Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Mungu Mwenye Utaratibu

Yehova Ni Mungu Mwenye Utaratibu

“Mungu si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.”1 KOR. 14:33.

1, 2. (a) Mungu alimuumba nani kwanza, na Yehova alimtumiaje? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba malaika wamepangwa vizuri?

YEHOVA, Muumba wa ulimwengu hufanya mambo kwa njia ya utaratibu. Alimuumba kwanza Mwana wake mzaliwa-pekee wa roho. Mwana huyo anaitwa “Neno” kwa sababu ni msemaji mkuu wa Mungu. Neno amekuwa akimtumikia Yehova kwa miaka mingi sana kwa kuwa Biblia inasema hivi: “Hapo mwanzo Neno alikuwako, na Neno alikuwa pamoja na Mungu.” Tunaambiwa hivi pia: “Vitu vyote vilikuja kuwako kupitia kwake [Neno], na bila yeye hakuna hata kitu kimoja kilichokuja kuwako.” Mungu alimtuma Neno duniani miaka zaidi ya 2,000 iliyopita. Akiwa mwanadamu mkamilifu, Yesu Kristo alifanya mapenzi ya Baba yake kwa uaminifu.—Yoh. 1:1-3, 14.

2 Kabla ya kuwa mwanadamu, Mwana wa Mungu alimtumikia Mungu kwa ushikamanifu akiwa ‘stadi Wake wa kazi.’ (Met. 8:30) Kupitia yeye, Yehova aliumba mamilioni ya viumbe wengine wa roho mbinguni. (Kol. 1:16) Simulizi moja la Biblia linasema hivi kuhusu malaika hao: “Kulikuwa na maelfu elfu walioendelea kumtumikia [Yehova], na elfu kumi mara elfu kumi walioendelea kusimama mbele zake.” (Dan. 7:10) Viumbe hao wengi  sana wa roho wanarejelewa kuwa “majeshi” ya Yehova yaliyopangwa vizuri.—Zab. 103:21.

3. Kuna nyota na sayari nyingi kadiri gani, na zimepangwaje?

3 Namna gani vitu vilivyoumbwa, kama vile sayari na nyota zisizohesabika? Gazeti moja (Chronicle) la Houston, Texas, linasema kwamba uchunguzi wa hivi karibuni unadokeza kwamba idadi ya nyota ni mara tatu zaidi ya walivyofikiri, yaani, kuna “nyota trilioni 3 mara bilioni 100.” Ripoti hiyo inaongezea hivi: “Yaani, 3 ikifuatwa na sifuri 23.” Nyota zimepangwa katika makundi yenye mabilioni ya nyota au hata matrilioni ya nyota pamoja na sayari nyingi. Makundi hayo yamepangwa katika makundi mengine makubwa zaidi.

4. Kwa nini ni jambo linalopatana na akili kufikia mkataa kwamba watumishi wa Mungu duniani wangepangwa kitengenezo?

4 Sawa na viumbe waadilifu wa roho walio mbinguni, mbingu halisi zimepangwa kwa utaratibu wa hali ya juu sana. (Isa. 40:26) Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kufikia mkataa kwamba Yehova angewapanga kitengenezo watumishi wake duniani. Anataka wadumishe utaratibu mzuri, na hilo ni jambo muhimu sana kwa sababu wana kazi nyingi muhimu za kufanya. Mifano mizuri sana ya waabudu wa Yehova waliomtumikia kwa uaminifu katika nyakati za zamani na leo, inathibitisha wazi kwamba amekuwa pamoja nao, naye si “Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.”—Soma 1 Wakorintho 14:33, 40.

MUNGU ALIWAPANGA KITENGENEZO WATU WAKE KATIKA NYAKATI ZA ZAMANI

5. Utaratibu wa familia ya wanadamu kuijaza dunia ulisitishwa jinsi gani?

5 Yehova alipowaumba wanadamu wa kwanza, aliwaambia hivi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha, na mtawale samaki wa baharini na viumbe vinavyoruka vya mbinguni na kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia.” (Mwa. 1:28) Familia ya wanadamu ilipaswa kukua kwa utaratibu ili ijaze dunia na kupanua Paradiso duniani pote. Kutekelezwa kwa utaratibu huo kulisitishwa kwa muda Adamu na Hawa walipokosa kutii. (Mwa. 3:1-6) Baada ya muda, “Yehova akaona kuwa ubaya wa mwanadamu ulikuwa mwingi duniani na kila mwelekeo wa fikira za moyo wake ulikuwa mbaya tu wakati wote.” Hivyo, “dunia ikaharibika machoni pa Mungu wa kweli, dunia ikajaa jeuri.” Basi, Mungu akakusudia kuleta gharika ambayo ingewaangamiza watu wasiomwogopa duniani pote.—Mwa. 6:5, 11-13, 17.

