Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtumikie Mungu kwa Ushikamanifu Licha ya “Dhiki Nyingi”

Mtumikie Mungu kwa Ushikamanifu Licha ya “Dhiki Nyingi”

“Lazima tuingie katika ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.”—MDO. 14:22.

1. Kwa nini watumishi wa Mungu hawashtuki wanapopatwa na dhiki?

JE, UNASHTUKA kujua kwamba utakabili “dhiki nyingi” kabla ya kupata zawadi ya uzima wa milele? Huenda usishtuke. Iwe umejifunza kweli hivi karibuni au umemtumikia Yehova kwa muda mrefu, unajua kwamba ni jambo la kawaida kukabili matatizo katika ulimwengu wa Shetani.—Ufu. 12:12.

2. (a) Mbali na matatizo yanayoathiri wanadamu wote wasio wakamilifu, Wakristo wanakabili dhiki gani? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Ni nani anayesababisha dhiki tunazokabili, na tunajuaje?

2 Mbali na hali ngumu zilizo za “kawaida kwa watu,” yaani, matatizo yanayoathiri wanadamu wote wasio wakamilifu, Wakristo wanakabili dhiki nyingine. (1 Kor. 10:13) Dhiki gani? Wanapingwa vikali kwa sababu wanatii kwa uthabiti sheria za Mungu. Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: “Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yoh. 15:20) Ni nani anayesababisha upinzani huo? Bila shaka ni Shetani, ambaye Biblia inasema kwamba ni ‘simba anayenguruma, akitafuta kuwameza’ watu wa Mungu. (1 Pet. 5:8) Shetani anatumia kila njia kujaribu kuvunja utimilifu wa wanafunzi wa Yesu. Fikiria mambo yaliyompata mtume Paulo.

DHIKI HUKO LISTRA

3-5. (a) Paulo alikabili dhiki gani huko Listra? (b) Wanafunzi waliimarishwaje na ujumbe wake kwamba wangekabili dhiki?

3 Paulo aliteswa mara nyingi kwa sababu ya imani yake. (2 Kor. 11:23-27) Kisa kimoja kilitokea huko Listra. Baada ya kumponya mwanamume aliyezaliwa akiwa kilema, Paulo na mwandamani wake, Barnaba, walitukuzwa kama miungu. Paulo na Barnaba walilazimika kusihi umati huo wenye msisimko usiwaabudu. Hata hivyo, baada ya muda mfupi, Wayahudi wapinzani waliwasili na kutumia uchongezi kuupotosha umati huo. Mambo yakabadilika ghafla! Watu wakampiga mawe Paulo na kumwacha wakiwazia amekufa.—Mdo. 14:8-19.

4 Baada ya kutembelea mji wa Derbe, Paulo na Barnaba “wakarudi Listra na Ikoniamu na Antiokia, wakizitia nguvu nafsi za wanafunzi, wakiwatia moyo kubaki katika imani na kusema: ‘Lazima tuingie katika ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.’” (Mdo. 14:21, 22) Huenda tukashangazwa na maneno hayo. Kwa kweli, wazo la kukabili “dhiki nyingi” huenda likatuvunja moyo na kutuhuzunisha. Basi Paulo na Barnaba ‘walizitiaje nguvu nafsi za wanafunzi’ kwa kuwaambia kwamba wangekabili dhiki zaidi?

5 Tunaweza kupata jibu la swali hilo kwa kuchunguza kwa makini maneno ya Paulo. Hakusema: “Ni lazima tuvumilie dhiki nyingi.” Badala yake, alisema: “Lazima tuingie katika ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.” Hivyo, Paulo aliwaimarisha wanafunzi kwa kukazia manufaa ya kuendelea kuwa waaminifu. Thawabu hiyo haikuwa ndoto. Kwa kweli, Yesu alisema hivi: “Yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”Mt. 10:22.

6. Wale wanaovumilia watapata thawabu gani?

6 Tukivumilia, tutapata thawabu. Wakristo watiwa-mafuta watapata thawabu ya uhai usioweza kufa mbinguni wakiwa watawala pamoja na Yesu. Nao “kondoo wengine” watapata uzima wa milele duniani ambamo “uadilifu utakaa.” (Yoh. 10:16; 2 Pet. 3:13) Hata hivyo, kama Paulo alivyosema, kwa sasa tutakabili dhiki nyingi. Fikiria majaribu ya aina mbili ambayo huenda tukakabili.

