Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanawake Wanatimiza Sehemu Gani Katika Kusudi la Yehova?

Wanawake Wanatimiza Sehemu Gani Katika Kusudi la Yehova?

“Wanawake wanaotangaza habari njema ni jeshi kubwa.”—ZAB. 68:11.

1, 2. (a) Ni zawadi gani ambazo Mungu alimpa Adamu? (b) Kwa nini Mungu alimpa Adamu mke? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

YEHOVA aliiumba dunia akiwa na kusudi. “Aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isa. 45:18) Alimuumba mtu wa kwanza mkamilifu, Adamu, na kumpa makao mazuri sana, bustani ya Edeni. Ni wazi kwamba Adamu alifurahia sana miti maridadi, vijito vya maji, na wanyama walioruka-ruka huku na kule. Hata hivyo, alikosa jambo fulani muhimu sana. Yehova alitaja jambo hilo aliposema hivi: “Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.” Kisha, Mungu akamletea Adamu usingizi mzito, akachukua ubavu wake mmoja, na ‘kuufanya ubavu huo kuwa mwanamke.’ Adamu alipoamka, alifurahi sana na kusema hivi: “Mwishowe huyu ni mfupa wa mifupa yangu na nyama ya nyama yangu. Huyu ataitwa Mwanamke, kwa sababu huyu alitolewa katika mwanamume.”—Mwa. 2:18-23.

2 Mwanamke alikuwa zawadi ya pekee kutoka kwa Mungu kwa sababu angekuwa msaidizi mkamilifu wa mwanamume. Angekuwa pia na pendeleo la pekee la kuzaa watoto. Kwa kweli, ‘Adamu alimwita mke wake jina Hawa, kwa sababu ndiye  angekuja kuwa mama ya kila mtu anayeishi.’ (Mwa. 3:20) Hiyo ilikuwa zawadi nzuri kama nini ambayo Mungu aliwapa wenzi hao wa kwanza! Walikuwa na uwezo wa kuzaa wanadamu wengine wakamilifu. Hatimaye, dunia ingekuwa paradiso iliyo na wanadamu wakamilifu ambao wangewatiisha viumbe wengine.—Mwa. 1:27, 28.

3. (a) Adamu na Hawa walihitaji kufanya nini ili Mungu awabariki, lakini ni nini kilichotokea? (b) Tutachunguza maswali gani?

3 Ili wapate baraka hizo, Adamu na Hawa walipaswa kumtii Yehova na kutambua utawala wake. (Mwa. 2:15-17) Wangeweza kutimiza kusudi la Mungu kwa kufanya hivyo tu. Hata hivyo, inasikitisha kwamba walishawishiwa na Shetani, “yule nyoka wa zamani,” na hivyo wakamwasi Mungu. (Ufu. 12:9; Mwa. 3:1-6) Uasi huo umeathirije wanawake? Wanawake waliomwogopa Mungu walitimiza nini katika nyakati za kale? Kwa nini wanawake Wakristo leo wanaitwa “jeshi kubwa”?—Zab. 68:11.

MATOKEO YA UASI

4. Ingawa Adamu na Hawa walifanya dhambi, ni nani aliyelaumiwa?

4 Adamu alipoulizwa kwa nini aliasi, alitoa kisingizio hiki: “Mwanamke uliyenipa awe pamoja nami, alinipa tunda kutoka katika ule mti nami nikala.” (Mwa. 3:12) Badala ya kukubali dhambi yake, alimlaumu mwanamke ambaye Mungu alimpa, na alimlaumu pia Mungu ambaye ni Mpaji mwenye upendo. Ingawa Adamu na Hawa walifanya dhambi, Adamu ndiye aliyelaumiwa kwa kosa lao. Hivyo, mtume Paulo aliandika kwamba “kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi.”—Rom. 5:12.

