Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Zamani, mara nyingi machapisho yetu yalieleza kwamba baadhi ya masimulizi ya Biblia yalikuwa ufananisho au kivuli cha jambo lingine, lakini katika miaka ya karibuni ni mara chache sana kuona ufafanuzi huo. Kwa nini?

Gazeti Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 1950, lilieleza kwamba nyakati nyingine mtu, tukio, au kitu fulani kinachotajwa katika Biblia kilikuwa ufananisho au kivuli cha jambo ambalo lingetimia wakati ujao.

Zamani, machapisho yetu yalisema kwamba wanaume na wanawake waaminifu kama vile Ayubu, Debora, Elihu, Rahabu, Rebeka, Yeftha, na wengine wengi walikuwa kivuli au walifananisha watiwa-mafuta au “umati mkubwa.” (Ufu. 7:9) Kwa mfano, ilidhaniwa kwamba Ayubu, Rebeka, na Yeftha walifananisha watiwa-mafuta, ilhali Debora na Rahabu walifananisha umati mkubwa. Hata hivyo, katika miaka ya karibuni hatujazungumzia ulinganifu kama huo. Kwa nini?

KIVULI

Mwana-kondoo aliyetolewa dhabihu katika Israeli la kale alikuwa kivuli.—Hes. 9:2

UFANANISHO

Paulo alimtambulisha Kristo kuwa “pasaka yetu.”—1 Kor. 5:7

Maandiko yanaonyesha kwamba baadhi ya watu wanaotajwa katika Biblia walifananisha jambo fulani kubwa. Kwenye Wagalatia 4:21-31, mtume Paulo anataja “tukio la mfano” kuhusu wanawake wawili. Hagari ambaye alikuwa kijakazi wa Abrahamu, alifananisha taifa la Israeli ambalo liliunganishwa na Yehova kupitia Sheria ya Musa. Lakini Sara, “yule mwanamke huru,” alifananisha mke wa Mungu, yaani, sehemu ya kimbingu ya tengenezo lake. Katika barua yake kwa Waebrania, Paulo anamfananisha Yesu na Melkizedeki ambaye alikuwa mfalme na kuhani, akikazia mambo hususa yanayowafananisha. (Ebr. 6:20; 7:1-3) Isitoshe, Paulo anamlinganisha Isaya na watoto wake na Yesu na wafuasi wake watiwa-mafuta. (Ebr. 2:13, 14) Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika mambo hayo; hivyo, tunakubali mambo aliyosema kuhusu ufananisho huo.

Hata hivyo, Biblia inapoonyesha kwamba mtu fulani anamfananisha mtu mwingine, hatupaswi kukata shauri kwamba kila jambo au tukio katika maisha ya mtu huyo ni ufananisho wa jambo lingine kubwa. Kwa mfano, ingawa Paulo anamfananisha Melkizedeki na Yesu, hataji chochote kuhusu wakati ambapo Melkizedeki alimpa Abrahamu mkate na divai baada ya Abrahamu kuwashinda wafalme wanne. Kwa hiyo, hakuna msingi wowote wa Kimaandiko wa kutafuta maana zaidi katika tukio hilo.—Mwa. 14:1, 18.

Waandishi fulani walioishi karne nyingi baada ya Kristo kufa walinaswa na mtego wa kutafuta ufananisho wa kila kitu. Kitabu kimoja (The International Standard Bible Encyclopaedia) kinasema hivi kuhusu mafundisho ya Origen, Ambrose, na Jerome: “Walitafuta ufananisho wa kila kisa na tukio, hata jambo dogo sana ambalo limeandikwa katika Maandiko, na bila shaka waliupata. Hata mambo ya kawaida yalidhaniwa kuwa yanaficha ukweli fulani . . . , hivi kwamba wengine walijaribu kutafuta maana ya idadi ya [wale] samaki 153, waliovuliwa na wanafunzi katika usiku ambao Mwokozi aliyefufuliwa aliwatokea—ilifananisha nini!”

Augustine wa Hippo alieleza kwa kina simulizi linalotaja kwamba Yesu aliwalisha wanaume 5,000 hivi, kwa mikate mitano ya shayiri na samaki wawili. Kwa kuwa shayiri ilionwa kuwa duni kuliko ngano, Augustine alikata shauri kwamba ile mikate mitano ilifananisha vile vitabu vitano vya Musa (“shayiri” ilifananisha “Agano la Kale” ambalo lilionwa kuwa duni likilinganishwa na “Agano Jipya”). Namna gani wale samaki wawili? Kwa sababu fulani aliwafananisha na mfalme na kuhani. Msomi mwingine alisema kwamba Yakobo aliponunua haki ya kuwa mzaliwa wa kwanza kwa bakuli la mchuzi mwekundu, hilo lilifananisha tendo la Yesu la kununua urithi wa mbinguni kwa ajili ya wanadamu kwa damu yake nyekundu!

Ikiwa unaona vigumu kuamini ufafanuzi huo, basi tatizo linaeleweka. Wanadamu hawawezi kujua ikiwa simulizi fulani la Biblia ni kivuli au si kivuli cha mambo yatakayokuja. Kwa hiyo jambo la hekima ni hili: Maandiko yanapofundisha kwamba mtu, tukio, au kitu fulani kinafananisha kitu kingine, sisi hukubali. Hata hivyo, hatupaswi kusema kwamba simulizi la Biblia lina maana ya mfano ikiwa hakuna msingi wowote wa Kimaandiko wa kusema hivyo.

Basi matukio na mifano iliyo katika Maandiko inaweza kutunufaishaje? Mtume Paulo alisema hivi kwenye Waroma 15:4: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” Paulo alimaanisha kwamba ndugu zake watiwa-mafuta katika karne ya kwanza wangejifunza mambo muhimu kutokana na matukio yaliyorekodiwa kwenye Maandiko. Hata hivyo, watu wa Mungu katika kila kizazi, iwe ni watiwa-mafuta au “kondoo wengine,” iwe wanaishi katika “siku za mwisho” au la, kwa kweli wamenufaika kutokana na “mambo yote yaliyoandikwa zamani.”—Yoh. 10:16; 2 Tim. 3:1.

Badala ya kuona kwamba masimulizi mengi ya Biblia yanawahusu tu watiwa-mafuta, umati mkubwa, au Wakristo wanaoishi wakati fulani hususa, watu wote wa Mungu ambao waliishi wakati uliopita na sasa wanaweza kujifunza mambo mengi kutokana na masimulizi hayo. Kwa mfano, hatupaswi kuona kwamba mambo yanayotajwa katika kitabu cha Ayubu yanawahusu tu watiwa-mafuta waliovumilia majaribu wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Watumishi wengi wa Mungu, wanaume kwa wanawake, watiwa-mafuta na wale wa umati mkubwa, wamepitia majaribu kama ya Ayubu, na ‘wamejionea matokeo ambayo Yehova huleta, kwamba Yehova ni mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema.’—Yak. 5:11.

Fikiria hili: Katika makutaniko yetu leo, je, hatuna wanawake wenye umri mkubwa ambao ni waaminifu kama Debora, wazee wa kutaniko vijana wenye hekima kama Elihu, mapainia wenye ujasiri na bidii kama ya Yeftha, na wanaume na wanawake waaminifu wenye subira kama Ayubu? Tunamshukuru sana Yehova kwa kuhifadhi “mambo yote yaliyoandikwa zamani,” ili “kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini”!

Kwa sababu hizo, katika miaka ya hivi karibuni machapisho yetu yamekazia mambo tunayojifunza kutokana na masimulizi ya Biblia badala ya kujaribu kutafuta ufananisho na utimizo wake.