Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Una Maoni Kama ya Yehova Kuhusu Udhaifu wa Kibinadamu?

Je, Una Maoni Kama ya Yehova Kuhusu Udhaifu wa Kibinadamu?

Viungo vya mwili vinavyoonekana kuwa dhaifu zaidi ni vya lazima.”1 KOR. 12:22.

1, 2. Kwa nini Paulo aliwahurumia walio dhaifu?

SOTE huhisi tukiwa dhaifu nyakati nyingine. Huenda magonjwa yakatudhoofisha na kutufanya tushindwe kuendelea na shughuli zetu za kila siku. Hebu wazia kwamba umekuwa dhaifu kwa miezi mingi mfululizo. Je, hutathamini kuona wengine wakikuhurumia na kukuonyesha hisia-mwenzi?

2 Mtume Paulo alijua jinsi mikazo kutoka nje na ndani ya kutaniko inavyoweza kumwathiri na hata kumdhoofisha mtu. Mara nyingi alihisi kwamba hawezi tena kuvumilia. (2 Kor. 1:8; 7:5) Paulo alikiri hivi kuhusu maisha yake na matatizo mengi aliyokabili akiwa Mkristo mwaminifu: “Ni nani aliye dhaifu, nami si dhaifu?” (2 Kor. 11:29) Paulo alilinganisha washiriki wa kutaniko la Kikristo na viungo mbalimbali vya mwili wa mwanadamu na kusema kwamba viungo “vinavyoonekana kuwa dhaifu zaidi ni vya lazima.” (1 Kor. 12:22) Alimaanisha nini? Kwa nini tunahitaji kuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu wale wanaoonekana kuwa dhaifu zaidi? Na tutanufaikaje tukiwa na maoni kama yake?

 MAONI YA YEHOVA KUHUSU UDHAIFU WA KIBINADAMU

3. Ni nini kinachoweza kuathiri maoni yetu kuhusu wale wanaohitaji msaada kutanikoni?

3 Tunaishi katika ulimwengu uliojaa mashindano ambao mara nyingi huwatukuza watu wenye nguvu na vijana. Watu wengi hufanya yote wawezayo ili kupata wanachotaka, na mara nyingi hawajali hisia za walio dhaifu. Ingawa hatuungi mkono tabia hiyo, huenda tukaathiriwa na kusitawisha maoni yasiyofaa kuhusu wale wanaohitaji msaada kwa ukawaida, hata kutanikoni. Lakini tunaweza kusitawisha maoni yenye usawaziko kama ya Mungu.

4, 5. (a) Mfano ulio katika 1 Wakorintho 12:21-23 unatusaidiaje kuelewa maoni ya Yehova kuhusu udhaifu wa kibinadamu? (b) Tutanufaikaje tukiwasaidia walio dhaifu?

4 Tunaweza kuelewa maoni ya Yehova kuhusu udhaifu wa kibinadamu kwa kuchunguza mfano ulio katika barua ya kwanza ya Paulo kwa Wakorintho. Katika sura ya 12, Paulo anatukumbusha kwamba hata sehemu ya mwili isiyovutia au iliyo dhaifu zaidi ina kazi yake. (Soma 1 Wakorintho 12:12, 18, 21-23.) Baadhi ya watu wanaoamini mageuzi husema kwamba viungo fulani vya mwili wa mwanadamu havihitajiki. Hata hivyo, uchunguzi wa mwili wa mwanadamu unaonyesha kwamba viungo vya mwili ambavyo vilionwa kuwa havina kazi yoyote, kwa kweli vinafanya kazi muhimu sana. * Kwa mfano, watu fulani hufikiri kwamba kidole kidogo cha mguu hakihitajiki; hata hivyo, wanasayansi wamegundua kwamba kinausaidia mwili mzima kuwa na usawaziko.

5 Mfano aliotoa Paulo unakazia kwamba washiriki wote wa kutaniko la Kikristo ni wenye thamani. Tofauti na Shetani, anayewashushia wanadamu heshima, Yehova huwaona watumishi wake wote kuwa viungo “vya lazima,” hata wale wanaoonekana kuwa dhaifu zaidi. (Ayu. 4:18, 19) Wazo hilo linapaswa kumsaidia kila mmoja wetu kuthamini jukumu analotimiza kutanikoni na kufurahia kuwa sehemu ya kutaniko la watu wa Mungu duniani pote. Kwa mfano, kumbuka jinsi ulivyonyoosha mkono ili kumsaidia mtu aliyezeeka aliyehitaji msaada. Labda ulilazimika kutembea polepole. Je, si kweli kwamba msaada wako ulimnufaisha nawe ukapata furaha? Naam, tunapowasaidia wengine, tunapata shangwe na pia kusitawisha subira, upendo, na ukomavu. (Efe. 4:15, 16) Baba yetu mwenye upendo anajua kwamba kutaniko linalowathamini washiriki wake wote, licha ya udhaifu wao, linaonyesha upendo na usawaziko.

