Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha Bidii Yako Katika Huduma

Dumisha Bidii Yako Katika Huduma

KUHUBIRI habari njema ndiyo kazi muhimu zaidi inayofanywa duniani leo. Ni wazi kwamba ukiwa mtumishi wa Yehova, unaona ni pendeleo kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi. Hata hivyo, bila shaka utakubali kwamba mara kwa mara mapainia na wahubiri hukabili changamoto katika kudumisha bidii yao katika huduma.

Ni nini kinachoweza kukusaidia kudumisha bidii yako katika huduma?

Ni vigumu kwa wahubiri fulani kuwapata watu wa kuwahubiria wanapohubiri nyumba kwa nyumba. Kwa kweli, watu wengi huenda wasipatikane nyumbani. Wenye nyumba wanapopatikana, huenda wasipendezwe na ujumbe wa Ufalme au huenda hata wakawa wakali. Wahubiri wengine wanahisi wanalemewa kwa sababu wana eneo kubwa la kuhubiri lenye matokeo mazuri na wana wasiwasi kwamba hawataweza kulihubiri lote. Na baadhi ya washiriki wengine wa kutaniko wamekuwa wakihubiri kwa miaka mingi—muda mrefu kuliko walivyotazamia—na hivyo wamevunjika moyo.

Je, tunapaswa kushangaa kwa sababu watu wote wa Yehova wanakabili changamoto ambazo zinaweza kuwafanya wapunguze bidii yao katika kazi ya kuhubiri? Hapana. Katika ulimwengu unaotawaliwa na “yule mwovu,” Shetani Ibilisi, je, yeyote kati yetu anapaswa kutazamia kwamba itakuwa rahisi kwetu kuhubiri ujumbe wa kweli tuliokabidhiwa na Mungu ambao unaokoa uhai?—1 Yoh. 5:19.

Hata iwe unakabili changamoto gani katika kazi ya kutangaza habari njema, uwe na hakika kwamba Yehova anaweza kukusaidia kushinda changamoto hizo. Hata hivyo, unaweza kufanya nini ili kuongeza bidii yako katika huduma ya Kikristo? Acheni tuchunguze mapendekezo machache.

WASAIDIE WASIO NA UZOEFU

Kila mwaka, maelfu wanabatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Ikiwa umejiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa hivi karibuni, bila shaka utathamini sana msaada kutoka kwa wale wenye uzoefu ambao wamekuwa wakihubiri kwa miaka mingi. Ikiwa umekuwa mhubiri wa Ufalme kwa miaka mingi, je, halingekuwa jambo linalofaa na lenye kuthawabisha kusaidia kuwazoeza wapya?

Yesu alijua kwamba wanafunzi wake walihitaji mwongozo ili wawe waeneza-injili stadi, na aliwaonyesha jinsi kazi hiyo inavyopaswa kufanywa. (Luka 8:1) Leo, pia, kuna uhitaji wa kuwazoeza wengine ili wawe wahudumu stadi.

Hatupaswi kufikiri kwamba mhubiri mpya atakuwa mwalimu stadi kwa kushiriki tu katika huduma. Mhubiri mpya anahitaji kuzoezwa kibinafsi na mwalimu mwenye fadhili na upendo. Mazoezi hayo yatatia ndani kumwonyesha mhubiri asiye na uzoefu jinsi ya (1) kutayarisha utoaji fulani na kufanya mazoezi, (2) kuzungumza na mwenye nyumba au mpita-njia, (3) kutoa machapisho, (4) kumrudia mtu anayependezwa, na (5) kuanzisha funzo la Biblia. Inaelekea kwamba matokeo yatakuwa mazuri ikiwa mhubiri anayezoezwa anaona na kuiga mbinu za kuhubiri zinazotumiwa na yule anayemzoeza. (Luka 6:40) Bila shaka, mhubiri huyo mpya atathamini kuwa na mtu ambaye anaweza kumsikiliza na kumsaidia anapohitaji msaada. Mhubiri asiye na uzoefu atafaidika pia akipongezwa na kupewa mapendekezo yatakayomsaidia.—Mhu. 4:9, 10.

