Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIMULIZI LA MAISHA

Yehova Amenisaidia Kwelikweli

Yehova Amenisaidia Kwelikweli

Baada ya arusi yetu, mimi na mke wangu Evelyn, tulisafiri kwa gari-moshi hadi mji wa Hornepayne katika eneo la mashambani huko kaskazini mwa Ontario, Kanada. Tulifika asubuhi na mapema, siku yenye baridi kali sana. Ndugu wa eneo hilo alikuja kutupokea na baada ya kufurahia kiamsha kinywa pamoja naye, mke wake, na mwana wao, tulitembea kwenye theluji tukihubiri nyumba kwa nyumba. Alasiri hiyo, nilitoa hotuba yangu ya kwanza ya watu wote nikiwa mwangalizi wa mzunguko. Tulikuwa watu watano tu katika mkutano huo.

KWA kweli, sikuhangaishwa na wazo la kwamba ni watu wachache tu waliosikiliza hotuba yangu katika mwaka huo wa 1957. Kwa kawaida mimi ni mtu mwenye haya sana. Nilipokuwa mtoto, nilijificha wageni walipotutembelea nyumbani, hata wale niliowafahamu.

Hata hivyo, huenda ukashangaa kujua kwamba migawo yangu mingi katika tengenezo la Yehova imenilazimu kuchangamana na watu wengi, yaani, rafiki zangu na watu nisiowafahamu. Lakini nimeendelea kupambana na hali ya kuwa na wasiwasi na kuona haya, hivyo siwezi kujisifu kuhusu migawo niliyoweza kutimiza. Badala yake, nimeona ukweli wa ahadi hii ya Yehova: “Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.” (Isa. 41:10) Njia moja kuu ambayo Yehova amenisaidia ni kupitia utegemezo wa Wakristo wenzangu. Acheni niwasimulie kuhusu baadhi yao, nitaanzia nilipokuwa mtoto.

ALITUMIA BIBLIA NA KITABU KIDOGO CHEUSI

Nikiwa kwenye shamba letu, kusini-magharibi mwa Ontario

Jumapili moja asubuhi yenye jua kali katika miaka ya 1940, Elsie Huntingford alitutembelea katika shamba letu, kusini-magharibi mwa Ontario. Mama alienda kuongea naye mlangoni na mimi na Baba,  aliyekuwa mwenye haya kama mimi, tulibaki ndani ya nyumba na kusikiliza. Akifikiri kwamba Dada Huntingford alikuwa muuzaji wa bidhaa, Baba alienda mlangoni kumwambia kwamba hatutaki chochote ili Mama asinunue tusichohitaji. Dada Huntingford aliuliza hivi: “Hamtaki kujifunza Biblia?” Baba akamjibu hivi: “Kama ni kujifunza Biblia, ni sawa.”

Dada Huntingford alitutembelea wakati unaofaa kabisa. Wazazi wangu walikuwa wafuasi wenye bidii wa kanisa la United Church of Canada lakini walikuwa wameamua kuacha kushirikiana na kanisa hilo. Kwa nini? Kwa sababu kasisi alibandika kwenye ukumbi wa kanisa orodha ya watu waliotoa michango kulingana na kiasi walichotoa. Kwa kawaida, wazazi wangu waliokuwa maskini walikuwa wa mwisho kwenye orodha hiyo, na makasisi waliwashinikiza kutoa pesa zaidi. Kasisi mmoja alikiri kwamba alifundisha mambo ambayo yeye mwenyewe hakuamini kwa sababu hakutaka kufutwa kazi. Hivyo, tuliacha kushirikiana na kanisa hilo lakini tuliendelea kutafuta njia ya kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho.

