Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Aliijua Njia’

‘Aliijua Njia’

GUY HOLLIS PIERCE, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova alikufa na kwenda mbinguni Jumanne, Machi 18, 2014. Alikuwa na umri wa miaka 79 tumaini lake la kuwa mmoja wa ndugu za Kristo waliofufuliwa lilipotimia.—Ebr. 2:10-12; 1 Pet. 3:18.

Guy Pierce alizaliwa Auburn, California, Marekani, Novemba 6, 1934, na alibatizwa mwaka wa 1955. Alimwoa mke wake mpendwa Penny mwaka wa 1977 na wakapata watoto, na hilo lilimsaidia kuwatendea wengine kama baba. Yeye na mke wake walianza kufanya upainia mwaka wa 1982, na mwaka wa 1986 alianza kutumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko nchini Marekani, mgawo ambao aliufanya kwa miaka 11.

Katika mwaka wa 1997, Guy na Penny Pierce walijiunga na familia ya Betheli ya Marekani. Ndugu Pierce alifanya kazi katika Idara ya Utumishi, na mwaka wa 1998 aliwekwa rasmi kuwa msaidizi katika Halmashauri ya Wafanyakazi ya Baraza Linaloongoza. Ndugu Pierce alitangazwa kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza katika mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania uliofanywa Oktoba 2, 1999. Katika miaka ya hivi karibuni, alitumikia katika halmashauri ya Wafanyakazi, Uandikaji, Uchapishaji, na Waratibu.

Watu kutoka malezi na tamaduni mbalimbali walivutiwa na Ndugu Pierce kwa sababu ya tabasamu yake changamfu na ucheshi wake. Hata hivyo, watu walivutiwa zaidi na upendo, unyenyekevu, imani yake thabiti katika Yehova, na pia kwa sababu aliheshimu sheria na kanuni za uadilifu. Imani ya Ndugu Guy Pierce ilikuwa thabiti sana hivi kwamba alikuwa akisema kwamba jua linaweza kukosa kuchomoza lakini ahadi za Yehova haziwezi kamwe kukosa kutimia, na alitaka kuwaambia watu ulimwenguni pote ukweli huo.

Ndugu Pierce alimtumikia Yehova bila kuchoka, na kwa kawaida alianza kufanya kazi asubuhi na mapema hadi usiku sana. Alienda kotekote ulimwenguni kuwatia moyo ndugu na dada zake Wakristo, na ingawa alikuwa na shughuli nyingi, alitenga wakati wa kuwa pamoja na ndugu na dada wa familia ya Betheli na wengine waliohitaji ushauri, ushirika, na msaada wake. Hata baada ya miaka mingi kupita, bado waamini wenzake wanakumbuka ukarimu na urafiki wake, na jinsi alivyowatia moyo kwa kutumia Maandiko.

Ndugu na rafiki yetu mpendwa ameacha mke, watoto sita, wajukuu, na pia vitukuu. Pia, alikuwa na watoto wengi sana wa kiroho. Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba kumhusu Ndugu Pierce Jumamosi, Machi 22, 2014, katika Betheli ya Brooklyn. Mbali na mambo mengine, alizungumzia tumaini la kwenda mbinguni ambalo Ndugu Pierce alikuwa nalo na kusoma maneno haya ya Yesu: “Katika nyumba ya Baba yangu mna makao mengi. . . . Nikienda na kuwatayarishia ninyi mahali, nitakuja tena nami nitawapokea ninyi nyumbani kwangu mwenyewe, ili mahali nilipo mimi, ninyi pia muwe hapo. Na mahali ninakoenda ninyi mnaijua njia.”—Yoh. 14:2-4.

Ni kweli kwamba tutamkosa sana Ndugu Pierce. Hata hivyo, tunashangilia kwamba ‘aliijua njia’ ya kwenda katika “makao” yake ya kudumu.