Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unasonga Mbele Pamoja na Tengenezo la Yehova?

Je, Unasonga Mbele Pamoja na Tengenezo la Yehova?

“Macho ya Yehova yako juu ya waadilifu.”—1 PET. 3:12.

1. Ni tengenezo gani lililokuwa watu kwa ajili ya jina la Yehova na kuchukua mahali pa taifa la Israeli lililoasi imani? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

YEHOVA ndiye aliyeanzisha kutaniko la Kikristo katika karne ya kwanza na kurudisha ibada ya kweli katika nyakati za karibuni. Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, tengenezo lililofanyizwa na wafuasi wa mapema wa Kristo lilichaguliwa kuwa watu kwa ajili ya jina la Yehova na kuchukua mahali pa taifa la Israeli lililoasi imani. Tengenezo hilo jipya lililompendeza sana Mungu, liliokoka uharibifu wa Yerusalemu katika mwaka wa 70 W.K. (Luka 21:20, 21) Matukio hayo ya karne ya kwanza yalionyesha kimbele utendaji wa watumishi wa Yehova leo. Hivi karibuni mfumo wa mambo wa Shetani utafikia mwisho wake, lakini tengenezo la Mungu litaokoka siku za mwisho. (2 Tim. 3:1) Tunawezaje kuwa na uhakika kuhusu hilo?

2. Yesu alisema nini kuhusu “dhiki kuu,” nayo itaanzaje?

2 Yesu alisema hivi kuhusu kuwapo kwake kusikoonekana na umalizio wa mfumo wa mambo: ‘Kutakuwa na dhiki kuu ya namna ambayo haijapata kutukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatukia tena.’ (Mt. 24:3,  21) Dhiki hiyo ambayo haijawahi kamwe kutokea itaanza Yehova atakapotumia mamlaka za kisiasa kuharibu “Babiloni Mkubwa,” ile milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo. (Ufu. 17:3-5, 16) Ni nini kitakachofuata?

SHAMBULIZI LA SHETANI LAONGOZA KWENYE HAR–MAGEDONI

3. Baada ya dini ya uwongo kuharibiwa, kutakuwa na jaribio gani la kuwashambulia watu wa Yehova?

3 Baada ya dini ya uwongo kuharibiwa, Shetani na sehemu mbalimbali za ulimwengu wake zitawashambulia watumishi wa Yehova. Kwa mfano, kuhusu “Gogu wa nchi ya Magogu,” Maandiko yanatabiri hivi: “Utaingia kama dhoruba. Utakuwa kama mawingu ya kuifunika nchi, wewe na vikosi vyako vyote na vikundi vingi vya watu pamoja nawe.” Mashahidi wa Yehova wataonekana kuwa shabaha rahisi kwa sababu hawana majeshi yenye silaha nao ni watu wenye amani zaidi duniani. Lakini hatua ya kuwashambulia itakuwa kosa kubwa kama nini!—Eze. 38:1, 2, 9-12.

4, 5. Yehova atakabilianaje na jitihada za Shetani za kuwaangamiza watumishi Wake?

4 Mungu atakabilianaje na jitihada za Shetani za kuwaangamiza watu Wake? Yehova ataingilia kati na kuwatetea akitumia haki yake akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Mzima. Watumishi wa Yehova wanaposhambuliwa, anahisi kwamba yeye ndiye anayeshambuliwa. (Soma Zekaria 2:8.) Kwa hiyo, Baba yetu wa mbinguni atachukua hatua ya haraka ili kutuokoa. Ukombozi huo utafikia kilele ulimwengu wa Shetani utakapoharibiwa kwenye Har–Magedoni, yaani, “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.”—Ufu. 16:14, 16.

5 Unabii wa Biblia ulitabiri hivi kuhusu Har–Magedoni: “‘Yehova ana ubishi na mataifa. Yeye binafsi atajiweka hukumuni na watu wote wenye mwili. Nao waovu atawatoa wauawe kwa upanga,’ asema Yehova. Yehova wa majeshi amesema hivi, ‘Tazama! Msiba utaenda toka taifa mpaka taifa, na tufani kuu itaamshwa kutoka katika sehemu za mbali zaidi za dunia. Na wale waliouawa na Yehova siku hiyo hakika watakuwa kutoka mwisho mmoja wa dunia mpaka mwisho wa pili wa dunia. Hawataombolezewa, wala kukusanywa wala kuzikwa. Watakuwa kama mbolea juu ya uso wa nchi.’” (Yer. 25:31-33) Vita vya Har–Magedoni vitakomesha mfumo huu mwovu wa mambo. Ulimwengu wa Shetani hautakuwapo tena, lakini sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova itaokoka.

