Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

KUTOKA KATIKA HIFADHI YA VITU VYETU VYA KALE

“Majira Muhimu Sana”

“Majira Muhimu Sana”

MNAMO mwaka wa 1870, kikundi kidogo kilichokuwa Pittsburgh (Allegheny), Pennsylvania, Marekani, kilianza kuchunguza Maandiko. Kikundi hicho kilichokuwa kikiongozwa na Charles Taze Russell, kilichunguza kuhusu fidia ya Kristo na punde si punde kikagundua kuwa fidia ni muhimu sana katika kusudi la Yehova. Walisisimka kama nini walipojifunza kwamba fidia huwapa watu nafasi ya kupata wokovu, hata wale ambao hawajawahi kusikia kuhusu Yesu! Walichochewa kuonyesha uthamini wao kwa kuadhimisha kifo cha Yesu kila mwaka ili kumkumbuka.—1 Kor. 11:23-26.

Ndugu Russell alianza kuchapisha gazeti Zion’s Watch Tower, ambalo lilitetea fundisho la fidia kuwa wonyesho mkubwa zaidi wa upendo wa Mungu. Gazeti hilo lilisema kwamba Ukumbusho wa kifo cha Kristo ni “majira muhimu sana” na liliwahimiza wasomaji waadhimishe Ukumbusho huko Pittsburgh au mahali pengine popote wakiwa kwenye vikundi vidogo. “Hata wakiwa watu wawili au watatu wenye imani moja yenye thamani”—au mtu mmoja tu—atakuwa ‘pamoja na Bwana kwa njia ya kiroho.’

Kila mwaka, watu wengi zaidi walikuja Pittsburgh kwa ajili ya Ukumbusho. Mwaliko ulisema hivi: “Utakaribishwa kwa moyo mchangamfu.” Kwa kweli, Wanafunzi wa Biblia wenyeji waliwakaribisha kwa hiari ndugu na dada zao wa kiroho nyumbani mwao na kuwapa chakula. Mnamo mwaka wa 1886, “Mkutano Mkuu” ulifanywa kwa siku kadhaa wakati wa majira ya Ukumbusho. Gazeti Zion’s Watch Tower lilihimiza hivi: “Njoo, moyo wako ukiwa umefurika upendo kwa Bwana, kwa ndugu zake, na kweli yake.”

Mchoro huu unaonyesha utaratibu uliotumiwa kupitisha mkate na divai ya Ukumbusho katika London Tabernacle

Kwa miaka mingi, Wanafunzi wa Biblia jijini Pittsburgh walifanya makusanyiko kwa ajili ya watu walioamini fidia ambao walihudhuria Ukumbusho huko. Kadiri idadi ya Wanafunzi wa Biblia ilivyoongezeka, ndivyo makusanyiko ya Ukumbusho yalivyokuwa mengi zaidi na makubwa zaidi ulimwenguni pote. Ray Bopp wa eklesia (kutaniko) ya Chicago, alikumbuka kwamba kati ya mwaka wa 1910 na 1919, ilichukua saa kadhaa kupitisha mkate na divai ya Ukumbusho kwa mamia ya wahudhuriaji kwa sababu karibu wote walikuwa wanakula mkate na kunywa divai.

Walitumia mifano gani? Ingawa walijua kuwa Yesu alitumia divai wakati wa Mlo wa Jioni wa Bwana, kwa kipindi fulani gazeti Mnara wa Mlinzi lilipendekeza maji ya zabibu au ya zabibu zilizochemshwa yatumiwe, ili wale ambao ni “dhaifu katika mwili” wasishawishiwe. Hata hivyo, divai ilitolewa kwa wale waliohisi kwamba “divai iliyochacha ilipaswa kutumiwa.” Baadaye Wanafunzi wa Biblia walielewa kwamba divai nyekundu isiyo na vikolezo ndiyo inayofananisha damu ya Yesu kwa njia inayofaa.

