Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakumbuke Watumishi wa Wakati Wote

Wakumbuke Watumishi wa Wakati Wote

“Daima sisi hukumbuka akilini kazi yenu ya uaminifu na kazi yenu ya jasho yenye upendo.”—1 THE. 1:3.

1. Paulo alihisije kuhusu wale wanaomtumikia Yehova kwa bidii?

MTUME PAULO aliwakumbuka wale waliohubiri habari njema kwa bidii. Paulo aliandika hivi: “Daima sisi hukumbuka akilini kazi yenu ya uaminifu na kazi yenu ya jasho yenye upendo na uvumilivu wenu kwa sababu ya tumaini lenu katika Bwana wetu Yesu Kristo mbele za Mungu wetu na Baba.” (1 The. 1:3) Ni wazi kwamba Yehova hukumbuka kazi ya jasho yenye upendo ya wote wanaomtumikia kwa uaminifu, iwe hali zao zinawaruhusu kufanya mengi au machache.—Ebr. 6:10.

2. Tutachunguza nini katika makala hii?

2 Watumishi wenzetu wengi katika nyakati za zamani na leo, wamejidhabihu sana ili kumtumikia Yehova wakati wote. Acheni tuone jinsi baadhi yao walivyomtumikia katika karne ya kwanza. Tutachunguza pia utumishi mbalimbali wa wakati wote leo na kuona jinsi tunavyoweza kuwakumbuka watumishi hao wapendwa waliojitoa wenyewe kwa njia za pekee.

WAKRISTO WA KARNE YA KWANZA

3, 4. (a) Baadhi ya Wakristo walitumikaje katika karne ya kwanza? (b) Walitegemezwaje kimwili?

3 Muda mfupi baada ya kubatizwa, Yesu alianzisha kazi ambayo ingeenea ulimwenguni pote. (Luka 3:21-23; 4:14, 15, 43) Baada ya kifo chake, mitume wake waliongoza katika kupanua kazi ya kuhubiri. (Mdo. 5:42; 6:7) Baadhi ya Wakristo, kama vile Filipo, walitumikia wakiwa waeneza-injili na wamishonari huko Palestina. (Mdo. 8:5, 40; 21:8) Paulo na wengine walienda kuhubiri katika maeneo ya mbali zaidi. (Mdo. 13:2-4; 14:26; 2 Kor. 1:19) Wengine, kama vile, Silvano (Sila), Marko, na Luka, walitumikia pia wakiwa waandishi au wanakili. (1 Pet. 5:12) Dada Wakristo walishirikiana na ndugu hao waaminifu. (Mdo. 18:26; Rom. 16:1, 2) Masimulizi yao yanayogusa moyo yamefanya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yawe yenye kusisimua na yanathibitisha kwamba Yehova huwakumbuka na kuwathamini watumishi wake.

4 Watumishi wa wakati wote walitegemezwaje kimwili katika nyakati za kale? Nyakati nyingine, Wakristo wenzao waliwakaribisha nyumbani mwao na kuwapa misaada, lakini hawakudai wapewe misaada hiyo. (1 Kor. 9:11-15) Baadhi ya makutaniko na Wakristo mmoja-mmoja waliwategemeza kwa hiari. (Soma Matendo 16:14, 15; Wafilipi 4:15-18.) Paulo na wasafiri wenzake walifanya pia kazi ya muda ili kugharimia mahitaji yao.

