Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unasadiki Kwamba Una Kweli? Kwa Nini?

Je, Unasadiki Kwamba Una Kweli? Kwa Nini?

“Mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—ROM. 12:2.

1. Makasisi wa dini zinazojiita za Kikristo wametendaje wakati wa vita?

JE, NI mapenzi ya Mungu kwamba Wakristo wa kweli waende vitani na kuua watu wa taifa lingine? Wengi wanaojiita Wakristo wamekuwa wakifanya hivyo katika kipindi cha miaka 100 iliyopita. Makasisi Wakatoliki wanaotumika jeshini wamebariki wanajeshi na silaha zao ili wapigane na Wakatoliki wa taifa adui. Makasisi Waprotestanti wamefanya vivyo hivyo. Kwa mfano, watu wanaojiita Wakristo walichinjana katika Vita vya Pili vya Ulimwengu kwa sababu hiyo.

2, 3. Mashahidi wa Yehova walichukua msimamo gani wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu na baadaye, na kwa nini?

2 Mashahidi wa Yehova walitendaje wakati wa vita hivyo? Historia inaonyesha kwamba walidumisha msimamo wao wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote. Walichukua msimamo huo kwa msingi gani? Walifuata hasa mfano na mafundisho ya Yesu. Alisema hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yoh. 13:35) Pia, walitumia kanuni aliyotaja mtume Paulo katika barua aliyowaandikia Wakristo Wakorintho.—Soma 2 Wakorintho 10:3, 4.

3 Kwa hiyo, Wakristo wa kweli, ambao dhamiri zao zimezoezwa na Biblia, hawajifunzi wala kushiriki katika vita. Kwa sababu ya kushikilia msimamo huo wa Kikristo, maelfu ya Mashahidi, vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake, wameteswa. Wengi wameteseka katika magereza na kambi za kazi ngumu. Na hata wengine waliuawa wakati wa utawala wa Wanazi nchini Ujerumani. Licha ya kwamba waliteswa kikatili barani Ulaya, Mashahidi hawakusahau kamwe kazi waliyopewa ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Yehova. Walihubiri kwa uaminifu magerezani, katika kambi za mateso, na uhamishoni. * Mashahidi hawakushiriki katika mauaji makubwa ya kikabila nchini Rwanda mwaka wa 1994. Pia, walidumisha msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote wakati wa mauaji makubwa ya hivi karibuni katika nchi za Balkani baada ya kuvunjika kwa Yugoslavia.

4. Msimamo wa Mashahidi wa Yehova wa kutounga mkono upande wowote umekuwa na matokeo gani kwa watu wengine?

4 Msimamo huo thabiti wa Mashahidi wa Yehova umewasadikishia maelfu ya watu ulimwenguni pote kwamba Mashahidi wanadhihirisha upendo wa kweli kwa Mungu na jirani. Kwa hakika, wao ni Wakristo wa kweli. Hata hivyo, kuna mambo mengine katika ibada yetu ambayo yamewasadikishia wengi kwamba Mashahidi wa Yehova ni Wakristo wa kweli.

KAZI KUBWA ZAIDI YA KIHISTORIA YA KUWAELIMISHA WATU

5. Wafuasi wa mapema wa Kristo walikabili badiliko gani?

5 Tangu mwanzo wa huduma yake, Yesu alikazia umuhimu wa kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Aliweka msingi wa kazi ya kuhubiri ambayo ingefanywa ulimwenguni pote kwa kuchagua mitume 12, na baadaye alizoeza kikundi cha wanafunzi 70. (Luka 6:13; 10:1) Wanafunzi hao walizoezwa kuwahubiria wengine habari njema, wakianza na Wayahudi. Kisha, mambo yakabadilika ghafla! Sasa, wanafunzi wa Yesu walipaswa kuwahubiria watu wa mataifa wasiotahiriwa. Hilo lilikuwa badiliko kubwa sana kwa wanafunzi Wayahudi wenye bidii.—Mdo. 1:8.

