Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Huongoza Kazi Yetu ya Kufundisha Ulimwenguni Pote

Yehova Huongoza Kazi Yetu ya Kufundisha Ulimwenguni Pote

“Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake.”—ISA. 48:17.

1. Leo Wakristo wamekabili matatizo gani katika kazi ya kuhubiri?

WANAFUNZI wa Biblia * walikabili matatizo mengi mwishoni mwa karne ya 19 na mwanzoni mwa karne ya 20. Sawa na Wakristo wa karne ya kwanza, walitangaza ujumbe ambao haukupendwa na wengi. Walikuwa wachache, na ulimwengu kwa ujumla uliwaona kuwa watu wasio na elimu. Isitoshe, baada ya muda wangekabili “hasira kali” ya Shetani Ibilisi. (Ufu. 12:12) Na wangefanya kazi yao ya kuhubiri katika “siku za mwisho,” ambazo zingekuwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.”—2 Tim. 3:1.

2. Yehova amekuwa akifanya nini ili kuendeleza kazi ya kuhubiri siku zetu?

2 Hata hivyo, Yehova alikusudia watu wake watangaze habari njema kwa kiwango kisicho na kifani siku zetu, na hakuna chochote kinachoweza kumzuia kutimiza kusudi hilo. Sawa na alivyolikomboa taifa la kale la Israeli kutoka Babiloni, Yehova amewakomboa watumishi wake leo kutoka katika “Babiloni Mkubwa,” ile milki ya ulimwenguni pote ya dini ya uwongo. (Ufu. 18:1-4) Ametufundisha ili tujifaidi wenyewe, ametubariki kwa kutupatia amani, na ametusaidia kuwafundisha wengine kweli zake. (Soma Isaya 48:16-18.) Hilo halimaanishi kwamba Yehova hutumia uwezo wake wa kuona matukio ya wakati ujao kujua na kuongoza kila jambo linalotukia duniani ili kuendeleza kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Hali fulani zimerahisisha kazi yetu ya kuhubiri, lakini ni kwa msaada wa Yehova tu kwamba tumeweza kuvumilia hali kama vile mateso na matatizo mengine ambayo yanafanya iwe vigumu kwetu kuhubiri katika ulimwengu huu unaokaa katika nguvu za Shetani.—Isa. 41:13; 1 Yoh. 5:19.

3. “Ujuzi wa kweli” umekuwa mwingi kwa njia gani?

3 Yehova alimwongoza nabii Danieli kutabiri kwamba “ujuzi wa kweli” ungekuwa mwingi wakati wa mwisho. (Soma Danieli 12:4.) Yehova aliwasaidia Wanafunzi wa Biblia kuelewa kweli za msingi za Kimaandiko ambazo zilikuwa zimefichwa kwa muda mrefu na mafundisho ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Sasa anawatumia watu wake kutangaza ujuzi wa kweli duniani pote. Leo, tunaona unabii wa Danieli ukitimizwa. Karibu watu 8,000,000 wamekubali kweli ya Biblia na wanaitangaza leo ulimwenguni pote. Ni baadhi ya mambo gani ambayo yametusaidia kutangaza ujumbe huo ulimwenguni pote?

JINSI AMBAVYO UTAFSIRI WA BIBLIA UMETUSAIDIA

4. Biblia ilitafsiriwa katika lugha ngapi katika karne ya 19?

4 Jambo moja ambalo limetusaidia kutangaza habari njema ni kusambazwa sana kwa Biblia. Kwa karne nyingi, viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walipinga na kuwakataza watu kusoma Biblia, hata waliwaua baadhi ya watu walioitafsiri. Hata hivyo, katika karne ya 19, mashirika yanayotafsiri Biblia yalitafsiri Biblia ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 400 hivi. Kufikia mwishoni mwa karne hiyo, watu wengi walikuwa na Biblia lakini hawakuwa na ujuzi sahihi wa mafundisho ya Maandiko.