MASHAMBULIZI YA MOJA KWA MOJA

7. Mashambulizi ya moja kwa moja yanatia ndani nini?

7 Yesu alitabiri hivi: “Watu watawapeleka mahakamani, nanyi mtapigwa katika masinagogi na kusimamishwa mbele ya magavana na wafalme.” (Marko 13:9) Kama maneno hayo yanavyoonyesha, baadhi ya Wakristo watakabili dhiki kwa kuteswa kimwili, labda kwa sababu ya uchochezi wa viongozi wa kidini au wa kisiasa. (Mdo. 5:27, 28) Fikiria tena mfano wa Paulo. Je, aliogopa kwa sababu ya kujua kwamba angeteswa? Hapana.—Soma Matendo 20:22, 23.

8, 9. Paulo alionyeshaje kwamba aliazimia kuvumilia, na wengine leo wameonyeshaje azimio hilo pia?

8 Paulo alikabiliana kwa ujasiri na mashambulizi ya moja kwa moja kutoka kwa Shetani. Alisema hivi: “Siifanyi nafsi yangu kuwa kitu chenye thamani sana kwangu, kama tu ningepata kumaliza mwendo wangu na huduma niliyopokea kutoka kwa Bwana Yesu, kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.” (Mdo. 20:24) Ni wazi kwamba Paulo hakuogopa mateso. Badala yake, aliazimia kuvumilia hali yoyote. Jambo kuu kwake lilikuwa “kutoa ushahidi kamili” licha ya dhiki yoyote ile.

9 Leo, ndugu na dada zetu wengi wameazimia kufanya vivyo hivyo. Kwa mfano, katika nchi moja, baadhi ya Mashahidi wamefungwa gerezani kwa miaka karibu 20 kwa sababu ya msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote. Kesi yao haijawahi kamwe kupelekwa mahakamani kwa kuwa nchi hiyo haitambui watu wanaokataa utumishi wa kijeshi kwa msingi wa dhamiri zao. Hawaruhusiwi kutembelewa gerezani na yeyote hata na familia yao, na baadhi ya wafunga hao wamepigwa na kuteswa kwa njia mbalimbali.

10. Kwa nini hatupaswi kuogopa dhiki zinazotokea ghafla?

10 Ndugu zetu katika maeneo mengine wanavumilia dhiki zinazotokea ghafla. Ukipatwa na dhiki za aina hiyo, usiogope. Mfikirie Yosefu. Aliuzwa utumwani, lakini Yehova ‘alimkomboa kutoka katika dhiki zake zote.’ (Mdo. 7:9, 10) Yehova anaweza kukukomboa pia. Usisahau kamwe kwamba “Yehova anajua jinsi ya kuwakomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu.” (2 Pet. 2:9) Je, utaendelea kumtegemea Yehova, ukijua kwamba anaweza kukukomboa kutoka katika mfumo huu mwovu wa mambo na kukuruhusu uishi milele chini ya utawala wa Ufalme wake? Una kila sababu ya kumtegemea na kukabiliana na mateso kwa ujasiri.—1 Pet. 5:8, 9.

MASHAMBULIZI YA HILA

11. Mashambulizi ya hila ya Shetani yanatofautianaje na ya moja kwa moja?

11 Aina nyingine ya dhiki ambayo huenda tukakabili ni mashambulizi ya hila. Yanatofautianaje na mashambulizi ya moja kwa moja? Mashambulizi ya moja kwa moja ni kama kimbunga kinachopiga mji wenu na kuharibu nyumba yako kwa ghafla. Mashambulizi ya hila ni kama mchwa wanaoharibu mbao za nyumba yako polepole, na mwishowe inaanguka. Huenda mtu asitambue hatari hiyo mpaka nyumba inapoanguka.

12. (a) Shetani anatumia mbinu gani ya hila, na kwa nini ina matokeo sana? (b) Paulo aliathiriwaje na hali ya kuvunjika moyo?

