Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufanya Kazi kwa Umoja Tunapokaribia Mwisho wa Ulimwengu Huu

Kufanya Kazi kwa Umoja Tunapokaribia Mwisho wa Ulimwengu Huu

“Sisi ni viungo vya mtu na mwenzake.”—EFE. 4:25.

1, 2. Mungu anataka waabudu wake vijana kwa wazee wafanye nini?

JE, WEWE ni kijana? Kama ndivyo, uwe na hakika kwamba ukiwa sehemu ya kutaniko la Yehova la ulimwenguni pote, unathaminiwa sana. Katika nchi nyingi, idadi kubwa ya wanaobatizwa ni vijana. Inatia moyo kama nini kuona vijana wengi wakijiunga na wale ambao wameamua kumtumikia Yehova!

2 Ukiwa kijana, je, unapenda kuwa na vijana wengine? Yaelekea unapenda. Kwa kawaida sisi hufurahia kuwa pamoja na watu wa rika letu. Hata hivyo, iwe sisi ni vijana au wazee na bila kujali malezi yetu, Mungu anataka tumwabudu kwa umoja. Mtume Paulo aliandika kuwa mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:3, 4) Andiko la Ufunuo 7:9 linasema kwamba waabudu wa Mungu wametoka katika “mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.”

3, 4. (a) Ni roho gani iliyoenea miongoni mwa vijana wengi leo? (b) Ni mtazamo gani unaopatana na Waefeso 4:25?

3 Kuna tofauti kubwa sana kati ya vijana wanaomtumikia Yehova na vijana wa ulimwengu huu! Vijana wengi wasiomtumikia  Yehova huishi maisha ya ubinafsi, wakikazia fikira mapendezi yao tu. Watafiti fulani huwaita vijana hao “Kizazi cha Mimi Kwanza.” Vijana hao huzungumza na kuvalia kwa njia inayoonyesha kwamba wanadharau wazee na kuwaona kuwa “washamba.”

4 Roho hiyo imeenea kila mahali. Hivyo, ni lazima vijana wanaomtumikia Yehova wajitahidi sana kuepuka roho hiyo na kukubali maoni ya Mungu. Hata katika karne ya kwanza, Paulo aliona uhitaji wa kuwahimiza waamini wenzake waepuke “roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii” na ambayo ‘wakati fulani walitembea’ ndani yake. (Soma Waefeso 2:1-3.) Vijana ambao huona umuhimu wa kuepuka roho hiyo na kufanya kazi kwa umoja na ndugu zao wote wanastahili kupongezwa. Mtazamo huo unapatana na maneno ya Paulo kwamba “sisi ni viungo vya mtu na mwenzake.” (Efe. 4:25) Tunapokaribia mwisho wa ulimwengu huu, kufanya kazi pamoja kwa umoja kutakuwa muhimu hata zaidi. Acheni tuzungumzie mifano ya Biblia itakayotusaidia kuthamini umuhimu wa kushikamana pamoja na kuwa na umoja.

WALISHIKAMANA PAMOJA

5, 6. Simulizi la Loti na binti zake linatufundisha nini kuhusu kushikamana pamoja?

5 Katika nyakati za kale, Yehova alifurahia kuwalinda watu wake walipoungana na kusaidiana nyakati za taabu. Leo, watumishi wa Mungu, vijana kwa wazee, wanaweza kujifunza kutokana na mifano inayotajwa katika Biblia. Mfano mmoja ni Loti.

6 Loti na familia yake walikuwa hatarini kwa sababu jiji la Sodoma walimokuwa wakiishi lingeharibiwa. Malaika wa Mungu walimhimiza Loti aondoke na kukimbilia mahali salama katika eneo lenye milima, walimwambia: “Kimbia kwa ajili ya nafsi yako!” (Mwa. 19:12-22) Loti alitii, na binti zake wawili walitoka pamoja naye katika jiji hilo. Kwa kusikitisha, baadhi ya watu wao wa karibu hawakutii. Machoni pa vijana waliokuwa wakiwachumbia binti za Loti, mzee huyo “alionekana kama mtu aliyekuwa anafanya mzaha.” Hilo lilifanya wapoteze uhai wao. (Mwa. 19:14) Loti na binti zake ambao walishikamana naye, ndio tu waliookoka.

