Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, ‘Unajitahidi Kufikia’ Mapendeleo?

Je, ‘Unajitahidi Kufikia’ Mapendeleo?

FERNANDO * alikuwa na wasiwasi kwa sababu wazee wawili walitaka kuzungumza naye faraghani. Baada ya kila ziara ya mwangalizi wa mzunguko, wazee walimwambia mambo aliyohitaji kufanya ili astahili kupata mapendeleo zaidi kutanikoni. Kadiri muda ulivyopita, Fernando alianza kujiuliza ikiwa atawahi kupendekezwa kuwa mzee. Na hivi karibuni, kutaniko lao lilikuwa na ziara nyingine ya mwangalizi wa mzunguko. Wazee watamwambia nini wakati huu?

Fernando alisikiliza mzee alipokuwa akizungumza naye. Ndugu huyo alirejelea andiko la 1 Timotheo 3:1 na kumwambia kwamba wazee wa kutaniko wamepokea barua inayoonyesha kwamba amewekwa rasmi kuwa mzee. Fernando alishtuka na kuuliza hivi: “Umesema nini?” Mzee huyo akarudia alichosema, Fernando akatabasamu. Baadaye kutaniko lilipotangaziwa kwamba amewekwa rasmi, wote walifurahi.

Je, ni kosa kutamani mapendeleo katika kutaniko? Si kosa. Kulingana na andiko la 1 Timotheo 3:1, “ikiwa mwanamume yeyote anajitahidi kufikia cheo cha mwangalizi, yeye anatamani kazi njema.” Wanaume wengi Wakristo hutii himizo hilo na kufanya maendeleo ya kiroho ili wastahili kufikia mapendeleo kutanikoni. Hivyo, watu wa Mungu wamebarikiwa kuwa na makumi ya maelfu ya wazee na watumishi wa huduma wenye uwezo. Hata hivyo, kuna uhitaji wa ndugu wengi zaidi kujitahidi kufikia mapendeleo kwa sababu ya ongezeko kubwa katika makutaniko. Ni njia gani inayofaa ya kufanya hivyo? Je, wale wanaotamani kuwa waangalizi wanapaswa kuhangaikia jambo hilo kama Fernando?

‘KUJITAHIDI KUFIKIA’ KUNAMAANISHA NINI?

Maneno ya Biblia ‘kujitahidi kufikia’ yametafsiriwa kutokana na kitenzi cha Kigiriki kinachomaanisha kutamani kwa bidii, kujinyoosha. Huenda maneno hayo yakaleta wazo la mtu anayejinyoosha kabisa ili kuchuma tunda lenye kuvutia linaloning’inia mtini. Hata hivyo, maneno hayo hayamaanishi kujitahidi kwa pupa kupata pendeleo la ‘kuwa mwangalizi.’ Kwa nini? Kwa sababu wale wanaotamani kwa unyoofu kutumika wakiwa wazee wanapaswa kuwa na lengo la kufanya “kazi njema” badala ya kupata cheo.

Andiko la 1 Timotheo 3:2-7 na Tito 1:5-9 yanaonyesha matakwa mengi ya kazi hiyo njema. Raymond, mzee aliyetumika kwa muda mrefu anasema hivi kuhusu viwango hivyo vya juu: “Kwa maoni yangu, jambo muhimu zaidi ni jinsi tulivyo. Ni muhimu kuwa msemaji na mwalimu stadi, hata hivyo, ni muhimu pia kuwa asiyelaumika, mwenye kiasi katika mazoea, mwenye utimamu wa akili, mwenye utaratibu, mkaribishaji-wageni, na mwenye usawaziko.”

‘Jitahidi kufikia’ mapendeleo kwa kushirikiana na kutaniko katika njia mbalimbali

Ndugu anayetaka kikweli kufikia mapendeleo hujitahidi kuwa asiyelaumika kwa kuwa mnyoofu katika mambo yote na kuepuka ukosefu wowote wa usafi. Yeye ni mwenye kiasi katika mazoea, mwenye utimamu wa akili, mwenye utaratibu, na mwenye usawaziko; kwa hiyo, waabudu wenzake wanamtegemea awaongoze na kuwasaidia wanapokuwa na matatizo. Kwa kuwa ni mkaribishaji-wageni, yeye huwatia moyo vijana na wapya katika kweli. Anawafariji na kuwasaidia wagonjwa na waliozeeka kwa sababu yeye ni mpenda-wema. Anasitawisha sifa hizo ili kuwanufaisha wengine, bali si kuongeza uwezekano wa kuwekwa rasmi kuwa mzee. *

