Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unathamini Mambo Ambayo Umepokea?

Je, Unathamini Mambo Ambayo Umepokea?

“Sisi tulipokea . . . roho inayotoka kwa Mungu, ili tuyajue mambo ambayo Mungu ametupa sisi kwa fadhili.”—1 KOR. 2:12.

1. Watu wengi husema nini?

HUENDA umesikia watu wengi wakisema: ‘Mtu hathamini kitu alicho nacho hadi anapokipoteza.’ Je, umehisi hivyo nyakati nyingine? Mtoto anayepewa chochote anachotaka anaweza kuwa na mwelekeo wa kukosa kuthamini vitu hivyo. Kwa mfano, mtoto anayetoka katika familia tajiri huenda asithamini vitu vingi alivyo navyo. Vivyo hivyo, huenda vijana wasio na uzoefu wakakosa kutambua vitu vyenye thamani maishani.

2, 3. (a) Vijana Wakristo wanapaswa kuwa waangalifu wasifanye nini? (b) Ni nini kitakachotusaidia kuthamini urithi wetu?

2 Ukiwa tineja au kijana mwenye umri wa miaka 20 hivi, ni mambo gani unayoona kuwa muhimu? Vijana wengi ulimwenguni hutanguliza vitu vya kimwili, yaani, mshahara mnono, nyumba nzuri, au vifaa vya kisasa zaidi vya teknolojia. Hata hivyo, ikiwa tunahangaikia tu mambo hayo, basi kuna jambo fulani muhimu linalokosekana—utajiri wa kiroho. Inasikitisha kwamba mamilioni ya watu leo hata hawajaanza kutafuta utajiri huo. Ninyi vijana ambao mmelelewa na wazazi Wakristo ni lazima muwe waangalifu ili msikose kuthamini urithi  wa kiroho ambao mmepokea. (Mt. 5:3) Ukikosa kuthamini urithi huo huenda ukapatwa na mambo mabaya yanayoweza kuharibu maisha yako yote.

3 Hata hivyo, mnaweza kuepuka jambo hilo. Ni nini kitakachowasaidia kuthamini urithi wenu? Acheni tuchunguze mifano fulani ya Biblia inayoweza kutusaidia kuona kwa nini ni jambo la hekima kuthamini urithi wetu wa kiroho. Mifano tutakayochunguza itamsaidia kila kijana na vilevile kila Mkristo kuthamini urithi wake wa kiroho.

HAWAKUTHAMINI URITHI WAO

4. Andiko la 1 Samweli 8:1-5 linafunua nini kuhusu wana wa Samweli?

4 Biblia ina masimulizi ya watu waliopokea urithi mwingi wa kiroho lakini hawakuuthamini. Ilikuwa hivyo katika familia ya nabii Samweli, ambaye alimtumikia Yehova tangu utotoni na alikuwa na sifa nzuri machoni pa Mungu. (1 Sam. 12:1-5) Samweli aliwawekea wanawe, Yoeli na Abiya, mfano mzuri ambao walipaswa kuiga. Hata hivyo, hawakuthamini jambo hilo, na hivyo wakawa watu wabaya. Masimulizi ya Biblia yanasema kwamba tofauti na baba yao, wana hao ‘walipotosha hukumu.’—Soma 1 Samweli 8:1-5.

5, 6. Wana wa Yosia na mjukuu wake walitendaje?

5 Ndivyo ilivyokuwa pia na wana wa Mfalme Yosia. Yosia aliweka mfano mzuri sana katika kumwabudu Yehova. Kitabu cha Sheria ya Mungu kilipopatikana na kusomwa mbele ya Yosia, alijitahidi sana kufuata maagizo ya Yehova. Aliondoa ibada ya sanamu na zoea la kuwasiliana na pepo, na aliwatia moyo watu wamtii Yehova. (2 Fal. 22:8; 23:2, 3, 12-15, 24, 25) Wana wa Yosia walikuwa na urithi mwingi sana wa kiroho! Wanawe watatu na mjukuu mmoja waliwekwa kuwa wafalme baadaye, lakini hakuna yeyote kati yao aliyethamini urithi aliopokea.

