Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sikia Sauti ya Yehova Popote Ulipo

Sikia Sauti ya Yehova Popote Ulipo

“Masikio yako yatasikia neno nyuma yako likisema: ‘Hii ndiyo njia.’”—ISA. 30:21.

1, 2. Yehova huwasilianaje na watumishi wake?

BIBLIA inaonyesha kwamba Yehova aliwapa wanadamu mwongozo kwa njia mbalimbali katika nyakati za kale. Mungu aliwajulisha baadhi yao mambo ya wakati ujao kupitia malaika, maono, au ndoto. Yehova aliwapa pia migawo hususa. (Hes. 7:89; Eze. 1:1; Dan. 2:19) Yehova aliwapa wengine maagizo kupitia wanadamu waliomwakilisha na kutumika katika sehemu ya kidunia ya tengenezo lake. Haidhuru Yehova alitumia njia gani kuwapa watu wake maagizo, wale walioyafuata walibarikiwa.

2 Leo, Yehova huongoza watu wake kwa kutumia Biblia, roho yake takatifu, na kutaniko. (Mdo. 9:31; 15:28; 2 Tim. 3:16, 17) Tunapokea mwongozo ulio wazi sana hivi kwamba ni kama ‘masikio yetu yanasikia neno nyuma yetu likisema: “Hii ndiyo njia. Tembea ndani yake.”’ (Isa. 30:21) Pia, Yesu anatufunulia sauti ya Yehova anapoliongoza kutaniko kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Tunahitaji kuchukua kwa uzito mwongozo na mwelekezo huo, kwa sababu hatutapata uzima wa milele tusipotii.—Ebr. 5:9.

3. Ni nini kinachoweza kuathiri jinsi tunavyoitikia miongozo ya Yehova? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

3 Shetani Ibilisi ameazimia kutupotosha ili tusitii mwongozo wa Yehova unaookoa uhai. Isitoshe, ‘moyo wetu wenye hila’  unaweza kuathiri jinsi tunavyoitikia miongozo ya Yehova. (Yer. 17:9) Kwa hiyo, acheni tuone jinsi tunavyoweza kushinda vipingamizi vinavyofanya iwe vigumu kwetu kusikiliza sauti ya Mungu. Tutazungumzia pia jinsi mawasiliano mazuri na Yehova yatakavyolinda uhusiano wetu naye licha ya hali zetu.

KUPINGA HILA ZA SHETANI

4. Shetani hujaribuje kupotosha fikira za watu?

4 Shetani hujaribu kupotosha fikira za watu kwa kueneza habari za uwongo na propaganda za udanganyifu. (Soma 1 Yohana 5:19.) Machapisho, redio, televisheni, na Intaneti zinaeneza habari duniani pote, hata katika maeneo ya mbali zaidi. Ingawa nyakati nyingine vyombo vya habari huzungumzia mambo yenye faida, mara nyingi vinatetea mwenendo na viwango visivyopatana na viwango vya Yehova. (Yer. 2:13) Kwa mfano, vyombo vya habari na burudani huzungumzia ndoa za watu wa jinsia moja kana kwamba zinakubalika, na watu wengi wanahisi kwamba mafundisho ya Biblia kuhusu mahusiano hayo yamepita kiasi.—1 Kor. 6:9, 10.

5. Tunawezaje kuepuka kupotoshwa na propaganda za Shetani?

5 Wale wanaopenda uadilifu wa Mungu wanawezaje kuepuka kupotoshwa na propaganda za Shetani zilizoenea sana leo? Wanawezaje kutofautisha mema na mabaya? ‘Kwa kujilinda kulingana na neno la Mungu’! (Zab. 119:9) Neno la Mungu lina mwongozo muhimu unaotuwezesha kutofautisha habari ya kweli na propaganda za uwongo. (Met. 23:23) Yesu alinukuu Maandiko aliposema kwamba “mwanadamu ataishi . . . kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mt. 4:4) Tunahitaji kujifunza jinsi ya kutumia kanuni za Biblia maishani mwetu. Kwa mfano, muda mrefu kabla ya Musa kuandika sheria ya Yehova kuhusu uzinzi, kijana Yosefu alielewa kwamba mwenendo huo ulikuwa dhambi dhidi ya Mungu. Mke wa Potifa alipomshawishi atende dhambi, hakufikiria kamwe kutomtii Yehova. (Soma Mwanzo 39:7-9.) Hata baada ya kushinikizwa kwa muda mrefu na mke wa Potifa, Yosefu alisikiliza sauti ya Yehova badala ya sauti ya mke wa Potifa. Ili kutofautisha mema na mabaya, ni muhimu tuisikilize sauti ya Yehova na kutosikiliza kamwe kelele zisizokoma za propaganda za Shetani.

