Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Huwabariki Sana Wenye Nia ya Kutoa

Yehova Huwabariki Sana Wenye Nia ya Kutoa

MUUMBA wetu amewaheshimu wanadamu kwa kuwapa zawadi yenye thamani sana ya hiari. Kwa kuongezea, Yehova huwabariki sana wale wanaotumia hiari yao kuendeleza ibada ya kweli na ambao hushiriki kutakasa jina lake takatifu na kuunga mkono kusudi lake kuu. Yehova hataki tumtii ili kutimiza wajibu tu au kwa kulazimishwa au kutishwa. Badala yake, anathamini sana tunapojitoa kwa hiari kwa sababu tunampenda kikweli na kumthamini kutoka moyoni.

Kwa mfano, Waisraeli walipokuwa katika nyika ya Sinai, Yehova aliwaagiza wajenge mahali pa ibada. Alisema hivi: “Kutoka katikati yenu toeni mchango kwa ajili ya Yehova. Kila mtu mwenye moyo wenye nia na aulete ukiwa mchango wa Yehova.” (Kut. 35:5) Kila Mwisraeli angetoa chochote alichoweza kutoa, na kila mchango wa hiari ulitumiwa kwa njia inayofaa ili kutimiza kusudi la Mungu, haidhuru mtu alitoa kitu gani au kiasi gani. Waisraeli waliitikiaje?

“Kila mtu ambaye moyo wake ulimsukuma” na “kila mtu ambaye roho yake ilimchochea” alitoa mchango wa hiari, “kila mtu mwenye moyo wenye nia.” Wanaume na wanawake walileta kwa hiari kitu fulani kwa ajili ya kazi ya Yehova. Walileta bizimu, vipuli, pete, dhahabu, fedha, shaba, uzi wa bluu, sufu iliyotiwa rangi ya zambarau, kitambaa chenye rangi nyekundu, kitani bora, manyoya ya mbuzi, ngozi za kondoo-dume zilizotiwa rangi nyekundu, ngozi za sili, mbao za mshita, mawe yenye thamani, zeri, na mafuta. Hatimaye, “vitu hivyo vikawa vya kutosha kwa ajili ya kazi yote iliyopasa kufanywa, na kuzidi.”—Kut. 35:21-24, 27-29; 36:7.

Jambo lililomfurahisha zaidi Yehova si vitu walivyotoa, bali ni roho ya kutoa kwa hiari ya wale ambao walitegemeza ibada safi. Walichochewa pia kutumia kwa hiari wakati na nguvu zao. Masimulizi hayo yanasema: “Wanawake wote waliokuwa wenye hekima ya moyo wakasokota kwa mikono yao.” Kwa kweli, “wanawake wote ambao mioyo yao iliwasukuma kwa hekima wakasokota manyoya ya mbuzi.” Isitoshe, Yehova alimpa Bezaleli ‘hekima, uelewaji, na ujuzi katika kila aina ya ufundi.’ Kwa kweli, Mungu aliwajaza Bezaleli na Oholiabu ustadi uliohitajiwa ili kufanya kazi aliyowaagiza.—Kut. 35:25, 26, 30-35.

Yehova alipowaomba Waisraeli watoe mchango, alikuwa na uhakika kabisa kwamba “kila mtu mwenye moyo wenye nia” angetegemeza ibada ya kweli. Na Yehova aliwabariki sana waliokuwa na roho ya kutoa kwa hiari kwa kuwaongoza na kuwapa shangwe isiyo na kifani. Kwa njia hiyo, Yehova alionyesha kwamba anapobariki roho ya kutoa kwa hiari ya watumishi wake, anaweza kuhakikisha kwamba wana mali na ujuzi wa kutimiza mapenzi yake. (Zab. 34:9) Unapomtumikia Yehova bila ubinafsi, kwa hakika atabariki nia yako ya kutoa.