Baraza la wazee liko tayari kutoa mashauri na kitia-moyo, lakini kila mmoja anayejitahidi kufikia mapendeleo anapaswa kutimiza kibinafsi matakwa hayo ya Kimaandiko. Henry, mwangalizi mwenye uzoefu, anasema hivi: “Ikiwa unatamani kufikia mapendeleo, jitahidi kuthibitisha kwamba unastahili.” Akirejelea andiko la Mhubiri 9:10, anasema hivi: “‘Yote ambayo mkono wako unapata kufanya, yafanye kwa nguvu zako zote.’ Jitahidi kabisa kutimiza mgawo wowote unaopewa na wazee. Furahia kufanya kazi zote unazopewa katika kutaniko, kutia ndani kufagia sakafu. Baada ya muda, kazi na jitihada zako zitaonekana wazi.” Ikiwa ungependa kutumika ukiwa mzee, fanya kazi kwa bidii na uwe mwenye kutegemeka katika sehemu zote za utumishi mtakatifu. Unapaswa kuwa mnyenyekevu maishani badala ya kujitafutia makuu kwa kiburi.—Mt. 23:8-12.

KATAA MAWAZO NA MATENDO YASIYOFAA

Baadhi ya ndugu wanaotamani mapendeleo katika kutaniko huenda wakaomba kwa ujanja wapendekezwe au kujaribu kujipendekeza kwa baraza la wazee. Wengine huudhika wanaposhauriwa na wazee. Watu wenye mtazamo huo wanapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninajitafutia faida za kibinafsi, au ninataka kwa unyenyekevu kuwatunza kondoo wa Yehova?’

Wale wanaojitahidi kufikia mapendeleo hawapaswi kusahau takwa lingine la kuwa mzee, yaani, “kuwa vielelezo kwa kundi.” (1 Pet. 5:1-3) Mtu ambaye ni kielelezo kwa kutaniko huepuka kufikiri na kutenda kwa hila. Iwe amewekwa rasmi au la, anasitawisha uvumilivu na subira. Kuwa mzee hakumfanyi mtu kuwa mkamilifu. (Hes. 12:3; Zab. 106:32, 33) Pia, huenda ndugu ‘asifahamu kitu chochote dhidi yake mwenyewe,’ lakini huenda wengine wanajua udhaifu wake. (1 Kor. 4:4) Hivyo, ikiwa wazee wanakupa kwa unyoofu mashauri yanayotegemea Biblia, jitahidi kusikiliza bila kuudhika. Kisha fuata shauri lao.

NAMNA GANI IKIWA UMESUBIRI KWA MUDA MREFU?

Ndugu wengi hufikiri kwamba wamesubiri kwa muda mrefu sana kuwekwa rasmi. Ikiwa ‘umejitahidi kwa miaka mingi kufikia cheo cha mwangalizi,’ je, nyakati nyingine unahangaishwa na jambo hilo? Ikiwa ndivyo, fikiria maneno haya yaliyoongozwa na roho: “Tarajio lililocheleweshwa linafanya moyo uwe mgonjwa, lakini kitu kinachotamaniwa kinapokuja ni mti wa uzima.”—Met. 13:12.

Huenda moyo ukawa mgonjwa mtu anapoona kwamba hawezi kufikia mradi anaopenda. Abrahamu alihisi hivyo. Yehova alimwahidi mwana, lakini miaka mingi ilipita bila yeye na Sara kupata watoto. (Mwa. 12:1-3, 7) Abrahamu aliyezeeka alisema hivi: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, utanipa nini, kwa sababu mimi naenda zangu bila mtoto . . . Hukunipa uzao wowote.” Yehova alimhakikishia kwamba angetimiza ahadi Yake kwa kumpa mwana. Lakini angalau miaka 14 zaidi ilipita kabla Mungu hajatimiza ahadi yake.—Mwa. 15:2-4; 16:16; 21:5.