6. Petro alitambuaje kwamba Yehova hana ubaguzi?

6 Mtume Petro aliambiwa aende katika nyumba ya Kornelio, mtu wa Mataifa asiyetahiriwa. Petro akatambua kwamba Mungu hana ubaguzi. Kornelio na watu wa nyumba yake wakabatizwa. Ukristo ukaanza kupanuka katika shamba kubwa jipya; watu wa mataifa yote wangeweza kusikia kweli na kuikubali. (Mdo. 10:9-48) Sasa shamba lilikuwa ulimwengu mzima.

7, 8. Tengenezo la Yehova limechukua hatua gani? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 7.)

7 Katika historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova, wale wanaoongoza wamepanga na kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri na kufundisha habari njema ulimwenguni pote. Leo, Mashahidi karibu milioni nane wenye bidii wanafanya yote wawezayo kueneza ujumbe wa Kristo katika lugha zaidi ya 600, na idadi hiyo ya lugha itaongezeka! Mashahidi wa Yehova wanatambuliwa waziwazi kwa sababu ya huduma yao ya nyumba kwa nyumba, ya barabarani, na nyakati nyingine wanatumia meza na vigari vya kukokotwa vyenye machapisho.

8 Watafsiri zaidi ya 2,900 wamezoezwa kwa njia ya pekee kutafsiri Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia. Bila shaka hawatafsiri katika lugha kubwa tu. Wanajitahidi kutafsiri katika mamia ya lugha zisizojulikana sana ingawa zinazungumzwa na mamilioni ya watu. Kwa mfano, nchini Hispania, mamilioni ya Wakataloni huzungumza lugha ya Kikatalani kwa ukawaida. Hivi karibuni watu wameanza tena kutumia Kikatalani na lahaja zake katika maeneo ya Andorra, Alicante, Visiwa vya Balearic, na Valencia. Sasa, Mashahidi wa Yehova wanachapisha machapisho ya Kikatalani yanayotegemea Biblia, na mikutano ya Kikristo inafanywa katika lugha inayogusa mioyo ya watu wanaozungumza lugha hiyo.

9, 10. Ni nini kinachoonyesha kwamba tengenezo la Mungu linapendezwa na mahitaji ya kiroho ya watu wote?

9 Kazi hiyo ya kutafsiri na kufundisha inafanywa duniani pote. Lugha kuu nchini Mexico ni Kihispania, hata hivyo kuna vikundi vingine vikubwa vya watu wanaozungumza lugha nyingine. Kikundi kimoja ni cha Wamaya. Ofisi ya tawi ya Mexico ilihamisha watafsiri wa lugha ya Kimaya na kuwapeleka mahali wanapoweza kuongea na kusikia lugha hiyo kila siku. Mfano mwingine ni lugha ya Kinepali inayozungumzwa na watu zaidi ya milioni 29 nchini Nepal. Lugha 120 zinazungumzwa katika nchi hiyo, hata hivyo, watu zaidi ya milioni 10 huzungumza Kinepali na wengine wengi huzungumza lugha hiyo ikiwa lugha ya pili. Machapisho yetu yanayotegemea Biblia yanapatikana katika lugha hiyo.

 

Kikundi cha watafsiri kikitafsiri machapisho ya lugha ya Low German (Tazama fungu la 10)

10 Tengenezo la Yehova linategemeza kazi ya vikundi vingi vya watafsiri kotekote ulimwenguni na hivyo kuthibitisha kwamba linachukua kwa uzito sana agizo la kuhubiri habari njema ya Ufalme ulimwenguni pote. Mamilioni ya trakti, broshua, na magazeti yamegawanywa bila malipo katika kampeni zinazofanywa ulimwenguni pote. Kazi hiyo hugharimiwa na michango ya hiari ya Mashahidi wa Yehova wanaofuata agizo hili la Yesu: “Mlipokea bure, toeni bure.”—Mt. 10:8.

Machapisho ya lugha ya Low German yanawanufaisha wengi nchini Paraguai (Tazama picha kwenye ukurasa wa 7)

 

11, 12. Kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote inayofanywa na Mashahidi wa Yehova imekuwa na matokeo gani mazuri kwa watu?