6, 7. (a) Kwa nini Noa alipata kibali machoni pa Yehova? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 21.) (b) Ilikuwaje kwa watu wote wasio na imani katika siku za Noa?

6 Hata hivyo, ‘Noa alipata kibali machoni pa Yehova’ kwa sababu “alikuwa mtu mwadilifu” ambaye “alionekana kuwa mtu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake.” Kwa sababu “Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli,” Yehova alimwagiza ajenge safina kubwa. (Mwa. 6:8, 9, 14-16) Safina hiyo ilijengwa kwa njia inayofaa ili kuhifadhi uhai wa wanadamu na wanyama. Kwa utii, “Noa akafanya kulingana na yote ambayo Yehova alikuwa amemwamuru,” naye akakamilisha ujenzi huo kwa njia ya utaratibu akishirikiana na familia yake. Baada ya viumbe kuingizwa ndani ya safina, “Yehova akafunga mlango.”—Mwa. 7:5, 16.

7 Gharika ilipokuja mwaka wa 2370 K.W.K., Yehova “akafutilia mbali kila kitu kilicho hai ambacho kilikuwa juu ya uso wa nchi,” lakini akamhifadhi Noa aliyekuwa mwaminifu pamoja na familia yake ndani ya safina. (Mwa. 7:23) Leo, kila mtu duniani ni mzao wa Noa, wanawe, na wake zao. Lakini watu wote wasio na imani waliokuwa nje ya safina walikufa kwa sababu walikataa kumsikiliza Noa, “mhubiri wa uadilifu.”—2 Pet. 2:5.

Utaratibu mzuri uliwasaidia watu wanane kuokoka Gharika (Tazama fungu la 6, 7)

8. Mungu alipowaagiza watu wake waingie katika Nchi ya Ahadi, ni nini kinachothibitisha kwamba kulikuwa na utaratibu mzuri wa kitengenezo katika taifa hilo?

 8 Zaidi ya karne nane baada ya Gharika, Mungu alilipanga kitengenezo taifa la Israeli. Maisha yao yote na hasa ibada yao ingefuata utaratibu mzuri. Kwa mfano, taifa hilo lilikuwa na makuhani na Walawi wengi na vilevile kulikuwa na “wanawake ambao walifanya utumishi uliopangwa kwenye mwingilio wa hema la mkutano.” (Kut. 38:8) Hata hivyo, Yehova Mungu alipowaagiza Waisraeli waingie katika nchi ya Kanaani, watu wa kizazi hicho waliasi. Yehova akawaambia hivi: “Nanyi hamtaingia katika nchi ambayo niliinua mkono wangu katika kiapo ya kwamba nitakaa pamoja nanyi, isipokuwa Kalebu mwana wa Yefune na Yoshua mwana wa Nuni” kwa sababu walileta habari nzuri baada ya kuipeleleza Nchi ya Ahadi. (Hes. 14:30, 37, 38) Kulingana na mwongozo wa Mungu, baadaye Musa alimweka rasmi Yoshua awe mrithi wake. (Hes. 27:18-23) Yoshua alipokuwa karibu kuwaongoza Waisraeli kuingia Kanaani, aliambiwa hivi: “Uwe hodari na mwenye nguvu. Usitetemeke wala usiwe na hofu, kwa maana Yehova Mungu wako yupo pamoja nawe kila mahali unapoenda.”—Yos. 1:9.

9. Rahabu alihisije kumhusu Yehova na watu Wake?

9 Kwa kweli, Yehova Mungu alikuwa pamoja na Yoshua mahali popote alipoenda. Kwa mfano, fikiria kilichotukia Waisraeli walipopiga kambi karibu na jiji la Wakanaani la Yeriko. Mwaka wa 1473 K.W.K., Yoshua aliwatuma wanaume wawili kupeleleza jiji la Yeriko ambamo walimkuta kahaba aliyeitwa Rahabu. Aliwaficha darini katika nyumba yake ili wasikamatwe na watu waliotumwa na mfalme wa Yeriko. Rahabu aliwaambia hivi wapelelezi hao Waisraeli: “Najua hakika ya kwamba Yehova atawapa nchi hii . . . , kwa maana tumesikia jinsi ambavyo Yehova aliyakausha maji ya Bahari Nyekundu mbele yenu . . . na yale mliyowatendea wale wafalme wawili wa Waamori.” Akaongezea hivi: “Yehova Mungu wenu ni Mungu juu mbinguni na chini duniani.” (Yos. 2:9-11)  Waisraeli waliposhinda Yeriko, Mungu alihakikisha kwamba Rahabu na familia yake wanaokolewa kwa sababu alijiunga na tengenezo la Mungu wakati huo. (Yos. 6:25) Rahabu alionyesha imani, alimhofu Yehova, na kuwaheshimu watu Wake.