WATUMISHI WA WAKATI WOTE LEO

5. Wenzi fulani wa ndoa walisema nini kuhusu maisha yao katika utumishi wa wakati wote?

5 Leo pia, wengi hujikakamua katika utumishi mbalimbali wa wakati wote. (Tazama sanduku lenye kichwa “ Utumishi Mbalimbali wa Wakati Wote.”) Wanahisije kuhusu utumishi waliochagua? Unaweza kuwauliza swali hilo, na inaelekea kwamba watakutia moyo sana. Kwa mfano, ndugu mmoja ambaye ametumika akiwa painia wa kawaida, painia wa pekee, mmishonari, na Mwanabetheli katika nchi ya kigeni anasema hivi: “Ninahisi kwamba uamuzi wa kufanya utumishi wa wakati wote ni kati ya maamuzi bora zaidi niliyowahi kufanya. Nilipokuwa na umri wa miaka 18, nilikabili uamuzi mgumu wa ama kujiunga na chuo kikuu, kufanya kazi ya kuajiriwa ya wakati wote, au kufanya upainia. Nimejionea mwenyewe kwamba Yehova hasahau jinsi unavyojidhabihu ili umtumikie kwa wakati wote. Ikiwa ningechagua kufanya kazi ya kimwili, singepata kamwe fursa ambazo nimepata za kutumia uwezo au vipaji mbalimbali ambavyo Yehova amenipa.” Mke wake anasema hivi: “Kila mgawo umenisaidia kukua. Tumeona Yehova akitulinda na kutuongoza katika pindi nyingi na kwa njia mbalimbali, jambo ambalo halingewezekana ikiwa tungeendelea na maisha yetu ya kawaida. Ninamshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya maisha yetu katika utumishi wa wakati wote.” Je, ungependa kuwa na maisha ya aina hiyo?

6. Yehova anahisije kuhusu utumishi wetu?

6 Bila shaka, baadhi ya Wakristo hawawezi kufanya utumishi wa wakati wote kwa sasa kwa sababu ya hali zao. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anathamini pia jitihada zao za nafsi yote. Wafikirie wale wanaotajwa na Paulo katika Filemoni 1-3, kutia ndani washiriki wote wa kutaniko la Kolosai. (Soma.) Paulo aliwathamini, na Yehova pia aliwathamini. Baba yetu wa mbinguni anathamini pia utumishi wako. Hata hivyo, unawezaje kuwategemeza watumishi wa wakati wote?

KUWASAIDIA MAPAINIA

7, 8. Utumishi wa painia unahusisha nini, na wengine kutanikoni wanawezaje kuwasaidia mapainia?

7 Mapainia wenye bidii wanayatia moyo sana makutaniko kama waeneza-injili wa karne ya kwanza walivyofanya. Wengi hujitahidi kutumia saa 70 katika huduma kila mwezi. Unawezaje kuwasaidia?

8 Dada mmoja painia anayeitwa Shari alisema hivi: “Mapainia huonekana wenye nguvu kwa sababu wanashiriki katika utumishi kila siku. Hata hivyo, wanahitaji kutiwa moyo.” (Rom. 1:11, 12) Dada mwingine aliyefanya upainia kwa miaka kadhaa alisema hivi kuhusu mapainia wa kutaniko lao: “Wanahubiri kwa bidii daima. Wanathamini wengine wanapojitolea kuwabeba kwa gari lao katika utumishi, wanapowaalika kwa ajili ya chakula, wanapowapa pesa kidogo za usafiri au wanapowasaidia kifedha kwa njia nyingine. Wanaona kwamba kwa kweli unawajali.”

9, 10. Baadhi ya Wakristo wamewasaidiaje mapainia wa kutaniko lao?

9 Je, ungependa kuwasaidia mapainia katika huduma? Painia anayeitwa Bobbi alisihi hivi: “Tunahitaji kuungwa mkono zaidi katikati ya juma.” Painia mwenzake kutanikoni aliongezea hivi: “Kupata mwenzi wa kuhubiri naye alasiri ni tatizo kubwa.” Dada anayetumika sasa katika Betheli ya Brooklyn anasema hivi kwa furaha kuhusu wakati alipofanya upainia: “Dada mmoja aliyekuwa na gari aliniambia, ‘Wakati wowote unapokosa mwenzi wa kuhubiri naye, nipigie simu, nitahubiri nawe.’ Kwa kweli, alinisaidia sana kuendelea na upainia.” Naye Shari anataja jambo hili muhimu: “Mara nyingi mapainia waseja hubaki peke yao baada ya utumishi. Mnaweza kuwaalika ndugu au dada waseja katika ibada yenu ya familia mara kwa mara. Kuwaalika katika utendaji mwingine huwasaidia pia kuendelea kuwa na nguvu.”

10 Dada mmoja ambaye amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka karibu 50 anasema hivi anapokumbuka jinsi alivyofanya upainia pamoja na dada wengine waseja: “Wazee wa kutaniko letu waliwatembelea mapainia kila baada ya miezi kadhaa. Walituuliza kuhusu afya yetu na kazi ya kimwili ili kujua mambo yaliyotuhangaisha. Walitujali kikweli. Walitutembelea nyumbani ili kuona ikiwa tulihitaji msaada.” Huenda hilo likatukumbusha jinsi Paulo alivyothamini utumishi aliopata kutoka kwa mtu mwenye familia huko Efeso.—2 Tim. 1:18.

11. Utumishi wa painia wa pekee unahusisha nini?

11 Makutaniko fulani yamebarikiwa kuwa na mapainia wa pekee. Wengi wa ndugu na dada hao wanajitahidi kushiriki katika utumishi wa shambani kwa muda wa saa 130 kila mwezi. Kwa kuwa wanatumia muda mwingi katika huduma na huwasaidia wengine katika njia nyingine, wana muda kidogo au hata hawana muda wa kufanya kazi ya kimwili. Ofisi ya tawi huwapa posho kidogo kila mwezi ili waweze kukazia fikira huduma.

12. Wazee na wahubiri wengine wanawezaje kuwasaidia mapainia wa pekee?

12 Tunawezaje kuwasaidia mapainia wa pekee? Mzee aliye katika ofisi ya tawi anayewasiliana na wengi wao anasema hivi: “Wazee wanahitaji kuzungumza nao, kujua hali zao, na kuona jinsi wanavyoweza kuwasaidia. Mashahidi fulani hufikiri kwamba mahitaji yote ya mapainia wa pekee yanatoshelezwa kwa sababu wanapata posho, lakini ndugu wanaweza kuwasaidia katika njia nyingi.” Sawa na mapainia wa kawaida, mapainia wa pekee huthamini sana wengine wanapohubiri nao. Je, unaweza kuwasaidia kwa njia hiyo?

KUWASAIDIA WAANGALIZI WANAOSAFIRI

13, 14. (a) Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu waangalizi wa mzunguko? (b) Unaweza kuwasaidiaje waangalizi wanaosafiri?

13 Mara nyingi waangalizi wa mzunguko na wake zao huonwa kuwa watu imara na wenye nguvu kiroho. Na hilo ni kweli, hata hivyo wanahitaji pia kutiwa moyo, kuungwa mkono katika huduma, na kualikwa katika tafrija yenye usawaziko. Vipi ikiwa ni wagonjwa na wamelazwa hospitalini, au wanahitaji upasuaji au matibabu mengine? Wanatiwa moyo sana wakati ndugu na dada wanapopendezwa nao kibinafsi na kuwasaidia kupata mahitaji yao. Tunaweza kuwazia jinsi “tabibu mpendwa,” Luka, aliyeandika kitabu cha Matendo, alivyomjali Paulo na wasafiri wenzake.—Kol. 4:14; Mdo. 20:5–21:18.

14 Waangalizi wanaosafiri na wake zao wanahitaji na wanathamini sana kupata marafiki wa karibu. Mwangalizi mmoja wa mzunguko aliandika hivi: “Ni kana kwamba rafiki zangu wanajua ninapohitaji kutiwa moyo. Wanauliza maswali ya utambuzi, na hivyo kunichochea kueleza mahangaiko yangu. Ninatiwa moyo sana wanaponisikiliza tu kwa makini.” Waangalizi wa mzunguko na wake zao huthamini sana ndugu na dada wanapopendezwa nao kibinafsi.

KUWATEGEMEZA WASHIRIKI WA FAMILIA YA BETHELI

15, 16. Wanabetheli na watumishi wa Majumba ya Kusanyiko hutumikaje, na tunawezaje kuwategemeza?

15 Ulimwenguni pote, Wanabetheli na watumishi wa Majumba ya Kusanyiko hutegemeza kazi ya Ufalme kwa njia muhimu sana katika nchi zinazosimamiwa na ofisi ya tawi. Ikiwa kutaniko au mzunguko wenu una Wanabetheli, unawezaje kuonyesha kwamba unawakumbuka?

16 Huenda Wanabetheli wapya wakatamani sana kurudi nyumbani, kwa kuwa wameacha familia na marafiki wapendwa. Wanathamini sana Wanabetheli wenzao na makutaniko yao mapya yanapowaonyesha urafiki. (Marko 10:29, 30) Ratiba yao ya kazi huwaruhusu kuhudhuria mikutano ya kutaniko na kushiriki katika utumishi wa shambani kila juma. Hata hivyo, Wanabetheli huwa na zamu za ziada mara kwa mara. Makutaniko yanapoelewa hilo na kuonyesha kwamba yanawathamini Wanabetheli na kazi wanayofanya, wote hunufaika.—Soma 1 Wathesalonike 2:9.

KUWASAIDIA WATUMISHI WA WAKATI WOTE KATIKA NCHI ZA KIGENI

17, 18. Wale wanaotumikia katika nchi za kigeni wanatimiza migawo gani?

17 Wale wanaokubali mgawo wa kutumikia katika nchi nyingine huenda wakalazimika kuzoea vyakula, lugha,  utamaduni, na hali tofauti kabisa na zile ambazo wamezoea. Kwa nini wanakubali changamoto ya kufanya mabadiliko hayo?

18 Wengine ni wamishonari wanaotumia muda mwingi katika utumishi wa shambani na kuwanufaisha wengi kwa mazoezi yao ya pekee. Ofisi ya tawi huhakikisha kwamba wamishonari wana makao yanayofaa na huwapa posho ili kugharimia mahitaji yao ya msingi. Wengine wanaotumikia katika nchi za kigeni hupewa mgawo katika ofisi ya tawi au kusaidia katika ujenzi wa ofisi za tawi, ofisi za utafsiri, Majumba ya Makusanyiko, au Majumba ya Ufalme. Wao hupewa makao yanayofaa, vyakula, na huduma nyingine. Sawa na Wanabetheli, wanayanufaisha makutaniko kwa njia nyingi wanapohudhuria mikutano na kushiriki kwa ukawaida katika huduma pamoja na makutaniko yao.

19. Tunapaswa kuzingatia nini kuhusu wale wanaotumikia katika nchi za kigeni?

19 Unawezaje kuwakumbuka watumishi hao wa wakati wote? Kumbuka kwamba huenda hawajazoea baadhi ya vyakula vyenu. Unaweza kuzingatia hilo unapowaalika kwenye mlo; huenda ukawauliza kwanza chakula wanachopenda au chakula ambacho wangependa kujaribu. Uwe mwenye subira wanapojifunza utamaduni na lugha yenu. Huenda ikawachukua muda kuelewa kila jambo unalosema, lakini unaweza kuwasaidia kwa fadhili kujifunza matamshi. Wanataka kujifunza!

20. Ni njia gani bora ya kuwakumbuka watumishi wa wakati wote na wazazi wao?

20 Watumishi wa wakati wote huzeeka, ndivyo na wazazi wao. Wazazi ambao ni Mashahidi hutamani sana watoto wao waendelee na migawo yao. (3 Yoh. 4) Bila shaka, ikiwa wazazi wanahitaji kutunzwa, watumishi wa wakati wote watafanya yote wawezayo na kuwatembelea mara nyingi iwezekanavyo ili kuwasaidia. Hata hivyo, wale walio nyumbani wanaweza kuwasaidia watumishi wa wakati wote kwa kuwa tayari kuwatunza wazazi waliozeeka wanaohitaji msaada. Kumbuka kwamba watumishi wa wakati wote wana majukumu mazito katika kazi muhimu zaidi ulimwenguni. (Mt. 28:19, 20) Je, wewe au kutaniko lenu mnaweza kuwasaidia wazazi wa watumishi wa wakati wote wanaohitaji msaada?

21. Watumishi wa wakati wote wanahisije kuhusu msaada na kitia-moyo kutoka kwa wengine?

21 Watumishi wa wakati wote walichagua utumishi huo ili wamtumikie Yehova na kuwasaidia wengine, bali si kupata fedha. Wanathamini sana msaada wowote kutoka kwako. Wengi wanahisi kama dada mmoja anayetumika katika nchi ya kigeni aliyesema hivi: “Hata barua fupi ya uthamini inaonyesha kwamba wengine wanakufikiria na wanafurahia utumishi wako.”

22. Unahisije kuhusu utumishi wa wakati wote?

22 Kwa kweli, kumtumikia Yehova kwa wakati wote ndiyo njia yenye kuthawabisha zaidi ya maisha. Ina changamoto zake, lakini inaelimisha na kuridhisha. Na ndiyo njia bora zaidi ya kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa milele wenye shangwe ambao watumishi wote waaminifu wa Yehova wanatazamia chini ya Ufalme wa Mungu. Acheni sote ‘tukumbuke daima kazi ya uaminifu na kazi ya jasho yenye upendo’ ya watumishi wa wakati wote.—1 The. 1:3.