12 Shetani angependa kuharibu uhusiano wako na Yehova kupitia mashambulizi ya moja kwa moja au kwa kudhoofisha imani yako polepole kupitia mashambulizi ya hila. Mbinu moja ya hila yenye matokeo sana anayotumia Shetani ni hali ya kuvunjika moyo. Mtume Paulo alikiri kwamba nyakati nyingine alivunjika moyo. (Soma Waroma 7:21-24.) Kwa nini Paulo, mwanamume mwenye nguvu kiroho, ambaye inaelekea alikuwa mshiriki wa baraza linaloongoza katika karne ya kwanza, alijiita “maskini”? Paulo alihisi hivyo kwa sababu ya kutokamilika kwake. Alitaka sana kufanya yaliyo sawa, lakini alihisi ni kana kwamba sheria nyingine ilikuwa ikimpinga. Ikiwa pindi fulani unapambana na hisia kama hizo, je, hufarijiwi kujua kwamba hata mtume Paulo alikabili hali kama hiyo?

13, 14. (a) Kwa nini baadhi ya watu wa Mungu huvunjika moyo? (b) Ni nani anayetaka imani yetu ivunjike, na kwa nini?

13 Nyakati fulani, ndugu na dada wengi wanavunjika moyo, wanakuwa na wasiwasi, na labda wanahisi kwamba hawafai. Kwa mfano, painia mwenye bidii tutakayemwita Deborah anasema hivi: “Kila mara mimi hufikiria kosa nililofanya na kuhisi vibaya zaidi. Ninapofikiria kila kosa nililofanya, ninahisi kwamba hakuna yeyote anayeweza kunipenda, na hata Yehova hawezi kunipenda.”

14 Kwa nini baadhi ya watumishi wenye bidii wa Yehova, kama Deborah, huvunjika moyo? Huenda kuna sababu kadhaa. Huenda wengine wana mtazamo usiofaa kujihusu na kuhusu hali zao maishani. (Met. 15:15) Huenda wengine wanahisi hivyo kwa sababu ya ugonjwa fulani unaoathiri hisia. Hata hali iweje, hatupaswi kamwe kusahau yule anayetaka kutumia vibaya hisia hizo. Kwa kweli ni nani anayetaka tuvunjike moyo kabisa na kukata tamaa? Ni nani anayetaka uhisi kwamba umehukumiwa na huna tumaini kama yeye? (Ufu. 20:10) Bila shaka ni Shetani. Ukweli ni kwamba iwe anatumia mashambulizi ya moja kwa moja au ya hila, Shetani ana lengo moja—anataka kutuogopesha, kutufanya tupunguze bidii yetu, na kuacha kumtumikia Mungu. Usisahau kamwe kwamba watu wa Mungu wanapigana vita vya kiroho!

15. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tumeazimia kutolemewa na hali ya kuvunjika moyo?

15 Azimia kutoacha pigano hilo. Endelea kukazia fikira thawabu. Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa Korintho: “Hatufi moyo, lakini hata ikiwa mtu tuliye kwa nje anachakaa, hakika mtu tuliye kwa ndani anafanywa upya siku baada ya siku. Kwa maana ingawa dhiki ni ya dakika na ni nyepesi, hiyo inatufanyizia utukufu wenye uzito mkubwa zaidi na zaidi na ni wa milele.”—2 Kor. 4:16, 17.

JITAYARISHE SASA KWA AJILI YA DHIKI

Wakristo vijana kwa wazee hujizoeza kutetea imani yao (Tazama fungu la 16)

16. Kwa nini ni muhimu kujitayarisha sasa kwa ajili ya dhiki?

16 Kama tulivyoona, Shetani hutumia “hila” mbalimbali. (Efe. 6:11) Kila mmoja wetu anahitaji kufuata himizo hili lililo kwenye 1 Petro 5:9: “Chukueni msimamo mkampinge yeye, mkiwa imara katika imani.” Ili tufanye hivyo, tunahitaji kutayarisha akili na moyo wetu, kujizoeza sasa kufanya yaliyo sawa. Fikiria mfano huu: Wanajeshi hufanya mazoezi makali kwa muda mrefu hata kabla ya vita kutokea. Jeshi la kiroho la Yehova hufanya vivyo hivyo. Hatujui vita vyetu vitahusisha nini wakati ujao. Basi, ni jambo la hekima kufanya mazoezi mengi wakati kuna amani ya kadiri, sivyo? Paulo aliwaandikia hivi Wakorintho: “Endeleeni kujijaribu kama ninyi mko katika imani, endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.”—2 Kor. 13:5.