5. Utawala wa wanadamu bila kumtegemea Mungu umethibitisha nini?

5 Mwanamume na mwanamke wa kwanza walishawishiwa kuamini kwamba hawakuhitaji Yehova awe Mtawala wao. Hilo lilitokeza swali hili muhimu kuhusu enzi kuu: Ni nani aliye na haki ya kutawala? Ili kujibu swali hilo kwa umilele wote, Mungu ameruhusu wanadamu wajitawale bila msaada wake. Alijua kwamba wanadamu wangejionea wenyewe kwamba hawawezi kujitawala. Kwa karne nyingi, utawala wa wanadamu umesababisha msiba mmoja baada ya mwingine. Katika karne iliyopita pekee, watu 100,000,000 hivi walikufa katika vita. Idadi hiyo inatia ndani mamilioni ya wanaume, wanawake, na watoto wasio na hatia. Hivyo, tayari kuna uthibitisho mwingi kwamba “mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yer. 10:23) Tunatambua ukweli huo na kumkubali Yehova kuwa Mtawala wetu.—Soma Methali 3:5, 6.

6. Wanawake hutendewaje katika nchi nyingi?

6 Wanaume na wanawake wameteseka katika ulimwengu huu unaokaa katika nguvu za Shetani. (Mhu. 8:9; 1 Yoh. 5:19) Wanawake ni miongoni mwa watu wanaotendewa kwa ukatili zaidi. Ulimwenguni pote, asilimia 30 hivi ya wanawake wametendewa vibaya na waume au rafiki zao wa kiume. Katika jamii fulani, wanaume wanapendelewa kwa sababu watu hufikiri kwamba wataendeleza ukoo wao na kuwatunza wazazi, babu, na nyanya waliozeeka. Katika nchi fulani, watoto wa kike huonwa kuwa hawafai, na wengi wao huuawa kupitia utoaji-mimba.

7. Mungu aliwapa wanaume na wanawake mwanzo wa aina gani?

7 Bila shaka Mungu hafurahi kuona wanawake wakitendewa vibaya, naye huwatendea kwa haki na heshima. Tunajua kwamba Yehova anawaheshimu wanawake kwa sababu alimuumba Hawa akiwa mkamilifu, na akiwa na sifa zilizomfanya kuwa kikamilisho bora kwa Adamu, bali si mtumwa wake. Ndiyo sababu mwishoni mwa siku ya sita ya uumbaji, Mungu “akaona  kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.” (Mwa. 1:31) Naam, “kila kitu” alichofanya Yehova “kilikuwa chema sana.” Aliwapa wanaume na wanawake mwanzo mzuri sana!

WANAWAKE WALIOKUWA NA KIBALI CHA YEHOVA

8. (a) Kwa ujumla, maadili ya wanadamu yakoje? (b) Katika historia yote ya wanadamu, Mungu amewaonyesha nani kibali?

8 Kwa ujumla, maadili ya wanaume na wanawake yalizorota baada ya uasi katika Edeni, na katika karne iliyopita, yamekuwa mabaya kuliko wakati mwingine wowote. Biblia ilitabiri kwamba matendo maovu yangeongezeka katika “siku za mwisho.” Uovu wa wanadamu umeenea sana kuonyesha kwamba kwa kweli hizi ni “nyakati za hatari.” (2 Tim. 3:1-5) Hata hivyo, katika historia yote ya wanadamu, “Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova” amewaonyesha kibali wanaume na wanawake wanaomtegemea, wanaotii sheria zake, na kujitiisha kwake akiwa Mtawala wao.—Soma Zaburi 71:5.

