Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Tulipata Kazi Yenye Kuridhisha Zaidi

Tulipata Kazi Yenye Kuridhisha Zaidi

TULIPOKUWA na umri wa miaka mitano, mimi na Gwen tulianza kujifunza kucheza dansi. Hatukuwa tunafahamiana wakati huo. Lakini tulipokuwa watu wazima, tuliamua kuwa wachezaji wa dansi inayoitwa bale. Tulipokuwa tukikaribia kuwa maarufu, tuliacha kucheza dansi. Kwa nini tulifanya uamuzi huo?

David: Nilizaliwa mwaka wa 1945 katika mkoa wa Shropshire, Uingereza. Baba yangu alikuwa na shamba katika eneo tulivu la vijijini. Baada ya shule, nilifurahia kuwapa kuku chakula na kuchukua mayai waliyotaga na pia kuwatunza ng’ombe na kondoo. Wakati wa likizo, nilisaidia kuvuna, na nyakati nyingine niliendesha matrekta yetu.

Hata hivyo, nilianza kupendezwa na jambo lingine. Baba yangu aligundua kwamba tangu nikiwa mtoto, nilitaka kucheza dansi kila mara niliposikia muziki. Kwa hiyo, nilipokuwa na umri wa miaka mitano, alimwomba mama anipeleke kwenye shule ya kucheza dansi ya kugongagonga viatu chini (tap dancing). Mwalimu wangu aliona kwamba ninaweza kucheza dansi ya bale, hivyo akanifundisha dansi hiyo pia. Nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilipata fursa ya kulipiwa masomo katika shule maarufu ya dansi ya bale jijini London (Royal Ballet School). Nikiwa huko, nilikutana na Gwen, akawa mwenzi wangu wa kucheza dansi.

Gwen: Nilizaliwa mwaka wa 1944 katika jiji la London lenye shughuli nyingi. Nikiwa msichana mdogo, nilikuwa na imani yenye nguvu katika Mungu. Nilijaribu kusoma Biblia yangu lakini nilishindwa kuielewa. Nikiwa na umri wa miaka mitano, nilienda shule ya kujifunza kucheza dansi. Miaka sita baadaye nilishinda shindano la wachezaji wote wa dansi nchini Uingereza, nikapewa fursa ya kujiunga na shule ya Royal Ballet iliyofundisha dansi ya bale. Shule hiyo ilikuwa katika nyumba maridadi iliyojengwa miaka ya 1720 iliyoitwa White Lodge, iliyo katika Mbuga ya Richmond, nje ya jiji la London. Nikiwa huko nilipata elimu na pia kufundishwa dansi ya bale na walimu walioheshimiwa sana. Nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilihudhuria shule ya sekondari ya Royal Ballet iliyo katikati ya jiji la London, na nikakutana na David huko. Baada ya miezi michache, tulikuwa tukicheza pamoja dansi ya bale kwenye michezo mbalimbali ya kuigiza katika Jumba la Royal Opera lililoko Covent Garden, London.

Tulisafiri sehemu mbalimbali ulimwenguni ili kucheza dansi ya bale

David: Kama Gwen alivyotaja, tuliweza kucheza bale katika jumba maarufu la Royal Opera na tulijiunga na kikundi cha London Festival Ballet (sasa kinaitwa English National Ballet). Mmoja wa walimu katika shule ya Royal Ballet alianzisha kikundi chake cha kimataifa huko Wuppertal, Ujerumani, na akatuchagua kuwa wachezaji dansi katika kikundi chake. Tulicheza bale katika majumba ya maonyesho ulimwenguni pote, tukiwa pamoja na wachezaji bale maarufu kama vile Dame Margot Fonteyn na Rudolf Nureyev. Maisha hayo ya mashindano humfanya mtu awe na kiburi, na tulijitoa kabisa katika kazi yetu ya kucheza bale.

Gwen: Nilitumia mwili na akili yangu yote kucheza dansi. Mimi na David tulitaka sana kuwa wachezaji dansi maarufu. Nilifurahia kutia sahihi vitabu vya mashabiki, kupewa maua, na kuwasikia mashabiki wakishangilia. Wasanii wenzangu walikuwa na maadili mapotovu, walivuta sigara, na kulewa; kama wasanii wengine, nilitegemea hirizi zangu za bahati njema.

MAISHA YETU YABADILIKA KABISA

Siku yetu ya harusi

David: Baada ya kucheza dansi kwa miaka mingi, nilichoka kusafiri-safiri. Kwa kuwa nililelewa vijijini, nilianza kutamani maisha rahisi ya vijijini. Kwa hiyo, mwaka wa 1967, niliacha kazi ya kucheza dansi na kuanza kufanya kazi kwenye shamba kubwa lililokuwa karibu na wazazi wangu. Mwenye shamba alikubali nikodi nyumba yake ndogo. Nilimpigia simu Gwen kwenye jumba la maonyesho na kumwomba tufunge ndoa. Alikuwa akicheza bale akiwa peke yake, na alianza kuwa maarufu. Basi haikuwa rahisi kwake kufanya uamuzi huo. Hata hivyo, alikubali tufunge ndoa na akajiunga nami ingawa hakuwa amezoea maisha ya vijijini.

