Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, ‘Unafahamu Maana’?

Je, ‘Unafahamu Maana’?

“Akafungua akili zao ili kuifahamu maana ya Maandiko.” LUKA 24:45.

1, 2. Yesu aliwaimarishaje wanafunzi wake siku aliyofufuliwa?

SIKU ambayo Yesu alifufuliwa, wanafunzi wake wawili walikuwa wakitembea kwenda kwenye kijiji kilichokuwa umbali wa kilomita 11.2 kutoka Yerusalemu. Hawakujua kwamba Yesu amefufuliwa, hivyo walihuzunishwa sana na kifo chake. Kwa ghafla, Yesu alitokea na kuanza kutembea nao. Aliwafariji wanafunzi hao. Jinsi gani? ‘Akianzia Musa na Manabii wote, aliwafasiria mambo yanayomhusu yeye mwenyewe katika Maandiko yote.’ (Luka 24:13-15, 27) Kisha, mioyo yao ikaanza kuwaka kwa sababu alikuwa ‘akiwafungulia’ au akiwafafanulia Maandiko waziwazi.—Luka 24:32.

2 Jioni hiyohiyo, wanafunzi hao wawili walirudi Yerusalemu. Walipokutana na mitume, waliwasimulia kilichotukia. Walipokuwa wakizungumza, Yesu akawatokea wote. Hata hivyo, mitume wake waliogopa sana. Wakawa na shaka mioyoni mwao. Yesu aliwaimarishaje? Tunaambiwa hivi: “Akafungua akili zao ili kuifahamu maana ya Maandiko.”—Luka 24:45.

3. Huenda tukakabili changamoto gani, na ni nini kinachoweza kutusaidia kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu huduma yetu?

3 Nyakati nyingine, huenda tukahuzunika sana kama wanafunzi hao. Labda tunafanya mengi katika kazi ya Bwana, lakini tumevunjika moyo kwa sababu watu hawaitikii. (1 Kor. 15:58)  Au huenda ikaonekana kwamba wale tunaojifunza nao Biblia hawafanyi maendeleo. Huenda baadhi yao wakamwacha Yehova. Tunaweza kufanya nini ili tuwe na maoni yenye usawaziko kuhusu huduma yetu? Jambo moja linaloweza kutusaidia ni kufahamu maana ya mifano ya Yesu inayotajwa katika Maandiko Matakatifu. Acheni tuchunguze mifano mitatu ili tuone mambo tunayojifunza kutokana nayo.

MPANDAJI ANAYELALA USINGIZI

4. Mfano wa Yesu wa mpandaji anayelala usingizi unamaanisha nini?

4 Soma Marko 4:26-29. Mfano wa Yesu wa mpandaji anayelala usingizi unamaanisha nini? Mpandaji anayetajwa katika mfano huo anafananisha watangazaji wa Ufalme wakiwa mtu mmoja-mmoja. Mbegu ni ujumbe wa Ufalme ambao watu wenye mioyo minyoofu wanahubiriwa. Kama ilivyo kawaida ya maisha, mpandaji “hulala usingizi usiku na huamka mchana.” Mbegu inachukua muda kukua, kuanzia inapopandwa mpaka wakati wa mavuno. Katika kipindi hicho “ile mbegu huota na hukua na kuwa ndefu.” Ukuzi huo hutokea “wenyewe” polepole na hatua kwa hatua. Vivyo hivyo, ukuzi wa kiroho hutokea polepole na hatua kwa hatua. Mtu anapofanya maendeleo na kuchochewa kumtumikia Mungu, anazaa matunda, yaani, anajiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

5. Kwa nini Yesu alitoa mfano wa mpandaji anayelala usingizi?

5 Kwa nini Yesu alitoa mfano huo? Yesu anatusaidia kutambua kwamba Yehova ndiye anayefanya kweli ikue katika mioyo ya watu ‘wenye mwelekeo unaofaa.’ (Mdo. 13:48; 1 Kor. 3:7) Tunapanda na kutia maji, lakini hatukuzi mbegu hiyo. Hatuwezi kulazimisha au kuharakisha ukuzi huo. Sawa na mtu anayetajwa katika mfano huo, hatujui jinsi ukuzi unavyotokea. Mara nyingi hatuoni ukuzi huo tunapoendelea na shughuli zetu za kawaida. Hata hivyo, huenda mbegu ya Ufalme ikazaa matunda baada ya muda. Kisha, mwanafunzi huyo mpya hujiunga nasi katika kazi ya mavuno, na tunafaidika kutokana na msaada wake.—Yoh. 4:36-38.