7. Yehova aliwasaidiaje wale walioonyesha roho ya umoja Waisraeli walipotoka Misri?

7 Fikiria mfano mwingine. Waisraeli walipoondoka Misri, hawakutoka wakiwa vikundi mbalimbali, kila kikundi kikifuata njia yake. Pia Musa ‘aliponyoosha mkono wake juu ya bahari’ na Yehova akayatenganisha maji, Musa hakuvuka akiwa peke yake au akiwa na Waisraeli wachache tu. Badala yake, kutaniko lote lilivuka na Yehova alililinda. (Kut. 14:21, 22, 29, 30) Walionyesha roho ya umoja, na walienda pamoja na “jamii kubwa iliyochangamana,” ya watu wasio Waisraeli ambao walijiunga nao. (Kut. 12:38) Lingekuwa jambo la kipumbavu kwa watu fulani wachache, labda kundi la vijana, kufuata njia yao wenyewe waliyoipenda, kwani kufanya hivyo kungefanya wakose ulinzi wa Yehova.—1 Kor. 10:1.

8. Katika siku za Yehoshafati, watu wa Mungu walionyeshaje umoja?

8 Katika siku za Mfalme Yehoshafati, watu wa Mungu walikabili adui wenye kuogofya, yaani, “umati mkubwa” kutoka maeneo yaliyowazunguka. (2 Nya. 20:1, 2) Inapendeza kwamba watumishi wa Mungu hawakujaribu kushinda adui hao kwa nguvu zao wenyewe. Badala yake, walimwomba Yehova awasaidie. (Soma 2 Mambo ya Nyakati 20:3, 4.) Hawakufanya hivyo kila mtu kivyake ama kama alivyopenda. Masimulizi ya Biblia yanasema hivi: “Watu wote wa Yuda walikuwa  wamesimama mbele za Yehova, hata watoto wao, wake zao na wana wao.” (2 Nya. 20:13) Wadogo kwa wakubwa, walijitahidi kwa imani kufuata mwongozo wa Yehova, na Yehova aliwalinda dhidi ya adui zao. (2 Nya. 20:20-27) Je, huo si mfano mzuri wa jinsi ya kukabili hali ngumu tukiwa watu wa Mungu?

9. Matendo na mtazamo wa Wakristo wa mapema unatufunza nini kuhusu umoja?

9 Wakristo wa mapema pia walifanya kazi pamoja. Kwa mfano, baada ya Wayahudi na wageuzwa-imani wengi kuwa Wakristo, walijitoa wenyewe “kwa fundisho la mitume na kushirikiana, katika kula milo na katika sala.” (Mdo. 2:42) Umoja huo ulionekana wazi kulipokuwa na mateso, wakati ambapo walihitaji hasa kutegemezana. (Mdo. 4:23, 24) Je, hukubali kwamba ni muhimu kufanya kazi pamoja nyakati za taabu?

IWENI NA UMOJA SIKU YA YEHOVA INAPOKARIBIA

10. Ni wakati gani ambapo umoja utakuwa muhimu sana?

10 Kipindi kibaya zaidi katika historia ya wanadamu kinakaribia. Nabii Yoeli alikiita kipindi hicho “siku yenye giza na weusi.” (Yoe. 2:1, 2; Sef. 1:14) Itakuwa muhimu sana kwa watu wa Mungu kuwa na umoja wakati huo. Kumbuka maneno haya ya Yesu: “Kila ufalme uliogawanyika na kupingana wenyewe unaangamia.”—Mt. 12:25.

11. Ni ulinganisho gani ulio katika Zaburi 122:3 na 4 ambao unaweza kuwahusu watu wa Mungu leo? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 22.)

11 Tutahitaji sana kuwa na umoja wakati unaokuja wa taabu. Umoja wa kiroho ambao tutahitaji kuwa nao miongoni mwetu unaweza kulinganishwa na jinsi ambavyo nyumba zilijengwa katika Yerusalemu la kale. Nyumba hizo zilijengwa zikiwa zimekaribiana sana hivi kwamba mtunga zaburi alisema kuwa jiji la Yerusalemu lilikuwa “limeunganishwa pamoja kwa umoja.” Jambo hilo liliwawezesha wakaaji wake kusaidiana na kulindana. Isitoshe, ukaribu wa nyumba zao unaweza kufananisha umoja wa kiroho wa taifa zima wakati ‘makabila yote ya Yah’ yalipokusanyika ili kuabudu. (Soma Zaburi 122:3, 4.) Leo na katika siku za hatari zilizo mbele yetu, tutahitaji pia kubaki tukiwa ‘tumeunganishwa pamoja kwa umoja.’