Gwen: Kwa kweli ilikuwa vigumu kuzoea maisha ya vijijini. Maisha yalikuwa tofauti kwa sababu nilikamua maziwa ya ng’ombe, nililisha nguruwe na kuku licha ya mabadiliko mbalimbali ya hali ya hewa. David alienda kwenye chuo cha kilimo kwa miezi tisa ili kujifunza mbinu mpya za ufugaji, hivyo nilihisi upweke hadi aliporudi nyumbani usiku. Wakati huo binti yetu wa kwanza, Gilly, alikuwa amezaliwa. David alipendekeza nijifunze udereva, nami nikakubali, na siku moja nilipokuwa katika mji uliokuwa karibu, nilimwona Gael, ambaye nilikutana naye alipokuwa akifanya kazi katika duka moja.

Miaka ya kwanza ya ndoa tukiwa katika shamba letu

Gael alinialika nyumbani kwake tukanywe chai. Alinionyesha picha zake za harusi na picha moja ilionyesha watu wakiwa wamesimama mahali palipoitwa Jumba la Ufalme. Nilimuuliza kuhusu kanisa hilo. Aliponiambia kwamba yeye na mume wake ni Mashahidi wa Yehova, nilifurahi sana. Nilikumbuka kwamba shangazi yangu alikuwa Shahidi. Hata hivyo, nilikumbuka jinsi baba yangu alivyochukizwa na kukasirishwa na jambo hilo, na hata alitupa machapisho yake ndani ya pipa la takataka. Nilijiuliza kwa nini baba ambaye kwa kawaida ni mtu mwenye urafiki alikasirishwa sana na shangazi yangu.

Hatimaye nilipata nafasi ya kujua tofauti kati ya mambo ambayo shangazi yangu aliamini na mafundisho ya dini nyingine. Gael alinionyesha yale ambayo Biblia inafundisha. Nilishangaa kugundua kwamba mafundisho mengi kama vile Utatu na kutokufa kwa nafsi, hayapatani na Maandiko. (Mhu. 9:5, 10; Yoh. 14:28; 17:3) Pia, kwa mara ya kwanza niliona jina la Mungu, Yehova, katika Biblia.—Kut. 6:3.

David: Gwen alinieleza yale aliyokuwa akijifunza. Nilikumbuka kwamba nilipokuwa mdogo, baba yangu aliniambia nisome kile Kitabu Kizuri, yaani, Biblia. Kwa hiyo, mimi na Gwen tulikubali Gael na mume wake, Derrick, watufundishe Biblia. Baada ya miezi sita tulihamia mji wa Oswestry, katika mkoa uleule wa Shropshire, kwa sababu tulipata shamba dogo la kukodi. Tukiwa huko, Shahidi aliyeitwa Deirdre aliendelea kutufundisha Biblia kwa subira. Mwanzoni tulifanya maendeleo polepole kwa kuwa tulijishughulisha sana na kazi ya kutunza mifugo. Hata hivyo, pole kwa pole kweli ilitia mizizi mioyoni mwetu.

Gwen: Kizuizi kikubwa ambacho nilihitaji kushinda ni ushirikina. Andiko la Isaya 65:11 lilinisaidia kuelewa maoni ya Yehova kuhusu “wale wanaoandaa meza kwa ajili ya mungu wa Bahati Njema.” Ilinichukua muda mrefu na nilihitaji kusali sana ili kutupa hirizi zangu za bahati njema. Baada ya kujifunza kwamba “yeyote yule anayejiinua atanyenyekezwa, na yeyote yule anayejinyenyekeza atainuliwa,” nilitambua watu ambao Yehova anatafuta. (Mt. 23:12) Nilitaka kumtumikia Mungu ambaye anatujali sana hivi kwamba alimtoa Mwana wake mpendwa ili awe fidia. Kufikia wakati huo tulikuwa tumepata binti mwingine, na tulisisimka tulipojifunza kwamba familia yetu inaweza kuishi milele katika dunia paradiso.

David: Nilisadiki kwamba nimepata kweli nilipoelewa jinsi ambavyo unabii kama ule ulio kwenye Mathayo sura ya 24, na katika kitabu cha Danieli umetimizwa kwa njia ya ajabu. Nilitambua kwamba hakuna kitu chochote katika mfumo huu wa mambo kilicho na thamani kuliko kuwa na uhusiano mzuri na Yehova. Hivyo, niliacha kujitafutia makuu kadiri miaka ilivyosonga. Nilielewa kwamba mke na binti zangu walikuwa muhimu sana. Andiko la Wafilipi 2:4 lilinisadikishia kwamba sipaswi kujifikiria tu na kukazia fikira tamaa yangu ya kuwa na shamba kubwa zaidi. Badala yake, ninapaswa kutanguliza utumishi wa Yehova maishani. Niliacha kuvuta sigara. Lakini haikuwa rahisi kuhudhuria mkutano uliofanywa Jumamosi jioni katika eneo lililokuwa umbali wa kilomita 10, kwa sababu tulihitaji kukamua maziwa ya ng’ombe saa hizo. Hata hivyo, Gwen alinisaidia sana na hatukukosa mkutano hata mmoja; wala hatukukosa kuandamana na binti zetu katika utumishi kila Jumapili asubuhi, baada ya kukamua maziwa.