Karatasi hii na penseli ilipitishwa kutoka chumba kimoja hadi kingine ili kuandika hudhurio la Ukumbusho gerezani nchini Nikaragua

Kukumbuka kifo cha Yesu kuliwapa watu fursa ya kutafakari kwa uzito kuhusu fidia. Hata hivyo, katika baadhi ya makutaniko huzuni ilitanda, na programu ilipokwisha wahudhuriaji wote waliondoka bila kusema neno lolote. Kitabu Yehova [cha Kiingereza] cha mwaka wa 1934, kilisema kwamba watu hawapaswi kuadhimisha Ukumbusho wakiwa na “huzuni” kwa sababu ya kifo cha Yesu chenye maumivu, bali wanapaswa “kushangilia” utawala wake akiwa Mfalme tangu mwaka wa 1914.

Ndugu wakiwa wamekusanyika katika kambi ya kazi ngumu Mordvinia, Urusi, ili kuadhimisha Ukumbusho mwaka wa 1957

Mwaka wa 1935, kulitokea badiliko kubwa sana ambalo lilibadili maadhimisho ya Ukumbusho yaliyofuata. Maana ya “mkutano mkubwa” (UV), au “umati mkubwa,” unaotajwa katika Ufunuo 7:9 ilirekebishwa. Kufikia wakati huo, watumishi wa Yehova walikuwa na maoni ya kwamba umati huo ni Wakristo waliojiweka wakfu ambao hawakuwa na bidii sana. Sasa umati huu mkubwa ulitambuliwa kuwa waabudu waaminifu ambao wana tumaini la kuishi katika dunia itakayokuwa paradiso. Baada ya rekebisho hilo, Russell Poggensee alikiri hivi baada ya kujichunguza kwa makini: “Yehova hakuwa ametumia roho yake takatifu kuweka ndani yangu tumaini la kwenda mbinguni.” Ndugu Poggensee na Wakristo wengine wengi washikamanifu kama yeye waliacha kula mkate na kunywa divai, lakini waliendelea kuhudhuria Ukumbusho.

Wakati wa ‘majira hayo muhimu sana,’ kampeni za pekee za kuhubiri ziliwapa wote fursa ya kuonyesha kwamba wanathamini fidia. Jarida Bulletin la 1932 liliwahimiza Wakristo wasiwe “watakatifu wa Ukumbusho,” yaani, watu waliokula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho lakini hawakuwa “wafanyakazi,” yaani, hawakuhubiri ujumbe wa kweli. Mnamo mwaka wa 1934, Bulletin liliwahimiza watu wawe “mapainia wasaidizi,” likiuliza hivi: “Je, 1,000 watajiandikisha kabla ya wakati wa Ukumbusho?” Jarida Informant lilisema hivi kuhusu watiwa-mafuta: “Watakuwa na shangwe kamili tu wakishiriki kutoa ushahidi kuhusu Ufalme.” Baada ya muda, wale walio na tumaini la kuishi milele duniani wangepata shangwe hiyohiyo. *

Harold King aliandika mashairi na nyimbo za Ukumbusho alipokuwa katika kifungo cha upweke

Kwa watu wote wa Yehova, usiku wa Ukumbusho ni usiku mtakatifu zaidi katika mwaka. Wanauadhimisha hata chini ya hali ngumu. Katika mwaka wa 1930, Pearl English na dada yake anayeitwa Ora, walitembea kilomita 80 hivi ili kuhudhuria Ukumbusho. Akiwa katika kifungo cha upweke gerezani nchini China, mmishonari Harold King aliandika mashairi na nyimbo kuhusu Ukumbusho na alitengeneza divai ya Ukumbusho kwa kutumia maji ya zabibu, na mkate kwa kutumia wali. Kuanzia Ulaya Mashariki, Amerika ya Kati mpaka Afrika, Wakristo wenye ujasiri wamekuwa wakiadhimisha kifo cha Yesu licha ya vita au marufuku. Haidhuru tunaishi wapi au tunakabili hali gani, tunakusanyika pamoja ili kumheshimu Yehova Mungu na Yesu Kristo wakati wa majira muhimu sana ya Ukumbusho.

^ fu. 10 Baadaye jarida Bulletin liliitwa Informant, sasa ni Huduma Yetu ya Ufalme.