Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unapata ‘Chakula kwa Wakati Unaofaa’?

Je, Unapata ‘Chakula kwa Wakati Unaofaa’?

TUNAISHI katika kipindi kigumu zaidi katika historia ya wanadamu. (2 Tim. 3:1-5) Upendo wetu kwa Yehova na azimio letu la kuishi kupatana na viwango vyake vya uadilifu hujaribiwa kila siku. Yesu alitabiri kuhusu kipindi hiki kigumu, aliwahakikishia wafuasi wake kwamba wangepata kitia-moyo wanachohitaji ili wavumilie mpaka mwisho. (Mt. 24:3, 13; 28:20) Ili kuwaimarisha, alimweka rasmi mtumwa mwaminifu aandae ‘chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.’—Mt. 24:45, 46.

Tangu mtumwa mwaminifu alipowekwa rasmi mwaka wa 1919, mamilioni ya ‘watumishi wa nyumbani’ kutoka katika lugha zote wamekusanywa katika tengenezo la Mungu na wanalishwa kiroho. (Mt. 24:14; Ufu. 22:17) Hata hivyo, machapisho yetu yote hayapatikani katika lugha zote. Na si wote wanaoweza kupata machapisho yetu kwa njia ya kielektroniki. Kwa mfano, wengi hawana video na makala zilizo katika tovuti ya jw.org. Je, hilo linamaanisha kwamba wengine hawapati chakula wanachohitaji ili waendelee kuwa na afya nzuri ya kiroho? Ili kufikia mkataa unaofaa, fikiria majibu ya maswali haya manne muhimu.

 1. Ni nini msingi wa chakula anachoandaa Yehova?

Shetani alipomjaribu Yesu ageuze mawe yawe mkate, Yesu alijibu hivi: “Mwanadamu ataishi, si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mt. 4:3, 4) Maneno ya Yehova yameandikwa katika Biblia. (2 Pet. 1:20, 21) Kwa hiyo, Biblia ndiyo msingi wa chakula chetu cha kiroho.—2 Tim. 3:16, 17.

Tengenezo la Yehova limechapisha Biblia TakatifuTafsiri ya Ulimwengu Mpya ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha zaidi ya 120, na idadi hiyo inaongezeka kila mwaka. Mbali na tafsiri hiyo, mabilioni ya tafsiri nyingine za Biblia zinapatikana zikiwa nzima au kwa sehemu katika maelfu ya lugha. Kazi hiyo imefanikiwa sana kwa sababu inapatana na mapenzi ya Yehova kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Na kwa sababu ‘hakuna kiumbe kisichokuwa wazi machoni pa Yehova,’ tuna hakika kwamba atawavuta katika tengenezo lake na kuwaandalia chakula cha kiroho wale “wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—Ebr. 4:13; Mt. 5:3, 6; Yoh. 6:44; 10:14.

2. Machapisho yetu yanatusaidiaje kupata chakula cha kiroho?

Ili mtu asitawishe imani yenye nguvu, haitoshi tu kusoma Biblia, ni lazima aelewe anayosoma na kutumia anayojifunza. (Yak. 1:22-25) Towashi Mwethiopia katika karne ya kwanza alijua jambo hilo. Alikuwa akisoma Neno la Mungu Filipo mweneza-injili alipomuuliza hivi: “Je, wewe kwa kweli unaelewa unayoyasoma?” Towashi akamjibu hivi: “Kwa kweli, ninawezaje kuelewa, mtu fulani asiponiongoza?” (Mdo. 8:26-31) Kisha Filipo akamsaidia kupata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu. Towashi huyo alichochewa sana na aliyojifunza hivi kwamba akaamua kubatizwa. (Mdo. 8:32-38) Vivyo hivyo, machapisho yetu yanayotegemea Biblia yametusaidia kupata ujuzi sahihi wa kweli. Yamegusa hisia zetu na kutuchochea kutumia tunayojifunza.—Kol. 1:9, 10.

Kupitia machapisho hayo, watumishi wa Yehova wanapata maandalizi mengi ya kiroho ya kula na kunywa. (Isa. 65:13) Kwa mfano, gazeti la Mnara wa Mlinzi linalochapishwa katika lugha zaidi ya 210, hufafanua unabii wa Biblia, hutusaidia kuelewa vizuri zaidi kweli za kiroho zenye kina, na kutuchochea kuishi kupatana na kanuni za Biblia. Gazeti la Amkeni! linalochapishwa katika lugha 100 hivi, hutusaidia kuelewa vizuri zaidi kazi za Yehova za uumbaji na kutuonyesha jinsi ya kutumia mashauri ya Biblia. (Met. 3:21-23; Rom. 1:20) Mtumwa mwaminifu huandaa habari zinazotegemea Biblia katika lugha zaidi ya 680! Je, wewe hutenga wakati wa kusoma Biblia kila siku? Je, unasoma kila gazeti na machapisho yote mapya yanayotolewa kila mwaka katika lugha yenu?