Kwa kuwa kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku nchini Kanada, Dada Huntingford alijifunza Biblia pamoja na familia yetu akitumia Biblia na habari alizoandika katika kitabu kidogo cheusi. Baadaye alipokuwa na uhakika kwamba hatuwezi kumsaliti kwa wenye mamlaka, alianza kutuletea machapisho ya Biblia. Tulificha kwa uangalifu machapisho hayo baada ya kila funzo. *

Wazazi wangu walihubiriwa katika huduma ya nyumba kwa nyumba na kubatizwa mwaka wa 1948

Licha ya upinzani na vizuizi vingine, Dada Huntingford alihubiri habari njema kwa bidii. Bidii yake ilinivutia na kunichochea kukubali kweli. Nilibatizwa ili kuonyesha wakfu wangu kwa Mungu mwaka mmoja baada ya wazazi wangu kubatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Nilibatizwa Februari 27, 1949, katika hori la chuma lililotumiwa kuwanywesha ng’ombe. Nilikuwa na umri wa miaka 17. Baada ya kubatizwa, niliazimia kuanza utumishi wa wakati wote.

YEHOVA ALINISAIDIA KUWA HODARI

Bila kutarajia, nilialikwa Betheli mwaka wa 1952

Nilisita kuanza upainia mara moja. Kwa kipindi fulani, nilifanya kazi kwenye benki na katika ofisi kwa sababu nilifikiri kwamba nilihitaji kutafuta pesa za kunitegemeza nikiwa painia. Hata hivyo,  nikiwa kijana asiye na uzoefu, nilitumia pesa zote nilizopata. Kwa hiyo, ndugu aliyeitwa Ted Sargent alinishauri niwe hodari na kuwa na imani katika Yehova. (1 Nya. 28:10) Shauri hilo la upole lilinichochea kuanza upainia mnamo Novemba 1951. Nilikuwa na dola 40 tu za Marekani, baiskeli ya zamani, na mkoba mpya. Lakini sikuzote Yehova alihakikisha kwamba nina kila kitu nilichohitaji. Ninashukuru kama nini kwamba Ted alinitia moyo kuanza utumishi wa upainia! Upainia uliniletea baraka nyingine nyingi.

Jioni moja mwishoni mwa mwezi wa Agosti 1952, nilipigiwa simu kutoka Toronto. Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Kanada ilinialika kuanza utumishi wa Betheli mwezi wa Septemba. Ingawa nilikuwa mwenye haya na sikuwahi kamwe kutembelea ofisi hiyo ya tawi, nilisisimuka kwa sababu mapainia wengine waliniambia mambo mazuri kuhusu Betheli. Mara moja nilipofika Betheli, nilijihisi nikiwa nyumbani.

“WAONYESHE AKINA NDUGU KWAMBA UNAWAJALI”

Miaka miwili baada ya kufika Betheli, nilichukua mahali pa Bill Yacos aliyekuwa mtumishi wa kutaniko (sasa anaitwa mratibu wa baraza la wazee) katika mojawapo ya makutaniko katika eneo la Shaw, jijini Toronto. Nikiwa na umri wa miaka 23 tu, nilijiona kuwa kijana wa mashambani asiye na uzoefu. Lakini Ndugu Yacos alinionyesha kwa fadhili na kwa upendo jambo la kufanya. Na Yehova alinisaidia kwelikweli.

Ndugu Yacos, mwanamume mwenye nguvu aliyetabasamu sikuzote, alipendezwa na watu. Aliwapenda akina ndugu, nao walimpenda pia. Aliwatembelea kwa ukawaida nyumbani, si wakati wa matatizo tu. Bill Yacos alinitia moyo kufanya vivyo hivyo na kuhubiri na ndugu na dada katika utumishi wa shambani. Alisema hivi: “Ken, waonyeshe akina ndugu kwamba unawajali. Hilo litafunika makosa mengi.”

MKE WANGU AONYESHA UPENDO MSHIKAMANIFU

Yehova amenisaidia kwa njia ya pekee tangu Januari 1957. Mwezi huo, nilimwoa Evelyn, mhitimu wa darasa la 14 la Shule ya Gileadi. Kabla sijamwoa, alitumika katika jimbo la Quebec, lenye watu wanaoongea Kifaransa. Wakati huo, Kanisa Katoliki ndiyo iliyokuwa dini kuu katika Quebec. Kwa hiyo, mgawo wa Evelyn ulikuwa mgumu sana, lakini aliendelea kuwa mshikamanifu kwa mgawo wake na kwa Yehova.