6. Tunapaswa kutambua nini kuhusu ukuzi wa kiroho?

6 Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano huo? Kwanza, ni lazima tukubali kwamba hatuwezi kulazimisha au kuharakisha ukuzi wa kiroho wa mwanafunzi wa Biblia. Sifa ya kiasi itatusaidia kuepuka kumshinikiza au kumlazimisha mwanafunzi abatizwe. Tunafanya yote tuwezayo kumsaidia na kumtegemeza kiroho mwanafunzi huyo, lakini tunatambua kwa unyenyekevu kwamba kujiweka wakfu ni uamuzi wake binafsi. Kujiweka wakfu ni uamuzi ambao mtu hufanya kwa hiari kutoka moyoni akichochewa na upendo wake kwa Mungu. Yehova hawezi kamwe kukubali wakfu wetu ikiwa hatumpendi kutoka moyoni.—Zab. 51:12; 54:6; 110:3.

7, 8. (a) Tunajifunza mambo gani mengine kutokana na mfano wa Yesu wa mpandaji anayelala usingizi? Toa mfano. (b) Mfano huo unatufundisha nini kumhusu Yehova na Yesu?

7 Pili, kuelewa maana ya mfano huo kutatusaidia kutovunjika moyo tusipopata matokeo mazuri mwanzoni. Tunahitaji kuwa na subira. (Yak. 5:7, 8) Ikiwa tumefanya yote tuwezayo kumsaidia mwanafunzi lakini hafanyi maendeleo, hilo halionyeshi kwamba sisi si waaminifu. Yehova huruhusu mbegu ya kweli isitawi ndani ya moyo wa mtu mnyenyekevu aliye tayari kufanya mabadiliko. (Mt. 13:23) Kwa hiyo, hatupaswi kupima mafanikio ya huduma yetu kulingana na matokeo tunayopata.  Machoni pa Yehova, mafanikio ya huduma yetu hayategemei itikio la watu tunaowafundisha. Yehova anathamini jitihada zetu za uaminifu haidhuru matokeo tunayopata.—Soma Luka 10:17-20; 1 Wakorintho 3:8.

8 Tatu, hatuwezi sikuzote kuona mabadiliko ambayo mtu anafanya. Kwa mfano, wenzi wa ndoa waliokuwa wakijifunza na mmishonari fulani walimfikia na kumwambia wangependa kuwa wahubiri ambao hawajabatizwa. Aliwakumbusha kwamba ili wastahili, walihitaji kuacha kuvuta sigara. Alishangaa sana walipomwambia kwamba waliacha kuvuta sigara miezi kadhaa iliyopita. Kwa nini waliacha? Walitambua kwamba Yehova anawaona wakivuta sigara na anachukia unafiki. Kwa hiyo, waliamua ama kuvuta sigara mbele ya mmishonari huyo au kuacha kabisa. Upendo wao kwa Yehova uliwasaidia kufanya uamuzi unaofaa. Walikuwa wamefanya maendeleo ya kiroho hata ingawa mmishonari huyo hakuwa ameona mabadiliko hayo.

WAVU WA KUKOKOTA

9. Mfano wa wavu wa kukokota unamaanisha nini?

9 Soma Mathayo 13:47-50. Mfano wa Yesu kuhusu wavu wa kukokota unamaanisha nini? Yesu alifananisha kazi ya kuwahubiria watu wote ujumbe wa Ufalme na kushushwa baharini kwa wavu mkubwa wa kukokota. Kama vile tu wavu unavyokusanya ‘samaki wengi wa kila aina,’ ndivyo kazi yetu ya kuhubiri inavyovutia mamilioni ya watu wa kila aina. (Isa. 60:5) Idadi kubwa ya watu wanaohudhuria Ukumbusho na makusanyiko yetu kila mwaka inathibitisha jambo hilo. Baadhi ya samaki hao wa mfano ni “wazuri” na hukusanywa katika kutaniko la Kikristo. Hata hivyo, wengine ‘hawafai’; si wote wanaokusanywa wanaokubaliwa na Yehova.