11 Wakiwa wahubiri na walimu Wakristo wenye bidii, Mashahidi wa Yehova wanasadiki kabisa kwamba wamepata kweli na hivyo wanajidhabihu sana ili waweze kuwahubiria watu wa jamii na mataifa mengine. Wengi wao wamerahisisha maisha yao, wamejifunza lugha nyingine, na kuzoea utamaduni tofauti ili washiriki katika kazi hiyo muhimu ya Kikristo. Pia, kazi hiyo ya kuhubiri na kufundisha inayofanywa ulimwenguni pote inawasadikishia watu wengi kwamba Mashahidi wa Yehova ni wafuasi wa kweli wa Kristo Yesu.

12 Mashahidi wanafanya yote hayo kwa sababu wanasadiki kwamba wamepata kweli. Hata hivyo, ni nini kingine kinachowasadikishia mamilioni ya watu kwamba Mashahidi wa Yehova wana kweli?—Soma Waroma 14:17, 18.

KWA NINI WANASADIKI KWAMBA WANA KWELI?

13. Mashahidi wamedumishaje usafi wa tengenezo lao?

13 Tunaweza kunufaika kutokana na maelezo ya Wakristo wenye bidii katika siku zetu wanaosadiki kwamba wana kweli. Ndugu mmoja ambaye amemtumikia Yehova kwa miaka mingi alisema hivi: “Kila jitihada hufanywa ili tengenezo la Yehova liendelee kuwa safi kiadili na bila unajisi, bila kujali ni nani atakayeshauriwa au kutiwa nidhamu.” Kiwango hicho cha juu cha maadili hudumishwaje? Kwa kufuata viwango vya Neno la Mungu na kuiga kielelezo cha Yesu na wanafunzi wake. Hivyo, katika historia ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova, ni wachache tu waliotengwa na ushirika wa Kikristo kwa sababu ya kukataa kufuata viwango vya Mungu. Hata hivyo, Mashahidi wengi, kutia ndani watu ambao zamani waliishi maisha yasiyompendeza Mungu, sasa wanaishi maisha safi yanayompendeza.—Soma 1 Wakorintho 6:9-11.

14. Watu wengi waliotengwa na ushirika wamefanya nini, na matokeo yamekuwa nini?

14 Namna gani wale ambao wametengwa na ushirika wa kutaniko kupatana na mwongozo wa Maandiko? Maelfu wametubu matendo yao yasiyo ya Kikristo na wamekaribishwa tena kutanikoni. (Soma 2 Wakorintho 2:6-8.) Kutaniko la Kikristo ni safi, linaaminika na kutegemeka kwa sababu ya kufuata viwango vya juu vya Biblia vya mwenendo. Wengi wamesadiki kwamba Mashahidi wa Yehova wanaishi kupatana na kweli kwa sababu wanafuata viwango vya Mungu, tofauti na makanisa mengi yanayoacha watu wafanye watakavyo.

15. Ni jambo gani lililomsadikishia ndugu mmoja kwamba amepata kweli?

15 Kwa nini baadhi ya Mashahidi ambao wamemtumikia Mungu kwa muda mrefu wanasadiki kwamba wamepata kweli? Ndugu mwenye umri wa miaka 50 hivi alisema: “Tangu ujanani, nimeamini kwamba imani yangu inategemea mambo matatu makuu ya msingi: (1) Mungu yupo; (2) Biblia imeandikwa kwa mwongozo wa roho yake; na (3) leo anatumia na kubariki kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova. Kadiri ambavyo nimekuwa nikijifunza kwa miaka mingi, ndivyo nimekuwa nikiyapima mambo hayo makuu ili kuona ikiwa yana msingi imara. Mwaka baada ya mwaka inakuwa dhahiri zaidi kwamba mambo hayo ni ya kweli, na hilo limeimarisha imani yangu na kunisadikishia zaidi kwamba kwa hakika tuna kweli.”