Mbali na machapisho, tengenezo la Yehova hutayarisha mihtasari ya hotuba zinazotegemea Biblia zinazotolewa kwenye mikutano na makusanyiko yetu. Je, wewe hufurahia hotuba, drama, maonyesho, na mahojiano katika mikutano na makusanyiko hayo? Ni wazi kwamba Yehova anatuandalia karamu ya kiroho.—Isa. 25:6.

 3. Ikiwa machapisho fulani yanayotolewa hayapatikani katika lugha yenu, je, afya yako ya kiroho itadhoofika?

Jibu ni hapana. Hata hivyo, hatupaswi kushangaa kwamba nyakati nyingine baadhi ya watumishi wa Yehova hupata chakula kingi cha kiroho kuliko wengine. Kwa nini? Wafikirie mitume. Walipata maagizo mengi kuliko wanafunzi wengine wengi katika karne ya kwanza. (Marko 4:10; 9:35-37) Hata hivyo, wanafunzi wengine hawakudhoofika kiroho; walipata chakula walichohitaji.—Efe. 4:20-24; 1 Pet. 1:8.

Pia, ni muhimu kukumbuka kwamba mambo mengi ambayo Yesu alisema na kufanya alipokuwa duniani hayakuandikwa katika masimulizi ya Injili. Mtume Yohana aliandika hivi: “Kwa kweli, kuna mambo mengine mengi pia aliyofanya Yesu, ambayo, kama yangeandikwa kirefu, nadhani ulimwengu wenyewe haungeweza kuwa na nafasi ya kuviweka vitabu vya kukunjwa ambavyo vingeandikwa.” (Yoh. 21:25) Ingawa wafuasi wa Yesu katika karne ya kwanza walikuwa na habari nyingi zaidi kuhusu mwanamume huyo mkamilifu, sisi pia tunajua mengi kumhusu. Yehova amehakikisha kwamba tunajua mambo ya kutosha kumhusu Yesu ili tufuate hatua zake kwa ukaribu.—1 Pet. 2:21.

Fikiria pia barua ambazo mitume waliandikia makutaniko ya karne ya kwanza. Huenda barua moja ya Paulo haikutiwa ndani ya Biblia. (Kol. 4:16) Je, hatuna chakula cha kiroho cha kutosha kwa sababu ya kukosa barua hiyo? Hapana. Yehova anajua tunachohitaji na ametupatia chakula cha kutosha ili tuendelee kuwa imara kiroho.—Mt. 6:8.

Yehova anajua tunachohitaji na ametupatia chakula cha kutosha ili tuendelee kuwa imara kiroho

Leo, baadhi ya watumishi wa Yehova wana chakula zaidi cha kiroho kuliko wengine. Je, lugha yenu ina machapisho machache tu? Ikiwa ndivyo ilivyo, uwe na uhakika kwamba Yehova anakujali. Jifunze machapisho yanayopatikana, na ikiwezekana, hudhuria mikutano inayofanywa katika lugha unayoelewa. Uwe na hakika kwamba Yehova atakuimarisha kiroho.—Zab. 1:2; Ebr. 10:24, 25.

4. Ikiwa hupati habari zilizo katika jw.org, je, utadhoofika kiroho?

Tovuti yetu ina magazeti na machapisho mengine ya kujifunzia Biblia. Tovuti hiyo huandaa pia habari zinazowasaidia wenzi wa ndoa, vijana, na wale walio na watoto wadogo. Familia nyingi hunufaika kwa kuchunguza habari hizo katika Ibada ya Familia. Isitoshe, Tovuti yetu huwa na habari kuhusu programu za pekee, kama vile kuhitimu kwa wanafunzi wa Gileadi na mkutano wa kila mwaka, na huwajulisha ndugu zetu ulimwenguni pote kuhusu misiba ya asili na mambo ya kisheria yanayohusu watu wa Yehova. (1 Pet. 5:8, 9) Pia, Tovuti hiyo inasaidia sana katika kazi ya kuhubiri. Kupitia Tovuti hiyo, habari njema hufika katika nchi ambazo kazi yetu imezuiwa au kupigwa marufuku.

Hata hivyo, unaweza kuendelea kuwa imara kiroho hata kama hupati habari zilizo katika Tovuti yetu. Mtumwa amejitahidi kuandaa machapisho ya kutosha ili kila mtumishi wa nyumbani alishwe vizuri kiroho. Hivyo, usihisi kwamba ni lazima ununue kifaa cha kielektroniki ili utembelee Tovuti ya jw.org. Huenda wengine wakafanya mipango ya kibinafsi ya kuchapisha habari fulani zilizo katika Tovuti yetu na kuwapa wale wasioweza kupata habari hizo, lakini makutaniko hayahitaji kufanya hivyo.

Tunamshukuru Yesu kwa kuwa ametimiza ahadi yake ya kutuandalia mahitaji yetu ya kiroho. Kadiri siku hizi za mwisho zilizo ngumu zinavyokaribia haraka mwisho wake, tuna hakika kwamba Yehova ataendelea kuandaa ‘chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.’