Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Yesu aliwaambia Masadukayo kwamba watakaofufuliwa ‘hawataoa wala kuolewa.’ (Luka 20:34-36) Je, alikuwa akizungumzia wale watakaofufuliwa na kuishi duniani?

Swali hilo ni muhimu sana, hasa kwa wale waliofiwa na mwenzi wao wa ndoa. Huenda wanatamani kuungana tena katika ulimwengu mpya na mwenzi wao wa ndoa atakayefufuliwa. Mjane mmoja alisema hivi: “Mimi na mke wangu tulitaka ndoa yetu idumu milele. Tulitamani moyoni kuendelea kumwabudu Mungu milele tukiwa mume na mke. Bado ninahisi hivyo mpaka sasa.” Je, kuna sababu nzuri ya kutumaini kwamba watakaofufuliwa watafunga ndoa? Kwa ufupi, hatujui.

Kwa miaka mingi, machapisho yetu yamesema kwamba maneno ya Yesu kuhusu ufufuo na kufunga ndoa huenda yanarejelea ufufuo wa wale watakaoishi duniani, na inaonekana kwamba watakaofufuliwa na kuishi katika ulimwengu mpya hawataoa au kuolewa. * (Mt. 22:29, 30; Marko 12:24, 25; Luka 20:34-36) Ingawa hatuna uhakika kuhusu jambo hilo, je, inawezekana kwamba maneno ya Yesu yanarejelea ufufuo wa wale watakaoishi mbinguni? Acheni tuchunguze alichosema Yesu.

Fikiria muktadha. (Soma Luka 20:27-33.) Masadukayo, ambao hawakuamini ufufuo, walimjaribu Yesu kwa kumuuliza swali kuhusu ufufuo na ndoa ya ndugu-mkwe. * Yesu alijibu hivi: “Watoto wa mfumo huu wa mambo huoa na huolewa, lakini wale ambao wamehesabiwa kustahili kuupata mfumo ule wa mambo na ufufuo kutoka kwa wafu hawaoi wala hawaolewi. Kwa kweli, wala hawawezi kufa tena kamwe, kwa maana wao ni kama malaika, nao ni watoto wa Mungu kwa kuwa watoto wa ufufuo.”—Luka 20:34-36.

Kwa nini machapisho yetu yalisema kwamba huenda Yesu alikuwa akizungumzia ufufuo wa wale watakaoishi duniani? Mkataa huo unategemea hasa sababu mbili. Kwanza, inaelekea Masadukayo walikuwa wakifikiria ufufuo wa duniani na hivyo Yesu angewajibu kwa kuzungumzia ufufuo huo. Pili, Yesu alimalizia kwa kutaja wazee wa ukoo waaminifu, yaani, Abrahamu, Isaka, na Yakobo, watakaofufuliwa na kuishi duniani.—Luka 20:37, 38.

Hata hivyo, inawezekana kwamba Yesu alikuwa akizungumzia ufufuo wa wale watakaoishi mbinguni. Kwa nini tunaweza kufikia mkataa huo? Acheni tuchunguze mambo mawili muhimu.

“Wale ambao wamehesabiwa kustahili kuupata . . . ufufuo kutoka kwa wafu.” Watiwa-mafuta waaminifu ‘wanahesabiwa kuwa wanastahili ufalme wa Mungu.’ (2 The. 1:5, 11) Wametangazwa kuwa waadilifu ili wapate uzima kwa msingi wa fidia, na hivyo hawafi wakiwa watenda-dhambi waliohukumiwa. (Rom. 5:1, 18; 8:1) Wanaitwa ‘wenye furaha na watakatifu’ na wanahesabiwa kuwa wanastahili kufufuliwa na kuishi mbinguni. (Ufu. 20:5, 6) Hata hivyo, wale watakaofufuliwa ili kuishi duniani watatia ndani “wasio waadilifu.” (Mdo. 24:15) Je, inaweza kusemwa kwamba wao pia ‘wanahesabiwa kuwa wanastahili’ kufufuliwa?

 “Wala hawawezi kufa tena kamwe.” Yesu hakusema: “Hawatakufa kamwe.” Badala yake, alisema hivi: “Wala hawawezi kufa tena kamwe.” Tafsiri nyingine zinasema “kifo hakina mamlaka juu yao tena” na “kifo hakina nguvu juu yao tena.” Watiwa-mafuta wanapokufa wakiwa waaminifu, wanafufuliwa mbinguni na kupewa uhai usioweza kufa, yaani, uhai usio na mwisho, usioweza kuharibika. (1 Kor. 15:53, 54) Kifo hakina tena nguvu juu ya wale wanaofufuliwa ili kuishi mbinguni. *

Hivyo, tunaweza kufikia mkataa gani tukizingatia mambo hayo? Inawezekana kwamba maneno ya Yesu kuhusu kufunga ndoa na ufufuo yanahusu ufufuo wa mbinguni. Ikiwa ni hivyo, basi maneno yake yanaonyesha mambo yafuatayo kuhusu wale wanaofufuliwa na kuishi mbinguni: Hawaoi au kuolewa, hawawezi kufa, na kwa kadiri fulani ni kama malaika, yaani, ni viumbe wa roho wanaoishi katika makao ya roho. Hata hivyo, mkataa huo unatokeza maswali mengi.