12. Ni nini kitakachotusaidia kuokoka wakati Gogu atakaposhambulia watu wa Mungu?

12 Kwa nini itakuwa muhimu sana kwetu ‘kuunganishwa pamoja’ wakati huo? Unabii wa Ezekieli sura ya 38 unasema kwamba “Gogu wa nchi ya Magogu” atawashambulia watu wa Mungu. Haitafaa kamwe kuruhusu jambo lolote litutenganishe wakati huo. Na bila shaka haitafaa kutafuta msaada wa ulimwengu wakati huo. Badala yake, litakuwa jambo la hekima kushikamana na ndugu zetu. Bila shaka, hatutaokolewa kwa sababu tu tumejiunga na kikundi. Yehova na Mwana wake watawaokoa wakati huo wa taabu wale wote wanaoliitia jina la Yehova. (Yoe. 2:32; Mt. 28:20) Hata hivyo, je, ni jambo linalopatana na akili kufikiri kwamba wale ambao wamejitenga na kundi la Mungu, yaani, wale ambao wamegeuka na kufuata njia yao wenyewe, wataokolewa?—Mika 2:12.

13. Vijana wanaomwogopa Mungu wanaweza kujifunza nini kutokana na mambo ambayo tumezungumzia kufikia sasa?

13 Ni wazi kwamba si jambo la hekima kufuata vijana wanaojitenga na kuwa peke yao. Tunakaribia wakati ambao kila mmoja wetu atamhitaji mwenzake, vijana kwa wazee. Naam, sasa ndio wakati wa kujifunza kufanya kazi pamoja, kusitawisha umoja ambao utakuwa muhimu sana siku za usoni.

 “VIUNGO VYA MTU NA MWENZAKE”

14, 15. (a) Yehova anawazoeza vijana na wazee leo akiwa na lengo gani? (b) Yehova anatupatia mashauri gani ili kututia moyo tuwe na umoja?

14 Yehova anatusaidia ili ‘tumtumikie bega kwa bega.’ (Sef. 3:8, 9) Anatuzoeza ili tutende kulingana na kusudi lake la milele. Hilo linatia ndani nini? Anakusudia “kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo.” (Soma Waefeso 1:9, 10.) Naam, anataka kuwaunganisha viumbe wote walio tayari kuunganishwa ulimwenguni pote, na atafanikiwa kufanya hivyo. Ukiwa kijana, je, jambo hilo halikusaidii kuona umuhimu wa kufanya kazi kwa umoja na tengenezo la Yehova?

15 Yehova anatufundisha kuwa na umoja sasa ili tuweze kuishi kwa umoja milele. Maandiko yanatuhimiza tena na tena ‘tutunzane kwa njia ileile,’ ‘tuwe na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake,’ ‘tuendelee kufarijiana,’ na “kujengana.” (1 Kor. 12:25; Rom. 12:10; 1 The. 4:18; 5:11) Yehova anajua kwamba Wakristo si wakamilifu, na hilo linaweza kufanya iwe vigumu kwetu kuwa na umoja, kwa hiyo tunahitaji kujitahidi ‘kusameheana kwa hiari.’—Efe. 4:32.

16, 17. (a) Kusudi moja la mikutano ni nini? (b) Vijana wanaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yesu akiwa kijana?

16 Pia, Yehova anatuandalia mikutano ya Kikristo ili itufundishe kushikamana pamoja. Tumesoma mara nyingi himizo lililo katika Waebrania 10:24 na 25. Kusudi moja la mikutano hiyo ni ‘kufikiriana ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.’ Hata hivyo, kusudi muhimu ni kwamba mikutano imeandaliwa ili tuweze ‘kutiana moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri tunavyoona siku ile kuwa inakaribia.’

17 Alipokuwa kijana, Yesu aliweka mfano mzuri kwa kuthamini mikutano. Alipokuwa na umri wa miaka 12, alienda na wazazi wake katika kusanyiko kubwa la kiroho. Wakiwa huko, alipotea lakini si kwa sababu alienda kuzurura na vijana wengine. Badala yake, Maria na Yosefu walimpata hekaluni akizungumza na walimu kuhusu mambo ya kiroho.—Luka 2:45-47.

18. Sala zetu zinawezaje kuchangia umoja wetu?

18 Mbali na kusitawisha upendo kati yetu na kutumia mikutano ya Kikristo kuimarisha kifungo cha umoja, tunaweza kusali kwa ajili ya Wakristo wenzetu. Tunaposali kwa Yehova kihususa kuhusu  ndugu zetu, tunakumbuka uhitaji wetu wa kuwajali wenzetu. Mambo hayo hayapaswi kufanywa tu na Wakristo walio watu wazima. Ikiwa wewe ni kijana, je, unatumia maandalizi hayo kusitawisha uhusiano wa karibu na familia yako ya kiroho? Ili uokoke mwisho wa ulimwengu huu, utahitaji kuwa karibu na ndugu zako wala si ulimwengu wa Shetani.

