Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Adui wa Mwisho, Kifo, Aangamizwa

Adui wa Mwisho, Kifo, Aangamizwa

“Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.”—1 KOR. 15:26.

1, 2. Ni hali gani ambazo Adamu na Hawa walifurahia mwanzoni, na ni maswali gani yanayotokea?

ADAMU na Hawa walipoumbwa, hawakuwa na adui yeyote. Walikuwa wanadamu wakamilifu na waliishi katika paradiso. Walikuwa na uhusiano wa karibu na Muumba wao wakiwa watoto wake. (Mwa. 2:7-9; Luka 3:38) Mgawo waliopewa na Mungu unaonyesha kusudi lake la kuwaumba. (Soma Mwanzo 1:28.) Baada ya muda, wangeweza ‘kuijaza dunia na kuitiisha.’ Hata hivyo, ili waendelee ‘kutawala kila kiumbe hai kinachotambaa juu ya dunia,’ Adamu na Hawa wangehitaji kuishi milele. Adamu hangekufa na kupoteza pendeleo lake la kusimamia viumbe wote.

2 Basi kwa nini hali ni tofauti sana leo? Kwa nini kuna maadui wengi sana wanaofanya wanadamu wakose furaha, adui mkubwa zaidi akiwa kifo? Mungu atawaangamizaje maadui hao wote? Biblia inajibu maswali hayo na mengine yanayohusiana nayo. Acheni tuchunguze majibu ya baadhi ya maswali hayo muhimu.

ONYO LA UPENDO

3, 4. (a) Mungu aliwapa Adamu na Hawa amri gani? (b) Kwa nini ilikuwa muhimu sana kutii amri hiyo?

3 Ingawa Adamu na Hawa walikuwa na tumaini la kuishi milele, hawakuwa na uhai usioweza kufa. Ili waendelee kuishi, ilikuwa lazima wanywe, wale chakula, walale, na kupumua hewa. Jambo muhimu zaidi ni kwamba uhai wao ulitegemea uhusiano wao na Mpaji-Uhai wao. (Kum. 8:3) Ili waendelee kufurahia maisha, walipaswa kukubali mwongozo wa Mungu. Yehova alimwambia Adamu jambo hilo waziwazi hata kabla ya kumuumba Hawa. Alimwambia nini? “Pia Yehova Mungu akamwekea mtu amri hii: ‘Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.’”—Mwa. 2:16, 17.

4 “Mti wa ujuzi wa mema na mabaya” uliwakilisha haki ya Mungu ya kuwaamulia yaliyo mema na mabaya. Bila shaka, tayari Adamu alikuwa na uwezo wa kujua mema na mabaya kwa sababu alikuwa na dhamiri na aliumbwa kwa mfano wa Mungu. Mti huo uliwakumbusha Adamu na Hawa kwamba walihitaji mwongozo wa Yehova sikuzote. Kula matunda ya mti huo kungeonyesha kwamba wanataka kuwa na uhuru wa kujiamulia mambo, na hivyo wao na wazao wao wangepata madhara makubwa sana. Amri ya Mungu na adhabu aliyotaja ilionyesha matokeo mabaya sana ya kufanya hivyo.

JINSI KIFO KILIVYOIFIKIA FAMILIA YA WANADAMU

5. Adamu na Hawa walishawishiwa jinsi gani kutomtii Yehova?

5 Baada ya Hawa kuumbwa, Adamu alimwambia amri ya Mungu. Hawa aliijua vizuri amri hiyo kwa sababu aliitaja tena neno kwa neno. (Mwa. 3:1-3) Alimtajia Shetani Ibilisi aliyezungumza naye kupitia nyoka, mnyama mwenye kujihadhari. Shetani alikuwa mwana wa roho wa Mungu aliyejiruhusu kusitawisha tamaa ya kujitegemea na kupata mamlaka. (Linganisha na Yakobo 1:14, 15.) Ili kutimiza malengo yake maovu, alidai kwamba Mungu alisema uwongo. Alimhakikishia Hawa kwamba ikiwa angejitegemea, hangekufa, badala yake angekuwa kama Mungu. (Mwa. 3:4, 5) Hawa alimwamini, akaamua kujitegemea kwa kula matunda hayo, kisha akamshawishi Adamu ajiunge naye. (Mwa. 3:6, 17) Ibilisi alisema uwongo. (Soma 1 Timotheo 2:14.) Hata hivyo, Adamu ‘aliisikiliza sauti ya mke wake.’ Ingawa nyoka alionekana kuwa rafiki, kwa kweli Shetani Ibilisi alikuwa adui mkatili aliyejua madhara makubwa sana ya uwongo aliomwambia Hawa.

