Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Rudi na Uwatie Nguvu Ndugu Zako’

‘Rudi na Uwatie Nguvu Ndugu Zako’

PETRO alilia kwa uchungu alipomkana Yesu. Ingawa mtume huyo alipaswa kujitahidi sana ili kupata tena usawaziko wake wa kiroho, Yesu alitaka kumtumia kuwasaidia wengine. Hivyo, Yesu alimwambia hivi: “Mara tu utakapokuwa umerudi, watie nguvu ndugu zako.” (Luka 22:32, 54-62) Petro alifanya maendeleo na kuwa miongoni mwa nguzo za kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza. (Gal. 2:9) Vivyo hivyo, ndugu aliyewahi kutumika akiwa mzee anaweza kutumika tena katika pendeleo hilo na kupata shangwe ya kuwatia nguvu kiroho waamini wenzake.

Baadhi ya ndugu waliotumika wakati fulani wakiwa waangalizi wamepoteza mapendeleo yao na huenda wakahisi hawafai. Julio, * aliyetumika akiwa mzee huko Amerika ya Kusini kwa miaka zaidi ya 20, alisema hivi: “Nilitumia sehemu kubwa ya maisha yangu kutayarisha hotuba, kuwatembelea akina ndugu, na kufanya uchungaji. Kwa ghafla nilipoteza mapendeleo yote hayo, sikujua la kufanya. Kwa ujumla, kilikuwa kipindi kigumu sana.” Sasa, Julio anatumika tena akiwa mzee.

“ONENI YOTE KUWA SHANGWE”

Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Oneni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mnapokutana na majaribu ya namna mbalimbali.” (Yak. 1:2) Yakobo alikuwa akirejelea majaribu yanayosababishwa na mateso na hali yetu ya kutokamilika. Alitaja tamaa za kichoyo, kuonyesha upendeleo, na mambo mengine. (Yak. 1:14; 2:1; 4:1, 2, 11) Yehova anapotutia nidhamu, tunaweza kuumia. (Ebr. 12:11) Hata hivyo, majaribu kama hayo hayapaswi kutufanya tupoteze shangwe yetu.

Hata ikiwa tumepoteza pendeleo kutanikoni, bado tuna nafasi ya kuchunguza ubora wa imani yetu na kuonyesha kwamba tunampenda Yehova. Tunaweza pia kutafakari kuhusu jambo lililotuchochea kutumika. Je, tulitumika ili kujinufaisha, au tulichochewa  kufikia pendeleo hilo kwa sababu tunampenda Mungu na tunasadiki kwamba kutaniko ni mali yake na linastahili kutunzwa kwa wororo? (Mdo. 20:28-30) Ndugu waliowahi kutumika wakiwa wazee zamani na ambao kwa shangwe wanaendelea kutoa utumishi mtakatifu wanawathibitishia wote, kutia ndani Shetani, kwamba wanampenda Yehova kikweli.

Mfalme Daudi alipotiwa nidhamu baada ya kufanya dhambi nzito, alikubali karipio naye akasamehewa. Daudi aliimba hivi: “Mwenye furaha ni mtu ambaye amesamehewa maasi yake, ambaye dhambi yake imefunikwa. Mwenye furaha ni mtu ambaye Yehova hamhesabii kosa, na ambaye katika roho yake hamna udanganyifu.” (Zab. 32:1, 2) Nidhamu iliboresha utu wa Daudi, na bila shaka ilimfanya kuwa mchungaji bora zaidi wa watu wa Mungu.

Mara nyingi, ndugu wanaotumika tena wakiwa wazee huwa wachungaji bora zaidi kuliko mwanzoni. Mzee mmoja anayetumika tena alisema hivi: “Sasa ninaelewa vizuri zaidi jinsi ya kuwasaidia waliofanya kosa.” Mzee mwingine alisema hivi: “Sasa ninathamini zaidi pendeleo langu la kuwatumikia akina ndugu.”

JE, UNAWEZA KURUDI?

