Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasaidie Waamini Wenzako Waliotalikiana—Jinsi Gani?

Wasaidie Waamini Wenzako Waliotalikiana—Jinsi Gani?

Inaelekea kwamba unamjua mtu au watu kadhaa waliotalikiana na wenzi wao kwa sababu wengi wanatalikiana. Kwa mfano, utafiti uliofanywa nchini Poland ulionyesha kwamba kuna uwezekano mkubwa wa wenzi wenye umri wa miaka 30 waliooana kwa miaka mitatu hadi sita kutalikiana, na si watu wenye umri huo tu wanaotalikiana.

Kwa kweli, Taasisi ya Sera za Familia nchini Hispania inaripoti hivi: “Takwimu zinaonyesha kwamba [katika Ulaya] nusu ya idadi ya watu wanaofunga ndoa watatalikiana.” Ndivyo ilivyo katika nchi nyingine zilizoendelea.

KULEMEWA NA HISIA ZINAZOBADILIKA

Ni nini kinachosababisha hali hiyo ya kawaida? Mshauri mmoja wa ndoa mwenye uzoefu kutoka Ulaya Mashariki alisema hivi: “Wenzi wanaotalikiana huwa tayari hawana uhusiano mzuri na wameachana, jambo linalosababisha maumivu makali ya kihisia.” Aliongezea hivi: ‘Mara nyingi watu waliotalikiana huwa na hisia kali zenye nguvu kama vile hasira, majuto, kuvunjika moyo, kukata tamaa, na aibu.’ Nyakati nyingine hisia hizo humfanya mtu atake kujiua. Mshauri huyo aliendelea kusema hivi: “Watu wanapotalikiana kwa njia rasmi kortini, kipindi kingine cha hisia huanza. Kwa sababu ya kuhisi kwamba ametengwa na hafai, huenda mtu aliyetalikiana na mwenzi wake akajiuliza hivi: ‘Sasa kwa kuwa nimetalikiana na mwenzi wangu, mimi ni nani hasa? Nina kusudi gani maishani?’”

Akikumbuka jinsi alivyohisi miaka kadhaa iliyopita, Ewa anasema hivi: “Baada ya kutalikiana na mume wangu, niliaibika sana hasa majirani na wafanyakazi wenzangu waliponiita ‘mtalikiwa.’ Nilikasirika sana. Kwa kuwa nilibaki na watoto wawili wadogo, nililazimika kuwa mama na baba.” * Adam, aliyetumika kwa miaka 12 akiwa mzee wa kutaniko mwenye kuheshimika, anasema hivi: “Ninahisi sifai hata kidogo. Nyakati nyingine ninakasirika sana na kushawishika kujitenga na watu wote.”

PAMBANO LA KUPATA TENA USAWAZIKO

Kwa sababu ya kulemewa na mahangaiko kuhusu wakati wao ujao, wengine wangali wanapambana ili kupata tena usawaziko, miaka mingi baada ya talaka. Huenda wakafikiri kwamba wengine hawapendezwi nao. Zaidi ya hilo, mwandishi mmoja wa masuala ya talaka anasema kwamba wanapaswa “kubadilika na kujifunza kukabiliana na matatizo wakiwa peke yao.”

Stanisław anakumbuka hivi: “Tulipotalikiana, aliyekuwa mke wangu alinizuia kuwatembelea binti zangu wawili wadogo. Nilihisi kwamba hakuna aliyenijali tena na hata Yehova alikuwa ameniacha. Nilitamani kufa. Baada ya muda, nilitambua  kwamba nilikosea katika kufikiri kwangu.” Wanda, mwanamke aliyetalikiwa, alihangaikia pia wakati wake ujao. Anasema hivi: “Nilikuwa na hakika kwamba baada ya muda, watu, kutia ndani waamini wenzangu, hawatanijali wala kuwajali hata kidogo watoto wangu. Hata hivyo, sasa ninaona jinsi akina ndugu walivyotujali na kunisaidia nilipokuwa nikijitahidi kuwalea watoto wangu ili wawe waabudu wa Yehova.”

Maelezo hayo yanaonyesha kwamba watu fulani hulemewa na hisia zisizofaa baada ya talaka. Huenda wakajiona hawafai na kufikiri hawana thamani wala hawastahili ufikirio. Na huenda pia wakaanza kuwachambua-chambua wale walio karibu nao. Hivyo, wanaweza kufikiri kwamba kutaniko haliwajali na halina huruma. Hata hivyo, visa kama vya Stanisław na Wanda vinaonyesha kwamba waliotalikiana huenda wakatambua baadaye kuwa ndugu na dada zao wanawajali kikweli. Kwa kweli, Wakristo wenzao wamekuwa wakiwajali kwa njia ya pekee, hata ikiwa mwanzoni hawakutambua hilo.

HISIA ZA UPWEKE NA ZA KUTOPENDWA ZINAPOANZA

Kumbuka kwamba hata tukijitahidi kadiri gani, huenda waamini wenzetu waliotalikiana wakahisi upweke mara kwa mara. Hasa akina dada waliotalikiana na wenzi wao wanaweza kuhisi kwamba ni watu wachache tu wanaowajali. Alicja anakiri hivi: “Miaka minane imepita tangu nilipotalikiana na mume wangu. Lakini nyakati nyingine bado ninahisi kwamba sifai. Nyakati hizo, mimi hujitenga na watu, hulia sana na kujihurumia.”

Ingawa ni kawaida kwa mtu aliyetalikiana na mwenzi wake kuhisi hivyo, Biblia hutushauri tusijitenge na wengine. Mtu asiyefuata shauri hilo huenda akakataa “hekima yote inayotumika.” (Met. 18:1) Hata hivyo, mtu anayehisi upweke anapaswa kuelewa kwamba ni hekima inayotumika kuepuka kutafuta tena na tena mashauri au faraja kutoka kwa mtu wa jinsia tofauti. Kwa njia hiyo, hawatashawishiwa kusitawisha hisia zisizofaa za kimahaba.

Waamini wenzetu waliotalikiana wanaweza kulemewa na hisia mbalimbali, kama vile mahangaiko kuhusu wakati ujao na hisia za upweke au kutopendwa. Tukitambua kwamba ni kawaida kwa wale waliotalikiana kuhisi hivyo na ni vigumu kushinda hisia hizo, tunapaswa kumwiga Yehova kwa kuwategemeza kwa ushikamanifu ndugu na dada hao. (Zab. 55:22; 1 Pet. 5:6, 7) Tunaweza kuwa na hakika kwamba watathamini sana msaada wowote tunaowapa. Kwa kweli, watasaidiwa na marafiki wa kweli kutanikoni.Met. 17:17; 18:24.

^ fu. 6 Baadhi ya majina yamebadilishwa.