Kwanza, kwa nini Yesu alirejelea ufufuo wa kimbingu alipowajibu Masadukayo ambao huenda walikuwa wakifikiria ufufuo wa duniani? Nyakati nyingine Yesu hakujibu wapinzani wake kulingana na mawazo yao. Kwa mfano, aliwaambia hivi Wayahudi waliotaka awaonyeshe ishara: “Libomoeni hekalu hili, na katika siku tatu nitalisimamisha.” Inaelekea kwamba Yesu alijua watu hao walifikiria hekalu halisi, “lakini alikuwa akiongea juu ya hekalu la mwili wake.” (Yoh. 2:18-21) Huenda Yesu hakuona sababu ya kuwajibu Masadukayo hao wasio wanyoofu na wasioamini ufufuo wala kuwapo kwa malaika. (Met. 23:9; Mt. 7:6; Mdo. 23:8) Badala yake, huenda alitaka kufunua kweli kuhusu ufufuo wa kimbingu kwa faida ya wanafunzi wake wanyoofu ambao siku moja wangepata ufufuo huo.

Pili, kwa nini Yesu alimalizia mazungumzo yake kwa kurejelea Abrahamu, Isaka, na Yakobo, watakaofufuliwa na kuishi duniani? (Soma Mathayo 22:31, 32.) Ona kwamba Yesu alianza mazungumzo yake kuhusu wazee hao wa ukoo kwa maneno, “kwa habari ya ufufuo wa wafu.” Maneno hayo yanaweza kutusaidia kukazia fikira jambo lingine. Akirejelea maandishi ya Musa ambayo Masadukayo walidai kwamba wanakubali, Yesu alitaja maneno ambayo Yehova alimwambia Musa alipokuwa karibu na mti uliokuwa ukiwaka moto. Alifanya hivyo ili kuthibitisha zaidi kwamba ufufuo wa wale watakaoishi duniani ni kusudi la Mungu ambalo litatimia kwa hakika.—Kut. 3:1-6.

Tatu, ikiwa maneno ya Yesu kuhusu ufufuo na kufunga ndoa yanawahusu wale wanaofufuliwa ili kuishi mbinguni, je, hilo linamaanisha kwamba wale watakaofufuliwa duniani wataweza kuoa au kuolewa? Neno la Mungu halijibu swali hilo moja kwa moja. Ikiwa Yesu alikuwa akizungumzia ufufuo wa kimbingu, basi maneno yake hayaonyeshi ikiwa wale watakaofufuliwa duniani wataweza kuoa au kuolewa katika ulimwengu mpya.

Hata hivyo, tunajua Neno la Mungu linasema kwa uhakika kwamba kifungo cha ndoa hufikia mwisho wakati wa kifo. Kwa hiyo, mjane hahitaji kuhisi hatia akiamua kufunga ndoa tena. Huo ni uamuzi wa kibinafsi, na wanaofanya hivyo hawapaswi kushutumiwa wanapoamua kutafuta mwenzi wa ndoa.—Rom. 7:2, 3; 1 Kor. 7:39.

Inaeleweka kwamba huenda tukawa na maswali mengi kuhusu maisha katika ulimwengu mpya. Badala ya kukisia-kisia majibu ya maswali hayo, tunahitaji kusubiri na kuona mambo yatakavyokuwa. Hata hivyo, tuna uhakika huu: Wanadamu watiifu watakuwa na furaha kwa kuwa Yehova atatosheleza mahitaji yao na tamaa zao zote kwa njia bora zaidi.—Zab. 145:16.

^ fu. 4 Tazama Mnara wa Mlinzi, Juni 1, 1987, ukurasa wa 30-31.

^ fu. 5 Katika nyakati za Biblia, ilikuwa desturi kuwa na ndoa ya ndugu-mkwe, ambapo mwanamume angemwoa mjane aliyeachwa na ndugu yake aliyekufa bila kuzaa mtoto wa kiume na kuendeleza ukoo wa ndugu yake.—Mwa. 38:8; Kum. 25:5, 6.

^ fu. 9 Wale watakaofufuliwa ili kuishi duniani wana tumaini la kupata uzima wa milele, bali si hali ya kutoweza kufa. Ili kujifunza mengi zaidi kuhusu tofauti kati ya hali ya kutoweza kufa na uzima wa milele, tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kiingereza la Aprili 1, 1984, ukurasa wa 30-31.