9. Ni watu wangapi waliookoka Gharika, na kwa nini?

9 Mungu alipoleta Gharika katika siku za Noa na kuharibu ulimwengu wa kale wenye jeuri, ni watu wachache sana waliookoka. Ikiwa ndugu na dada za Noa walikuwa hai wakati huo, wao pia walikufa katika Gharika. (Mwa. 5:30) Lakini idadi ya wanaume na wanawake waliookoka Gharika hiyo ililingana. Noa, mke wake, wanawe watatu, na wake zao ndio waliookoka. Walihifadhiwa hai kwa sababu walimwogopa Mungu na kufanya mapenzi yake. Mabilioni ya watu wanaoishi sasa walitokana na watu hao wanane waliokuwa na kibali cha Yehova.—Mwa. 7:7; 1 Pet. 3:20.

10. Kwa nini wake wa wazee waaminifu wa ukoo walipata kibali cha Yehova?

10 Miaka mingi baadaye, wake wa wazee waaminifu wa ukoo walikuwa pia na kibali cha Mungu kwa sababu walimwogopa Mungu. Hawangepata kibali chake ikiwa wangelalamika juu ya fungu lao maishani. (Yuda 16) Ni wazi kwamba Sara, mke mtiifu wa Abrahamu hakulalamika kwa uchungu walipoondoka katika jiji la Uru lenye starehe na kuishi katika mahema wakiwa wakaaji wa muda katika nchi nyingine. Badala yake, ‘Sara alikuwa akimtii Abrahamu, akimwita “bwana.”’ (1 Pet. 3:6) Mfikirie pia Rebeka, aliyekuwa mke mzuri sana na zawadi bora kutoka kwa Yehova. Haishangazi kwamba mume wake, Isaka, ‘alimpenda na kupata faraja baada ya kumpoteza mama yake.’ (Mwa. 24:67) Tunafurahi kama nini kwamba miongoni mwetu kuna wanawake wanaomwogopa Mungu, kama Sara na Rebeka!

11. Wanawake wawili wazalishaji Waebrania walionyeshaje ujasiri?

11 Waisraeli walipokuwa watumwa nchini Misri, idadi yao iliongezeka sana hivi kwamba Farao akaamuru watoto wote wa kiume Waebrania wauawe wanapozaliwa. Hata hivyo, wafikirie wazalishaji Waebrania, Shifra na Pua, ambao huenda walisimamia wazalishaji wenzao. Walikataa kwa ujasiri kuwaua watoto Waebrania kwa sababu walimheshimu na kumwogopa Yehova. Hivyo, Yehova aliwathawabisha kwa kuwapa familia zao wenyewe.—Kut. 1:15-21.

12. Ni jambo gani lililokuwa la pekee kuhusu Debora na Yaeli?

12 Katika siku za waamuzi wa Israeli, nabii wa kike Debora alipata kibali cha Mungu. Alimtia moyo Mwamuzi Baraka na alisaidia kulikomboa taifa la Israeli kutokana na wakandamizaji, lakini alitabiri kwamba Baraka hangewashinda Wakanaani na kupata utukufu. Badala yake, Mungu angemtia Sisera, mkuu wa jeshi la Kanaani, “katika mkono wa mwanamke.” Hilo lilitukia wakati Yaeli, mwanamke asiye  Mwisraeli, alipomuua Sisera.—Amu. 4:4-9, 17-22.

13. Biblia inatuambia nini kumhusu Abigaili?

13 Abigaili alikuwa mwanamke wa pekee aliyeishi katika karne ya 11 K.W.K. Alikuwa mwenye busara, lakini mume wake Nabali, alikuwa mkali, asiyefaa kitu, na asiye na akili. (1 Sam. 25:2, 3, 25) Daudi na wanaume wake walilinda mali ya Nabali kwa muda fulani, lakini walipoomba chakula, ‘aliwakemea kwa sauti kali’ na hakuwapa chochote. Jambo hilo lilimkasirisha sana Daudi hivi kwamba alipanga kumuua Nabali na wanaume wake. Abigaili aliposikia hilo, alichukua chakula na vinywaji na kumpelekea Daudi na wanaume wake, na hivyo akamzuia Daudi asimwage damu. (1 Sam. 25:8-18) Baadaye, Daudi alimwambia hivi Abigaili: “Abarikiwe Yehova Mungu wa Israeli, aliyekutuma leo unipokee!” (1 Sam. 25:32) Nabali alipokufa, Daudi alimwoa Abigaili.—1 Sam. 25:37-42.

