Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Yehova Anavyotukaribia

Jinsi Yehova Anavyotukaribia

“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—YAK. 4:8.

1. Wanadamu wana uhitaji gani? Ni nani anayeweza kuutosheleza?

WANADAMU wana uhitaji mkubwa sana wa kuhisi kwamba wana uhusiano wa karibu na wengine. Kamusi moja inasema kwamba watu huwa na “uhusiano wa karibu wanapopendana na kufahamiana vizuri sana.” Kwa kawaida sisi hufurahi tukiwa na uhusiano mzuri na watu wa familia na marafiki wanaotuelewa, kututhamini, na kutupenda. Hata hivyo, Mtu tunayehitaji kusitawisha uhusiano wa karibu zaidi naye ni Muumba wetu Mkuu.—Mhu. 12:1.

2. Yehova anatuahidi nini? Lakini kwa nini watu wengi hawaamini ahadi hiyo?

2 Yehova anatuhimiza katika Neno lake ‘tumkaribie,’ na anatuahidi kwamba ‘atatukaribia’ tukifanya hivyo. (Yak. 4:8) Hilo linatia moyo kama nini! Hata hivyo, watu wengi wanafikiri kwamba Mungu hawezi kuwakaribia; wanahisi hawastahili kumkaribia au yuko mbali sana. Je, kwa kweli tunaweza kumkaribia Yehova?

3. Ni jambo gani tunalopaswa kujua kumhusu Yehova?

3 Ukweli ni kwamba Yehova “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu” anayetaka kumpata; na tunaweza kumjua. (Soma Matendo 17:26, 27; Zaburi 145:18.) Mungu wetu alikusudia wanadamu  wasio wakamilifu wawe na uhusiano wa karibu naye, na yuko tayari kuwakubali ili wawe rafiki zake wa karibu. (Isa. 41:8; 55:6) Kutokana na mambo aliyojionea maishani, mtunga-zaburi aliandika hivi kumhusu Yehova: “Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja. Mwenye furaha ni yule unayemchagua na kumfanya akaribie.” (Zab. 65:2, 4) Biblia inaonyesha jinsi Mfalme Asa wa Yuda alivyomkaribia Yehova, na jinsi Yehova alivyomkaribia. *

JIFUNZE KUTOKANA NA KIELELEZO CHA KALE

4. Mfalme Asa aliwawekea watu wa Yuda kielelezo gani?

4 Mfalme Asa alikuwa na bidii nyingi kwa ajili ya ibada safi. Aliondoa makahaba hekaluni na kukomesha ibada ya sanamu iliyoenea sana katika nchi. (1 Fal. 15:9-13) Akiwa na uhuru wa kusema, aliwahimiza watu “wamtafute Yehova Mungu wa mababu zao na kutenda sheria na amri.” Yehova alimbariki Asa na kwa miaka kumi ya kwanza ya utawala wake kulikuwa na amani kamili. Asa alisema ni kwa nini kulikuwa na amani? Alisema hivi: ‘Nchi bado inapatikana kwa ajili yetu, kwa sababu tumemtafuta Yehova Mungu wetu. Tumemtafuta, naye ametupa pumziko kuzunguka pande zote.’ (2 Nya. 14:1-7) Fikiria kilichotukia baadaye.

5. Ni hali gani iliyojaribu imani ya Asa, na matokeo yalikuwa nini?

5 Jiwazie ukiwa katika hali ya Asa. Zera Mwethiopia amekuja na watu 1,000,000 na magari 300 ili kupigana na Yuda. (2 Nya. 14:8-10) Ungetendaje ikiwa ungeona jeshi hilo kubwa likija kuwavamia? Una wanajeshi 580,000 tu! Idadi ya wanajeshi maadui ni karibu maradufu ya idadi ya wanajeshi wako. Je, ungeanza kujiuliza ni kwa nini Mungu ameruhusu uvamizi huo? Je, ungekabiliana na hatari hiyo ukitegemea hekima yako mwenyewe? Asa alitenda kwa njia iliyoonyesha kwamba alimtegemea Yehova na alikuwa na uhusiano wa karibu naye. Alisali hivi kwa bidii: “Utusaidie, Ee Yehova Mungu wetu, kwa maana sisi tunakuegemea wewe, nasi kwa jina lako tumekuja kupigana na umati huu. Ee Yehova, wewe ni Mungu wetu. Usiache mwanadamu anayeweza kufa apate nguvu juu yako.” Mungu alijibuje sala ya Asa iliyotoka moyoni? “Yehova akawashinda Waethiopia.” Hakuna adui hata mmoja aliyeokoka pambano hilo!—2 Nya. 14:11-13.