ZUNGUMZA NA MWANDAMANI WAKO

Pindi nyingine hutaweza kuzungumza na wenye nyumba licha ya jitihada zako, kwa hiyo utazungumza tu na mwandamani wako katika utumishi wa shambani. Kumbuka kwamba Yesu aliwatuma wanafunzi wake wakiwa “wawili-wawili” ili kuhubiri. (Luka 10:1) Wanafunzi walipohubiri pamoja, wangeweza kuchocheana na kutiana moyo. Kwa hiyo, tunapohubiri na mwamini mwenzetu tunapata fursa nzuri ya kuwa na “ubadilishanaji wa kitia-moyo.”—Rom. 1:12.

Mnaweza kuzungumzia mambo gani? Je, hivi karibuni mmoja wenu amepata jambo lililoonwa lenye kutia moyo katika huduma? Je, umepata jambo linalopendeza katika funzo lako la kibinafsi au la familia? Je, ulijengwa na jambo fulani ulilosikia kwenye mkutano? Nyakati nyingine, huenda ukahubiri na mtu ambaye kwa kawaida huhubiri naye. Je, unajua alipataje kweli? Ni nini kilichomsadikishia kwamba hili ni tengenezo la Yehova? Amepata mapendeleo au mambo gani yaliyoonwa? Labda unaweza kumsimulia mambo fulani uliyoona katika utumishi wako kwa Yehova. Haidhuru itikio la mwenye nyumba, tunapohubiri na mtu mwingine katika utumishi wa shambani tunapata fursa nzuri ya ‘kuendelea kujengana.’—1 The. 5:11.

DUMISHA MAZOEA MAZURI YA KUJIFUNZA

Ili udumishe bidii katika huduma ni muhimu kusitawisha na kudumisha mazoea mazuri ya kujifunza. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” huchapisha habari zinazozungumzia mambo mbalimbali. (Mt. 24:45) Kwa hiyo, kuna habari nyingi mbalimbali unazoweza kujifunza ili kujilisha kiroho. Acheni tufikirie habari unayoweza kujifunza kibinafsi: Kwa nini kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme ni muhimu sana? Sanduku linaloonyeshwa kwenye ukurasa wa 16 linataja baadhi ya sababu.

Kuchunguza sababu zilizoorodheshwa kwenye sanduku hilo kunaweza kukuchochea kuendelea kuhubiri kwa bidii. Wakati wa funzo lako, kwa nini usiwe na mradi wa kutafuta sababu nyingine unazoweza kuongeza kwenye orodha hiyo? Kisha tafakari sababu hizo na maandiko yanayoziunga mkono. Bila shaka, kufanya hivyo kutaimarisha bidii yako katika huduma.

UWE TAYARI KUTUMIA MAPENDEKEZO

Tengenezo la Yehova huandaa kwa ukawaida mapendekezo yanayokusudiwa kutusaidia kuboresha huduma yetu. Kwa mfano, mbali na kuhubiri nyumba kwa nyumba, tunaweza kuhubiri kupitia barua, simu, barabarani au kwenye maeneo mengine ya umma, na kuhubiri habari njema isivyo rasmi na katika maeneo ya kibiashara. Tunaweza pia kufanya mipango ili tuweze kuhubiri katika eneo lisilohubiriwa kwa ukawaida.

Je, uko tayari kutumia mapendekezo hayo? Je, umejaribu kutumia baadhi ya mapendekezo hayo? Wengi ambao wameyatumia wamepata matokeo yenye kufurahisha sana. Fikiria mifano mitatu.

