Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, ‘Utaendelea Kukesha’?

Je, ‘Utaendelea Kukesha’?

“Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamwijui ile siku wala saa.”—MT. 25:13.

1, 2. (a) Yesu alifunua nini kuhusu siku za mwisho? (b) Tutazungumzia maswali gani?

BILA shaka, ilisisimua sana kuketi kwenye Mlima wa Mizeituni ulio ng’ambo ya hekalu la Yerusalemu na kumsikia Yesu akitoa unabii wake wenye kuvutia sana. Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana walimsikiliza Yesu kwa makini sana alipotabiri mambo ambayo yangetukia wakati ujao. Aliwaambia mambo mengi kuhusu siku za mwisho za mfumo mwovu wa ulimwengu huu, wakati ambapo angekuwa Mtawala wa Ufalme wa Mungu. Aliwaambia kwamba katika kipindi hicho cha mwisho, ‘mtumwa wake mwaminifu na mwenye busara’ angemwakilisha duniani, akiwapa watumishi wake chakula cha kiroho wanachohitaji kwa wakati unaofaa.—Mt. 24:45-47.

2 Kisha, katika unabii huohuo, Yesu alisimulia mfano wa mabikira kumi. (Soma Mathayo 25:1-13.) Acheni tukazie fikira maswali haya: (1) Mfano huo una ujumbe gani muhimu? (2) Watiwa-mafuta waaminifu wametumiaje shauri la mfano huo, na matokeo ni nini? (3) Kila mmoja wetu anawezaje kunufaika na mfano huo wa Yesu?

MFANO HUO UNA UJUMBE GANI?

3. Zamani machapisho yetu yalifafanuaje mfano wa mabikira kumi, na huenda matokeo yalikuwa nini?

3 Katika makala iliyotangulia tuliona kwamba katika miaka ya karibuni, mtumwa mwaminifu amekuwa akifafanua Maandiko hatua kwa hatua, akikazia zaidi mambo tunayojifunza badala ya maana ya kinabii ya masimulizi ya Biblia. Zamani, machapisho yetu yalisema kwamba hata mambo madogo yanayotajwa katika mfano wa Yesu wa mabikira kumi kama vile taa, mafuta, vyombo vya mafuta, na kadhalika, yalifananisha mambo fulani. Hata hivyo, je, inawezekana kwamba tulikazia fikira mambo madogo-madogo badala ya kukazia fikira ujumbe rahisi na muhimu wa mfano huo? Kama tutakavyoona, jibu la swali hilo ni muhimu sana.

4. Katika mfano wa Yesu, ni nani anayefananishwa na (a) bwana-arusi? (b) mabikira?

4 Acheni tuchunguze ujumbe muhimu wa Yesu katika mfano huo. Kwanza, fikiria wahusika wakuu. Bwana-arusi katika mfano huo ni nani? Ni wazi kwamba Yesu ndiye bwana-arusi. Tunajua hivyo kwa sababu alijiita bwana-arusi katika pindi nyingine. (Luka 5:34, 35) Namna gani mabikira? Katika mfano huo, Yesu anasema kwamba mabikira wanapaswa kuwa tayari na taa zilizowashwa wakati bwana-arusi anapowasili. Fikiria maneno haya ambayo Yesu aliliambia “kundi dogo” la wafuasi wake watiwa-mafuta: “Viuno vyenu na vifungwe mishipi na taa zenu ziwe zikiwaka, nanyi mtakuwa kama watu wanaomngoja bwana wao wakati anaporudi kutoka kwenye karamu ya ndoa.” (Luka 12:32, 35, 36) Isitoshe, kwa mwongozo wa roho takatifu, mtume Paulo na mtume Yohana waliwafananisha wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo na mabikira safi kiadili. (2 Kor. 11:2; Ufu. 14:4) Ni wazi kwamba Yesu alitoa mfano ulio kwenye Mathayo 25:1-13 ili kuwashauri na kuwaonya wafuasi wake watiwa-mafuta.