6 Yehoahazi, alirithi ufalme baada ya Yosia, baba yake kufa, lakini alifanya “yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.” Alitawala kwa miezi mitatu tu kisha Farao wa Misri akamtia kifungoni, na hatimaye Yehoahazi akafa utekwani. (2 Fal. 23:31-34) Kisha Yehoyakimu, ndugu yake, akatawala kwa miaka 11. Yeye pia hakuthamini urithi wa kiroho aliopokea kutoka kwa baba yake. Kwa sababu ya mwenendo mbaya wa Yehoyakimu, Yeremia alitabiri hivi kumhusu: “Atazikwa kwa maziko ya punda-dume.” (Yer. 22:17-19) Sedekia, mwana wa Yosia, na Yehoyakini, mjukuu wa Yosia, waliokuwa wafalme baadaye, walitenda mabaya na hawakufuata mfano mzuri wa Yosia.—2 Fal. 24:8, 9, 18, 19.

7, 8. (a) Sulemani alipotezaje urithi wake wa kiroho? (b) Tunajifunza nini kutokana na mifano inayotajwa katika Biblia ya wale waliopoteza urithi wao wa kiroho?

7 Mfalme Sulemani alipokea mambo mengi kutoka kwa Daudi, baba yake. Ingawa Sulemani alilelewa katika familia iliyopenda mambo ya kiroho, na aliyathamini mwanzoni, lakini baadaye aliacha kuyathamini. “Sulemani alipokuwa mzee, wake zake wakawa wameugeuza moyo wake ukaifuata miungu mingine; na moyo wake haukuwa mkamilifu kwa Yehova Mungu wake, kama moyo wa Daudi baba yake.” (1 Fal. 11:4) Kwa sababu hiyo, Sulemani alipoteza kibali cha Yehova.

8 Inasikitisha kwamba wanaume hao waliokuwa na malezi mazuri na fursa ya kufanya mema, hawakutumia fursa hiyo. Lakini si vijana wote wanaotajwa katika Biblia waliopoteza urithi wao wa kiroho, wala si vijana wote wanaofanya hivyo leo. Acheni tuchunguze baadhi ya vijana walioweka mfano mzuri wa kuigwa na vijana Wakristo.

 WALITHAMINI MAMBO WALIYOPOKEA

9. Wana wa Noa walituwekeaje mfano mzuri sana? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 27.)

9 Wana wa Noa walituwekea mfano mzuri sana. Baba yao aliamriwa ajenge safina na kuingiza familia yake ndani ya safina hiyo. Bila shaka, wana wa Noa walitambua uhitaji wa kufanya mapenzi ya Yehova. Ni wazi kwamba walishirikiana na baba yao. Walimsaidia kujenga safina, kisha wakaingia ndani yake. (Mwa. 7:1, 7) Walikuwa na lengo gani? Andiko la Mwanzo 7:3 linasema kwamba waliingiza wanyama ndani ya safina “ili kuhifadhi hai uzao juu ya uso wa dunia yote.” Wanadamu pia waliokolewa. Kwa sababu wana wa Noa walithamini kile walichopokea kutoka kwa baba yao, walipata pendeleo la kusaidia kuhifadhi jamii ya wanadamu na kuanzisha tena ibada ya kweli katika dunia iliyosafishwa.—Mwa. 8:20; 9:18, 19.

10. Vijana wanne Waebrania waliokuwa Babiloni walionyeshaje kwamba walithamini kweli walizokuwa wamejifunza?

10 Karne nyingi baadaye, vijana wanne Waebrania walionyesha kwamba walijua kilichokuwa muhimu zaidi. Hanania, Mishaeli, Azaria, na Danieli walipelekwa Babiloni mwaka wa 617 K.W.K. Walikuwa vijana wenye sura nzuri na wenye akili ambao wangefanikiwa sana Babiloni. Lakini matendo yao yalionyesha wazi kwamba walikumbuka urithi wao, yaani, mambo waliyokuwa wamefundishwa. Vijana hao wanne walibarikiwa sana kwa kufuata mambo ya kiroho waliyojifunza wakiwa watoto.—Soma Danieli 1:8, 11-15, 20.

11. Wengine walinufaikaje na urithi wa kiroho ambao Yesu alipokea?

11 Yesu, Mwana wa Mungu aliweka mfano bora zaidi kwa kuthamini urithi wake wa kiroho. Alipokea mambo mengi kutoka kwa Baba yake, naye aliyathamini sana. Maneno haya aliyosema yanaonyesha wazi kwamba alithamini mambo aliyofundishwa: “Kama vile Baba alivyonifundisha, ndivyo ninavyosema mambo haya.” (Yoh. 8:28) Alitamani sana kuwafundisha wengine mambo aliyopokea. Aliwaambia watu hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:18, 43) Aliwasaidia wasikilizaji wake kuona uhitaji wa kutokuwa “sehemu ya ulimwengu,” ambao kwa ujumla hauthamini mambo ya kiroho.—Yoh. 15:19.