Nilimuoa Evelyn mwaka wa 1957

Evelyn ameshikamana nami pia. (Efe. 5:31) Kwa kweli, ushikamanifu wake ulijaribiwa mara tu tulipooana! Tulikuwa tumepanga kusafiri hadi Florida, Marekani, lakini siku moja baada ya harusi yetu, ofisi ya tawi iliniomba kuhudhuria mkutano uliochukua juma moja katika Betheli ya Kanada. Bila shaka, mkutano huo ulivuruga mipango yetu, lakini mimi na Evelyn tulitaka kufanya lolote ambalo Yehova alituomba tufanye. Hivyo, tukaahirisha fungate yetu. Juma hilo, Evelyn alihubiri katika eneo lililo karibu na ofisi ya tawi. Ingawa eneo hilo lilitofautiana sana na eneo la Quebec, alikuwa mvumilivu.

Mwishoni mwa juma hilo, bila kutarajia nilipokea mgawo wa kuwa mwangalizi wa mzunguko  kaskazini mwa Ontario. Nilikuwa nimetoka tu kuoa, nilikuwa na umri wa miaka 25 tu na sikuwa na uzoefu wowote, lakini tulienda kwenye mgawo wetu huku tukimtumaini Yehova. Wakati wa majira ya baridi kali nchini Kanada, tulisafiri usiku kucha kwa gari-moshi pamoja na waangalizi kadhaa wa mzunguko wenye uzoefu waliokuwa wakirudi kwenye migawo yao. Walitutia moyo sana! Hata ndugu mmoja alisisitiza kwamba tulale kwenye chumba alichokodi katika gari-moshi ili tusiketi usiku kucha kwenye viti. Asubuhi iliyofuata, siku 15 tu baada ya harusi yetu, tulitembelea kikundi kidogo huko Hornepayne, kama nilivyosimulia mwanzoni.

Mimi na Evelyn tulihitaji kufanya mabadiliko mengi sana. Tulipokuwa katika kazi ya wilaya mwishoni mwa mwaka wa 1960, nilipata mwaliko wa kuhudhuria darasa la 36 la Shule ya Gileadi. Mtaala huo wa miezi kumi ulipaswa kuanza mwanzoni mwa Februari 1961 huko Brooklyn, New York. Bila shaka, nilisisimka, lakini sikufurahi sana kwa kuwa Evelyn hakualikwa kuhudhuria shule hiyo. Badala yake, sawa na wake wa ndugu wengine walioalikwa, Evelyn aliombwa aandike barua kusema kwamba yuko tayari kuishi mbali nami kwa angalau miezi kumi. Evelyn alilia, lakini tukakubaliana nihudhurie, na alifurahi kwamba ningepata mazoezi muhimu nikiwa Gileadi.

Nilipokuwa shuleni, Evelyn alitumika katika ofisi ya tawi ya Kanada. Alipata pendeleo la pekee la kuishi katika chumba kimoja na Margaret Lovell, dada mpendwa mtiwa-mafuta. Ingawa hivyo, mimi na Evelyn tulitamani sana kuwa pamoja tena. Lakini kwa msaada wa Yehova, tuliendelea vizuri na migawo yetu ya muda. Niliguswa moyo sana nilipoona utayari wake wa kudhabihu wakati tuliopaswa kuwa pamoja ili tutumiwe zaidi na Yehova na tengenezo lake.

Baada ya kuwa katika Shule ya Gileadi kwa miezi mitatu hivi, Ndugu Nathan Knorr, aliyekuwa akisimamia kazi ya ulimwenguni pote, aliniambia jambo lisilo la kawaida. Aliniuliza ikiwa ninaweza kuacha Shule ya Gileadi na kurudi Kanada ili kutumika kwa muda nikiwa mwalimu wa Shule ya Huduma ya Ufalme kwenye ofisi ya tawi. Ndugu Knorr aliniambia kwamba si lazima nikubali mgawo huo. Ningemaliza mtaala wa Shule ya Gileadi ikiwa ningependa, kisha huenda ningepewa mgawo wa umishonari. Aliniambia pia kwamba nikiamua kurudi Kanada, huenda nisialikwe tena Gileadi, na huenda baadaye ningepewa tena mgawo katika utumishi wa shambani nchini Kanada. Aliniambia nizungumze na mke wangu kuhusu hilo na kufanya uamuzi.