5. Mashahidi wa Yehova wametimiza sehemu gani katika kazi ya kutafsiri Biblia?

5 Wanafunzi wa Biblia walijua kwamba walipaswa kuhubiri, na walifafanua kwa bidii mafundisho ya Biblia. Isitoshe, watu wa Yehova wametumia na kusambaza tafsiri mbalimbali za Biblia. Tangu mwaka wa 1950, wamechapisha Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko Matakatifu, ikiwa nzima au kwa sehemu, katika lugha zaidi ya 120. Itakuwa rahisi zaidi kutafsiri Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kiingereza toleo la mwaka wa 2013 katika lugha nyingine. Na kutumia Biblia inayosomeka na kueleweka kwa urahisi hutusaidia katika kazi yetu ya kuhubiri.

JINSI AMBAVYO AMANI IMETUSAIDIA

6, 7. (a) Vita vimeenea kwa kadiri gani leo? (b) Amani ya kadiri katika nchi fulani imenufaishaje kazi yetu ya kuhubiri?

6 Huenda ukauliza hivi: ‘Amani imekuwapo kwa kadiri gani ulimwenguni?’ Kwa mfano, katika karne ya 20, vita vilisababisha vifo vya mamilioni ya watu, hasa vita viwili vya ulimwengu. Hata hivyo, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokuwa vimepamba moto katika mwaka wa 1942, Nathan Knorr, aliyekuwa akiongoza kazi ya Mashahidi wa Yehova, alitoa hotuba ya kusanyiko yenye kichwa “Amani—Je, Inaweza Kudumu?” Hotuba hiyo ilitumia Ufunuo sura ya 17 kuthibitisha kwamba vita vilivyokuwa vikiendelea havingeongoza kwenye Har–Magedoni, badala yake kipindi cha amani kingeanza.—Ufu. 17:3, 11.

7 Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokwisha hakukuwa na amani kila mahali. Ripoti moja ilionyesha kwamba kulikuwa na vita 331 kati ya mwaka wa 1946 na 2013. Mamilioni ya watu walikufa. Hata hivyo, katika miaka hiyo nchi nyingi zilikuwa na amani kwa kadiri fulani, na watu wa Yehova walitumia hali hiyo kutangaza habari njema. Matokeo yamekuwa nini? Katika mwaka wa 1944, kulikuwa na wahubiri wa Ufalme wasiozidi 110,000 ulimwenguni pote. Leo, kuna wahubiri 8,000,000 hivi! (Soma Isaya 60:22.) Je, hatushukuru tunapoweza kuhubiri habari njema katika hali za amani?

JINSI AMBAVYO MFUMO MZURI WA USAFIRI UMETUSAIDIA

8, 9. Ni maendeleo gani ambayo yamefanywa katika usafiri, na yametusaidiaje katika kazi yetu?

8 Maendeleo katika usafiri yamerahisisha kazi ya kuhubiri. Katika mwaka wa 1900—miaka 21 hivi baada ya gazeti la kwanza la Mnara wa Mlinzi kuchapishwa—ni magari 8,000 tu yaliyokuwa yamesajiliwa katika nchi nzima ya Marekani, na kulikuwa na barabara chache nzuri. Leo ulimwenguni pote kuna magari zaidi ya bilioni moja na nusu yaliyosajiliwa na kuna barabara nyingi sana nzuri. Magari na barabara huwezesha wengi wetu kuwahubiria habari njema watu wanaoishi katika maeneo ya mbali. Hata hivyo, tunajitahidi kabisa kufanya wanafunzi hata tunapolazimika kutembea mbali sana kwa sababu ya tatizo la usafiri.—Mt. 28:19, 20.

9 Njia nyingine za usafiri zimetusaidia pia katika kazi yetu. Malori, meli, na treni zinatusaidia kusafirisha machapisho ya Biblia katika maeneo ya mbali kwa majuma machache tu. Ndege huwezesha waangalizi wa mzunguko, washiriki wa Halmashauri za Tawi, wamishonari, na wengine kufika haraka kwenye makusanyiko au kushughulikia haraka migawo mingine ya kitheokrasi. Isitoshe, washiriki wa Baraza Linaloongoza na ndugu wengine kutoka katika makao makuu husafiri kwa ndege kwenda nchi nyingi ili kuwatia moyo na kuwafundisha waamini wenzao. Kwa hiyo, maendeleo katika usafiri yanasaidia kudumisha umoja wa watu wa Yehova.—Zab. 133:1-3.

