Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wajapani Wapokea Zawadi Ambayo Hawakutarajia

Wajapani Wapokea Zawadi Ambayo Hawakutarajia

KATIKA mkutano wa pekee uliofanywa Nagoya, Japani, Aprili 28, 2013, Anthony Morris wa Baraza Linaloongoza aliushangaza umati alipotoa tangazo lenye kusisimua kuhusu chapisho jipya la Kijapani lenye kichwa Biblia—Injili ya Mathayo. Watu zaidi ya 210,000 waliohudhuria au kusikiliza tangazo hilo kupitia Intaneti walipiga makofi kwa muda mrefu sana.

Kitabu hicho cha Injili ya Mathayo chenye kurasa 128 kilichochapishwa upya kutoka katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Kijapani ni cha pekee. Ndugu Morris alieleza kwamba kimetayarishwa “hasa kwa ajili ya Wajapani.” Kitabu hicho cha Biblia kina mambo gani? Kwa nini kilitayarishwa? Na watu wameitikiaje?

KINA MAMBO GANI?

Mpangilio wa kitabu hicho cha Mathayo uliwashangaza wasikilizaji. Herufi za Kijapani zinaweza kuandikwa kutoka juu hadi chini au kushoto kwenda kulia, na machapisho mengi, kutia ndani machapisho yetu ya karibuni, yameandikwa kutoka kushoto kwenda kulia. Hata hivyo, maandishi ya kitabu hiki kipya yameandikwa kutoka juu hadi chini, yakifuata mpangilio ambao hutumiwa katika magazeti na vitabu vingi vya Kijapani. Wasomaji wengi Wajapani hupendelea mpangilio huo kwa sababu maandishi yanasomeka kwa urahisi. Pia, vichwa vilivyo juu ya kurasa vimehamishwa na kuwa vichwa vidogo katika maandishi ili iwe rahisi kwa wasomaji kuona mambo makuu.

Ndugu na dada nchini Japani walianza mara moja kutumia mambo mbalimbali yaliyo katika kitabu hicho cha Mathayo. Dada mmoja mwenye umri wa miaka 80 na kitu alisema: “Nilikuwa nimesoma kitabu cha Mathayo mara nyingi, lakini mpangilio wa kutoka juu hadi chini na vichwa vidogo vya kitabu hiki kipya vimenisaidia kuelewa vizuri zaidi yale Mahubiri ya Mlimani.” Dada mmoja kijana aliandika hivi: “Nilisoma kitabu chote cha Mathayo mara tu nilipokipokea. Nimezoea mpangilio wa kutoka kushoto kwenda kulia, lakini Wajapani wengi hupendelea mpangilio wa kutoka juu hadi chini.”

KIMETAYARISHWA HASA KWA AJILI YA WAJAPANI

Kwa nini kitabu hicho cha Biblia kinawafaa hasa Wajapani? Ingawa Wajapani wengi hawaifahamu Biblia, wako tayari kuisoma. Kitabu hiki cha Injili ya Mathayo kitawapa watu ambao hawajawahi kamwe kuiona Biblia fursa ya kupata na kusoma sehemu hiyo ya Biblia Takatifu.

Kwa nini kitabu cha Mathayo kilichaguliwa? Wajapani wengi huhusianisha neno “Biblia” na Yesu Kristo. Kwa hiyo, kitabu cha Mathayo kilichaguliwa kwa sababu kina masimulizi kuhusu ukoo na kuzaliwa kwa Yesu, Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, na unabii wa pekee aliotoa kuhusu siku za mwisho—habari ambazo zitawavutia Wajapani wengi.

Wahubiri wa Ufalme nchini Japani walianza kusambaza kwa bidii kitabu hicho kipya nyumba kwa nyumba na katika ziara za kurudia. Dada mmoja aliandika hivi: “Sasa nina fursa zaidi za kuwaachia watu Neno la Mungu katika eneo letu. Nilifanikiwa kumwachia mtu nakala ya kitabu cha Mathayo alasiri ileile baada tu ya mkutano wa pekee!”

WATU WAMEITIKIAJE?

Wahubiri hutumia njia gani kutoa kitabu cha Mathayo? Wenye nyumba wengi Wajapani wanafahamu misemo kama vile “lango jembamba,” ‘lulu mbele ya nguruwe,’ na “msihangaike kamwe juu ya kesho.” (Mt. 6:34; 7:6, 13) Wanashangaa wanapojifunza kwamba maneno hayo yalisemwa na Yesu Kristo. Wanapoona maneno hayo katika Injili ya Mathayo, wengi husema hivi: “Sikuzote nimetamani kupata fursa ya kusoma Biblia angalau mara moja.”

Wahubiri wanapowarudia wale waliokubali kitabu cha Mathayo, mara nyingi wenye nyumba husema kwamba walikisoma chote au sehemu fulani bila kukawia. Mwanamume mwenye umri wa miaka 60 na kitu alimwambia mhubiri mmoja hivi: “Nilikisoma mara nyingi sana na kilinifariji. Tafadhali nifundishe mengi zaidi kuhusu Biblia.”

Kitabu cha Mathayo kinatolewa pia katika mahubiri ya hadharani. Shahidi mmoja aliyekuwa akishiriki katika mahubiri hayo, alimpa msichana mmoja aliyekubali kitabu cha Mathayo anwani yake ya barua-pepe. Baada ya saa moja, msichana huyo alimwandikia dada huyo barua-pepe akisema kwamba alikuwa amesoma sehemu ya kitabu hicho cha Biblia na alitaka kujua mengi zaidi. Baada ya juma moja, alianza kujifunza Biblia, na baada ya muda mfupi akaanza kuhudhuria mikutano.

Nakala zaidi ya 1,600,000 za Biblia—Injili ya Mathayo zimepelekwa katika makutaniko nchini Japani, na kila mwezi, Mashahidi wanawaachia watu maelfu ya vitabu hivyo. Dibaji ya kitabu hicho inaonyesha hisia za wachapishaji wa kitabu hicho kwa kusema hivi: “Tunatumaini kwa dhati kwamba kusoma kitabu hiki kutakuchochea upendezwe zaidi na Biblia.”