KWA NINI TENGENEZO LA YEHOVA LINASITAWI LEO?

6, 7. (a) Washiriki wa “umati mkubwa” wanatoka wapi? (b) Kumekuwa na maongezeko gani katika miaka ya karibuni?

6 Tengenezo la Mungu limedumu na kusitawi duniani kwa sababu lina watu wenye kibali chake. Biblia inatuhakikishia hivi: “Macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yanaielekea dua yao.” (1 Pet. 3:12) Waadilifu wanatia ndani ‘umati mkubwa unaotoka katika ile dhiki kuu.’ (Ufu. 7:9, 14) Waokokaji hao si “umati” tu, wao ni “umati mkubwa,” yaani, ni idadi kubwa sana ya watu. Je, unajiona ukiwa miongoni mwa waokokaji hao wa “dhiki kuu”?

7 Washiriki wa umati huo mkubwa wanatoka wapi? Wanakusanywa kupitia kazi ambayo Yesu alitabiri kwamba ingekuwa sehemu ya ishara ya kuwapo kwake. Alisema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14) Katika siku hizi za mwisho, hiyo ndiyo kazi kuu ya tengenezo la Mungu.  Kwa sababu ya kazi ya Mashahidi wa Yehova ya kuhubiri na kufundisha ulimwenguni pote, mamilioni ya watu wamejifunza kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli.” (Yoh. 4:23, 24) Kwa mfano, hivi karibuni katika kipindi cha miaka kumi, yaani, mwaka wa utumishi wa 2003 hadi wa 2012, watu zaidi ya 2,707,000 walibatizwa na hivyo kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Mungu. Leo kuna Mashahidi zaidi ya 7,900,000 ulimwenguni pote, na mamilioni ya watu wanashirikiana nao, hasa katika mwadhimisho wa kila mwaka wa Ukumbusho. Lakini hatujigambi kwa sababu ya ongezeko hilo, kwa kuwa ‘Mungu ndiye anayeendelea kukuza.’ (1 Kor. 3:5-7) Hata hivyo, ni wazi kwamba umati mkubwa unaongezeka hata zaidi kila mwaka.

8. Kwa nini kuna ongezeko kubwa katika tengenezo la Yehova leo?

8 Idadi ya watumishi wa Mungu imeongezeka sana kwa sababu Yehova mwenyewe anawategemeza Mashahidi wake. (Soma Isaya 43:10-12.) Ongezeko hilo lilitabiriwa kwa maneno haya ya kinabii: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa lenye nguvu. Mimi mwenyewe, Yehova, nitaharakisha jambo hilo kwa wakati wake.” (Isa. 60:22) Pindi moja, watiwa-mafuta walio duniani walikuwa kama “mdogo,” lakini idadi yao iliongezeka Waisraeli wengine wa kiroho walipoletwa ndani ya tengenezo la Mungu. (Gal. 6:16) Kila mwaka, Yehova amewabariki na kuna ongezeko kwa sababu umati mkubwa unaendelea kukusanywa.

YEHOVA ANATAKA TUFANYE NINI?

9. Ni lazima tufanye nini ikiwa tunataka kufurahia wakati ujao mzuri unaoahidiwa katika Neno la Mungu?

9 Iwe sisi ni Wakristo watiwa-mafuta au umati mkubwa, tunaweza kufurahia wakati ujao mzuri unaoahidiwa katika Neno la Mungu. Hata hivyo, ni lazima tutimize matakwa ya Yehova. (Isa. 48:17, 18) Wafikirie Waisraeli waliokuwa chini ya Sheria ya Musa. Kusudi moja la Sheria lilikuwa kuwalinda Waisraeli kwa kuwapa maagizo yanayofaa kuhusu mwenendo wa kingono, shughuli za kibiashara, kuwatunza watoto, njia inayofaa ya kuwatendea wanadamu wengine, na kadhalika. (Kut. 20:14; Law. 19:18, 35-37; Kum. 6:6-9) Tunanufaika katika njia hizo tunapotii matakwa ya Mungu, na bila shaka hatuoni kufanya mapenzi yake kuwa mzigo mzito. (Soma 1 Yohana 5:3.) Kwa kweli, kama Waisraeli walivyolindwa na Sheria, ndivyo sheria na kanuni za Yehova Mungu zinavyotulinda tunapotii, na zinatusaidia pia kuwa wenye “afya katika imani.”—Tito 1:13.