6, 7. Yehova alitekelezaje hukumu dhidi ya wakosaji hao?

6 Kwa sababu za kibinafsi, Adamu na Hawa walimwasi Yule aliyewapa uhai na kila kitu walichokuwa nacho. Bila shaka, Yehova aliona mambo yote yaliyotukia. (1 Nya. 28:9; soma Methali 15:3.) Aliwaruhusu Adamu, Hawa, na Shetani waonyeshe jinsi walivyohisi kumhusu. Akiwa Baba yao, bila shaka Yehova aliumia sana moyoni. (Linganisha na Mwanzo 6:6.) Lakini akiwa Hakimu, aliwahukumu waasi hao kama alivyosema.

7 Mungu alikuwa amemwambia Adamu hivi: “Siku utakapokula [matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya], utakufa hakika.” Huenda Adamu alielewa kwamba “siku” hiyo ingekuwa ya saa 24. Baada ya kuasi amri ya Mungu, huenda alitarajia Yehova angewachukulia hatua kabla ya jua kutua. Yehova aliwafikia wenzi hao “wakati wenye upepo mtulivu wa siku.” (Mwa. 3:8) Alitenda kama hakimu mahakamani kwa kusikiliza majibu ya Adamu na Hawa ili athibitishe ukweli wa mambo. (Mwa. 3:9-13) Kisha akatangaza hukumu juu ya wakosaji hao. (Mwa. 3:14-19) Kama angewaangamiza papo hapo, kusudi lake kuhusu Adamu na Hawa na wazao wao halingetimia. (Isa. 55:11) Ingawa aliwahakikishia kwamba wangekufa, na wakaanza kuathiriwa na dhambi mara moja, aliwaruhusu Adamu na Hawa wazae watoto ambao wangenufaika na maandalizi mengine kutoka Kwake. Kwa hiyo, machoni pa Mungu, Adamu na Hawa walikufa siku ileile waliyotenda dhambi kwa kuwa miaka 1,000 ni kama “siku” moja kwa Yehova.—2 Pet. 3:8.

8, 9. Wazao wa Adamu waliathiriwaje na dhambi yake? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 23.)

8 Je, watoto wa Adamu na Hawa wangeathiriwa na kosa la wazazi wao? Ndio. Andiko la Waroma 5:12 linasema hivi: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” Abeli aliyekuwa mwaminifu ndiye aliyekufa kwanza. (Mwa. 4:8) Kisha, wazao wengine wa Adamu walizeeka na kufa. Je, walirithi dhambi na pia kifo? Mtume Paulo alijibu hivi: “Kupitia kutotii kwa mtu mmoja wengi walifanywa watenda-dhambi.” (Rom. 5:19) Wanadamu walirithi dhambi na kifo, maadui wasio na huruma na wanadamu wasio wakamilifu hawangeweza kuepuka maadui hao. Ingawa hatujui kwa uhakika jinsi wazao wote wa Adamu walivyorithi dhambi na kifo, tunaona matokeo yake.

9 Kwa kufaa, Biblia inasema kwamba dhambi na kifo tulichorithi ni “kifuniko kinachovifunika vikundi vyote vya watu, na mfumo uliofumwa kwa kusokotana juu ya mataifa yote.” (Isa. 25:7) Kifuniko au mfumo huo tata wa laana uliosokotwa na unaobana, unawanasa watu wote. Ukweli ni kwamba “katika Adamu wote wanakufa.” (1 Kor. 15:22) Basi Paulo aliuliza hivi: “Ni nani atakayeniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?” Je, kuna yeyote ambaye angeweza kumwokoa? *Rom. 7:24.

KUANGAMIZWA KWA DHAMBI NA KIFO TULICHORITHI KUTOKA KWA ADAMU

10. (a) Taja baadhi ya maandiko yanayoonyesha kwamba Yehova ataangamiza kifo tulichorithi kutoka kwa Adamu. (b) Maandiko hayo yanafunua nini kumhusu Yehova na Mwana wake?