JINSI AMBAVYO LUGHA IMETUSAIDIA

10. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Kiingereza ndiyo lugha inayozungumzwa ulimwenguni pote?

10 Katika karne ya kwanza, Kigiriki cha kawaida, yaani, Koine, kilizungumzwa na watu wengi katika Milki ya Roma. Je, kuna lugha inayozungumzwa na watu wengi sana leo? Inasemekana kwamba Kiingereza ndiyo lugha inayozungumzwa na watu wengi leo ulimwenguni. Kitabu kimoja (English as a Global Language) kinasema hivi: “Karibu robo ya watu ulimwenguni wanaelewa au wanazungumza Kiingereza kwa ufasaha.” Kiingereza ndiyo lugha ya kigeni inayofundishwa kotekote na inatumiwa ulimwenguni pote katika biashara, siasa, sayansi, na teknolojia.

11. Lugha ya Kiingereza imesaidiaje kuendeleza ibada safi?

11 Kutumiwa sana kwa Kiingereza kumesaidia kuendeleza ibada safi. Kwa miaka mingi, Mnara wa Mlinzi na machapisho mengine yanayotegemea Biblia yalichapishwa kwanza katika Kiingereza. Ndiyo lugha rasmi inayotumiwa katika makao makuu ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova. Na kwa ujumla inatumiwa kuwafundisha wanafunzi katika Kituo cha Elimu cha Watchtower, Patterson, New York, Marekani.

12. Watumishi wa Yehova wametafsiri machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha ngapi, na teknolojia imewasaidiaje?

12 Kwa kuwa tuna pendeleo la kuwahubiria watu wa mataifa yote habari njema ya Ufalme, tumetafsiri machapisho yetu katika lugha 700 hivi. Maendeleo katika teknolojia ya kompyuta, kutia ndani kubuniwa kwa mfumo wa kompyuta wa kutayarisha maandishi kwa ajili ya uchapishaji (MEPS), kumetusaidia kufanya kazi hiyo kubwa. Maendeleo hayo yametusaidia kueneza ujumbe wa Ufalme na kuwa na umoja ulimwenguni pote. Lakini tuna umoja hasa kwa sababu tunazungumza “lugha safi” ya kweli ya Kimaandiko ambayo ni muhimu zaidi.—Soma Sefania 3:9.

JINSI AMBAVYO SHERIA ZIMETUSAIDIA

13, 14. Sheria na maamuzi ya mahakama yamewanufaishaje Wakristo leo?

13 Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, sheria ya Roma iliyofuatwa katika milki hiyo iliwanufaisha Wakristo wa mapema. Leo pia, sheria huwanufaisha Wakristo. Kwa mfano, nchini Marekani, ambako kuna makao yetu makuu ya ulimwenguni pote, Katiba inawapa watu uhuru wa kidini, wa kusema, na kukusanyika. Kwa hiyo, ndugu nchini Marekani wana uhuru wa kukusanyika na kuzungumzia Biblia hadharani na kuwaambia wengine mambo wanayojifunza. Hata hivyo, walilazimika kwenda mahakamani ili kutetea kisheria haki zao. (Flp. 1:7) Mahakama za chini zilipowanyima haki yao ya kuhubiri kuhusu Ufalme, watu wa Yehova nchini Marekani walikata rufani katika mahakama za juu na mara nyingi walishinda kesi.

14 Mahakama katika nchi nyingine zimetetea pia uhuru wetu wa ibada na haki ya kuhubiri hadharani. Katika nchi fulani, tumeshindwa kesi, lakini tumekata rufani katika mahakama za kimataifa. Kwa mfano, kufikia Juni 2014, Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu imetuunga mkono katika kesi 57 na maamuzi hayo yanapaswa kufuatwa na mataifa yote katika Baraza la Ulaya. Hata ingawa ‘tunachukiwa na mataifa yote,’ katika nchi nyingi mahakama zimeamua kwamba tuna haki ya kumwabudu Yehova.—Mt. 24:9.