5. Yesu alionyesha mfano huo unatimia katika kipindi gani?

5 Sasa, fikiria wakati unaohusika. Shauri la Yesu linahusu kipindi gani cha wakati? Yesu alionyesha wazi kipindi kinachohusika aliposema hivi mwishoni mwa mfano huo: “Bwana-arusi akafika.” (Mt. 25:10) Kama ilivyozungumziwa katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2013, unabii wa Yesu katika Mathayo sura ya 24 na 25 unataja mara nane kuhusu “kuja” kwake; na katika kila kisa, neno lilelile la Kigiriki linatumika. Katika visa vyote, Yesu alikuwa akirejelea wakati wa dhiki kuu atakapokuja kutekeleza hukumu na kisha kuharibu mfumo wa mambo wa ulimwengu huu. Basi ni wazi kwamba mfano huo unatimia katika siku za mwisho, lakini Yesu atakuja wakati wa dhiki kuu.

6. Kama muktadha unavyoonyesha, mfano huo una ujumbe gani muhimu?

6 Ujumbe muhimu wa mfano huo ni nini? Fikiria muktadha. Yesu alitoa mfano huo baada tu ya kuzungumza kuhusu “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Mtumwa huyo angekuwa kikundi kidogo cha wanaume watiwa-mafuta ambao wangewaongoza wafuasi wa Kristo katika siku za mwisho. Yesu aliwaonya wanaume hao kwamba ni lazima wawe waaminifu. Kisha, akatumia mfano huo kuwahimiza wafuasi wake wote watiwa-mafuta katika siku za mwisho ‘waendelee kukesha’ ili wasipoteze thawabu yao. (Mt. 25:13) Acheni sasa tuchunguze mfano huo na kuona jinsi ambavyo watiwa-mafuta wametumia shauri la Yesu.

WATIWA-MAFUTA WAMETUMIAJE SHAURI LA MFANO HUO?

7, 8. (a) Ni sababu gani mbili zilizofanya mabikira wenye busara wawe tayari? (b) Watiwa-mafuta wameonyeshaje kwamba wako tayari?

7 Mfano wa Yesu unakazia kwamba tofauti na mabikira wapumbavu, mabikira wenye busara walikuwa tayari bwana-arusi alipokuja. Kwa nini? Kwa sababu mbili: walikuwa wamejitayarisha na walikuwa macho. Mabikira hao waliokuwa wakimsubiri bwana-arusi awasili, walipaswa kuhakikisha kwamba taa zao zinaendelea kuwaka, na kuendelea kukaa macho kwa saa nyingi mpaka wakati huo wenye kusisimua. Hata hivyo, tofauti na mabikira wapumbavu, mabikira watano walijitayarisha vya kutosha na kubeba taa zao pamoja na mafuta ya ziada katika vyombo vyao. Je, watiwa-mafuta wamejitayarisha vivyo hivyo?

8 Kwa hakika wamejitayarisha! Katika siku za mwisho, watiwa-mafuta wametenda kama wale mabikira wenye busara, wakiwa tayari kutimiza mgawo wao kwa uaminifu mpaka mwisho. Wanahesabu gharama ya kumtumikia Mungu kwa uaminifu, wakitambua tangu mwanzoni kwamba ili kutimiza mgawo wao wanahitaji kuacha kufuatilia vitu vingi vya kimwili vya ulimwengu huu wa Shetani. Wanajitoa kikamili kwa Yehova na kumtumikia, si kwa sababu mwisho uko karibu, bali kwa sababu ya upendo na ushikamanifu wao kwake na kwa Mwana wake. Wanadumisha utimilifu wao, wakiipinga roho ya ulimwengu huu mwovu na mtazamo wake wa kufuatilia vitu vya kimwili, maadili mapotovu, na ubinafsi. Hivyo wanaendelea kuwa tayari, wakiangaza daima kama mianga, bila hofu yoyote kwamba huenda Bwana-arusi anakawia.—Flp. 2:15.