Mfano wa kwanza unaonyesha matokeo ya kutumia jambo lililozungumziwa katika makala ya Huduma ya Ufalme kuhusu jinsi ya kuanzisha mafunzo ya Biblia. Makala hiyo ilimchochea dada anayeitwa April kuwaeleza wafanyakazi wenzake watatu kuhusu mpango wa kujifunza Biblia. Alishangaa na kusisimka wakati wafanyakazi wote watatu walipokubali kujifunza Biblia, nao wakaanza pia kuhudhuria mikutano ya kutaniko.

Mfano wa pili unahusu jinsi ya kutoa magazeti yetu. Tumekuwa tukihimizwa kutafuta watu ambao huenda wakavutiwa na makala hususa katika magazeti yetu. Mwangalizi fulani wa mzunguko nchini Marekani aliripoti kwamba aliwapelekea wasimamizi wa maduka yote ya magurudumu katika eneo fulani gazeti la Amkeni! lenye makala kuhusu magurudumu. Yeye na mke wake walipeleka pia mfululizo wa makala zenye kichwa “Kuwaelewa Madaktari,” kwenye ofisi zaidi ya 100 za madaktari katika mzunguko wao. Anasema hivi: “Ziara hizo zimewasaidia sana watu kutufahamu sisi na machapisho yetu. Baada ya kusitawisha urafiki na watu katika maeneo hayo, tumeweza kuwatembelea mara nyingi.”

Mfano wa tatu unahusu kuhubiri kupitia simu. Dada anayeitwa Judy aliandikia makao yetu makuu akishukuru kwa kitia-moyo cha kuhubiri kupitia simu. Alisema kwamba mama yake mwenye umri wa miaka 86, aliye na matatizo mengi ya afya, kwa kawaida hushiriki aina hii ya utumishi mtakatifu, na amekuwa akipata shangwe nyingi kwa kujifunza Biblia kupitia simu na mwanamke mwenye umri wa miaka 92!

Mapendekezo ya kuhubiri yaliyo katika machapisho yetu yana matokeo sana. Yatumie! Yanaweza kukusaidia kudumisha shangwe na bidii yako katika huduma.

WEKA MIRADI UNAYOWEZA KUTIMIZA

Mafanikio yetu katika kazi ya kuhubiri hayapimwi kwa idadi ya machapisho tunayosambaza, idadi ya mafunzo ya Biblia tunayoongoza, au idadi ya watu tunaowasaidia kuwa watumishi wa Yehova. Kwa kweli, Noa aliwasaidia watu wangapi ambao hawakuwa wa familia yake kuwa waabudu wa Yehova? Hata hivyo, ni wazi kwamba Noa alikuwa mhubiri mwenye mafanikio. Jambo muhimu ni kwamba tunamtumikia Yehova kwa uaminifu.—1 Kor. 4:2.

Wahubiri wengi wa Ufalme huona kwamba ili kuchochea bidii yao katika kazi ya kuhubiri, wanahitaji kuweka miradi wanayoweza kutimiza. Miradi gani? Sanduku kwenye ukurasa huu lina mapendekezo machache.

Kwa msaada wa Yehova, tafuta njia za kufanya utumishi wako ufurahishe na uwe wenye matokeo. Ukitimiza miradi yako, utapata shangwe na kuridhika kwa sababu unafanya yote uwezayo kuhubiri habari njema.

Ni kweli kwamba kuhubiri habari njema kunaweza kuwa na changamoto. Hata hivyo, kuna mambo ambayo unaweza kufanya ili uwe mtangazaji wa Ufalme mwenye bidii. Furahia badilishano la kitia-moyo na mwandamani wako, sitawisha na udumishe mazoea mazuri ya kujifunza, tumia mapendekezo ya mtumwa mwaminifu, na uweke miradi unayoweza kutimiza. Zaidi ya yote, kumbuka kwamba Mungu amekupa pendeleo lisilo na kifani la kutangaza habari njema ukiwa Shahidi wake. (Isa. 43:10) Utapata shangwe kubwa kama nini unapoendelea kudumisha bidii yako katika huduma!