Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Lainisha Mapito ya Mguu Wako” Ili Ufanye Maendeleo

“Lainisha Mapito ya Mguu Wako” Ili Ufanye Maendeleo

WATU wa Mungu walipoondoka Babiloni mwaka wa 537 K.W.K., Yehova alipendezwa na njia waliyotumia kurudi Yerusalemu. Aliwaambia hivi: “Fungueni njia ya watu. Fanyeni matuta, fanyeni matuta kwa ajili ya njia kuu. Ondoeni mawe juu yake.” (Isa. 62:10) Wazia jinsi Wayahudi walivyotii agizo hilo. Huenda wale waliotangulia waliitengeneza barabara hiyo, labda kwa kufunika mashimo na kuondoa mawe. Kufanya hivyo kungewasaidia ndugu zao waliokuwa nyuma yao.

Sisi pia tunapaswa kulainisha njia yetu ili kufikia miradi ya kiroho. Yehova anataka watumishi wake wote watembee kwenye njia hiyo bila vizuizi vyovyote visivyo vya lazima. Neno lake linatuhimiza hivi: “Lainisha mapito ya mguu wako, nazo njia zako zote na zifanywe imara.” (Met. 4:26) Iwe wewe ni kijana au una umri wa makamo, unaweza kuona hekima ya kutumia shauri hilo linalotoka kwa Mungu.

TAYARISHA NJIA KWA KUFANYA MAAMUZI MAZURI

Huenda umesikia watu wakisema hivi kuhusu kijana fulani: ‘Ana fursa nzuri sana ya kufanikiwa,’ au, ‘Atafika mbali.’ Kwa ujumla, vijana wana afya nzuri, wanajifunza mambo haraka, na wanatamani sana kufanikiwa maishani. Ndiyo sababu Biblia inasema hivi: “Uzuri wa vijana ni nguvu zao.” (Met. 20:29) Kijana anayetumia vipaji na nguvu zake kumtumikia Yehova anaweza kufikia miradi ya kiroho na kupata furaha ya kweli.

Hata hivyo, kama ujuavyo, ulimwengu unataka sana kutumia uwezo wa vijana wetu. Kijana Shahidi anapofanya vizuri shuleni, huenda mshauri, mwalimu, au mwanafunzi mwenzake akamshinikiza kufuatilia elimu ya juu ili afanikiwe katika mfumo huu wa mambo. Ndugu au dada kijana mwenye uwezo wa kuwa mwanariadha anaweza kushawishiwa kufuatilia michezo maishani. Je,  umekabili hali kama hiyo, au unajua mtu fulani anayekabili mkazo kama huo? Ni nini kitakachomsaidia Mkristo kufanya uamuzi wa hekima?

Mafundisho ya Biblia yanaweza kumsaidia mtu ajitayarishe kutembea kwenye njia bora zaidi maishani. Andiko la Mhubiri 12:1 linasema hivi: “Mkumbuke, sasa, Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.” Wewe au rafiki yako kijana mnawezaje ‘kumkumbuka Muumba wenu Mkuu’ kwa njia bora zaidi?

Mfikirie Eric * kutoka Afrika Magharibi. Alipenda kucheza mpira wa miguu. Alianza kuchezea timu ya taifa akiwa na umri wa miaka 15. Punde si punde, angepata mazoezi ya pekee ya kucheza mpira barani Ulaya, na huenda baadaye angekuwa mchezaji wa kulipwa. Lakini shauri la ‘kumkumbuka Muumba wake Mkuu’ lingemsaidiaje? Wewe na rafiki zako vijana mnaweza kujifunza nini?

Eric alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova alipokuwa shuleni. Alijifunza kwamba Muumba wake ataondoa kabisa matatizo ya wanadamu. Eric alijifunza kwamba ni muhimu kutumia wakati na nguvu zake kufanya mapenzi ya Mungu. Kwa msingi wa hekima hiyo, Eric alichagua kutokuwa mwanamichezo wa kulipwa. Badala yake, alibatizwa na kujitahidi kufanya maendeleo ya kiroho. Baadaye, akawa mtumishi wa huduma na kisha akaalikwa kuhudhuria Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja.