Baada ya kusoma Mathayo 13:47-50 . . .

10. Kwa nini Yesu alitoa mfano wa wavu wa kukokota?

10 Kwa nini Yesu alitoa mfano huo? Kutenganishwa kwa samaki kwa njia ya mfano hakurejelei hukumu ya mwisho wakati wa dhiki kuu. Badala yake, kunaonyesha jambo litakalotukia katika siku za mwisho za mfumo huu mwovu. Yesu alimaanisha kwamba si wote wanaovutiwa na kweli watasimama upande wa Yehova. Watu wengi wameshirikiana nasi katika mikutano yetu. Wengine wamekubali kujifunza Biblia pamoja nasi lakini hawako tayari kujiweka wakfu kwa Yehova. (1 Fal. 18:21) Wengine wameacha kushirikiana na kutaniko la Kikristo. Baadhi ya vijana wamelelewa na wazazi Wakristo, lakini bado hawajasitawisha upendo kuelekea viwango vya Yehova. Vyovyote vile, Yesu alikazia kwamba kila mtu anahitaji kufanya uamuzi wa kibinafsi. Yehova anawaona wale wanaofanya uamuzi huo kuwa vitu “vyenye kutamanika,” au vyenye thamani “vya mataifa yote.”—Hag. 2:7.

. . . fikiria jinsi tunavyoweza kutumia mfano huo leo

11, 12. (a) Tunawezaje kunufaika kutokana na mfano wa wavu wa kukokota? (b) Mfano huo unatufundisha nini kumhusu Yehova na Yesu?

11 Tunawezaje kunufaika kutokana na mfano wa wavu wa kukokota? Kuelewa maana ya mfano huo hutusaidia kuepuka kuhangaika kupita kiasi au kuvunjika moyo wakati mwanafunzi wa Biblia au mtoto wetu anapokosa kufanya kweli iwe mali yake. Hilo linaweza kutokea licha ya jitihada zetu zote. Kulelewa katika kweli au kukubali kujifunza Biblia hakumaanishi kwamba mtu atasitawisha uhusiano wa karibu sana na Yehova. Wale ambao hawataki kujitiisha chini ya utawala wa Yehova hatimaye wataondolewa kutoka kati ya watu wa Mungu.

Baadhi ya wale wanaovutiwa na kweli watachukua msimamo upande wa Yehova (Tazama fungu la 9-12)

 12 Je, hilo linamaanisha kwamba wale ambao wameacha kweli hawataruhusiwa kamwe kurudi kutanikoni? Au mtu asipojiweka wakfu kwa Yehova, je, ataonwa milele kuwa ‘asiyefaa’? Hapana. Watu hao bado wana fursa ya kurudi kabla ya dhiki kuu kuanza. Ni kana kwamba Yehova anawasihi hivi: “Rudini kwangu, nami nitarudi kwenu.” (Mal. 3:7) Jambo hilo linakaziwa na mfano mwingine uliotolewa na Yesu, mfano wa mwana mpotevu.—Soma Luka 15:11-32.

MWANA MPOTEVU

13. Mfano wa mwana mpotevu unamaanisha nini?

13 Mfano wa Yesu kuhusu mwana mpotevu unamaanisha nini? Baba mwenye huruma katika mfano huo anafananisha Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo, Yehova. Mwana anayeomba urithi wake na kuutapanya anafananisha wale walioacha kutaniko. Waliondoka kana kwamba wanasafiri kwenda “nchi ya mbali,” yaani, ulimwengu wa Shetani ambao umetengwa mbali na Yehova. (Efe. 4:18; Kol. 1:21) Hata hivyo, baada ya muda, baadhi yao wanarudiwa na fahamu na kufunga safari ngumu ya kurudi katika tengenezo la Yehova. Watu hao wanyenyekevu ambao wametubu wanakaribishwa kwa uchangamfu na Baba yetu mwenye kusamehe.—Isa. 44:22; 1 Pet. 2:25.