10 Naam, Yehova angeweza kumwokoa Paulo. Baada tu ya kutaja “kifuniko,” Isaya aliandika hivi: “Atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” (Isa. 25:8) Kama baba anayeondoa hali inayofanya watoto wake wateseke na kufuta machozi yao, Yehova anatazamia kwa shangwe nyingi kuangamiza kifo tulichorithi kutoka kwa Adamu! Yesu anashirikiana naye kutimiza hilo. Andiko la 1 Wakorintho 15:22 linasema hivi: “Kwa maana kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.” Vivyo hivyo, baada ya Paulo kuuliza “Ni nani atakayeniokoa?” alisema hivi: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Rom. 7:25) Ni wazi kwamba upendo uliomchochea Yehova kuwaumba wanadamu haukupoa baada ya Adamu na Hawa kuasi. Na yule aliyeshirikiana na Yehova kuwafanya wenzi wawili wa kwanza hakupoteza upendo wake wa pekee kuelekea wazao wao. (Met. 8:30, 31) Lakini wanadamu wangeokolewaje?

11. Yehova alitoa uandalizi gani wa kuwasaidia wanadamu?

11 Wanadamu si wakamilifu na wanakufa kwa sababu ya dhambi ya Adamu na hukumu ya uadilifu ya Yehova. (Rom. 5:12, 16) Tunasoma hivi: “Kupitia kosa moja matokeo kwa watu wa namna zote yalikuwa kuhukumiwa hatia.” (Rom. 5:18) Yehova angeondoaje hukumu yake ya hatia bila kukiuka viwango vyake mwenyewe? Yesu alijibu swali hilo aliposema hivi: ‘Mwana wa binadamu alikuja kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.’ (Mt. 20:28) Baada ya kuzaliwa duniani akiwa mwanadamu mkamilifu, Mwana huyo wa Yehova aliyekuwa kiumbe wa kwanza wa roho alisema wazi kwamba angeandaa fidia. Fidia hiyo ingetimizaje haki?—1 Tim. 2:5, 6.

12. Ni fidia gani inayolingana iliyotimiza haki?

12 Akiwa mwanadamu mkamilifu, Yesu alikuwa na fursa ambazo Adamu alikuwa nazo kabla ya kufanya dhambi. Kusudi la Yehova lilikuwa kwamba dunia ijae wazao wakamilifu wa Adamu. Kwa hiyo, Yesu alidhabihu uhai wake wa kibinadamu kwa sababu alimpenda sana Baba yake na wazao wa Adamu. Naam, Yesu alidhabihu uhai wake mkamilifu wa kibinadamu uliolingana na uhai ambao Adamu alipoteza. Kisha, Yehova akamrudishia Mwana wake uhai akiwa kiumbe wa roho. (1 Pet. 3:18) Yehova aliikubali kwa haki dhabihu hiyo ya mwanadamu mmoja mkamilifu, Yesu, kuwa fidia, au bei ya kuinunua familia ya Adamu na kuwapa tumaini la uhai ambalo Adamu alipoteza. Kwa njia fulani, Yesu alichukua mahali pa Adamu. Paulo anasema hivi: “Hata imeandikwa hivi: ‘Mtu wa kwanza Adamu akawa nafsi hai.’ Adamu wa mwisho akawa roho inayotoa uhai.”—1 Kor. 15:45.

Abeli, mwanadamu wa kwanza kufa, atanufaishwa na fidia ya Yesu (Tazama fungu la 13)

13. “Adamu wa mwisho” atawasaidiaje wafu?

13 Hivi karibuni, “Adamu wa mwisho” atatenda akiwa “roho inayotoa uhai” kuelekea wanadamu kwa ujumla. Wazao wengi wa Adamu watafufuliwa. Kwa nini? Kwa sababu tayari wameishi na kufa. Watahitaji kufufuliwa, yaani, kurudishwa kwenye uhai duniani.—Yoh. 5:28, 29.