10. Kwa nini tunapaswa kutenga wakati wa kujifunza Biblia na kuwa na jioni ya Ibada ya Familia kila juma?

10 Sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova inasonga mbele kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, uelewaji wetu wa kweli ya Biblia unaendelea kuwa wazi zaidi. Ni lazima iwe hivyo kwa sababu “njia ya waadilifu ni kama nuru inayong’aa, inayozidi kuongezeka mpaka mchana mkamilifu.” (Met. 4:18) Lakini tunahitaji kujiuliza hivi: ‘Je, ninaenda sambamba na marekebisho ya uelewaji wetu wa kweli ya Kimaandiko? Je, nina zoea la kusoma Biblia kila siku? Je, ninasoma machapisho yetu kwa bidii? Je, mimi na wapendwa wangu tunakuwa na jioni ya Ibada ya Familia kila juma?’ Wengi wetu tutakubali kwamba si vigumu sana kufanya mambo hayo. Mara nyingi tunahitaji tu kutenga wakati wa kuyafanya. Ni muhimu sana kupata ujuzi sahihi wa Maandiko, kuutumia, na kufanya maendeleo ya kiroho, hasa sasa kwa kuwa dhiki kuu iko karibu sana!

11. Sherehe, mikutano, na makusanyiko yamewanufaishaje watu wa Mungu zamani na leo?

 11 Tengenezo la Yehova linatujali linapotuhimiza tutii shauri hili la Paulo: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.” (Ebr. 10:24, 25) Sherehe za kila mwaka na makusanyiko mengine ya ibada yaliwajenga Waisraeli kiroho. Isitoshe, sherehe kama vile Sherehe ya pekee ya Vibanda katika siku za Nehemia zilikuwa pindi za shangwe. (Kut. 23:15, 16; Neh. 8:9-18) Tunafaidika vivyo hivyo tunapohudhuria mikutano na makusanyiko yetu. Acheni tunufaike kikamili na maandalizi hayo ili tuwe na afya nzuri ya kiroho na kupata furaha.—Tito 2:2.

12. Tunapaswa kuhisije kuhusu kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme?

12 Tukiwa katika tengenezo la Mungu, tuna shangwe ya kushiriki katika “kazi takatifu ya habari njema ya Mungu.” (Rom. 15:16) Tunaposhiriki katika ‘kazi hiyo takatifu’ tunakuwa “wafanyakazi wenzi” wa Yehova ambaye ni “Mtakatifu.” (1 Kor. 3:9; 1 Pet. 1:15) Kuhubiri habari njema huchangia kutakaswa kwa jina takatifu la Yehova. Na bila shaka ni pendeleo lisilo na kifani kukabidhiwa “habari njema yenye utukufu ya Mungu mwenye furaha.”—1 Tim. 1:11.

13. Afya nzuri ya kiroho na uhai wetu unategemea nini?

13 Mungu anataka tudumishe afya nzuri ya kiroho kwa kushikamana naye na kuunga mkono tengenezo lake katika utendaji wake mbalimbali. Musa aliwaambia hivi Waisraeli: “Nachukua mbingu na dunia kuwa mashahidi juu yenu leo, kwamba nimeweka uzima na kifo mbele yako, baraka na laana; nawe lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako, kwa kumpenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye; kwa maana yeye ni uhai wako na urefu wa siku zako, ili ukae katika nchi ambayo Yehova aliwaapia mababu zako Abrahamu, Isaka na Yakobo kwamba atawapa wao.” (Kum. 30:19, 20) Uhai wetu unategemea kufanya mapenzi ya Yehova, kumpenda, kusikiliza sauti yake kwa utii, na kushikamana naye.

14. Ndugu mmoja alihisije kuhusu sehemu inayoonekana ya tengenezo la Mungu?

14 Ndugu Pryce Hughes, ambaye alishikamana kabisa na Mungu na kusonga mbele pamoja na tengenezo Lake, aliandika hivi: “Ninashukuru sana kwamba nimeishi kulingana na ujuzi wa makusudi ya Yehova tangu siku za mapema kabla ya 1914 . . . Ikiwa kuna jambo ambalo limekuwa muhimu zaidi kwangu, ni kuendelea kuwa karibu na tengenezo la Yehova lionekanalo. Mambo niliyojionea zamani yalinifundisha kwamba si jambo la hekima kutegemea mawazo ya kibinadamu. Baada ya kufikia mkataa huo, niliazimia kushikamana na tengenezo hili lenye uaminifu. Mtu anawezaje kupata kibali na baraka za Yehova asipofanya hivyo?”