THAMINI MAMBO AMBAYO UMEPOKEA

12. (a) Andiko la 2 Timotheo 3:14-17 linawahusuje vijana wengi leo? (b) Vijana Wakristo wanapaswa kujiuliza maswali gani?

12 Kama vijana ambao tumezungumzia, huenda wewe pia umelelewa na wazazi wanaomwabudu Yehova Mungu. Ikiwa ndivyo, yale ambayo Maandiko yanasema kumhusu Timotheo yanakuhusu. (Soma 2 Timotheo 3:14-17.) “Ulijifunza” kutoka kwa wazazi wako kumhusu Mungu wa kweli na jinsi ya kumpendeza. Huenda wazazi wako walianza kukufundisha tangu utoto mchanga. Bila shaka, mafundisho hayo yamekusaidia sana kuwa “mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia imani kuhusiana na Kristo Yesu” na kukusaidia uwe na “vifaa kamili” kwa ajili ya utumishi wako kwa Mungu. Swali muhimu sasa ni, Je, utathamini yale ambayo umepokea? Huenda swali hilo likakuchochea kujichunguza. Jiulize maswali kama haya: ‘Ninahisije kuwa miongoni mwa mashahidi wengi waaminifu? Ninahisije kuwa miongoni mwa watu wachache sana duniani ambao wanajulikana na Mungu? Je, ninaona kujua kweli kuwa pendeleo kubwa na la pekee?’

Unahisije kuwa miongoni mwa mashahidi wengi waaminifu? (Tazama fungu la 9, 10, na 12)

13, 14. Vijana fulani Wakristo wanapata vishawishi gani, lakini kwa nini si jambo la hekima kukubali kushindwa na vishawishi hivyo? Toa mfano.

 13 Huenda vijana fulani waliolelewa na wazazi Wakristo wasione tofauti kubwa iliyopo kati ya paradiso yetu ya sasa ya kiroho na ulimwengu wa Shetani wenye giza. Wengine hata wameshawishiwa kuonja maisha ya ulimwengu. Fikiria hili: Je, ungekimbia barabarani ili uone ikiwa utaumia au kufa ukigongwa na gari? Bila shaka hungefanya hivyo! Vivyo hivyo, hakuna haja ya kuingia kwenye ‘dimbwi la chini la upotovu’ la ulimwengu huu ili uone madhara yatakayokupata.—1 Pet. 4:4.

14 Gener, ambaye anaishi barani Asia, alilelewa katika familia ya Kikristo. Alibatizwa akiwa na umri wa miaka 12. Hata hivyo, alipokuwa tineja alivutiwa na mambo ya ulimwengu. Anasema hivi: “Nilitaka kufurahia ‘uhuru’ ambao ulimwengu unaahidi.” Gener alianza kuishi maisha ya kinafiki. Alipofikia umri wa miaka 15, tayari alikuwa akiishi maisha mabaya kama rafiki zake. Alikuwa akilewa na kutumia matusi kama wao. Gener alizoea kurudi nyumbani usiku sana baada ya kucheza mchezo wa biliadi na michezo ya kompyuta yenye jeuri pamoja na rafiki zake. Hata hivyo, baada ya muda, alianza kutambua kwamba mambo yenye kuvutia ya ulimwengu huu hayakumletea furaha ya kweli. Yalikuwa maisha ya ubatili. Anasema hivi baada ya kurudi kutanikoni: “Bado ninapata vishawishi vingi, lakini Yehova amenibariki sana.”

15. Vijana ambao hawakulelewa na wazazi Wakristo wanapaswa kutafakari kuhusu nini?

15 Bila shaka, kuna vijana wengine wanaoshirikiana na kutaniko ambao hawakulelewa na wazazi Wakristo. Ikiwa wewe ni mmoja wao, hebu wazia pendeleo kubwa ulilo nalo sasa kwa sababu unamjua na unamtumikia Muumba! Kuna mabilioni ya watu duniani. Kwa hiyo, ni pendeleo kubwa kuwa miongoni mwa wale ambao kwa fadhili Yehova amewavuta na kuwafunulia kweli ya Biblia. (Yoh. 6:44, 45) Ni mtu 1 tu kati ya watu 1,000 duniani leo ambaye ana ujuzi sahihi wa kweli, na wewe ni mmoja wao. Je, hilo halipaswi kutufanya sisi sote tushangilie, haidhuru jinsi tulivyojifunza kweli? (Soma 1 Wakorintho 2:12.) Gener anasema hivi: “Mimi hutetemeka ninapofikiria jambo hilo. Mimi ni nani ili nijulikane na Yehova, Mmiliki wa ulimwengu mzima?”  (Zab. 8:4) Dada mmoja Mkristo ambaye ni jirani ya Gener alisema hivi: “Wanafunzi hufurahi sana mwalimu anapowajua. Ni pendeleo kubwa kama nini kujulikana na Yehova, yule Mfundishaji Mkuu!”