Mtunga-zaburi aliandika hivi: “[Yehova] hataendelea kutafuta makosa wakati wote.” (Zab. 103:9) Kwa hiyo, hatupaswi kufikiria kwamba Mungu hawezi kumtumia tena mtu aliyefanya kosa zito. Ricardo, aliyepoteza mapendeleo yake baada ya kutumika akiwa mzee kwa miaka mingi anasema hivi: “Nilivunjika moyo sana kwa sababu ya makosa yangu. Kwa muda mrefu, hisia za kujiona sifai zilinizuia kurudi ili kuwatumikia tena akina ndugu nikiwa mwangalizi. Nilihisi kwamba siwezi kutegemeka tena. Lakini kwa kuwa mimi hufurahia kuwasaidia wengine, niliongoza mafunzo ya Biblia, nikawatia moyo akina ndugu katika Jumba la Ufalme, na kushiriki nao katika huduma ya shambani. Mambo hayo yalinisaidia kupata tena uhakika, na sasa ninatumika tena nikiwa mzee.”

Yehova amewasaidia wanaume kupata tena shangwe yao na kutamani tena kutumika

Kuwa na kinyongo kunaweza kumzuia ndugu kutumika akiwa mzee. Ni bora zaidi kuwa kama Daudi, mtumishi wa Yehova, aliyelazimika kumkimbia Mfalme Sauli mwenye wivu! Daudi alikataa  kulipiza kisasi dhidi ya Sauli, hata alipopata nafasi za kufanya hivyo. (1 Sam. 24:4-7; 26:8-12) Sauli alipokufa vitani, Daudi aliomboleza kifo chake, na kumrejelea Sauli na Yonathani mwanaye kuwa watu “wenye kupendwa na wenye kupendeza.” (2 Sam. 1:21-23) Daudi hakuwa na kinyongo moyoni.

Ikiwa unahisi kwamba wengine hawakuelewi au umetendewa isivyo haki, usiruhusu kinyongo kitawale mawazo yako. Kwa mfano, William alipoondolewa kuwa mzee baada ya kutumika kwa miaka 30 hivi nchini Uingereza, alikuwa na kinyongo kuelekea baadhi ya wazee. Ni nini kilichomsaidia William kupata tena usawaziko? Anasema hivi: “Nilitiwa moyo niliposoma kitabu cha Ayubu. Ikiwa Yehova alimsaidia Ayubu kufanya amani na wale waandamani wake watatu, bila shaka atanisaidia hata zaidi kufanya amani na wazee Wakristo!”—Ayu. 42:7-9.

MUNGU HUWABARIKI WALE WANAOTUMIKA TENA WAKIWA WACHUNGAJI

Ikiwa uliamua kuacha pendeleo la kulichunga kundi la Mungu, ni vizuri kufikiria kwa nini uliacha pendeleo hilo. Je, uliacha kwa sababu ya matatizo mengi ya kibinafsi? Je, ulitanguliza mambo mengine uliyoona kuwa muhimu zaidi maishani mwako? Je, ulivunjwa moyo na kutokamilika kwa wengine? Kwa vyovyote vile, kumbuka kwamba ulikuwa na nafasi ya kuwasaidia wengine kwa njia nyingi zaidi ulipotumika ukiwa mzee. Hotuba zako ziliwaimarisha, kielelezo chako kiliwatia moyo, na ziara zako za uchungaji ziliwasaidia kuvumilia majaribu. Kazi yako ukiwa mzee mwaminifu iliufanya moyo wa Yehova ushangilie, na wako pia.—Met. 27:11.

Thibitisha kwamba unampenda Yehova kwa kushiriki kwa shangwe katika utumishi mtakatifu

Yehova amewasaidia wanaume kupata tena shangwe yao na kutamani tena kuongoza katika kutaniko. Ikiwa uliacha pendeleo la kuwa mzee au uliondolewa, unaweza ‘kujitahidi tena kufikia cheo cha mwangalizi.’ (1 Tim. 3:1) Paulo ‘hakuacha kusali’ kwamba Wakristo Wakolosai wajazwe ujuzi sahihi wa mapenzi ya Mungu ‘ili watembee kwa kumstahili Yehova kwa kusudi la kumpendeza yeye kikamili.’ (Kol. 1:9, 10) Ikiwa umepata tena pendeleo la kutumika ukiwa mzee, mwombe Yehova akupe nguvu, subira, na shangwe. Katika siku hizi za mwisho, watu wa Mungu wanahitaji utegemezo wa kiroho wa wachungaji wenye upendo. Je, unaweza na uko tayari kuwaimarisha ndugu zako?

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.