17-19. (a) Tunaweza kujijaribu kwa njia gani? (b) Vijana wanawezaje kujitayarisha ili watetee imani yao shuleni?

17 Njia moja tunayoweza kutii shauri la Paulo lilioongozwa na roho ni kujichunguza kwa makini. Jiulize maswali kama vile: ‘Je, mimi hudumu katika sala? Je, mimi humtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu ninapokabili msongo wa marafiki? Je, ninahudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida? Je, ninazungumza kuhusu imani yangu kwa ujasiri? Je, ninajitahidi kuvumilia makosa ya waamini wenzangu, kama tu wanavyovumilia makosa yangu? Je, ninajitiisha kwa wanaoongoza kutanikoni na kwa wale walio na daraka la kuongoza kutaniko la ulimwenguni pote?’

18 Ona kwamba maswali mawili yanahusu kutetea imani yetu kwa ujasiri na kukabiliana na msongo wa marafiki. Vijana wetu wengi hufanya hivyo shuleni. Wamejifunza kutoogopa au kutoaibikia imani yao. Badala yake, wanaitetea kwa ujasiri. Magazeti yetu yana mapendekezo mazuri yanayoonyesha jinsi ya kufanya hivyo. Kwa mfano, gazeti la Amkeni! la Julai 2009 linapendekeza kwamba ikiwa mwanafunzi mwenzako anauliza hivi: “Kwa nini huamini mageuzi?” unaweza kujibu hivi: “Kwa nini niamini mageuzi? Hata wanasayansi wenyewe hawakubaliani kuhusu mageuzi, na eti hao ndio wataalamu!” Wazazi, hakikisheni kwamba mnafanya mazoezi pamoja na watoto wenu ili wawe tayari kukabiliana na msongo kama huo kutoka kwa wanafunzi wenzao shuleni.

19 Kwa kweli, sikuzote si rahisi kuitetea imani kwa ujasiri au kufanya mambo mengine ambayo Yehova anataka tufanye. Baada ya siku yenye shughuli nyingi kazini, huenda tukahitaji kujikaza sana ili kuhudhuria mikutano. Huenda ikawa vigumu sana kuamka asubuhi ili kushiriki katika huduma ya shambani. Lakini kumbuka kwamba ikiwa una mazoea mazuri ya kiroho sasa, itakuwa rahisi zaidi kwako kukabiliana na majaribu makubwa wakati ujao.

20, 21. (a) Kutafakari kuhusu fidia kunaweza kutusaidiaje kukabiliana na hisia zisizofaa? (b) Tunapaswa kuazimia nini kuhusu dhiki?

20 Namna gani kuhusu mashambulizi ya hila? Kwa mfano, tunawezaje kukabiliana na hisia za kuvunjika moyo? Mojawapo ya njia bora zaidi za kufanya hivyo ni kutafakari kuhusu fidia. Mtume Paulo alifanya hivyo. Nyakati nyingine alihisi kwamba yeye ni maskini au mnyonge. Lakini alijua pia kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya watenda-dhambi, bali si kwa ajili ya watu wakamilifu. Na Paulo alikuwa miongoni mwa watenda-dhambi hao. Ndiyo sababu aliandika hivi: “Naishi kwa imani ambayo ni kumwelekea Mwana wa Mungu, aliyenipenda mimi na kujitoa mwenyewe kwa ajili yangu.” (Gal. 2:20) Naam, Paulo aliikubali fidia. Alitambua kwamba fidia ilimhusu yeye binafsi.

21 Kuwa na mtazamo huohuo kwamba fidia ni zawadi ya kibinafsi kutoka kwa Yehova kunaweza kukusaidia sana. Hilo halimaanishi kwamba hisia za kuvunjika moyo zitatoweka kwa ghafla. Kwa kadiri fulani, huenda baadhi yetu tukahitaji kupambana na shambulizi hilo la hila mpaka ulimwengu mpya utakapokuja. Lakini kumbuka jambo hili: Wale ambao hawatakata tamaa ndio watakaopata zawadi. Tunakaribia zaidi siku tukufu ambayo Ufalme wa Mungu utaleta amani na kuwasaidia wanadamu wote waaminifu kuwa wakamilifu. Azimia kuingia katika Ufalme huo hata kama ni kupitia dhiki nyingi.