TENGENEZO LENYE BIDII KATIKA KARNE YA KWANZA

10. Yesu aliwaambia nini viongozi wa dini ya Kiyahudi katika siku zake, na kwa nini alisema hivyo?

10 Chini ya uongozi wa Yoshua, Waisraeli walishinda jiji baada ya jiji na hatimaye kuimiliki nchi ya Kanaani. Lakini ni nini kilichotukia baadaye? Kwa karne nyingi, Waisraeli waliasi sheria za Mungu tena na tena. Yehova alipomtuma duniani Mwana wake, hali ya Waisraeli ya kutomtii Mungu na kutowasikiliza manabii wake ilikuwa mbaya sana hivi kwamba Yesu aliliita Yerusalemu “muuaji wa manabii.” (Soma Mathayo 23:37, 38.) Mungu aliwakataa viongozi wa dini ya Kiyahudi kwa sababu hawakuwa waaminifu kwake. Hivyo, Yesu aliwaambia hivi: “Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa taifa lenye kuzaa matunda yake.”—Mt. 21:43.

11, 12. (a) Ni nini kinachothibitisha kwamba Yehova alianza kutumia tengenezo lingine katika karne ya kwanza badala ya taifa la Wayahudi? (b) Tengenezo jipya lenye kibali cha Mungu lilitia ndani nani?

11 Katika karne ya kwanza W.K., Yehova alikataa kabisa taifa la Israeli lililokosa uaminifu. Hata hivyo, haikumaanisha kwamba hangekuwa na tengenezo la watumishi washikamanifu duniani. Yehova alianza kutumia tengenezo jipya lenye bidii ambalo msingi wake ulikuwa Yesu Kristo na mafundisho yake. Lilianzishwa siku ya Pentekoste ya 33 W.K. Wakati huo, wanafunzi wapatao 120 wa Yesu walikusanyika huko Yerusalemu ambapo kwa ‘ghafula kulitokea kutoka mbinguni kelele kama ile ya upepo wenye nguvu unaovuma, nao ukaijaza nyumba yote.’ Kisha “wakaona ndimi kama za moto, nazo zikagawanyika huku na huku, na mmoja ukaketi juu ya kila mmoja wao, nao wote wakajazwa roho takatifu wakaanza kusema katika lugha tofauti, kama vile roho ilivyokuwa ikiwawezesha kusema.” (Mdo. 2:1-4) Tukio hilo la kustaajabisha lilithibitisha wazi kwamba Yehova alikuwa akilitegemeza tengenezo hilo jipya la wanafunzi wa Kristo.

12 Katika siku hiyo yenye kusisimua, “nafsi karibu elfu tatu zikaongezwa” kwenye idadi ya wafuasi wa Yesu. Zaidi ya hayo, “Yehova akaendelea kuongezea kwao kila siku wale waliokuwa wakiokolewa.” (Mdo. 2:41, 47) Wahubiri hao wa karne ya kwanza walikuwa na matokeo mazuri sana hivi kwamba “neno la Mungu likaendelea kukua, na hesabu ya wanafunzi ikazidi kuongezeka sana katika Yerusalemu.” Hata “umati mkubwa wa makuhani ukaanza kuitii imani.” (Mdo. 6:7) Hivyo, watu wengi wanyoofu wakakubali kweli zilizotangazwa na washiriki wa tengenezo hilo jipya. Baadaye, Yehova alithibitisha kwamba alikuwa akilitegemeza pia kutaniko la Kikristo alipoanza kuwaleta “watu wa mataifa” katika kutaniko hilo.—Soma Matendo 10:44, 45.