6, 7. Ni lazima tufanye nini ili tuepuke mashauri maovu ya Shetani?

6 Ulimwengu umejaa sana mafundisho na imani za kidini zinazopingana hivi kwamba watu wengi wanahisi kwamba ni ubatili kutafuta dini ya kweli. Hata hivyo, Yehova ametoa miongozo iliyo wazi kabisa kwa ajili ya wale wanaotaka kunufaika nayo. Ni lazima tuamue ni nani tutakayemsikiliza. Kwa kuwa haiwezekani kusikiliza sauti mbili wakati uleule, tunahitaji ‘kuijua sauti’ ya Yesu na kumsikiliza. Ndiye  aliyewekwa rasmi na Yehova kuongoza kondoo Zake.—Soma Yohana 10:3-5.

7 Yesu alisema hivi: “Sikilizeni kwa makini mambo ambayo mnasikia.” (Marko 4:24) Mashauri ya Yehova yako wazi na yanafaa, lakini ni lazima tutayarishe moyo wetu ili tusikilize kwa makini na kuyafuata. Tusipokuwa waangalifu, tunaweza kusikiliza mashauri maovu ya Shetani badala ya mashauri ya Mungu ya upendo. Usiruhusu kamwe ulimwengu uongoze maisha yako, iwe ni kupitia muziki, video, vipindi vya televisheni, vitabu, watu unaoshirikiana nao, walimu, au wale wanaoitwa wataalamu.—Kol. 2:8.

8. (a) Moyo wetu unawezaje kutufanya tunaswe kwa urahisi na hila za Shetani? (b) Tunaweza kupatwa na nini tukipuuza dalili zozote za kuonya?

8 Shetani anajua kwamba tuna mielekeo ya dhambi, naye hujaribu kutushawishi tuifuate. Shetani anapotushawishi kwa njia hiyo, inakuwa vigumu sana kwetu kuendelea kuwa watimilifu. (Yoh. 8:44-47) Tunawezaje kushinda kishawishi hicho? Mfikirie mtu anayeshawishiwa sana kutosheleza tamaa ya muda na hivyo kufanya kosa ambalo hakufikiri angetenda kamwe. (Rom. 7:15) Ni nini kilichosababisha hali hiyo yenye kuhuzunisha? Inaelekea kwamba pole kwa pole, mtu huyo aliacha kusikiliza sauti ya Yehova. Huenda hakutambua dalili zilizomwonya kuhusu hali ya moyo wake au aliamua kuzipuuza. Kwa mfano, huenda aliacha kusali, akapunguza bidii yake katika huduma, au akaanza kukosa kuhudhuria mikutano. Hatimaye, tamaa yake ilimwongoza kufanya jambo alilojua kwamba ni kosa. Tunaweza kuepuka kufanya kosa kama hilo linaloleta msiba tukiendelea kuwa macho ili kutambua dalili zozote za kuonya na kufanya marekebisho mara moja. Na ikiwa tunaisikiliza sauti ya Yehova, tutakataa kabisa mawazo yoyote ya waasi-imani.—Met. 11:9.

9. Kwa nini ni muhimu sana kugundua mapema mielekeo ya dhambi?

9 Uhai wa mtu unaweza kuokolewa ugonjwa ukigunduliwa mapema. Vivyo hivyo, tunaweza kuepuka msiba tukitambua haraka mielekeo inayoweza kutuongoza kwenye kishawishi. Baada tu ya kugundua mielekeo hiyo, ni jambo la hekima kwetu kuchukua hatua ya haraka kabla Shetani ‘hajatushika tukiwa hai kwa ajili ya mapenzi yake.’ (2 Tim. 2:26) Tunapaswa kufanya nini tukigundua kwamba tumeanza kufikiri na kutamani mambo yasiyopatana na matakwa ya Yehova? Ni lazima tumrudie kwa unyenyekevu bila kukawia,  tusikilize mashauri yake, na kumsikiliza kwa moyo wetu wote. (Isa. 44:22) Ni lazima tutambue kwamba tukifanya uamuzi mbaya, tunaweza kuumia sana na kupata madhara makubwa katika mfumo huu wa mambo. Ni bora kuchukua hatua ya haraka ili kuepuka kufanya kosa zito kama hilo.