JINSI AMBAVYO MAMBO MENGINE YAMETUSAIDIA KATIKA KAZI YETU YA KUFUNDISHA

Tunawasambazia watu machapisho ya Biblia duniani pote

15. Ni maendeleo gani yamefanywa katika uchapishaji, na yametusaidiaje?

15 Maendeleo katika uchapishaji yametusaidia kuhubiri habari njema ulimwenguni pote. Kwa karne nyingi, watu walitumia mashine ya kuchapisha iliyobuniwa na Johannes Gutenberg mwaka wa 1450 hivi. Hata hivyo, katika karne mbili zilizopita, mabadiliko makubwa yamefanywa katika kazi ya uchapishaji. Leo mashine za kuchapisha ni kubwa zaidi, zinafanya kazi kwa kasi zaidi, na ni bora zaidi. Gharama za kutengeneza karatasi na kujalidi vitabu zimepungua. Mashine za kisasa zimechukua mahali pa mashine za zamani, na hivyo uchapishaji unafanywa kwa kasi zaidi na picha ni bora zaidi. Mambo hayo yote yamenufaishaje kazi yetu? Fikiria hili: Toleo la kwanza la Mnara wa Mlinzi (Julai 1879), lilichapishwa katika lugha moja tu, Kiingereza. Halikuwa na picha na ni nakala 6,000 tu zilizochapishwa. Leo, miaka 136 baadaye, nakala zaidi ya 50,000,000 za kila toleo la Mnara wa Mlinzi huchapishwa na kusambazwa. Gazeti hili linachapishwa katika lugha zaidi ya 200 na lina picha maridadi za rangi.

16. Ni vifaa gani ambavyo vimetusaidia kuhubiri duniani pote? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 24.)

16 Fikiria vifaa fulani vilivyobuniwa katika muda wa miaka 200 iliyopita ambavyo watu wa Mungu wametumia kuhubiri habari njema. Tumetaja treni, magari, na ndege, lakini pia kuna baiskeli, taipureta, mashine zinazotayarisha maandishi ya vipofu, telegrafu, simu, kamera, vifaa vya kurekodi sauti na video, redio, televisheni, sinema, kompyuta, na Intaneti. Vifaa hivyo vimetusaidia kwa njia mbalimbali kutimiza kazi yetu ya kufanya wanafunzi. Tumetimiza unabii unaosema kwamba watu wa Yehova ‘watanyonya maziwa ya mataifa’ kwa kutumia kwa hekima mali za mataifa, kama vile teknolojia ya kisasa, ili kuandaa Biblia na machapisho ya Biblia katika lugha nyingi.—Soma Isaya 60:16.

17. (a) Uthibitisho unaonyesha nini? (b) Kwa nini Yehova anaturuhusu kuwa “wafanyakazi wenzi”?

17 Ni wazi kwamba tuna uthibitisho ulio wazi unaoonyesha kwamba Mungu anabariki kazi ya kuhubiri. Bila shaka Yehova hategemei msaada wetu ili atimize makusudi yake. Hata hivyo, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anaturuhusu kuwa “wafanyakazi wenzi,” na hivyo kutupatia fursa ya kuonyesha kwamba tunampenda na tunapenda jirani yetu. (1 Kor. 3:9; Marko 12:28-31) Acheni tutumie vizuri fursa tunazopata za kutangaza ujumbe wa Ufalme, kwa kuwa hiyo ndiyo kazi muhimu zaidi duniani. Na tufanye yote tuwezayo kumshukuru Yehova kwa sababu ameongoza na kubariki kazi yetu ya kufundisha ulimwenguni pote.

^ fu. 1 Wanafunzi wa Biblia walianza kutumia jina Mashahidi wa Yehova katika mwaka wa 1931.—Isa. 43:10.