9. (a) Yesu alitoa onyo gani kuhusu mwelekeo wa kulala usingizi? (b) Watiwa-mafuta wameitikiaje ule mwito: “Huyu hapa bwana-arusi!”? (Ona pia maelezo ya chini.)

9 Sababu nyingine iliyowasaidia wale mabikira kuwa tayari ni kuwa macho. Je, Mkristo mtiwa-mafuta anaweza kusinzia anaposubiri kuja kwa Kristo? Bila shaka. Ona kwamba Yesu anasema hivi kuhusu wale mabikira kumi, “wote walisinzia na kuanza kulala” ilipoonekana kuwa bwana-arusi anachelewa. Yesu alijua kwamba hata mtu mwenye mtazamo wa kuendelea kukesha anaweza kudhoofishwa au kukengeushwa. Watiwa-mafuta waaminifu wametii onyo hilo na wamejitahidi hata zaidi kubaki macho na kukesha. Katika mfano huo, mabikira wote waliitikia mwito uliotolewa usiku: “Huyu hapa bwana-arusi!” Lakini mabikira waliokesha tu ndio waliovumilia hadi mwisho. (Mt. 25:5, 6; 26:41) Namna gani watiwa-mafuta waaminifu leo? Katika kipindi chote cha siku za mwisho, wameona uthibitisho ulio wazi ambao ni kana kwamba unatoa mwito huu, “Huyu hapa bwana-arusi!”—anakaribia kufika. Nao wameitikia mwito huo. Pia wamevumilia, na kuendelea kuwa tayari kabisa kwa ajili ya kuwasili kwa Bwana-arusi. * Hata hivyo, sehemu ya mwisho ya mfano huo inahusu kipindi hususa cha wakati. Jinsi gani?

WENYE BUSARA WATHAWABISHWA NA WAPUMBAVU WAHUKUMIWA

10. Mazungumzo kati ya mabikira wenye busara na mabikira wapumbavu yanazusha swali gani lenye kutatanisha?

10 Labda sehemu yenye kutatanisha zaidi ni sehemu ya mwisho ya mfano huo, ambayo ni mazungumzo kati ya mabikira wapumbavu na mabikira wenye busara. (Soma Mathayo 25:8, 9.) Mazungumzo hayo yanazusha swali hili: “Ni wakati gani katika historia ya watu wa Mungu ambapo watumishi waaminifu wangekataa kuwasaidia wale wenye uhitaji?” Swali hilo linajibiwa tunapofikiria wakati unaohusika wa kutimia kwa mfano huo. Kumbuka uelewaji wetu uliorekebishwa kwamba Yesu, yaani, Bwana-arusi, anakuja karibu na mwisho wa dhiki kuu ili kuhukumu. Kwa hiyo, inaelekea kwamba mazungumzo hayo yanahusu mambo yanayotokea kabla tu ya mwisho wa dhiki kuu. Tunaweza kusema hivyo, kwa kuwa kufikia wakati huo watiwa-mafuta watakuwa tayari wametiwa muhuri wa mwisho.

11. (a) Ni nini kitakachotokea kabla tu ya dhiki kuu kuanza? (b) Mabikira wenye busara walimaanisha nini walipowaambia mabikira wapumbavu waende kwa wauzaji wa mafuta?