Mazoea mazuri ya kiroho yanawezaje kukulinda dhidi ya hila za Shetani? (Tazama fungu la 4-9)

KUSHINDA KIBURI NA PUPA

10, 11. (a) Huenda mtu mwenye kiburi akatendaje? (b) Tunajifunza nini kutokana na uasi wa Kora, Dathani, na Abiramu?

10 Ni lazima tutambue kwamba moyo wetu unaweza kutupotosha. Mielekeo ya dhambi ina nguvu sana juu yetu! Kwa mfano, fikiria kiburi na pupa. Fikiria jinsi kila moja ya tabia hizo inavyoweza kuathiri jinsi tunavyosikiliza sauti ya Yehova na kutuongoza kwenye msiba. Mtu mwenye kiburi anajiona kuwa bora sana. Huenda akahisi kwamba ana haki ya kufanya lolote analotaka na hakuna yeyote anayeweza kumwambia jambo la kufanya. Basi anaweza kuhisi kwamba Wakristo wenzake, wazee, au hata tengenezo la Mungu halipaswi kumpa maagizo na mashauri. Ni kana kwamba hasikii vizuri sauti ya Yehova.

11 Waisraeli walipokuwa nyikani, Kora, Dathani, na Abiramu waliasi mamlaka ya Musa na Haruni. Kwa sababu ya kiburi, waasi hao walifanya mipango yao wenyewe ya kumwabudu Yehova. Yehova alitendaje? Aliwaangamiza. (Hes. 26:8-10) Simulizi hilo la kihistoria linatufundisha somo muhimu kama nini! Kumwasi Yehova huongoza kwenye msiba. Acheni pia tukumbuke kwamba “kiburi hutangulia kuanguka.”—Met. 16:18; Isa. 13:11.

12, 13. (a) Ni mfano gani unaoonyesha kwamba pupa inaweza kusababisha msiba? (b) Eleza jinsi pupa inavyoweza kukua haraka isipong’olewa.

12 Pia, fikiria kuhusu pupa. Mara nyingi mtu mwenye pupa huchukua vitu visivyo vyake na kujiendesha kwa njia isiyofaa. Naamani, mkuu wa jeshi la Siria alipoponywa ukoma, alimpa nabii Elisha zawadi, lakini alizikataa. Hata hivyo, Gehazi, mtumishi wa Elisha alitamani zawadi hizo. Gehazi akajiambia hivi: “Kama Yehova anavyoishi, nitakimbia nimfuate [Naamani], nichukue kitu fulani kutoka kwake.” Bila kumwambia Elisha, alikimbia na kumfuata Naamani na kusema uwongo ulio wazi ili apate “talanta moja ya fedha na mavazi mawili.” Ni nini kilichotokea baada ya Gehazi kufanya hivyo na kumdanganya nabii wa Yehova? Ukoma wa Naamani ulimshika Gehazi mwenye pupa.—2 Fal. 5:20-27.

13 Huenda pupa ikaanza pole kwa pole, lakini isipong’olewa, inaweza kukua haraka na kumnasa mtu. Simulizi la Biblia kumhusu Akani linaonyesha nguvu za pupa. Angalia jinsi pupa ya Akani ilivyositawi haraka. Alisema hivi: “Nilipoona katikati ya nyara vazi rasmi kutoka Shinari, lenye kupendeza, na shekeli 200 za fedha na kipande kimoja cha dhahabu, uzito wake ukiwa shekeli 50, ndipo nikavitamani vitu hivyo, halafu nikavichukua.” Badala ya kukataa kabisa tamaa mbaya, Akani aliiba kwa pupa vitu hivyo na kuvificha katika hema lake. Dhambi ya Akani ilipojulikana, Yoshua alimwambia kwamba Yehova angeleta laana juu yake. Akani na familia yake waliuawa kwa kupigwa mawe siku hiyohiyo. (Yos. 7:11, 21, 24, 25) Tunakabili daima hatari ya kunaswa na pupa. Kwa hiyo, acheni ‘tujilinde na kila namna ya tamaa,’ yaani, pupa. (Luka 12:15) Ingawa nyakati fulani huenda tukafikiria au kuwazia mambo yasiyofaa, ni muhimu sana kudhibiti akili yetu na kutoruhusu tamaa zetu kusitawi na kutuchochea kutenda dhambi.—Soma Yakobo 1:14, 15.