6. Tunapaswa kumwiga Asa jinsi gani?

6 Ni nini kilichomsaidia Asa kutegemea kabisa mwongozo na ulinzi wa Mungu? Biblia inasema kwamba ‘Asa alifanya yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova’ na kwamba “moyo wa Asa ulikuwa mkamilifu kwa Yehova.” (1 Fal. 15:11, 14) Sisi pia tunapaswa kumtumikia Mungu tukiwa na moyo mkamilifu. Ni muhimu sana kufanya hivyo ili tuwe na uhusiano wa karibu naye sasa na wakati ujao. Tunashukuru sana kwamba Yehova amechukua hatua ya kwanza kutuvuta kwake na kutusaidia kusitawisha na kudumisha uhusiano wa karibu pamoja naye. Fikiria njia mbili ambazo Mungu ametumia kufanya hivyo.

YEHOVA AMETUVUTA KUPITIA FIDIA

7. (a) Yehova amefanya mambo gani na hivyo kutuvuta kwake? (b) Mungu anatuvuta kupitia njia gani hasa?

7 Yehova alionyesha kwamba anaipenda familia ya wanadamu kwa kuumba dunia, makao yetu maridadi. Anaendelea kutuonyesha upendo kwa kutuandalia mahitaji mazuri sana ya kimwili yanayoendeleza uhai wetu. (Mdo. 17:28; Ufu. 4:11) Jambo  muhimu zaidi ni kwamba Yehova anatuandalia mahitaji yetu ya kiroho. (Luka 12:42) Anatuhakikishia pia kwamba yeye mwenyewe ndiye anayesikiliza sala zetu. (1 Yoh. 5:14) Hata hivyo, upendo ambao Mungu alituonyesha kupitia fidia ndio hasa unaotuvuta kwake na ndio unaotufanya tumkaribie. (Soma 1 Yohana 4:9, 10, 19.) Yehova alimtuma “Mwana wake mzaliwa-pekee” duniani ili tuweze kukombolewa kutoka katika dhambi na kifo.—Yoh. 3:16.

8, 9. Yesu anatimiza jukumu gani katika kusudi la Yehova?

8 Yehova amehakikisha kwamba wale walioishi kabla ya fidia ya Kristo kutolewa wananufaika pia. Tangu Yehova alipotabiri kuhusu Mwokozi wa wanadamu, kwa maoni yake ni kana kwamba fidia ilikuwa tayari imelipwa, kwa kuwa alijua kwamba kusudi lake halitashindwa. (Mwa. 3:15) Karne nyingi baadaye, mtume Paulo alimshukuru Mungu kwa “kuachiliwa huru kwa njia ya fidia ambayo Kristo Yesu alilipa.” Paulo aliongezea hivi: “Alikuwa akizisamehe dhambi zilizotokea wakati uliopita wakati Mungu alipokuwa akivumilia kwa subira.” (Rom. 3:21-26) Kwa kweli, Yesu anatimiza jukumu muhimu sana katika kutusaidia kumkaribia Mungu.

9 Watu wanyenyekevu wanaweza kumjua Yehova na kuwa na uhusiano mzuri na wa karibu pamoja naye kupitia Yesu tu. Maandiko yanakaziaje ukweli huo? Paulo aliandika hivi: “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Rom. 5:6-8) Dhabihu ya fidia ya Yesu ilitolewa si kwa sababu tunastahili, bali kwa sababu tunapendwa. Yesu alisema hivi: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.” Katika pindi nyingine, alisema hivi: “Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yoh. 6:44; 14:6) Yehova anatumia roho takatifu kumvuta mtu mmoja-mmoja kupitia Yesu, na kumsaidia kubaki katika upendo Wake ili apate uzima wa milele. (Soma Yuda 20, 21.) Fikiria njia nyingine anayotumia Yehova kutuvuta kwake.