Huenda Eric angetajirika na kuwa mashuhuri ikiwa angefuatilia michezo. Lakini alitambua ukweli wa kanuni hii ya Biblia: “Vitu vyenye thamani vya tajiri ni mji wake wenye nguvu, navyo ni kama ukuta wa ulinzi katika mawazo yake.” (Met. 18:11) Kwa kweli, mtu anajidanganya anapofikiri kwamba utajiri unaweza kumlinda. Isitoshe, wale wanaofuatilia utajiri kwa bidii mara nyingi ‘hujichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.’—1 Tim. 6:9, 10.

Inapendeza kwamba vijana wengi wamepata shangwe na usalama wa kudumu kwa kufanya utumishi wa wakati wote. Eric anasema hivi: “Nimejiunga na ‘timu’ kubwa ya watumishi wa Yehova wa wakati wote. Hiyo ndiyo timu bora zaidi, na ninamshukuru Yehova kwa kunionyesha njia pekee ya kupata furaha ya kweli na mafanikio maishani.”

Namna gani wewe? Badala ya kufuatilia miradi ya kilimwengu, kwa nini usiimarishe “njia zako” mbele za Yehova kwa kutumika ukiwa painia?—Tazama sanduku lenye kichwa “ Kupata Manufaa Yasiyopatikana Chuo Kikuu.”

KUONDOA VIZUIZI NJIANI

Wenzi fulani wa ndoa walipotembelea ofisi ya tawi ya Marekani waliona kwamba Wanabetheli walimtumikia Yehova kwa furaha. Dada aliandika hivi baadaye: “Tuliridhika sana na maisha yetu.” Wenzi hao waliamua kutumia wakati na nguvu zao kufanya mengi zaidi katika utumishi.

Mwanzoni, walihisi kwamba hawawezi kufanya mabadiliko yaliyohitajika. Lakini siku moja, walitafakari andiko la siku lililozungumzia maneno ya Yesu katika Yohana 8:31, linalosema hivi: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu.” Hivyo, wakaamua hivi: “Manufaa tunayopata tunaporahisisha maisha yetu yanastahili dhabihu hiyo.” Waliuza nyumba yao kubwa na vitu wasivyohitaji na kuhamia kutaniko lililohitaji msaada. Sasa, wanafanya upainia, na pia wanasaidia katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme na kujitolea katika makusanyiko ya wilaya. Wanahisije? “Kuishi maisha rahisi zaidi kumetuletea shangwe nyingi sana kwa sababu tunafanya kile ambacho tengenezo la Yehova linatuhimiza kufanya.”

ENDELEA KUFANYA MAENDELEO YA KIROHO

Sulemani aliandika hivi: “Macho yako yatazame mbele moja kwa moja, naam, macho yako yenye kung’aa yanapaswa kutazama mbele yako moja kwa moja.” (Met. 4:25) Kama dereva anayekazia fikira barabara, tunapaswa kuepuka mambo yanayoweza kutukengeusha na kutuzuia kuweka na kufikia miradi ya kiroho.

Unaweza kuweka na kufikia miradi gani ya kiroho? Bila shaka, kuwa mtumishi wa wakati wote ni mradi mzuri. Unaweza pia kuhamia kutaniko la karibu linalohitaji wahubiri wenye uzoefu ili kuhubiri  eneo lake kubwa. Au huenda kutaniko lina wahubiri wengi wenye uzoefu lakini halina wazee na watumishi wa huduma wa kutosha. Je, unaweza kusaidia katika mojawapo ya njia hizo? Kwa nini usizungumze na mwangalizi wa mzunguko ili akueleze jinsi unavyoweza kusaidia? Ikiwa unataka kuhamia eneo la mbali zaidi, unaweza kuomba habari kuhusu makutaniko ya mbali yanayohitaji msaada. *

Acheni tufikirie tena Isaya 62:10. Huenda baadhi ya Wayahudi walifanya kazi ngumu ya kulima na kutengeneza njia ili watu wa Mungu wafike Yerusalemu. Ikiwa unajitahidi kabisa kufikia miradi fulani katika utumishi mtakatifu, usife moyo. Kwa msaada wa Mungu, wewe pia unaweza kufikia miradi hiyo. Endelea kumwomba Yehova akupe hekima unapojitahidi kuondoa vizuizi kwenye njia yako. Kwa wakati unaofaa, inaelekea kwamba utaona Yehova akikusaidia ‘kulainisha mapito ya mguu wako.’—Met. 4:26.

^ fu. 8 Jina limebadilishwa.

^ fu. 18 Tazama kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova, ukurasa wa 111 hadi 112.