14. Kwa nini Yesu alitoa mfano wa mwana mpotevu?

14 Kwa nini Yesu alitoa mfano huo? Yesu alitumia mfano huo wenye kuvutia sana kuonyesha kwamba Yehova anataka watu waliomwacha wamrudie. Baba katika mfano huo hakuacha kamwe kutumaini kwamba mwana wake atarudi. Alipomwona mwana wake akirudi, hata ingawa ‘alikuwa angali mbali,’ baba alikimbia na kumkaribisha. Mfano huo unapaswa kuwachochea wale ambao wameacha kweli wamrudie Yehova bila kukawia. Huenda wamechoka kiroho, na huenda wakaona aibu na kushindwa kurudi. Lakini jitihada zao si za bure, na kurudi kwao kutaleta shangwe hata mbinguni.—Luka 15:7.

15, 16. (a) Ni mambo gani tunayojifunza kutokana na mfano wa Yesu kuhusu mwana mpotevu? Toa mifano. (b) Hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova na Yesu?

15 Tunawezaje kunufaika kutokana na mfano wa mwana mpotevu? Tunapaswa kuiga mfano wa Yehova. Hatutaki kamwe kuwa ‘waadilifu kupita kiasi’ na kukataa  kuwakaribisha watenda-dhambi wanaotubu. Tutajiletea tu “ukiwa” au madhara ya kiroho tukifanya hivyo. (Mhu. 7:16) Tunaweza kujifunza jambo lingine kutokana na mfano huo. Mtu yeyote anayeliacha kutaniko anapaswa kuonwa kuwa “kondoo aliyepotea,” bali si kondoo asiyeweza kubadilika. (Zab. 119:176) Tukikutana na mtu aliyeliacha kutaniko lakini hakutengwa na ushirika, je, tutamsaidia kwa upendo kurudi kutanikoni? Je, tutawajulisha wazee bila kukawia ili wampe msaada unaofaa? Tutafanya hivyo ikiwa tutafuata kwa hekima mambo tunayojifunza kutokana na mfano wa mwana mpotevu.

16 Hebu ona jinsi ambavyo baadhi ya wana wapotevu leo wamethamini rehema na upendo wa Yehova na utegemezo wa kutaniko. Ndugu aliyekuwa ametengwa na ushirika kwa miaka 25 anasema hivi: “Shangwe yangu imezidi kuongezeka tangu niliporudishwa kutanikoni kwa kuwa nimepata ‘majira ya kuburudisha’ kutoka kwa Yehova. (Mdo. 3:19) Kila mtu ananitegemeza na kunipenda sana! Nina familia nzuri sana ya kiroho sasa.” Dada mmoja kijana aliyemwacha Yehova kwa miaka mitano alisema hivi aliporudi: “Siwezi kueleza jinsi nilivyohisi nilipoona upendo aliozungumzia Yesu ukidhihirishwa waziwazi kunielekea. Kuwa katika tengenezo la Yehova ni pendeleo kubwa sana!”

17, 18. (a) Tumejifunza mambo gani muhimu kutokana na mifano mitatu tuliyochunguza? (b) Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

17 Tumejifunza mambo gani muhimu kutokana na mifano hiyo mitatu? Kwanza, tunapaswa kutambua kwamba hatutokezi ukuzi wa kiroho. Hiyo ni kazi ya Yehova. Pili, hatuwezi kutarajia kwamba wote wanaoshirikiana nasi na kujifunza nasi watakubali kweli. Mwishowe, hata ingawa huenda baadhi ya Wakristo wakaacha kweli na kumwacha Yehova, hatupaswi kamwe kukata tamaa na kufikiri kwamba hawatarudi. Na wakirudi, acheni tuwakaribishe kwa upendo kama Yehova.

18 Kila mmoja wetu na aendelee kutafuta ujuzi, uelewaji, na hekima. Tunaposoma mifano ya Yesu, tujiulize inamaanisha nini, kwa nini iliandikwa katika Biblia, tunaweza kutumiaje mambo tunayojifunza, na inatufundisha nini kumhusu Yehova na Yesu? Tukifanya hivyo, tutaonyesha kikweli kwamba tunafahamu maana ya maneno ya Yesu.