nyumba.

13. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunamheshimu mwenye nyumba?

13 Ni njia gani nyingine ya kuonyesha  kwamba tunamheshimu mwenye nyumba? Tunapokutana na mtu anayeitikia vizuri, tunapaswa kumtolea ushahidi mzuri lakini hatupaswi kutumia muda mwingi sana. Huenda mwenye nyumba amepanga kufanya mambo mengine anayoona kuwa muhimu. Akisema ana shughuli nyingi, tunaweza kumwambia kwamba tutazungumza kwa ufupi, na tunapaswa kufanya kama tulivyoahidi. (Mt. 5:37) Tunapomalizia mazungumzo, ni vizuri kumuuliza mwenye nyumba wakati unaofaa ambao angependa turudi. Baadhi ya wahubiri wamepata matokeo mazuri kwa kusema hivi: “Nitafurahi kukutembelea tena. Je, ungependa nikupigie simu au kukutumia ujumbe kabla ya kuja?” Tunapobadili ratiba yetu ili iwafae watu katika eneo letu, tunamwiga mtume Paulo ambaye ‘hakutafuta faida yake mwenyewe bali ile ya walio wengi, ili wapate kuokolewa.’—1 Kor. 10:33.

NITATUMIA UTANGULIZI GANI?

14-16. (a) Kwa nini tunapaswa kuwajulisha moja kwa moja wenye nyumba kusudi la kuwatembelea? Toa mfano. (b) Mwangalizi mmoja anayesafiri amepata matokeo mazuri kwa kutumia utangulizi gani?

14 Wazia kwamba mtu usiyemjua anakupigia simu na kukuuliza vyakula unavyopenda. Hujui ni nani na kwa nini anakuuliza swali hilo. Huenda ukazungumza naye kwa muda kwa sababu hutaki kumuudhi, lakini inaelekea kwamba utakatisha mazungumzo. Lakini namna gani ikiwa mtu anayekupigia simu anajitambulisha na kukujulisha kuwa yeye ni mtaalamu wa mambo ya lishe, na kwa fadhili  anakueleza kwamba ana habari muhimu. Inaelekea utamsikiliza kwa makini zaidi. Kwa kweli, sisi huthamini mtu anapotaja moja kwa moja kwa busara kusudi la kuzungumza nasi. Tutawaonyeshaje ufikirio kama huo watu tunaokutana nao katika huduma yetu?

15 Katika maeneo mengi, tunahitaji kuwajulisha moja kwa moja wenye nyumba kusudi letu la kuwatembelea. Ni kweli kwamba tuna habari muhimu tunazotaka kumjulisha mwenye nyumba. Hata hivyo, itakuwaje tukimuuliza swali hili bila kujitambulisha: “Kama ungekuwa na uwezo wa kuondoa matatizo ulimwenguni, ungeondoa tatizo gani?” Tunajua kwamba tunauliza swali hilo ili kujua maoni ya mtu huyo na kisha kumwonyesha maoni ya Biblia. Hata hivyo, huenda mwenye nyumba akajiuliza hivi: ‘Huyu ni nani, na kwa nini ananiuliza swali hili? Anataka nini?’ Kwa hiyo, tunapaswa kumstarehesha mwenye nyumba. (Flp. 2:3, 4) Tunawezaje kufanya hivyo?

16 Mwangalizi mmoja anayesafiri amepata matokeo mazuri kwa kutumia utangulizi ufuatao. Baada ya kumsalimu mwenye nyumba, anampa trakti yenye kichwa Je, Ungependa Kujua Ukweli? na kusema hivi: “Leo tunawapa watu wote trakti hii. Inazungumzia maswali sita ambayo watu wengi huuliza. Hii ni nakala yako.” Ndugu huyo anasema kwamba watu wengi hustarehe kwa kiasi fulani wanapojua kusudi letu la kuwatembelea. Mara nyingi ni rahisi kuendeleza mazungumzo baada ya utangulizi huo. Kisha, mwangalizi huyo humuuliza hivi mwenye nyumba: “Je, umewahi kujiuliza mojawapo ya maswali haya?” Mwenye nyumba akichagua swali moja, ndugu huyo hufungua trakti na kuzungumzia jibu la Biblia. Au anachagua swali moja na kulizungumzia bila kumuuliza mwenye nyumba maswali magumu. Bila shaka, kuna njia nyingi za kuanzisha mazungumzo. Katika maeneo fulani, huenda wenye nyumba wakatarajia tufuate desturi fulani kabla ya kuwaeleza kusudi letu la kuwatembelea. Ni muhimu sana kubadili utangulizi wetu ili uwafae watu katika eneo letu.

ENDELEA KUTUMIA ILE KANUNI BORA KATIKA HUDUMA

17. Kama tulivyozungumzia katika makala hii, tunaweza kutumia ile Kanuni Bora katika njia zipi?

17 Hivyo basi, tunawezaje kutumia ile Kanuni Bora katika huduma yetu? Kwa kumtendea kila mwenye nyumba kulingana na hali yake. Kuheshimu nyumba na mali za wale tunaowahubiria. Kujitahidi kuhubiri wakati ambapo inaelekea wenye nyumba wanapatikana nyumbani na wataitikia vizuri. Na kutoa utangulizi kwa njia inayokubaliwa katika eneo letu.

18. Kuna faida gani za kuwatendea watu katika eneo letu kama vile ambavyo tungependa kutendewa?

18 Kuna faida nyingi za kuwatendea watu katika eneo letu kama vile ambavyo tungependa kutendewa. Tukitenda kwa fadhili na ufikirio, tunaacha nuru yetu ing’ae, tunaonyesha wazi umuhimu wa kutumia kanuni za Biblia, na tunampa utukufu Baba yetu wa mbinguni. (Mt. 5:16) Huenda watu wengi zaidi wakakubali kujifunza kweli ikiwa tutawafikia kwa njia nzuri. (1 Tim. 4:16) Iwe wale tunaowahubiria wanakubali au hawakubali ujumbe wa Ufalme, tunaridhika kujua kwamba tunajitahidi kadiri tuwezavyo kutimiza huduma yetu. (2 Tim. 4:5) Kila mmoja wetu na amwige mtume Paulo aliyeandika hivi: “Ninafanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili niishiriki hiyo pamoja na wengine.” (1 Kor. 9:23) Basi, acheni sikuzote tutumie ile Kanuni Bora katika huduma yetu.