ENDELEA KUSONGA MBELE PAMOJA NA TENGENEZO LA MUNGU

15. Toa mfano wa Kimaandiko unaonyesha maoni tunayopaswa kuwa nayo kuhusu marekebisho yanayofanywa katika uelewaji wetu wa mafundisho ya Biblia.

15 Ikiwa sisi binafsi tunataka kupata kibali na baraka za Yehova, ni lazima tuunge mkono tengenezo lake na kukubali marekebisho yanayofanywa katika uelewaji wetu wa Kimaandiko. Fikiria hili: Baada ya kifo cha Yesu, maelfu ya Wakristo Wayahudi waliendelea kufuata Sheria kwa bidii na haikuwa rahisi kwao kuiacha. (Mdo. 21:17-20) Hata hivyo, barua ya Paulo  kwa Waebrania iliwasaidia kukubali uhakika wa kwamba hawakuwa wametakaswa kupitia dhabihu ‘zilizotolewa kulingana na Sheria,’ bali “kupitia toleo la mwili wa Yesu Kristo mara moja kwa wakati wote.” (Ebr. 10:5-10) Hapana shaka kwamba wengi kati ya Wakristo hao waliokuwa Wayahudi wa asili walirekebisha maoni yao na kusonga mbele kiroho. Sisi pia tunahitaji kujifunza kwa bidii na kuwa tayari kukubali marekebisho yanayofanywa katika uelewaji wetu wa Neno la Mungu au katika kazi yetu ya kuhubiri.

16. (a) Ni baraka gani zitakazofanya maisha yawe mazuri sana katika ulimwengu mpya? (b) Unatazamia nini katika ulimwengu mpya?

16 Yehova ataendelea kuwabariki wote wanaoendelea kuwa washikamanifu kwake na kwa tengenezo lake. Watiwa-mafuta waaminifu watapata mapendeleo ya pekee wakiwa warithi pamoja na Kristo mbinguni. (Rom. 8:16, 17) Ikiwa una tumaini la kuishi milele duniani, wazia jinsi maisha yatakavyofurahisha katika Paradiso. Tukiwa sehemu ya tengenezo la Yehova, ni shangwe kubwa kama nini kuwaambia wengine kuhusu ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu! (2 Pet. 3:13) Andiko la Zaburi 37:11 linasema hivi: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” Watu “watajenga nyumba na kukaa ndani yake” nao watafurahia “kazi ya mikono yao wenyewe.” (Isa. 65:21, 22) Hakutakuwa tena na uonevu, umaskini, na njaa. (Zab. 72:13-16) Babiloni Mkubwa hatakuwapo tena ili kumdanganya mtu yeyote. (Ufu. 18:8, 21) Wafu watafufuliwa na kupewa nafasi ya kuishi milele. (Isa. 25:8; Mdo. 24:15) Mamilioni ya watu waliojiweka wakfu kwa Yehova wana tumaini lenye kusisimua kama nini! Ili sisi binafsi tufurahie ahadi hizo za Kimaandiko, ni lazima tuendelee kufanya maendeleo ya kiroho, tusonge mbele pamoja na tengenezo la Mungu, na kwenda sambamba nalo sikuzote.

Je, unajiona ukiwa katika Paradiso? (Tazama fungu la  16)

17. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuelekea ibada ya Yehova na tengenezo lake?

17 Mfumo huu unapokaribia mwisho wake, acheni tuendelee kuwa imara katika imani na kuthamini sana mpango wa Mungu wa ibada. Huo ndio mtazamo aliokuwa nao mtunga-zaburi Daudi aliyeimba hivi: “Nimemwomba Yehova jambo moja—ndilo nitakalolitafuta, kwamba nipate kukaa katika nyumba ya Yehova siku zote za maisha yangu, ili kuuona uzuri wa Yehova na kulitazama kwa uthamini hekalu lake.” (Zab. 27:4) Kila mmoja wetu na ashikamane na Mungu, asonge pamoja na watu wake, na kuendelea kusonga mbele pamoja na tengenezo la Yehova.