6. Pindi nyingine Paulo alitumiaje maneno “dhaifu” na “nguvu”?

6 Paulo alipowaandikia Wakorintho, alitumia maneno “dhaifu” na “udhaifu” kwa sababu alijiona hivyo, na watu wasio waamini waliwaona hivyo Wakristo wa karne ya kwanza. (1 Kor. 1:26, 27; 2:3) Paulo aliposema kwamba baadhi ya Wakristo wana “nguvu,” hakutaka Wakristo hao wajione kuwa bora. (Rom. 15:1) Badala yake, alikuwa akisema kwamba Wakristo wenye uzoefu zaidi wanapaswa kuwa wenye subira kuelekea wapya katika kweli.

JE, TUNAHITAJI KUBADILI MAONI YETU?

7. Kwa nini huenda tukasita kuwasaidia wenye uhitaji?

7 Tunapomsaidia “mtu wa hali ya chini,” tunamwiga Yehova na pia tunapata kibali chake. (Zab. 41:1; Efe. 5:1) Hata hivyo, nyakati nyingine huenda tukasita kuwasaidia  wenye uhitaji kwa sababu ya kuwa na maoni yasiyofaa. Au huenda tukaogopa na kuwaepuka kwa sababu hatujui tuwaambie nini watu wanaokabili matatizo. Cynthia, * dada aliyeachwa na mume wake anasema hivi: “Inaumiza kuona ndugu wakikuepuka au kutotenda jinsi unavyotarajia marafiki wa karibu kutenda. Unapokabili majaribu, unahitaji watu wawe karibu nawe.” Mfalme Daudi aliumia pia alipoepukwa na rafiki zake.Zab. 31:12.

8. Ni nini kitakachotusaidia kuwa wenye hisia-mwenzi zaidi?

8 Inaelekea tutakuwa wenye hisia-mwenzi zaidi tukikumbuka kwamba baadhi ya ndugu na dada zetu wapendwa wamedhoofishwa na matatizo, labda kwa sababu ni wagonjwa, wanaishi katika nyumba iliyogawanyika kidini, au wameshuka moyo. Huenda tukakabili hali hiyo siku moja. Kabla ya kuingia katika Nchi ya Ahadi, Waisraeli waliokuwa dhaifu na maskini katika nchi ya Misri, walikumbushwa kwamba hawakupaswa ‘kuufanya moyo wao kuwa mgumu’ kuelekea ndugu zao wenye uhitaji. Yehova alitarajia wawasaidie maskini.Kum. 15:7, 11; Law. 25:35-38.

9. Tunapaswa kufanya nini kwanza tunapowasaidia wale wanaokabili matatizo? Toa mfano.

9 Badala ya kuwatilia shaka au kuwahukumu watu wanaokabili matatizo, tunapaswa kuwafariji kiroho. (Ayu. 33:6, 7; Mt. 7:1) Kwa mfano: Mwendesha-pikipiki anapojeruhiwa katika aksidenti na kupelekwa hospitalini, je, madaktari wataanza kuchunguza ikiwa yeye ndiye aliyesababisha aksidenti hiyo? Hapana, watamtibu haraka. Vivyo hivyo, ikiwa mwamini mwenzetu amedhoofishwa na matatizo ya kibinafsi, tunapaswa kumsaidia kwanza kiroho.Soma 1 Wathesalonike 5:14.

10. Baadhi ya watu wanaoonekana kuwa dhaifu zaidi ni “matajiri katika imani” jinsi gani?

10 Tukitua na kufikiria hali za ndugu zetu, huenda tukagundua kwamba wao si dhaifu kama tulivyodhani. Wafikirie akina dada ambao wamekuwa wakivumilia upinzani wa familia kwa miaka mingi. Huenda baadhi yao wakaonekana kuwa dhaifu na wa hali ya chini. Hata hivyo, je, si wazi kwamba wana imani ya pekee na nguvu za kiroho? Unapomwona mama asiye na mume akihudhuria mikutano kwa ukawaida akiwa na mtoto au watoto wake, je, huvutiwi na imani na azimio lake la kutoacha? Je, huvutiwi pia na vijana wanaoshikamana na kweli licha ya kushinikizwa kufanya mambo mabaya shuleni? Kwa unyenyekevu, tunatambua kwamba wote ambao wanaonekana kuwa dhaifu zaidi huenda ni “matajiri katika imani” sawa tu na wale wenye hali nzuri kati yetu.Yak. 2:5.