11 Hivyo basi, kabla ya dhiki kuu kuanza, watiwa-mafuta wote waaminifu walio duniani watakuwa tayari wametiwa muhuri wa mwisho. (Ufu. 7:1-4) Kuanzia wakati huo na kuendelea, itakuwa hakika kwamba wataenda mbinguni. Lakini mambo yatakuwaje kabla ya dhiki kuu kuanza? Ni nini kitawapata watiwa-mafuta ambao wataacha kuwa waaminifu na kutoendelea kukesha? Hawatapewa thawabu yao ya uhai wa mbinguni. Hivyo, ni wazi kwamba hawatatiwa muhuri wa mwisho kabla ya dhiki kuu kuanza. Wakati huo, waaminifu wengine watatiwa mafuta ili kuchukua nafasi zao. Dhiki kuu inapoanza, huenda wale wapumbavu watashtuka kumwona Babiloni Mkubwa akiharibiwa. Huenda huo ndio wakati ambao watagundua kwamba hawako tayari kwa ajili ya kuwasili kwa Bwana-arusi. Ni nini kitatokea ikiwa wataomba msaada katika dakika za mwisho? Mfano wa Yesu unatupatia jibu lenye kusikitisha. Mabikira wenye busara walikataa kuwapa mafuta wale mabikira wapumbavu, na kuwaambia waende kwa wauzaji wa mafuta. Hata hivyo, kumbuka kwamba ilikuwa “katikati ya usiku.” Je, wangewakuta wauzaji wa mafuta wakati huo? Hapana. Ingekuwa kuchelewa mno.

12. (a) Wakati wa dhiki kuu, ni nini kitakachowapata wale ambao wakati fulani walikuwa watiwa-mafuta lakini wakaacha kuwa waaminifu kabla ya kutiwa muhuri wa mwisho? (b) Ni nini kitakachowapata wale watakaothibitika kuwa kama mabikira wapumbavu?

12 Vivyo hivyo, wakati wa dhiki kuu, watiwa-mafuta waaminifu hawataweza kumsaidia mtu yeyote ambaye ameacha kuwa mwaminifu. Hakutakuwa na msaada wowote. Itakuwa kuchelewa mno. Kwa hiyo, ni nini kitakachowapata wale wasio waaminifu? Yesu anaeleza kilichotokea wale mabikira wapumbavu walipoenda kutafuta mafuta: “Bwana-arusi akafika, na wale mabikira waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye kwenye karamu ya arusi; nao mlango ukafungwa.” Kristo atakapokuja katika utukufu wake karibu na mwisho wa dhiki kuu, atawakusanya watiwa-mafuta wake waaminifu mbinguni. (Mt. 24:31; 25:10; Yoh. 14:1-3; 1 The. 4:17) Kwa kweli, watu wasio waaminifu ambao watathibitika kuwa kama mabikira wapumbavu hawataweza kuingia kwa kuwa mlango utakuwa umefungwa. Huenda watasema: “Bwana, bwana, tufungulie!” Lakini watapewa jibu kama lile watakalopewa wale wanaofananishwa na mbuzi katika saa ya hukumu: “Ninawaambia ninyi kweli, Siwajui ninyi.” Inasikitisha sana!—Mt. 7:21-23; 25:11, 12.

13. (a) Kwa nini hatuhitaji kufikia mkataa kwamba wafuasi wengi watiwa-mafuta wa Kristo wataacha kuwa waaminifu? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba onyo la Yesu linaonyesha kwamba ana uhakika na watumishi wake? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 12.)

13 Tufikie mkataa gani kutokana na mambo tuliyochunguza? Je, Yesu alimaanisha kwamba watumishi wake wengi watiwa-mafuta hawangekuwa waaminifu na hivyo kungehitajika watu wa kuchukua nafasi zao? Hapana. Kumbuka kwamba alikuwa ametoka tu kumwonya ‘mtumwa wake mwaminifu na mwenye busara’ asiwe kamwe mtumwa mwovu. Hakumaanisha kwamba anatazamia wataacha kuwa waaminifu. Vivyo hivyo, katika mfano huo anatoa onyo kali sana. Kama vile tu ambavyo mabikira watano walikuwa wapumbavu na mabikira watano walikuwa wenye busara, kila mtiwa-mafuta ana uwezo wa kuamua kuwa tayari na kukesha au kuwa mpumbavu na kuacha kuwa mwaminifu. Mtume Paulo alisema jambo kama hilo alipowaandikia Wakristo wenzake watiwa-mafuta. (Soma Waebrania 6:4-9; linganisha na Kumbukumbu la Torati 30:19.) Ona kwamba onyo la Paulo lilikuwa thabiti sana, lakini lilifuatiwa na maneno yenye kutia moyo yaliyowahakikishia ndugu na dada zake Wakristo kuwa watapata “mambo yaliyo bora.” Vivyo hivyo, onyo la Yesu katika mfano aliotoa linaonyesha kwamba alikuwa na uhakika huohuo. Kristo anajua kwamba kila mtumishi wake mtiwa-mafuta anaweza kubaki mwaminifu na kupokea thawabu yenye kusisimua sana!