YEHOVA ANATUVUTA KUPITIA NENO LAKE LILILOANDIKWA

10. Biblia inatufundisha nini kinachotusaidia kumkaribia zaidi Mungu?

10 Katika mazungumzo yetu, tumenukuu au kutaja maandiko kutoka katika vitabu 14 vya Biblia. Kama hatungekuwa na Biblia, tungejuaje kwamba tunaweza kumkaribia Muumba wetu? Tungejifunzaje kuhusu fidia na kwamba Yehova ametuvuta kupitia Yesu? Yehova alitumia roho yake kuwaongoza watu kuandika Biblia inayotufunulia utu wake unaovutia na makusudi yake matukufu. Kwa mfano, katika andiko la Kutoka 34:6 na 7, Yehova alimwambia Musa kuwa yeye ni “Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli, anayehifadhi fadhili zenye upendo kwa ajili ya maelfu, anayesamehe kosa na ubaya na dhambi.” Sote huvutiwa na mtu wa namna hiyo, sivyo? Yehova anajua kwamba kadiri tunavyojifunza kumhusu kupitia Biblia, ndivyo atakavyokuwa halisi zaidi kwetu na ndivyo tutavyomkaribia zaidi.

11. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kujifunza kuhusu sifa na njia za Mungu? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 16.)

11 Utangulizi wa kitabu Mkaribie Yehova unasema hivi kuhusu jinsi tunavyoweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu: “Ili kuwa na urafiki na mtu yeyote, ni lazima tumjue mtu huyo, tuvutiwe na sifa zake za pekee na kuzithamini. Hivyo  basi, ni muhimu sana kwetu kujifunza kuhusu sifa na njia za Mungu za kutenda mambo, kama zinavyofunuliwa na Biblia.” Tunashukuru sana kwamba Yehova alihakikisha Neno lake limeandikwa kwa njia ambayo sisi wanadamu tunaweza kuelewa.

12. Kwa nini Yehova alitumia wanadamu kuandika Biblia?

12 Yehova angeweza kutumia malaika kuandika Biblia. Kwa kweli, wanapendezwa sana nasi na yale tunayofanya. (1 Pet. 1:12) Bila shaka, malaika wangeweza kuandika ujumbe wa Mungu kwa wanadamu. Hata hivyo, je, wangekuwa na maoni kama ya wanadamu kuhusu mambo? Je, wangeweza kuelewa mahitaji yetu, udhaifu wetu, na mapendezi yetu? Hapana, na Yehova alijua jambo hilo. Kwa kutumia wanadamu kuandika Biblia, Yehova ameifanya iguse hisia zetu. Tunaweza kuelewa mawazo na hisia za waandikaji wa Biblia na watu wengine wanaotajwa katika Maandiko. Biblia inaposema kwamba walivunjika moyo, walikuwa na shaka, hofu, na kwamba walikosea, tunaweza kuelewa hisia zao. Tunaweza pia kushangilia tunaposoma kuhusu shangwe na mafanikio yao. Sawa na nabii Eliya, waandikaji wote wa Biblia walikuwa na “hisia kama zetu.”—Yak. 5:17.

Kuchunguza jinsi Yehova alivyoshughulika na Yona na Petro kunakusaidiaje kumkaribia zaidi? (Tazama fungu la 13 na 15)

13. Unahisije unaposoma sala ya Yona?

13 Kwa mfano, fikiria jambo hili: Je, malaika angeweza kueleza kikamili hisia za Yona alipokimbia mgawo aliopewa na Mungu? Ni vyema kwamba Yehova alimtumia Yona kuandika simulizi lake, kutia ndani sala aliyotoa kwa bidii alipokuwa katika vilindi vya bahari. Yona alisema hivi: “Nafsi yangu ilipozimia ndani yangu, Yehova Ndiye niliyemkumbuka.”—Yona 1:3, 10; 2:1-9.

14. Kwa nini unaweza kuelewa mambo aliyoandika Isaya kuhusu hali yake?

14 Fikiria pia yale ambayo Yehova  alimwongoza Isaya kuandika kuhusu hali yake. Baada ya kuona utukufu wa Mungu katika maono, nabii huyo aliandika hivi kuhusu hali yake ya dhambi: “Ole wangu! Kwa maana ni kama nimenyamazishwa, kwa sababu mimi ni mtu asiye na midomo safi, nami ninakaa katikati ya watu wasio na midomo safi; kwa maana macho yangu yamemwona Mfalme, Yehova wa majeshi, mwenyewe!” (Isa. 6:5) Je, unafikiri malaika angehisi hivyo? Lakini Isaya alihisi hivyo, nasi tunaweza kuelewa hisia zake.