14. Tunapaswa kufanya nini tukigundua kwamba tuna mielekeo ya kiburi na pupa?

 14 Kiburi na pia pupa inaweza kusababisha msiba. Kutafakari kuhusu matokeo ya kufuatilia mwenendo usiofaa kutatusaidia kutoruhusu mielekeo kama hiyo ituzuie kuisikiliza sauti ya Yehova. (Kum. 32:29) Katika Biblia, Mungu wa kweli hatuambii tu njia inayofaa bali pia anatueleza faida za kuifuata na matokeo ya kufuata njia isiyofaa. Moyo wetu ukitushawishi kutenda jambo lisilofaa kwa sababu ya kiburi au pupa, ni jambo la hekima kufikiria matokeo. Tunapaswa kufikiria jinsi kosa hilo litakavyotuathiri, litakavyoathiri wapendwa wetu, na hasa uhusiano wetu na Yehova.

DUMISHA MAWASILIANO MAZURI NA YEHOVA

15. Mfano wa Yesu unatufundisha nini kuhusu mawasiliano na Yehova?

15 Yehova anataka tuwe na maisha bora. (Zab. 1:1-3) Anaandaa msaada wa kutosha wakati tunapouhitaji. (Soma Waebrania 4:16.) Ingawa Yesu alikuwa mkamilifu, alitegemea mawasiliano ya kawaida pamoja na Yehova, naye alisali bila kuacha. Yehova alimtegemeza na kumwongoza Yesu kwa njia nzuri sana. Aliwatuma malaika wamhudumie, akampa roho Yake takatifu ili imsaidie, na kumwongoza alipowachagua wale mitume 12. Sauti ya Yehova ilisikika kutoka mbinguni, akionyesha kwamba alimuunga mkono na kumkubali Yesu. (Mt. 3:17; 17:5; Marko 1:12, 13; Luka 6:12, 13; Yoh. 12:28) Tunahitaji kumimina moyo wetu katika sala kwa Mungu kama Yesu alivyofanya. (Zab. 62:7, 8; Ebr. 5:7) Kupitia sala, tunaweza kudumisha mawasiliano mazuri na Yehova na kuishi maisha yanayomletea heshima.

16. Yehova anatusaidiaje kuisikia sauti yake?

16 Ingawa Yehova hufanya iwe rahisi kwa yeyote kupata mashauri yake, halazimishi mtu yeyote kuyafuata. Tunahitaji kumwomba roho yake takatifu, naye atatupatia kwa ukarimu. (Soma Luka 11:10-13.) Hata hivyo, ni muhimu kwetu ‘kukazia uangalifu jinsi tunavyosikiliza.’ (Luka 8:18) Kwa mfano, lingekuwa jambo la kinafiki kumwomba Yehova atusaidie kuepuka mwelekeo wa kupenda mambo machafu na huku tukiendelea kutazama ponografia au sinema chafu. Ili atusaidie, tunahitaji kuwa katika hali au mahali penye roho ya Yehova. Tunajua kwamba roho yake iko kwenye mikutano ya kutaniko. Watumishi wengi wa Yehova wameepuka msiba kwa kumsikiliza Yehova mikutanoni. Hilo limewasaidia kugundua tamaa mbaya zinazositawi moyoni mwao na kurekebisha njia zao.—Zab. 73:12-17; 143:10.

ENDELEA KUSIKILIZA KWA MAKINI SAUTI YA YEHOVA

17. Kwa nini ni hatari kujitegemea?

17 Mfikirie Mfalme Daudi wa taifa la kale la Israeli. Akiwa kijana, alimshinda jitu Mfilisti Goliathi. Daudi akawa askari-jeshi, mfalme, mlinzi, na mfanya-maamuzi wa taifa la Israeli. Lakini Daudi alipojitegemea, moyo wake ulimdanganya naye akatenda dhambi nzito na Bath-sheba, hata alipanga ili Uria mume wake auawe. Daudi alipotiwa nidhamu, alikiri kwa unyenyekevu kosa lake na kurekebisha uhusiano wake na Yehova.—Zab. 51:4, 6, 10, 11.

18. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuendelea kusikiliza sauti ya Yehova?

18 Acheni tutii shauri linalopatikana katika 1 Wakorintho 10:12 na kutojiamini kupita kiasi. Kwa kuwa hatuwezi ‘kuongoza hatua yetu,’ tutasikiliza ama sauti ya Yehova au sauti ya Adui yake. (Yer. 10:23) Na tusali daima, tufuate mwongozo wa roho takatifu, na kusikiliza sikuzote kwa makini sauti ya Yehova.