“KONDOO WENGINE” WA KRISTO WANAWEZA KUFAIDIKAJE?

14. Kwa nini “kondoo wengine” wanaweza kufaidika pia na mfano wa wale mabikira kumi?

14 Kwa kuwa Yesu alielekeza mfano wa mabikira kumi kwa wafuasi wake watiwa-mafuta, je, hilo linaonyesha kwamba mfano huo hauna faida yoyote kwa “kondoo wengine” wa Kristo? (Yoh. 10:16) Sivyo hata kidogo! Kumbuka kwamba ujumbe wa mfano huo uko wazi: “Endeleeni kukesha.” Je, maneno hayo yanawahusu tu watiwa-mafuta? Yesu alisema hivi: “Lakini lile ninalowaambia ninyi ninawaambia wote, Endeleeni kukesha.” (Marko 13:37) Yesu anawataka wafuasi wake wote wawe tayari kumtumikia kwa uaminifu na kuendelea kukesha. Kwa hiyo, Wakristo wote wanafuata mfano uliowekwa na watiwa-mafuta wa kukesha, nao wanatanguliza huduma maishani mwao. Kila mmoja wetu na akumbuke kwamba mabikira wapumbavu waliwaomba mabikira wenye busara wawape mafuta. Ombi lao linatukumbusha kwamba hakuna mtu anayeweza kuwa mwaminifu kwa niaba yetu, kubaki katika kweli kwa niaba yetu, au kuendelea kukesha kwa niaba yetu. Kila mmoja wetu atajibu mbele ya Hakimu mwadilifu ambaye Yehova amemweka rasmi. Tunapaswa kuwa tayari. Naye anakuja hivi karibuni!

Ombi la kupata mafuta linatukumbusha kwamba hakuna mtu anayeweza kuwa mwaminifu kwa niaba yetu au kukesha kwa niaba yetu

15. Kwa nini Wakristo wote wanaitarajia kwa hamu ndoa ya Kristo na bibi-arusi wake?

15 Tukio muhimu katika mfano wa Yesu linaweza kuwanufaisha Wakristo wote. Ni nani kati yetu asiyevutiwa na ndoa hiyo ambayo itafungwa hivi karibuni? Watiwa-mafuta watakuwa mbinguni; baada ya vita vya Har–Magedoni, watakuwa bibi-arusi wa Kristo. (Ufu. 19:7-9) Hatimaye, kila mtu duniani atafaidika kutokana na ndoa hiyo itakayofungwa mbinguni, kwa kuwa italeta serikali kamilifu. Iwe tuna tumaini la kwenda mbinguni au kushi milele duniani, acheni tuazimie kujifunza jambo muhimu katika mfano wa mabikira kumi. Acheni tuendelee kuwa macho kwa kuitayarisha mioyo yetu, kubaki imara, na kuendelea kukesha, ili tuweze kufurahia baraka zijazo ambazo Yehova ametuandalia!

^ fu. 9 Katika mfano huo, muda fulani unapita kati ya kutolewa kwa ule mwito, “Huyu hapa bwana-arusi!” (mstari wa 6) na kuja au kuwasili kwa bwana-arusi (mstari wa 10). Katika kipindi chote cha siku za mwisho, watiwa-mafuta walio macho wametambua ishara ya kuwapo kwa Yesu. Kwa hiyo, wanajua kwamba Yesu yuko “hapa,” yaani, anatawala akiwa Mfalme. Hata hivyo, wanapaswa kuendelea kukesha hadi atakapokuja, au atakapowasili.