13. Tengenezo jipya la Mungu lilikuwa na kazi gani?

13 Hapakuwa na shaka kuhusu kazi ambayo Mungu aliwapa wafuasi wa Kristo. Yesu mwenyewe aliwawekea kielelezo kwa sababu baada ya kubatizwa, alianza kuhubiri kuhusu “ufalme wa mbinguni.” (Mt. 4:17) Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kufanya kazi hiyohiyo. Aliwaambia hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Bila shaka, wafuasi wa mapema wa Kristo walielewa mambo waliyopaswa kutimiza. Kwa mfano, huko Antiokia katika eneo la Pisidia, Paulo na Barnaba waliwaambia  hivi kwa ujasiri Wayahudi wapinzani: “Ilikuwa lazima neno la Mungu lihubiriwe kwenu kwanza. Kwa kuwa mnalisukumia mbali kutoka kwenu na hamjioni kuwa mnastahili uzima wa milele, tazameni! tunawageukia mataifa. Kwa kweli, Yehova ameweka amri juu yetu kwa maneno haya, ‘Nimewaweka ninyi kuwa nuru ya mataifa, ili muwe wokovu mpaka sehemu ya mwisho ya dunia.’” (Mdo. 13:14, 45-47) Kuanzia karne ya kwanza, sehemu ya kidunia ya tengenezo la Mungu imekuwa ikitangaza kuhusu uandalizi wake wa wokovu.

WENGI WAANGAMIA, LAKINI WATUMISHI WA MUNGU WAOKOKA

14. Jiji la Yerusalemu lilipatwa na nini katika karne ya kwanza, lakini ni nani waliookoka?

14 Wayahudi kwa ujumla hawakukubali habari njema, na wangepatwa na msiba kwa sababu Yesu alikuwa amewaonya hivi wanafunzi wake: “Mtakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwake kumekaribia. Ndipo wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani, na wale walio katikati yake na waondoke, nao wale walio katika sehemu za mashambani wasiingie ndani.” (Luka 21:20, 21) Mambo aliyotabiri Yesu yalitukia. Katika mwaka wa 66 W.K., majeshi ya Roma yakiongozwa na Sesho Galo yalizingira Yerusalemu baada ya uasi wa Wayahudi. Hata hivyo, kwa ghafla majeshi hayo yaliondoka na hivyo wafuasi wa Yesu wakapata nafasi ya kuondoka Yerusalemu na Yudea. Mwanahistoria Eusebio anasema kwamba wengi walivuka Mto Yordani na kukimbilia Pela huko Perea. Katika mwaka wa 70 W.K., majeshi ya Roma yakiongozwa na Jenerali Tito yalirudi na kuharibu kabisa Yerusalemu. Hata hivyo, Wakristo waaminifu waliokoka kwa sababu walitii onyo la Yesu.

15. Ukristo ulisitawi licha ya nini?

15 Licha ya kwamba wafuasi wa Kristo walikabili magumu, mateso, na majaribu mengine ya imani, Ukristo ulisitawi katika karne ya kwanza. (Mdo. 11:19-21; 19:1, 19, 20) Wakristo hao wa mapema walisitawi kiroho kwa sababu Mungu aliwabariki.—Met. 10:22.

16. Kila Mkristo alipaswa kufanya nini ili aendelee vyema kiroho?

16 Kila Mkristo alipaswa kujitahidi kibinafsi ili aendelee vyema kiroho. Kujifunza Maandiko kwa bidii, kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya ibada, na kuhubiri kwa bidii kuhusu Ufalme yalikuwa mambo muhimu. Utendaji huo uliwasaidia watu wa Yehova wakati huo kuwa na afya nzuri ya kiroho na umoja, kama ilivyo leo. Wale walioshirikiana na makutaniko ya karne ya kwanza yaliyopangwa vizuri kitengenezo, walinufaika sana kwa sababu waangalizi na watumishi wa huduma walijitahidi kwa hiari kuwasaidia. (Flp. 1:1; 1 Pet. 5:1-4) Ni wazi kwamba makutaniko yalifurahi sana yalipotembelewa na wazee wanaosafiri, kama Paulo. (Mdo. 15:36, 40, 41) Kuna ulinganifu mkubwa kati ya ibada yetu na ibada ya Wakristo katika karne ya kwanza. Tunashukuru kama nini kwamba Yehova aliwapanga watumishi wake kitengenezo wakati huo na amefanya hivyo leo pia! *

17. Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

17 Ulimwengu wa Shetani unapokaribia mwisho wake katika siku hizi za mwisho, sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova la ulimwenguni pote inasonga mbele kwa kasi hata zaidi. Je, unasonga mbele pamoja na sehemu hiyo? Je, unafanya maendeleo ya kiroho? Makala inayofuata itaonyesha jinsi unavyoweza kufanya hivyo.

^ fu. 16 Tazama makala zenye kichwa “Wakristo Huabudu kwa Roho na Kweli” na “Wanaendelea Kutembea Katika Kweli” katika Mnara wa Mlinzi, Julai 15, 2002. Habari zenye kina kuhusu sehemu ya kidunia ya tengenezo la Mungu zimechapishwa katika kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu.