Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ufufuo wa Yesu—Kwa Nini Ni Muhimu Kwetu?

Ufufuo wa Yesu—Kwa Nini Ni Muhimu Kwetu?

Alifufuliwa.”MT. 28:6.

1, 2. (a) Viongozi fulani wa kidini walitaka kujua nini, na Petro aliwajibuje? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Petro alipata wapi ujasiri pindi hiyo?

SIKU chache baada ya Yesu kufa, mtume Petro alikabiliana na kikundi cha wanaume wenye kuogofya na wenye chuki. Walikuwa viongozi wa dini ya Kiyahudi wenye mamlaka, waliopanga njama ya kumuua Yesu. Petro alikuwa amemponya mtu aliyezaliwa akiwa kilema, na viongozi hao walitaka kujua alimponya kwa nguvu gani au katika jina la nani. Mtume huyo aliwajibu hivi kwa ujasiri: “Katika jina la Yesu Kristo Mnazareti, ambaye mlimtundika mtini lakini ambaye Mungu alimfufua kutoka kwa wafu, kupitia kwake, mtu huyu anasimama hapa akiwa na afya mbele yenu.”—Mdo. 4:5-10.

2 Mapema, Petro alikuwa amemkana Yesu mara tatu kwa sababu ya woga. (Marko 14:66-72) Sasa Petro anapata wapi ujasiri wa kukabiliana na viongozi hao wa kidini? Roho takatifu ilimsaidia sana, na pia Petro mwenyewe alikuwa na uhakika kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa. Kwa nini mtume Petro alikuwa na uhakika kwamba Yesu alikuwa hai? Na kwa nini tunaweza kuwa na uhakika huo?

3, 4. (a) Ni nani waliofufuliwa kabla ya mitume wa Yesu kuzaliwa? (b) Yesu aliwafufua nani?

3 Ufufuo haukuwa jambo geni kwa mitume wa Yesu kwa  sababu kuna watu waliofufuliwa kabla ya mitume hao kuzaliwa. Walijua kwamba Mungu aliwapa manabii Eliya na Elisha nguvu za kufufua watu kimuujiza. (1 Fal. 17:17-24; 2 Fal. 4:32-37) Isitoshe, mtu mmoja aliyekufa alifufuka mwili wake ulipotupwa katika kaburi na kugusa mifupa ya Elisha. (2 Fal. 13:20, 21) Sawa na tunavyoamini kuwa Neno la Mungu ni kweli, ndivyo Wakristo wa mapema walivyoamini masimulizi hayo ya Biblia.

4 Inaelekea kwamba sisi sote huguswa moyo sana tunaposoma masimulizi kuhusu watu waliofufuliwa na Yesu. Bila shaka yule mjane alistaajabu sana Yesu alipomfufua mwana wake wa pekee. (Luka 7:11-15) Pindi nyingine, Yesu alimfufua msichana mwenye umri wa miaka 12. Hebu wazia jinsi wazazi wa msichana huyo waliokuwa na huzuni walivyofurahi na kushangaa binti yao alipofufuliwa! (Luka 8:49-56) Na bila shaka watazamaji walisisimuka sana walipomwona Lazaro akitoka kaburini akiwa hai na mwenye afya!—Yoh. 11:38-44.

KWA NINI UFUFUO WA YESU ULIKUWA WA PEKEE?

5. Ufufuo wa Yesu ulitofautianaje na ufufuo wowote uliotangulia?

5 Mitume walijua kwamba ufufuo wa Yesu ulikuwa tofauti na ufufuo wowote uliotangulia. Watu waliofufuliwa mapema walifufuliwa wakiwa na miili ya kibinadamu na hatimaye walikufa tena. Yesu alifufuliwa akiwa na mwili wa roho ambao haungeweza kuharibika. (Soma Matendo 13:34.) Petro aliandika kwamba Yesu “aliuawa katika mwili, lakini akafanywa kuwa hai katika roho.” Zaidi ya hayo, “yuko mkono wa kuume wa Mungu, kwa maana alienda zake mbinguni; na malaika na mamlaka na nguvu vilitiishwa kwake.” (1 Pet. 3:18-22) Ufufuo wowote uliotangulia ufufuo wa Yesu ulikuwa muujiza wenye kustaajabisha, lakini ufufuo wa Yesu ulikuwa muujiza mkubwa hata zaidi.

6. Ufufuo wa Yesu uliwachocheaje wanafunzi wake?

6 Ufufuo wa Yesu uliwatia moyo sana wanafunzi wake. Hakuwa mfu kama maadui zake walivyoamini. Yesu alikuwa hai akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu ambaye hakuna mwanadamu angeweza kumdhuru. Ufufuo wake ulithibitisha kwamba alikuwa Mwana wa Mungu, na kujua jambo hilo kuliwatia moyo wanafunzi wake, wakawa na shangwe kubwa badala ya huzuni. Na pia wakawa na ujasiri badala ya hofu. Ufufuo wa Yesu ulikuwa muhimu sana katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova na ulikuwa msingi wa habari njema waliyohubiri kwa ujasiri kotekote.

7. Yesu anafanya nini sasa, na ni maswali gani yanayozuka?

7 Tukiwa watumishi wa Yehova, tunajua vizuri kwamba Yesu hakuwa tu mtu mkuu. Yuko hai leo na anaongoza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. Akiwa Mfalme anayetawala wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu, hivi karibuni Yesu Kristo ataondoa uovu duniani na kuigeuza kuwa paradiso ambamo watu wataishi milele. (Luka 23:43) Mambo hayo yote hayangewezekana ikiwa Yesu hangefufuliwa. Hivyo basi, tuna sababu gani za kuamini kwamba Yesu alifufuliwa? Kwa nini ufufuo wake ni muhimu kwetu?

YEHOVA AONYESHA NGUVU ZAKE JUU YA KIFO

8, 9. (a) Kwa nini viongozi wa dini ya Kiyahudi waliomba kaburi la Yesu lilindwe? (b) Ilikuwaje wanawake walipofika kaburini?

8 Baada ya Yesu kuuawa, wakuu wa makuhani na Mafarisayo walienda kwa Pilato na kumwambia hivi: “Bwana, tumekumbuka kwamba mjanja huyo alisema alipokuwa bado yuko hai, ‘Baada ya siku tatu nitafufuliwa.’  Kwa hiyo amuru kaburi lilindwe mpaka siku ya tatu, ili wanafunzi wake wasipate kamwe kuja na kumwiba na kuwaambia watu, ‘Alifufuliwa kutoka kwa wafu!’ na ujanja huu wa mwisho utakuwa mbaya zaidi kuliko ule wa kwanza.” Pilato akawaambia: “Ninyi mna walinzi. Nendeni mkalilinde jinsi mnavyojua.” Na hivyo ndivyo walivyofanya.—Mt. 27:62-66.

9 Mwili wa Yesu ulikuwa umelazwa katika kaburi lililochimbwa katika mwamba, na jiwe kubwa kuviringishwa mlangoni. Viongozi wa dini ya Kiyahudi walitaka Yesu abaki humo milele, akiwa mfu kaburini. Lakini Yehova alikuwa na mawazo tofauti kabisa. Maria Magdalene na yule Maria mwingine walipoenda kaburini siku ya tatu, walikuta jiwe limeviringishwa kutoka kaburini na malaika alikuwa ameketi juu yake. Malaika aliwahimiza wanawake hao waangalie ndani na kuona kwamba kaburi lilikuwa tupu. Malaika akasema hivi: “Hayupo hapa, kwa maana alifufuliwa.” (Mt. 28:1-6) Yesu alikuwa hai!

10. Mtume Paulo alitoa uthibitisho gani kuwa Yesu alifufuliwa?

10 Mambo yaliyotukia kwa siku 40 zilizofuata yalithibitisha kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa. Akieleza kwa ufupi uthibitisho huo, mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakorintho: “Niliwapa ninyi, kati ya mambo ya kwanza, yale niliyopokea pia, kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko; na kwamba alizikwa, ndiyo, kwamba alifufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko; na kwamba alimtokea Kefa, kisha wale kumi na wawili. Baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano kwa wakati mmoja, ambao walio wengi kati yao wapo mpaka sasa, lakini wengine wamelala usingizi katika kifo. Baadaye alimtokea Yakobo, kisha mitume wote; lakini mwisho kabisa alinitokea mimi pia kana kwamba kwa mmoja aliyezaliwa kabla ya wakati wake.”—1 Kor. 15:3-8.

TUNAJUAJE KWAMBA YESU ALIFUFULIWA?

11. Ufufuo wa Yesu ulitokeaje “kulingana na Maandiko”?

11 Kwanza, tunajua kwamba Yesu alifufuliwa kwa sababu ufufuo wake ulitokea “kulingana na Maandiko.” Neno la Mungu lilitabiri ufufuo huo. Kwa mfano, Daudi aliandika kwamba mtumishi “mshikamanifu” zaidi wa Mungu hataachwa katika Kaburi. (Soma Zaburi 16:10.) Katika siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K., mtume Petro alionyesha kwamba maneno hayo ya kinabii yalimhusu Yesu. Alisema hivi: “[Daudi] aliona kimbele na kusema kuhusu ufufuo wa Kristo, kwamba hakuachwa katika Kaburi wala mwili wake haukuona uharibifu.”—Mdo. 2:23-27, 31.

12. Ni nani waliomwona Yesu aliyefufuliwa?

12 Pili, tunajua kwamba Yesu alifufuliwa kwa sababu tuna ushuhuda wa mashahidi wengi. Kwa siku 40, Yesu aliyefufuliwa aliwatokea wanafunzi wake katika bustani ambamo kaburi lake lilikuwa, na pia aliwatokea njiani wakielekea Emau, na wakiwa sehemu nyingine. (Luka 24:13-15) Katika pindi hizo, aliongea na mtu mmoja-mmoja kutia ndani Petro, na pia aliongea na vikundi vya watu. Hata pindi fulani, Yesu aliyefufuliwa alitokea umati wa watu zaidi ya 500! Ushuhuda wa mashahidi wengi hivyo waliomwona Yesu aliyefufuliwa hauwezi kukanushwa.

13. Bidii ya wanafunzi ilionyeshaje kwamba walikuwa na uhakika Yesu alikuwa amefufuliwa?

13 Tatu, tunajua kwamba Yesu alifufuliwa kwa sababu wanafunzi wake walitangaza ufufuo wake kwa bidii. Walinyanyaswa, wakateswa, na kuuawa kwa sababu ya kutangaza kwa bidii ufufuo wa Kristo. Kama Yesu hangekuwa amefufuliwa, yaani, ikiwa huo ulikuwa uwongo, kwa nini  Petro alihatarisha uhai wake kwa kuwatangazia viongozi wa kidini kuhusu ufufuo wa Kristo ilhali viongozi hao walimchukia Yesu na kupanga njama auawe? Kwa sababu Petro na wanafunzi wengine walikuwa na uhakika kwamba Yesu alikuwa hai na alikuwa akiongoza kazi ambayo Mungu alitaka ifanywe. Isitoshe, ufufuo wa Yesu uliwahakikishia wafuasi wake kwamba wao pia wangefufuliwa. Kwa mfano, Stefano alikufa akiwa na uhakika kwamba wafu watafufuliwa.—Mdo. 7:55-60.

14. Kwa nini unaamini kwamba Yesu yuko hai?

14 Nne, tunajua kwamba Yesu alifufuliwa kwa sababu tuna uthibitisho kwamba anatawala sasa akiwa Mfalme, naye ni Kichwa cha kutaniko la Kikristo. Jambo hilo limewezesha Ukristo wa kweli kusitawi. Je, Ukristo ungesitawi ikiwa Yesu hangekuwa amefufuliwa? Kwa kweli, huenda tusingesikia kamwe juu yake ikiwa hangekuwa amefufuliwa. Lakini tuna sababu nzuri za kuamini kwamba Yesu yuko hai na sasa anatuongoza na kutuelekeza tunapotangaza habari njema kotekote ulimwenguni.

KWA NINI UFUFUO WA YESU NI MUHIMU KWETU?

15. Kwa nini ufufuo wa Yesu unatupatia ujasiri wa kuhubiri?

15 Ufufuo wa Kristo unatupatia ujasiri wa kuhubiri. Kwa miaka 2,000, maadui wa Mungu wametumia kila aina ya silaha kukomesha kazi ya kuhubiri habari njema—wametumia uasi-imani, dhihaka, vikundi vyenye ghasia, marufuku, mateso, na kuwaua watumishi wa Mungu. Hata hivyo, hakuna chochote, yaani, hakuna ‘silaha yoyote iliyofanywa juu yetu’ imekomesha kazi yetu ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi. (Isa. 54:17) Hatuwaogopi watumishi au watumwa wa Shetani. Yesu yuko pamoja nasi, na anatusaidia kama alivyoahidi. (Mt. 28:20) Hatuna sababu yoyote ya kuogopa kwa kuwa hata adui zetu wafanye nini, hawataweza kamwe kutunyamazisha!

Ufufuo wa Yesu unatupatia ujasiri wa kuhubiri (Tazama fungu la 15)

16, 17. (a) Ufufuo wa Yesu unathibitishaje kwamba mambo aliyofundisha ni kweli? (b) Kulingana na Yohana 11:25, Mungu amempa Yesu nguvu za kufanya nini?

16 Ufufuo wa Yesu unathibitisha kwamba mambo yote aliyofundisha ni ya kweli. Paulo aliandika kwamba ikiwa Kristo hangekuwa amefufuliwa, imani ya Kikristo na kazi ya kuhubiri ingekuwa ya bure. Msomi mmoja wa Biblia aliandika hivi: “Ikiwa Kristo hakufufuliwa, . . . basi Wakristo ni watu wa kusikitikiwa kwa sababu wamepotoshwa na ulaghai mkubwa.” Kama Yesu hakufufuliwa, masimulizi ya Injili ni hadithi tu inayohuzunisha ya mtu mzuri mwenye hekima ambaye aliuawa na adui zake. Lakini Kristo alifufuliwa, na hilo linathibitisha kwamba mambo yote aliyofundisha ni ya kweli, kutia ndani mambo aliyosema kuhusu wakati ujao.—Soma 1 Wakorintho 15:14, 15, 20.

17 Yesu alisema: “Mimi ndiye ufufuo na uzima. Yule anayeniamini, hata akifa, atarudi kwenye uzima.” (Yoh. 11:25) Kwa hakika, maneno hayo yenye kusisimua yatatimia. Yehova amempa Yesu nguvu za kuwafufua wale wanaopata uhai wa kiroho mbinguni, na pia kuwafufua mabilioni ya watu wanaotumaini kuishi milele duniani. Dhabihu ya Yesu inayofunika dhambi na pia ufufuo wake unatuhakikishia kwamba kifo hakitakuwapo tena. Je, kujua mambo hayo hakukupi nguvu za kuvumilia jaribu lolote lile na hata kukabili kifo kwa ujasiri?

18. Ufufuo wa Yesu unatuhakikishia nini?

18 Ufufuo wa Yesu unatuhakikishia kwamba wakaaji wa dunia watahukumiwa kulingana na viwango vya Yehova vya upendo. Paulo alisema hivi alipokuwa akihutubia kikundi cha wanaume na wanawake katika  jiji la kale la Athene: “[Mungu] anakusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia kwa mwanamume ambaye amemweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.” (Mdo. 17:31) Naam, Yesu amewekwa rasmi na Mungu kuwa Hakimu, na tunaweza kuwa na uhakika kwamba atahukumu kwa upendo na bila upendeleo.—Soma Isaya 11:2-4.

19. Kuamini ufufuo wa Kristo kunatuchochea kufanya nini?

19 Kuamini ufufuo wa Yesu kunatuchochea kufanya mapenzi ya Mungu. Kama hangekufa kifo cha kidhabihu na baadaye kufufuliwa, tungebaki chini ya hukumu ya dhambi na kifo. (Rom. 5:12; 6:23) Ikiwa Yesu hakufufuliwa, basi tunaweza kusema: “Tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Kor. 15:32) Hata hivyo, sisi hatufuatilii maisha ya anasa. Badala yake, tunathamini sana tumaini la ufufuo na tuna kila sababu ya kutii mwongozo wa Yehova katika mambo yote.

20. Ufufuo wa Yesu unatoaje ushuhuda kuhusu ukuu wa Mungu?

20 Ufufuo wa Kristo unatoa ushuhuda wa kimyakimya, lakini wenye kusadikisha kuhusu ukuu wa Yehova ambaye “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Ebr. 11:6) Yehova alitumia nguvu na hekima iliyoje kumfufua Yesu na kumpa uhai wa mbinguni usioweza kufa! Isitoshe, Mungu alipomfufua Yesu alionyesha uwezo wake wa kutimiza ahadi Zake zote. Ahadi hizo zinatia ndani ahadi ya Mungu ya kinabii ya kwamba “uzao” wa pekee ungetimiza sehemu muhimu katika kutatuliwa kwa lile suala la enzi kuu ya ulimwengu mzima. Ili ahadi hiyo itimie, Yesu alipaswa kufa na kufufuliwa.—Mwa. 3:15.

21. Kwa nini tumaini la ufufuo ni muhimu kwako?

21 Je, hupaswi kumshukuru Yehova aliyetupatia tumaini hakika la ufufuo? Maandiko yanatuhakikishia hivi: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Mtume Yohana aliyekuwa mwaminifu, alipewa ahadi hiyo nzuri ajabu na kuambiwa hivi: “Andika, kwa sababu maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli.” Ni nani aliyempa Yohana ufunuo huo ulioongozwa na roho? Ni Mungu aliyempa kupitia Yesu Kristo aliyefufuliwa.Ufu. 1:1; 21:3-5.