14. Binti za Shalumu walishiriki katika kazi gani, na wanawake Wakristo wanafanyaje hivyo leo?

14 Wanaume, wanawake, na watoto wengi walikufa majeshi ya Babiloni yalipoharibu Yerusalemu na hekalu lake mwaka wa 607 K.W.K. Kuta za jiji hilo zilijengwa upya mwaka wa 455 K.W.K. chini ya usimamizi wa Nehemia. Miongoni mwa waliosaidia kurekebisha kuta hizo ni binti za Shalumu, mkuu wa nusu ya wilaya ya Yerusalemu. (Neh. 3:12) Walifanya kwa hiari kazi hiyo ya hali ya chini. Tunawathamini sana wanawake wengi Wakristo wanaoshiriki kwa shangwe katika miradi ya ujenzi ya kitheokrasi kwa njia mbalimbali leo.

WANAWAKE WA KARNE YA KWANZA WALIOMWOGOPA MUNGU

15. Mungu alimpa pendeleo gani mwanamke aliyeitwa Maria?

15 Kabla na katika karne ya kwanza W.K., Yehova aliwabariki wanawake wengi kwa kuwapa mapendeleo mazuri. Miongoni mwao ni bikira aliyeitwa Maria. Alipokuwa akichumbiwa na Yosefu, alipata mimba kimuujiza kupitia roho takatifu. Kwa nini Mungu alimchagua Maria awe mama ya Yesu? Bila shaka alikuwa na sifa za kiroho zilizohitajiwa ili kumlea mwana huyo mkamilifu kuanzia utotoni mpaka alipokuwa mtu mzima. Lilikuwa pendeleo kubwa kama nini kuwa mama ya mtu mkuu zaidi aliyewahi kuishi duniani!—Mt. 1:18-25.

16. Toa mfano unaoonyesha mtazamo wa Yesu kuelekea wanawake.

16 Yesu aliwatendea kwa fadhili sana wanawake. Kwa mfano, mfikirie mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu kwa miaka 12. Alikuja kutoka nyuma katika ule umati na kugusa vazi la Yesu. Badala ya kumkemea, Yesu alimwambia hivi kwa fadhili: “Binti yangu, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani, na uwe na afya njema kutokana na ugonjwa wako wenye kuhuzunisha.”—Marko 5:25-34.

17. Ni muujiza gani uliotukia katika Pentekoste 33 W.K.?

17 Baadhi ya wanawake waliokuwa wanafunzi wa Yesu walimhudumia yeye na mitume wake. (Luka 8:1-3) Na katika Pentekoste 33 W.K., wanaume na wanawake 120 hivi walipokea roho ya Mungu kwa njia ya pekee. (Soma Matendo 2:1-4.) Biblia ilitabiri kwamba roho takatifu ingemiminwa. Ilisema hivi: “Nitaimimina [Yehova] roho yangu juu ya kila namna ya mwili, na wana wenu na binti zenu watatoa unabii . . . Na hata juu ya watumishi wa kiume na juu ya wajakazi nitaimimina roho yangu.” (Yoe. 2:28, 29) Muujiza huo uliotokea katika siku ya Pentekoste ulionyesha kwamba Mungu aliliacha taifa la Israeli lililoasi imani na kuchagua taifa la “Israeli wa Mungu,” lililofanyizwa na wanaume na wanawake. (Gal. 3:28; 6:15, 16) Binti wanne wa Filipo yule mweneza-injili walikuwa miongoni mwa wanawake Wakristo waliohudumu katika karne ya kwanza.—Mdo. 21:8, 9.