Kwa kuwa tayari nilijua maoni ya Evelyn kuhusu migawo ya kitheokrasi, mara moja nilimwambia Ndugu Knorr hivi: “Jambo lolote ambalo tengenezo la Yehova linataka tufanye, tutafurahia kufanya.” Licha ya mapendezi yetu, kila mara tumehisi kwamba tunapaswa kwenda mahali popote ambapo tengenezo Yehova linatuambia twende.

Hivyo, mnamo Aprili 1961, nilitoka Brooklyn na kurudi Kanada ili kufundisha Shule ya Huduma ya Ufalme. Baadaye, tulianza kutumika tukiwa  Wanabetheli. Kisha, nilishangaa kupata mwaliko wa kuhudhuria darasa la 40 la Shule ya Gileadi, ambalo lingeanza mwaka wa 1965. Kwa mara nyingine, ilibidi Evelyn aandike barua ya kukubali kuishi mbali nami. Lakini majuma machache baadaye, tulifurahi sana Evelyn alipopokea mwaliko wa kuhudhuria shule hiyo pamoja nami.

Tulipofika kwenye Shule ya Gileadi, Ndugu Knorr alituambia kwamba wanafunzi watakaohudhuria madarasa ya lugha ya Kifaransa, kama sisi, watatumwa barani Afrika. Hata hivyo, tulipohitimu, tulipokea mgawo wa kurudi Kanada! Niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi mpya wa ofisi hiyo ya tawi (sasa anaitwa mratibu wa Halmashauri ya Tawi). Kwa sababu nilikuwa na umri wa miaka 34 tu, nilimkumbusha Ndugu Knorr hivi: “Nina umri mdogo sana.” Lakini alinitia moyo. Na tangu mwanzoni, nilijitahidi kutafuta ushauri wa ndugu wa Betheli wenye umri mkubwa zaidi na walio na uzoefu zaidi kabla ya kufanya maamuzi yoyote mazito.

BETHELI—MAHALI PA KUJIFUNZA NA KUWAFUNDISHA WENGINE

Utumishi wa Betheli umenipa fursa nzuri sana za kujifunza kutoka kwa wengine. Ninawaheshimu na kuwapenda sana washiriki wenzangu wa Halmashauri ya Tawi. Nimechochewa na mifano mizuri ya mamia ya ndugu na dada Wakristo, wadogo kwa wakubwa, ambao tumetumika nao kwenye ofisi hii na katika makutaniko mbalimbali.

Nikiongoza ibada ya asubuhi katika Betheli ya Kanada

Pia, utumishi wa Betheli umenipa fursa ya kuwafundisha wengine na kuimarisha imani yao. Mtume Paulo alimwambia hivi Timotheo: “Endelea katika mambo uliyojifunza.” Alisema hivi pia: “Mambo uliyoyasikia kutoka kwangu kwa uthibitisho wa mashahidi wengi, mambo hayo uwakabidhi watu waaminifu, ambao nao watakuwa na sifa za kustahili vya kutosha kufundisha wengine.” (2 Tim. 2:2; 3:14) Nyakati nyingine, Wakristo wenzangu huniuliza mambo ambayo nimejifunza kwa miaka 57 hivi ya utumishi wangu wa Betheli. Mimi huwajibu hivi: “Fanya kwa hiari na upesi jambo lolote ambalo tengenezo la Yehova linataka ufanye, ukimtegemea kabisa Yehova akusaidie.”

Ninahisi ni kana kwamba nilifika Betheli juzi tu nikiwa kijana mwenye haya na asiye na uzoefu. Hata hivyo, kwa miaka yote hiyo, Yehova ‘ameushika mkono wangu wa kuume.’ Yehova anaendelea kunihakikishia hivi hasa kupitia fadhili na msaada wa wakati unaofaa wa waamini wenzangu: “Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.”—Isa. 41:13.

^ fu. 10 Katika Mei 22, 1945, serikali ya kanada iliondoa marufuku ya kazi yetu.