Sisi sote tunaweza kusali kwa ajili ya ndugu zetu (Tazama fungu la 18)

KUONYESHA KWAMBA ‘SISI NI VIUNGO AMBAVYO KILA KIMOJA NI CHA KILE KINGINE’

19-21. (a) Ni njia gani nzuri ya kuonyesha kwamba ‘sisi ni viungo ambavyo kila kimoja ni cha kile kingine’? Toa mifano. (b) Unajifunza nini kutokana na jinsi ndugu walivyotenda misiba ilipotokea?

19 Tayari watu wa Yehova wanaishi kulingana na kanuni ya Waroma 12:5 inayosema: ‘Sisi ni viungo ambavyo kila kimoja ni cha kile kingine.’ Tunaona uthibitisho wa jambo hilo misiba inapotokea. Mnamo Desemba 2011, dhoruba ilisababisha mafuriko makubwa katika kisiwa cha Mindanao nchini Ufilipino. Kwa usiku mmoja, nyumba zaidi ya 40,000 zilifunikwa na maji, kutia ndani nyumba nyingi za ndugu zetu. Hata hivyo, ofisi ya tawi inaripoti kwamba “hata kabla halmashauri za kutoa misaada kuanza kazi, ndugu zetu Wakristo kutoka maeneo mengine walituma misaada.”

20 Vivyo hivyo, tetemeko kubwa sana la nchi pamoja na tsunami zilipopiga mashariki mwa Japani, ndugu na dada wengi walipoteza mali nyingi. Baadhi yao walipoteza karibu kila kitu. Yoshiko, ambaye nyumba yake iliharibiwa kabisa, aliishi umbali wa kilomita 40 hivi kutoka kwenye Jumba la Ufalme. Dada huyo anasema hivi: “Baadaye, tulishangaa kujua kwamba siku moja baada ya tetemeko hilo, mwangalizi wa mzunguko na ndugu mwingine walikuja kututafuta.” Kisha akasema hivi huku akitabasamu: “Tulithamini sana kuona mahitaji yetu ya kiroho yakitoshelezwa kikamili kupitia kutaniko. Isitoshe, tulipewa makoti, viatu, mikoba, na nguo za kulalia.” Mshiriki mmoja wa halmashauri ya kutoa misaada anasema hivi: “Ndugu kutoka kotekote nchini Japani walifanya kazi kwa umoja na kujitahidi kusaidiana. Hata ndugu wengine walisafiri kutoka Marekani kuja kusaidia. Walipoulizwa kwa nini wametoka mbali ili kuja kusaidia, walisema, ‘Tuna umoja na ndugu zetu wa Japani, na wanahitaji msaada.’” Je, hujivunii kuwa sehemu ya tengenezo linalowatunza sana washiriki wake? Uwe na uhakika kwamba Yehova anafurahi sana kuona roho hiyo ya umoja.

21 Kuwa na roho hiyo sasa kutatusaidia kukabili taabu zilizo mbele yetu kwa umoja hata tukitenganishwa na ndugu zetu walio katika sehemu nyingine za dunia. Kwa kweli, kuwa na umoja sasa kunatuzoeza kwa ajili ya hali ngumu ambazo inaelekea tutakabili mfumo huu utakapoangamia. Fumiko, aliyeathiriwa na kimbunga kilichotokea Japani, anasema hivi: “Mwisho uko karibu sana. Tunahitaji kuendelea kuwasaidia waamini wenzetu huku tukitazamia wakati ambapo hakutakuwa na misiba tena.”

22. Umoja wetu wa Kikristo utatunufaishaje wakati ujao?

22 Kwa kweli, vijana na wazee ambao wanajifunza sasa kuwa na umoja wanajitayarisha kuokoka mwisho wa ulimwengu huu mwovu usio na umoja. Kama ilivyokuwa nyakati za kale, Mungu wetu atawakomboa watu wake. (Isa. 52:9, 10) Sikuzote kumbuka kwamba unaweza kuwa miongoni mwa watu waliokombolewa ukijitahidi kuwa sehemu ya watu wa Mungu wenye umoja. Jambo lingine litakalotusaidia ni kuthamini sana mambo ambayo tayari tumepokea. Makala ifuatayo itazungumzia jambo hilo.