16. Kwa nini dada mmoja anaithamini kweli?

16 Dada aliyefunga ndoa anayetumika katika makao makuu ya Mashahidi wa Yehova jijini New York anasema hivi kuhusu tengenezo la Yehova: “Ndilo tengenezo pekee linalotangaza jina la Yehova bila kuyumbayumba. Jambo hilo linapatana na akili kabisa tunapokumbuka kwamba jina la Mungu linapatikana mara 7,000 hivi katika Biblia. Ninathamini maneno yanayotia moyo yaliyo katika 2 Mambo ya Nyakati 16:9: ‘Macho ya Yehova yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.’” Anaendelea kusema hivi: “Kweli imenisaidia kuona jinsi ninavyoweza kuwa na moyo mkamilifu ili Yehova asisite kuonyesha nguvu zake kwa ajili yangu. Uhusiano wangu na Yehova ni wenye thamani sana kwangu. Ninathamini pia jinsi Yesu anavyonisaidia kumjua vizuri zaidi Mungu, na hilo hunitegemeza.”

17. Mtu ambaye hakuamini kuwapo kwa Mungu anasadiki nini, na kwa nini?

17 Mtu mmoja ambaye hakuamini kuwapo kwa Mungu alikiri hivi: “Uumbaji unanisadikishia kwamba Mungu anataka wanadamu wafurahie maisha na hivyo hataacha tuendelee kuteseka milele. Pia, ulimwengu unapozidi kuwa mwovu, watu wa Yehova wanaendelea kuwa na imani, bidii, na upendo zaidi. Ni roho ya Yehova tu inayoweza kufanya muujiza huo katika siku zetu.”—Soma 1 Petro 4:1-4.

18. Unahisije kuhusu walichosema ndugu wawili?

18 Ndugu mwingine ambaye amekuwa Shahidi kwa miaka mingi alieleza sababu zinazomfanya aamini kweli tunayohubiri. Alisema hivi: “Mambo ambayo nimejifunza kwa miaka mingi yamenisadikishia kwamba Mashahidi wamejitahidi sana kufuata kielelezo cha Wakristo wa karne ya kwanza. Nimetembelea maeneo mbalimbali na kujionea umoja ambao Mashahidi wa Yehova wanao ulimwenguni pote. Kweli ya Biblia imenifanya niridhike na kupata furaha.” Ndugu mwenye umri wa miaka zaidi ya 60 alipoulizwa kwa nini anasadiki kwamba amepata kweli, alisema hivi kuhusu Yesu Kristo: “Tumejifunza kwa makini maisha na huduma ya Yesu na kuthamini mfano wake. Tumefanya marekebisho maishani ili kumkaribia Mungu zaidi kupitia Kristo Yesu. Tunatambua kwamba dhabihu ya fidia ya Kristo ndiyo msingi wa wokovu. Tunajua pia kwamba alifufuliwa kutoka kwa wafu. Tuna ushahidi unaotegemeka kutoka kwa waliomwona.”—Soma 1 Wakorintho 15:3-8.

NI LAZIMA TUFANYE NINI NA KWELI?

19, 20. (a) Ni jukumu gani alilokazia Paulo alipoliandikia kutaniko la Roma? (b) Tuna pendeleo gani tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu?

19 Tukiwa Wakristo wanaompenda jirani, hatuwezi kuwanyima wengine ujuzi wa kweli wenye thamani tulio nao. Paulo aliwaambia hivi ndugu zake katika kutaniko la Roma: “Ukitangaza waziwazi lile ‘neno lililo katika kinywa chako mwenyewe,’ kwamba Yesu ni Bwana, na kuonyesha imani moyoni mwako kwamba Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, utaokolewa. Kwa maana kwa moyo mtu huonyesha imani kwa ajili ya uadilifu, lakini kwa kinywa mtu hufanya tangazo la hadharani kwa ajili ya wokovu.”—Rom. 10:9, 10.

20 Tukiwa Mashahidi wa Yehova waliojiweka wakfu, tunasadiki kwamba tuna kweli na tunajua kwamba tuna pendeleo la kuwafundisha wengine habari njema ya utawala wa Ufalme wa Mungu. Tunapoendelea kutimiza mgawo wetu wa kuhubiri, wengine watavutiwa na mambo tunayofundisha kutoka katika Biblia na pia usadikisho wetu ulio wazi.

^ fu. 3 Tazama kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, ukurasa wa 191-198 na 448-454.