15, 16. (a) Kwa nini tunaweza kuelewa hisia za wanadamu wenzetu? Toa mifano. (b) Ni nini kitakachotusaidia kumkaribia Yehova zaidi?

15 Je, malaika wangeweza kusema ‘hawastahili,’ kama Yakobo alivyosema, au kuhisi wakiwa ‘wenye dhambi,’ kama Petro alivyohisi? (Mwa. 32:10; Luka 5:8) Je, huenda ‘wangeogopa,’ kama wanafunzi wa Yesu, au je, malaika waadilifu wangehitaji ‘kujipa ujasiri’ ikiwa wangepingwa katika kazi ya kuhubiri habari njema, kama Paulo na wengine walivyohitaji kufanya? (Yoh. 6:19; 1 The. 2:2) Hapana, malaika ni wakamilifu katika kila jambo na wana nguvu zinazozidi za wanadamu. Hata hivyo, wanadamu wasio wakamilifu wanapoonyesha hisia hizo, tunaelewa mara moja kwa kuwa sisi pia ni wanadamu. Kwa kweli, tunaposoma Neno la Mungu, tunaweza ‘kushangilia pamoja na watu wanaoshangilia; kulia pamoja na watu wanaolia.’—Rom. 12:15.

16 Tukitafakari inachosema Biblia kuhusu jinsi Yehova alivyoshughulika na watumishi wake waaminifu wa kale, tutajifunza mambo mengi sana yenye kupendeza kuhusu Mungu wetu, ambaye kwa subira na upendo, aliwakaribia wanadamu hao wasio wakamilifu. Hivyo, tutamjua Yehova vizuri zaidi na kumpenda sana. Na hivyo tutaweza kumkaribia zaidi.—Soma Zaburi 25:14.

SITAWISHA UHUSIANO IMARA PAMOJA NA MUNGU

17. (a) Azaria alimpa Asa shauri gani zuri? (b) Asa alipuuzaje shauri la Azaria, na matokeo yalikuwa nini?

17 Baada ya Mfalme Asa kupata ushindi mkubwa dhidi ya jeshi la Waethiopia, Azaria, nabii wa Mungu, alimwambia mfalme na watu wake maneno ya hekima. Azaria alisema hivi: “Yehova yuko pamoja nanyi ikiwa ninyi mko pamoja naye; nanyi mkimtafuta, atawaruhusu mumpate, lakini mkimwacha yeye atawaacha ninyi.” (2 Nya. 15:1, 2) Hata hivyo, baadaye Asa hakufuata shauri hilo zuri. Ufalme wa kaskazini wa Israeli ulipotisha kushambulia ufalme wake, Asa aliwaomba Wasiria wamsaidie. Badala ya kumwomba tena Yehova msaada, alifanya agano na wapagani. Kwa kufaa, Asa aliambiwa hivi: “Umetenda kwa upumbavu kwa habari hii, kwa maana tangu sasa na kuendelea kutakuwa na vita juu yako.” Na kwa kweli vita viliendelea katika miaka iliyobaki ya utawala wake. (2 Nya. 16:1-9) Tunajifunza nini?

18, 19. (a) Tufanye nini ikiwa tumeanza kujitenga na Mungu? (b) Tunawezaje kumkaribia zaidi Yehova?

18 Hatupaswi kamwe kujitenga na Yehova. Ikiwa tumeanza kujitenga naye, tunapaswa kutenda kulingana na andiko la Hosea 12:6 linalosema hivi: “Wewe inakupasa kurudi kwa Mungu wako, ushike fadhili zenye upendo na haki; nawe umtumaini Mungu wako sikuzote.” Hivyo, na tuendelee kumkaribia zaidi Yehova kwa kutafakari kwa uthamini fidia na kujifunza kwa bidii Neno lake, Biblia.—Soma Kumbukumbu la Torati 13:4.

19 Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Kumkaribia Mungu ni kwema kwangu.” (Zab. 73:28) Sote na tuendelee kujifunza mambo mapya kumhusu Yehova ili tuthamini hata zaidi sababu nyingi tulizo nazo za kumpenda. Yehova na aendelee kutukaribia zaidi sasa na kwa umilele wote!

^ fu. 3 Tazama makala kuhusu Asa yenye kichwa “Kuna Thawabu kwa Ajili ya Kazi Yenu,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, Agosti 15, 2012.