 “JESHI KUBWA” LA WANAWAKE

18, 19. (a) Kuhusiana na ibada ya kweli, Mungu amewapa wanaume na wanawake pendeleo gani? (b) Mtunga-zaburi anasema nini kuhusu wanawake wanaotangaza habari njema?

18 Mwishoni mwa miaka ya 1800, wanaume na wanawake wachache walipendezwa sana na ibada ya kweli. Walikuwa wa kwanza kutimiza unabii huu wa Yesu: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mt. 24:14.

19 Kikundi hicho kidogo cha Wanafunzi wa Biblia kimeongezeka na sasa kuna Mashahidi wa Yehova 8,000,000 hivi. Watu wengine zaidi ya 11,000,000 wanaonyesha kwamba wanapendezwa na Biblia na kazi yetu kwa kuhudhuria Ukumbusho wa kifo cha Yesu kila mwaka. Katika nchi nyingi, idadi kubwa ya wanaohudhuria ni wanawake. Pia, idadi kubwa ya wahubiri wa Ufalme wa wakati wote zaidi ya 1,000,000 ulimwenguni pote ni wanawake. Kwa kweli Mungu amewapa wanawake pendeleo la kushiriki katika kutimiza maneno haya ya mtunga-zaburi: “Yehova mwenyewe anasema neno hili; wanawake wanaotangaza habari njema ni jeshi kubwa.”—Zab. 68:11.

Wanawake wanaotangaza habari njema kwa kweli ni “jeshi kubwa” (Tazama fungu la 18 na 19)

WANAWAKE WANAOMWOGOPA MUNGU WATAPATA BARAKA NYINGI

20. Tunaweza kuwa na miradi gani ya kujifunza?

20 Hatuwezi kuzungumzia wanawake wengi waaminifu wanaotajwa katika Biblia. Hata hivyo, sote tunaweza kusoma kuwahusu katika Neno la Mungu na katika makala zinazopatikana katika machapisho yetu. Kwa mfano, tunaweza kutafakari kuhusu ushikamanifu wa Ruthu. (Rut. 1:16, 17) Imani yetu inaweza kuimarika tukisoma kitabu cha Biblia kilichopewa jina la Malkia Esta na makala mbalimbali kumhusu. Tunaweza kunufaika tukiwa na miradi ya kujifunza masimulizi kama hayo katika jioni za Ibada ya Familia. Ikiwa tunaishi peke yetu, tunaweza kufanya hivyo katika funzo letu la kibinafsi.

21. Wanawake wanaomwogopa Mungu wameonyeshaje ujitoaji wao kwa Yehova katika nyakati ngumu?

21 Ni wazi kwamba Yehova huwabariki wanawake Wakristo wanapohubiri, naye huwategemeza nyakati za majaribu. Kwa mfano, kwa msaada wa Yehova, wanawake waliomwogopa walidumisha utimilifu wao wakati wa utawala wa Wanazi na Wakomunisti. Wengi wao waliteseka na hata baadhi yao waliuawa kwa sababu ya kumtii Mungu. (Mdo. 5:29) Kama ilivyokuwa katika nyakati za kale, dada zetu pamoja na waabudu wenzao wote wanaunga mkono enzi kuu ya Mungu leo. Kama ilivyokuwa kwa taifa la kale la Israeli, ni kana kwamba Yehova anaushika mkono wao wa kuume na kusema: “Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.”—Isa. 41:10-13.

22. Tunatazamia mapendeleo gani ya wakati ujao?

22 Hivi karibuni, wanaume na wanawake wanaomwogopa Mungu wataifanya dunia kuwa paradiso na kuwafundisha mamilioni ya watu watakaofufuliwa makusudi ya Yehova. Kabla ya wakati huo, iwe sisi ni wanaume au wanawake, acheni tuthamini pendeleo letu la kumtumikia Yehova “bega kwa bega.”—Sef. 3:9.