Alipokuwa akisubiri, je, Abrahamu alipoteza shangwe yake ya kumtumikia Yehova? Hapana. Hakutilia shaka kamwe ahadi ya Mungu. Aliendelea kutazamia ahadi hiyo. Mtume Paulo aliandika hivi: “Baada ya Abrahamu kuonyesha subira, aliipata ahadi hiyo.” (Ebr. 6:15) Mwishowe, Mungu Mweza-Yote alimbariki mwanamume huyo mwaminifu kuliko alivyotarajia. Unaweza kujifunza nini kutoka kwa Abrahamu?

Ikiwa unatamani kutumika ukiwa mzee lakini hujapata pendeleo hilo licha ya miaka mingi kupita, endelea kumtumaini Yehova. Usipoteze shangwe yako unapomtumikia. Warren, ambaye amewasaidia ndugu wengi kufanya maendeleo ya kiroho, anasema hivi: “Wakati wa kutosha unahitajika ili ndugu athibitishe kwamba anastahili kuwekwa rasmi. Baada ya muda, uwezo na mtazamo wa ndugu huonekana hatua kwa hatua kupitia mwenendo wake na jinsi anavyotimiza migawo yake. Wengine wanafikiri kwamba kupata pendeleo fulani au kuwekwa rasmi kunaonyesha kwamba wamefanya maendeleo ya kiroho. Hayo ni mawazo yasiyofaa na yanaweza kumfanya mtu ahangaikie sana kupata mapendeleo. Jambo muhimu ni kumtumikia Yehova kwa uaminifu popote ulipo na kwa njia yoyote ile.”

Ndugu mmoja aliwekwa rasmi kuwa mzee baada ya kusubiri kwa zaidi ya miaka kumi. Akirejelea maneno yanayojulikana sana yaliyo katika kitabu cha Ezekieli sura ya 1, anaeleza somo alilojifunza: “Yehova anaendesha gari lake, yaani, tengenezo lake, kwa mwendo anaotaka. Jambo la maana ni maoni ya Yehova kuhusu wakati, bali si maoni yetu. Kupata pendeleo la kutumika nikiwa mzee hakutegemei mapendezi yangu au kile ninachotamani. Huenda kile ninachotamani si kile ambacho Yehova anajua ninahitaji.”

Ikiwa unatamani kufanya kazi njema ukiwa mwangalizi Mkristo, jitahidi kuchangia furaha ya kutaniko. Ikiwa inaonekana kwamba muda mrefu umepita, jitahidi kuwa na subira na kutohangaika. Raymond aliyetajwa mwanzoni anasema hivi: “Mtu anayejitafutia makuu hawezi kamwe kuridhika. Wale wanaohangaika daima hukosa shangwe nyingi inayotokana na kumtumikia Yehova.” Sitawisha kikamili zaidi tunda la roho ya Mungu, hasa ustahimilivu. Jitahidi kuboresha hali yako ya kiroho kwa kujifunza Maandiko. Hubiri kwa bidii zaidi habari njema na ujifunze Biblia na wale wanaopendezwa. Ongoza familia yako katika utendaji wa kiroho na katika ibada ya familia. Furahia kila fursa unayopata ya kuwa na ndugu na dada zako. Unapojitahidi kufikia mradi wako, utafurahia kumtumikia Yehova.

Yehova ametupa fursa ya pekee ya kujitahidi kustahili kupata mapendeleo kutanikoni; Yehova na tengenezo lake halitaki wale wanaojitahidi kufikia mapendeleo wavunjike moyo na kukosa furaha katika utumishi. Mungu huwategemeza na kuwabariki wote wanaomtumikia kwa nia nzuri. Na Yehova ‘haongezi maumivu pamoja na baraka’ zake zote.—Met. 10:22.

Hata ikiwa umejitahidi kufikia mapendeleo kwa muda mrefu, bado unaweza kufanya maendeleo mazuri sana ya kiroho. Yehova hatasahau kamwe utumishi wako unapojitahidi kusitawisha sifa zinazohitajika na kufanya kazi kwa bidii kutanikoni bila kupuuza familia yako. Uwe na shangwe daima unapomtumikia Yehova katika migawo yoyote unayopewa.

^ fu. 2 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 8 Kanuni zilizotajwa katika makala hii zinawahusu pia wale wanaotamani kutumika wakiwa watumishi wa huduma. Matakwa ambayo ni lazima watimize yanapatikana katika andiko la 1 Timotheo 3:8-10, 12, 13.