BADILI MAONI YAKO ILI YAPATANE NA YA YEHOVA

11, 12. (a) Ni nini kitakachotusaidia kubadili maoni yetu kuhusu udhaifu wa kibinadamu? (b) Tunajifunza nini tunapochunguza jinsi Yehova alivyoshughulika na Haruni?

11 Kuchunguza jinsi Yehova alivyoshughulika na baadhi ya watumishi wake kutatusaidia kubadili maoni yetu ili yapatane na maoni yake kuhusu udhaifu wa kibinadamu. (Soma Zaburi 130:3.) Kwa mfano, kama ungekuwa pamoja na Musa wakati Haruni alipotengeneza sanamu ya ndama wa dhahabu, ungehisije kuhusu visingizio visivyo na msingi ambavyo Haruni alitoa? (Kut.32:21-24) Au ungekuwa na maoni gani kuhusu mtazamo wa Haruni alipochochewa na Miriamu, dada yake, kumshutumu Musa kwa sababu ya kuoa mke wa kigeni? (Hes. 12:1, 2) Ungetendaje wakati Haruni na Musa walipokosa  kumheshimu Yehova alipowapa maji kimuujiza huko Meriba?Hes. 20:10-13.

12 Katika hali hizo zote, Yehova angemwadhibu Haruni papo hapo. Lakini Alitambua kwamba Haruni hakuwa mtu mbaya au kosa lake halikuwa zito sana. Inaonekana kwamba Haruni aliruhusu hali au ushawishi wa wengine umpotoshe. Hata hivyo, Haruni alipotambua amekosea, alikubali kosa lake na kuunga mkono maamuzi ya Yehova. (Kut. 32:26; Hes. 12:11; 20:23-27) Yehova aliamua kukazia fikira imani ya Haruni na mtazamo wake wa kutubu. Baada ya karne nyingi kupita, Haruni na wazao wake waliendelea kukumbukwa kwa kuwa walimwogopa Yehova.Zab. 115:10-12; 135:19, 20.

13. Tunawezaje kujua maoni tuliyonayo kuhusu udhaifu wa kibinadamu?

13 Ili tuwe na maoni kama ya Yehova, tunapaswa kuchunguza maoni yetu kuhusu wale wanaoonekana kuwa dhaifu. (1 Sam. 16:7) Kwa mfano, tunatendaje kijana anapochagua burudani kwa njia isiyo ya busara au anapoonyesha mtazamo wa kutojali? Badala ya kumchambua-chambua, kwa nini tusifikirie jinsi tunavyoweza kumsaidia kukomaa? Tunaweza kuchukua hatua ya kuwasaidia wenye uhitaji, na tunapofanya hivyo, tutawaelewa vizuri na kuwapenda zaidi.

14, 15. (a) Yehova alihisije alipomwona Eliya akikosa ujasiri kwa muda fulani? (b) Tunajifunza nini kutokana na kisa cha Eliya?

14 Kulinganisha maoni yetu na maoni ya Yehova kuhusu watumishi wake walioshuka moyo kutatusaidia pia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu wengine. Fikiria mfano wa Eliya. Ingawa Eliya alipambana kwa ujasiri na manabii 450 wa Baali, alikimbia alipopata habari kwamba Malkia Yezebeli amepanga njama ya kumuua. Baada  ya kutembea kwenye jua kali umbali wa kilomita 150 hivi, alifika Beer-sheba na kuingia nyikani. Nabii huyo aliyechoka sana aliketi chini ya mti na “kuomba kwamba nafsi yake ife.”1 Fal. 18:19; 19:1-4.