Watu wetu wa ukoo hawakufurahia mabadiliko tuliyofanya. Baba ya Gwen hakuzungumza naye kwa miaka sita. Pia, wazazi wangu walijaribu kutuzuia tusishirikiane na Mashahidi.

Gwen: Yehova alitusaidia kuvumilia matatizo hayo. Baada ya muda, ndugu na dada wa Kutaniko la Oswestry wakawa familia yetu mpya, na walitutegemeza kwa upendo wakati wa majaribu. (Luka 18:29, 30) Tulijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa mwaka wa 1972. Nilitaka sana kuwasaidia watu wengi iwezekanavyo kujua kweli, kwa hiyo nilianza kufanya upainia.

KAZI MPYA YENYE KURIDHISHA

David: Kwa miaka mingi tulifanya kazi yenye kuchosha katika shamba letu; hata hivyo tulijitahidi kuwawekea binti zetu mfano mzuri katika mambo ya kiroho. Baada ya muda, serikali ilipunguza msaada wa kifedha kwa wakulima, kwa hiyo ilibidi tuache shamba hilo. Tulisali ili Yehova atusaidie na kutuongoza kwa sababu hatukuwa na makao wala ajira, na binti yetu wa tatu alikuwa na umri wa mwaka mmoja tu. Ili kuiruzuku familia yetu, tuliamua kutumia kipaji chetu cha kucheza dansi na hivyo tukafungua shule ya kufundisha kucheza dansi. Tulipata matokeo mazuri kwa sababu ya kuazimia kutanguliza mambo ya kiroho. Tulifurahi sana binti zetu watatu walipoanza kufanya upainia baada ya kumaliza shule. Gwen pia alikuwa painia na hivyo aliweza kuandamana na binti zetu kila siku.

Baada ya binti zetu wawili wa kwanza, Gilly na Denise, kuolewa, tulifunga shule ya dansi. Tuliandikia ofisi ya tawi ili kujua eneo lenye uhitaji ambako tungeweza kusaidia. Ofisi ilitutuma kwenye miji iliyo kusini-mashariki mwa Uingereza. Kwa kuwa sasa binti yetu Debbie ndiye aliyebaki nyumbani, nilianza kufanya upainia pia. Baada ya miaka mitano, tuliombwa tukasaidie makutaniko mengine upande wa kaskazini. Baada ya Debbie kuolewa, tulipata pendeleo la kushiriki katika miradi ya ujenzi kwa miaka kumi nchini Zimbabwe, Moldova, Hungaria, na Côte d’Ivoire. Kisha tulirudi Uingereza ili kusaidia katika ujenzi wa Betheli ya London. Kwa sababu nilikuwa na ujuzi wa kilimo, niliombwa nisaidie katika shamba la Betheli wakati huo. Kwa sasa tunafanya upainia kaskazini-magharibi mwa Uingereza.

Tulipata shangwe kubwa tulipotumikia kwenye miradi ya ujenzi katika nchi mbalimbali

Gwen: Mwanzoni tulijitoa kabisa kucheza dansi ya bale ambayo ilitupatia furaha ya muda mfupi. Sasa tumejitoa kabisa katika kazi muhimu zaidi, yaani, kufanya mapenzi ya Yehova. Kazi hiyo ni ya kudumu, nayo imetuletea shangwe kubwa. Leo, badala ya kutumia miguu yetu kucheza dansi pamoja, tunatumia miguu yetu kuhubiri pamoja. Tumepata furaha isiyo na kifani kwa kuwasaidia watu wengi kujifunza kweli zenye thamani zinazookoa uhai. ‘Barua hizo za pendekezo’ ni bora kuliko umashuhuri wowote katika ulimwengu. (2 Kor. 3:1, 2) Ikiwa hatungepata kweli, tungebaki tu na kumbukumbu, picha za zamani, na programu za maonyesho tuliyokuwa tukifanya.

David: Kumtumikia Yehova kumeboresha sana maisha yetu. Najua kazi hiyo imenisaidia kuwa mume na baba mzuri. Biblia inatuambia kwamba Miriamu, Mfalme Daudi, na wengine walifurahi na kucheza dansi. Sisi na wengine wengi, tunatazamia kwa hamu kucheza dansi kwa shangwe katika ulimwengu mpya wa Yehova.—Kut. 15:20; 2 Sam. 6:14.