UTAFANYA NINI?

16. Vijana Wakristo leo wanapaswa kufanya uamuzi gani wenye hekima?

16 Unapofikiria pendeleo kubwa ulilo nalo, azimia kabisa kuwa miongoni mwa watu wachache sana wanaotumia maisha yao kwa njia inayofaa. Ukifanya hivyo, utakuwa miongoni mwa watumishi wengi waaminifu wa Mungu. Hilo ndilo jambo la hekima zaidi unaloweza kufanya badala ya kuwafuata kama kipofu vijana wengi na kuangamia pamoja na ulimwengu huu.—2 Kor. 4:3, 4.

17-19. Ni nini kitakachokusaidia kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu kuwa tofauti na ulimwengu?

17 Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba sikuzote itakuwa rahisi kuwa tofauti na ulimwengu. Hata hivyo, ni jambo la hekima kuwa tofauti. Kwa mfano: Fikiria mwanariadha anayeshiriki katika mashindano ya Olimpiki. Bila shaka alijitahidi kuwa tofauti ili afikie kiwango cha kushiriki katika mashindano hayo. Inaelekea kwamba alijinyima mambo mengi ambayo yangempotezea wakati na kumzuia asifanye mazoezi ifaavyo. Kwa upande mwingine, kuwa tofauti na marafiki wake kutamsaidia kufanya mazoezi na kufikia lengo lake.

18 Watu wengi katika ulimwengu hawafikirii wakati wao ujao. Lakini ukifikiria wakati wako ujao, ukiwa tofauti na ulimwengu, na kuepuka upotovu wa maadili na mambo mengine yanayoweza kudhuru hali yako ya kiroho, ‘utashika imara uzima ulio wa kweli.’ (1 Tim. 6:19) Dada aliyetajwa awali anasema hivi: “Ikiwa utasimama imara na kutetea imani yako, baadaye utafurahi sana kwamba ulifanya hivyo. Hilo litathibitisha kwamba una ujasiri wa kuwa tofauti na ulimwengu wa Shetani. Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba utamfurahisha Yehova Mungu na kumfanya atabasamu. Hilo litafanya ufurahi kwamba ulikuwa tofauti!”

19 Maisha ni ubatili ikiwa mtu anakazia fikira yale tu anayoweza kupata sasa. (Mhu. 9:2, 10) Ikiwa wewe ni kijana na unafikiria kwa uzito kusudi la maisha yako na fursa uliyo nayo ya kuishi milele, je, si jambo la hekima kuepuka “kutembea kama vile mataifa wanavyotembea” na badala yake kuishi maisha yenye kusudi sasa?—Efe. 4:17; Mal. 3:18.

20, 21. Tukifanya maamuzi mazuri, tutatarajia nini, lakini tunapaswa kufanya nini?

20 Tukifanya maamuzi mazuri, tunaweza kuwa na maisha yenye kuridhisha sasa na kutarajia ‘kuirithi dunia,’ yaani, kupata uzima wa milele. Tunatarajia baraka nyingi ajabu, hata hatuwezi kuwazia baraka zote tutakazopata. (Mt. 5:5; 19:29; 25:34) Ni kweli kwamba Mungu hatubariki bila sisi kufanya jitihada zozote. Anataka tufanye jambo fulani. (Soma 1 Yohana 5:3, 4.) Lakini bila shaka kuna faida ya kumtumikia kwa uaminifu sasa!

21 Ni pendeleo kubwa kama nini kupokea mambo mengi sana kutoka kwa Mungu! Tuna ujuzi sahihi wa Neno lake na tunaelewa vizuri ukweli kumhusu na kuhusu makusudi yake. Tuna pendeleo la kuitwa kwa jina lake na kuwa Mashahidi wake. Mungu anatuahidi kwamba yuko upande wetu. (Zab. 118:7) Acheni sisi sote, vijana kwa wazee, tuonyeshe uthamini wetu kwa kuishi katika njia inayoonyesha kwamba tunatamani kumpa Yehova “utukufu milele.”—Rom. 11:33-36; Zab. 33:12.