Yehova alitilia maanani udhaifu wa Eliya na kumtuma malaika amtie moyo (Tazama fungu la 14 na 15)

15 Yehova alihisije alipotazama kutoka mbinguni na kumwona nabii wake mwaminifu akiwa ameshuka moyo? Je, alimkataa mtumishi wake kwa sababu alikuwa ameshuka moyo kwa muda fulani na kukosa ujasiri? La hasha! Yehova alitilia maanani udhaifu wa Eliya na kumtuma malaika amtie moyo. Mara mbili, malaika huyo alimhimiza Eliya ale ili safari ‘isiwe ndefu mno kwake.’ (Soma 1 Wafalme 19:5-8.) Naam, hata kabla ya kutoa mwelekezo wowote, Yehova alimsikiliza nabii wake na kumpa msaada aliohitaji.

16, 17. Tunawezaje kuwasaidia ndugu zetu kama Yehova alivyomsaidia Eliya?

16 Tunawezaje kumwiga Mungu wetu anayejali? Hatupaswi kuwa wepesi katika kutoa ushauri. (Met. 18:13) Kwanza, ni vizuri kuwahurumia wale ambao kwa sababu ya hali zao huenda wanahisi kwamba wao ni kama sehemu za mwili ‘zenye heshima kidogo.’ (1 Kor. 12:23) Kisha tutakuwa tayari kuwapa msaada wanaohitaji kikweli.

17 Kwa mfano, mfikirie Cynthia, aliyenukuliwa awali. Mume wake alipomwacha na binti zake wawili, walihisi upweke. Baadhi ya Mashahidi wenzake walitendaje? Anaeleza hivi: “Baada ya kupiga simu na kuwajulisha kilichotukia, walifika baada ya dakika 45 tu. Walitokwa na machozi. Walikaa nasi siku mbili au tatu za kwanza. Walitukaribisha nyumbani mwao kwa muda kwa sababu hatukuwa na hamu ya kula na tulihuzunika sana.” Inaelekea kwamba kisa hicho kinakukumbusha maneno haya aliyoandika Yakobo: “Ikiwa ndugu au dada yuko uchi naye hana chakula cha kutosha kwa ajili ya siku, na mmoja wenu amwambie: ‘Nenda kwa amani, jipashe moto na kula vizuri,’ lakini ninyi mkose kumpa mahitaji ya mwili wake, ina faida gani? Vivyo hivyo, pia, imani, ikiwa haina matendo, imekufa yenyewe.” (Yak. 2:15-17) Kwa sababu ya msaada wa wakati unaofaa kutoka kwa ndugu na dada wa kutaniko lao, Cynthia na binti zake walipata nguvu za kutumikia wakiwa mapainia wasaidizi baada ya miezi sita tu.2 Kor. 12:10.

WENGI HUNUFAIKA

18, 19. (a) Tunawezaje kuwasaidia wale ambao ni dhaifu kwa sasa? (b) Ni nani wanaonufaika tunapowasaidia walio dhaifu?

18 Huenda umejionea kwamba inaweza kuchukua muda mrefu kupona ugonjwa mbaya. Vivyo hivyo, Mkristo ambaye amedhoofishwa na matatizo ya kibinafsi au majaribu makali huenda akahitaji muda ili apate nguvu za kiroho. Ni kweli kwamba mwamini mwenzetu atahitaji kuimarisha imani yake mwenyewe kwa kujifunza kibinafsi, kusali, na kushiriki katika utendaji mwingine wa Kikristo. Hata hivyo, je, tutamwonyesha subira hadi atakapopata tena usawaziko? Je, tutaendelea kumwonyesha upendo wakati anapopona kiroho? Je, tutajitahidi kuwasaidia wale ambao ni dhaifu kwa sasa, ili wahisi kwamba tunawapenda?2 Kor. 8:8.

19 Usisahau kamwe kwamba tunapowategemeza ndugu zetu, tunapata shangwe inayopatikana tu kwa kutoa. Tunasitawisha pia uwezo wetu wa kuonyesha subira na hisia-mwenzi. Zaidi ya hayo, upendo na uchangamfu husitawi katika kutaniko lote. Na zaidi ya yote, tunamwiga Yehova, anayemwona kila mtu kuwa mwenye thamani. Naam, sote tuna sababu nzuri za kutii himizo la ‘kuwasaidia wale walio dhaifu.’Mdo. 20:35.

^ fu. 4 Charles Darwin alisema katika kitabu chake (The Descent of Man) kwamba viungo kadhaa vya mwili wa mwanadamu “havihitajiki.” Mwana-mageuzi mwingine alisema kwamba kuna ‘viungo vingi visivyohitajika’ katika mwili wa mwanadamu, kutia ndani kidole-tumbo na tezi za dundumio.

^ fu. 7 Jina limebadilishwa.