14. Ni uandalizi gani wa Yehova utakaoondoa hali ya kutokamilika ambayo wazao wa Adamu walirithi?

14 Wanadamu watawekwaje huru ili wasipambane tena na hali ya kutokamilika waliyorithi? Yehova alianzisha serikali ya Ufalme inayofanyizwa na “Adamu wa mwisho” na washiriki wenzake waliochaguliwa kutoka kati ya wanadamu. (Soma Ufunuo 5:9, 10.) Wale watakaotawala na Yesu mbinguni hawakuwa wakamilifu kwa hiyo wataelewa hali hiyo. Kwa miaka elfu moja, utawala wa Yesu na watawala wenzake utawasaidia wale walio duniani kuwa wakamilifu, hali ambayo hawangeweza kufikia kwa uwezo wao.—Ufu. 20:6.

15, 16. (a) Kwa nini ‘adui wa mwisho ni kifo,’ na kitaangamizwa wakati gani? (b) Kulingana na 1 Wakorintho 15:28, Yesu atafanya nini hatimaye?

15 Kufikia mwishoni mwa miaka elfu moja ya utawala wa Ufalme, wanadamu watiifu watakuwa wamewekwa huru kutokana na maadui wote walioletwa na uasi wa Adamu. Biblia inasema hivi: “Kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai. Lakini kila mmoja katika daraja lake mwenyewe: Kristo aliye matunda ya kwanza, baadaye wale walio wa Kristo [watawala wenzake] wakati wa kuwapo kwake. Halafu, ule mwisho, wakati atakapomkabidhi ufalme Mungu wake ambaye pia ni Baba yake, wakati atakapokuwa ameangamiza serikali yote na mamlaka yote na nguvu zote. Kwa maana ni lazima atawale akiwa mfalme mpaka Mungu awe ameweka adui zote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.” (1 Kor. 15:22-26) Naam, kifo tulichorithi kutoka kwa Adamu kitaangamizwa hatimaye. “Kifuniko” kinachoifunika familia yote ya wanadamu kitakuwa kimeondolewa milele.—Isa. 25:7, 8.

16 Mtume Paulo anamalizia maneno yake yaliyoongozwa na roho kwa kusema hivi: “Vitu vyote vitakapokuwa vimetiishwa kwake, ndipo Mwana mwenyewe atakapojitiisha pia kwa Yeye aliyevitiisha vitu vyote kwake, ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.” (1 Kor. 15:28) Kusudi la utawala wa Mwana litakuwa limetimia. Kisha, akiwa ameridhika kabisa, atamrudishia Yehova mamlaka na kumpa familia ya wanadamu iliyo kamilifu.

17. Shetani atachukuliwa hatua gani mwishowe?

17 Namna gani Shetani, aliyesababisha mateso yote ambayo wanadamu wamekabili? Andiko la Ufunuo 20:7-15 linajibu swali hilo. Katika mtihani wa mwisho wa wanadamu wote wakamilifu, Shetani ataruhusiwa kujaribu kuwapotosha. Ibilisi na wale watakaomfuata wataangamizwa milele katika “kifo cha pili.” (Ufu. 21:8) Kifo hiki hakitaangamizwa kamwe kwa sababu wale watakaokufa katika kifo hicho watatoweka milele. Hata hivyo, “kifo cha pili” si adui wa wanadamu wanaompenda na kumtumikia Muumba wao.

18. Mgawo ambao Mungu alimpa Adamu utatimizwaje?

18 Wakati huo, wanadamu wakamilifu watasimama mbele za Yehova wakiwa wamekubaliwa kikamili kupata uzima wa milele, na hakutakuwa na maadui wowote. Mgawo ambao Adamu alipewa utakuwa umetimizwa bila yeye kuwapo. Dunia itajaa wazao wake, nao wataisimamia kwa shangwe na kufurahia viumbe mbalimbali waliomo. Tusikose kamwe kuthamini jinsi ambavyo Yehova kwa upendo atamwangamiza adui wa mwisho, kifo!

^ fu. 9 Kitabu Insight on the Scriptures kinasema hivi kuhusu jitihada za wanasayansi za kueleza kwa nini wanadamu wanazeeka na kufa: “Wanapuuza uhakika wa kwamba Muumba mwenyewe ndiye aliyetangaza hukumu ya kifo juu ya wanadamu wawili wa kwanza, na kuitekeleza kwa njia ambayo wanadamu hawaelewi kikamili.”—Buku la 2, uku. 247.