Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Wazee Wanavyowazoeza Wengine

Jinsi Wazee Wanavyowazoeza Wengine

“Mambo uliyoyasikia kutoka kwangu . . . , uwakabidhi watu waaminifu.”—2 TIM. 2:2.

1. (a) Tangu zamani, watumishi wa Mungu wamekuwa na maoni gani kuhusu mazoezi? Leo tuna maoni gani kuhusu jambo hilo? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

TANGU zamani, watumishi wa Mungu wanaelewa kwamba mazoezi huchangia mafanikio. Mzee wa ukoo, Abramu, ‘aliwakusanya watu wake waliozoezwa’ ili kumwokoa Loti—nao walifanikiwa. (Mwa. 14:14-16) Katika siku za Mfalme Daudi, waimbaji katika nyumba ya Mungu ‘walizoezwa’ kuimba nyimbo za kumsifu Yehova. (1 Nya. 25:7) Leo, tunapigana vita dhidi ya Shetani na wafuasi wake. (Efe. 6:11-13) Pia, tunajitahidi sana kumsifu Yehova. (Ebr. 13:15, 16) Hivyo, kama ilivyokuwa kwa watumishi wa Mungu wa kale, tunahitaji kuzoezwa ili tufanikiwe. Katika kutaniko, Yehova amewakabidhi wazee wajibu wa kuwazoeza wengine. (2 Tim. 2:2) Wazee wenye uzoefu wanatumia njia gani kuwazoeza wengine ili wastahili kulichunga kundi?

MWIMARISHE KIROHO NDUGU UNAYEMZOEZA

2. Huenda mzee akahitaji kufanya nini kabla ya kumzoeza ndugu, na kwa nini?

2 Mzee anaweza kufananishwa na mtunza bustani. Kabla ya kupanda mbegu huenda mtunza bustani akahitaji kuweka mbolea ili udongo uwe na rutuba zaidi. Vivyo hivyo, kabla ya kumzoeza ndugu, huenda ikafaa kuzungumzia naye kanuni fulani za Biblia ambazo zitamsaidia awe tayari zaidi kupokea mazoezi utakayompa.—1 Tim. 4:6.

3. (a) Unaweza kutumiaje andiko la Marko 12:29, 30 unapomzoeza ndugu? (b) Sala ya mzee inaweza kuwa na matokeo gani kwa ndugu anayezoezwa?

3 Ili kujua ni kwa kadiri gani ndugu anafikiri na kutenda kupatana na kweli ya Ufalme, unaweza kumuuliza hivi, ‘Wakfu wako kwa Yehova umebadilije njia yako ya maisha?’ Swali hilo linaweza kuanzisha mazungumzo mazuri kuhusu jinsi tunavyoweza kumtumikia Yehova kwa nafsi yote. (Soma Marko 12:29, 30.) Huenda baada ya mazungumzo ukaamua kusali ili Yehova ampe ndugu huyo roho takatifu itakayomsaidia katika mazoezi yake. Bila shaka atatiwa moyo sana akikusikia ukisali kwa niaba yake!

4. (a) Ni masimulizi gani ya Biblia yanaweza kumchochea ndugu anayezoezwa afanye maendeleo ya kiroho? (b) Wazee wanapaswa kuwa na lengo gani wanapomzoeza ndugu?

4 Unapoanza kumzoeza ndugu, zungumzieni masimulizi ya Biblia yanayoweza kumsaidia awe tayari, mwenye kutegemeka, na mnyenyekevu. (1 Fal. 19:19-21; Neh. 7:2; 13:13; Mdo. 18:24-26) Sifa hizo ni muhimu sana kama vile rutuba kwenye udongo. Zitamsaidia akue haraka kiroho. Jean-Claude, mzee kutoka Ufaransa, anasema hivi: “Ninapomzoeza ndugu, lengo langu kuu ni kumsaidia awe mtu wa kiroho. Ninatafuta nafasi za kusoma naye andiko fulani ili kumsaidia aone ‘mambo ya ajabu’ yaliyo katika Neno la Mungu.” (Zab. 119:18) Je, kuna njia nyingine za kumwimarisha ndugu anayezoezwa?

TOA MAPENDEKEZO​—ELEZA SABABU

5. (a) Kwa nini ni muhimu kuzungumza na ndugu unayemzoeza kuhusu malengo ya kiroho? (b) Kwa nini wazee wanapaswa kuwazoeza vijana? (Tazama maelezo ya chini.)

5 Muulize ndugu unayemzoeza, ‘Una malengo gani ya kiroho?’ Ikiwa hana miradi au malengo yoyote hususa, msaidie ajiwekee lengo linalomfaa ambalo anaweza kutimiza. Mwambie lengo hususa ambalo wewe ulijiwekea, na ueleze kwa shauku jinsi ulivyofurahi ulipolitimiza. Ingawa huenda njia hiyo ikaonekana kuwa rahisi, inafaa sana. Victor, mzee na painia kutoka Afrika, anakumbuka hivi: “Nilipokuwa kijana, mzee fulani aliniuliza maswali machache kuhusu malengo yangu. Maswali hayo yalinifanya nianze kufikiria kwa kina kuhusu huduma yangu.” Wazee wenye uzoefu wanasema kwamba ni muhimu kuanza kuwazoeza ndugu wakiwa vijana—mwanzoni mwa miaka yao ya ujana—kwa kuwapa migawo inayolingana na umri wao. Mazoezi hayo yatawasaidia vijana kukazia fikira malengo ya kiroho wanapozidi kukua na kupambana na vishawishi mbalimbali.—Soma Zaburi 71:5, 17. *

Eleza kwa nini kazi inapaswa kufanywa, na umpongeze ndugu anapojitahidi kuitimiza (Tazama fungu la 5-8)

6. Yesu alitumia njia gani muhimu kuwazoeza wengine?

6 Ili kumchochea ndugu unayemzoeza awe na tamaa ya kutumikia ni vizuri umweleze jambo la kufanya na sababu ya kulifanya. Unapofanya hivyo, unamwiga Yesu, yule Mwalimu Mkuu. Kwa mfano, kabla ya kuwaagiza mitume wake wakafanye wanafunzi, Yesu aliwaeleza sababu ya kutii agizo hilo. Alisema hivi: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” Kisha akaongezea: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.” (Mt. 28:18, 19) Unawezaje kuiga njia ambayo Yesu alitumia kuwazoeza wengine?

7, 8. (a) Wazee wanawezaje kuiga njia ya Yesu ya kuzoeza? (b) Kwa nini ni muhimu kumpongeza ndugu unayemzoeza? (c) Ni mapendekezo gani yatakayowasaidia wazee kuwazoeza wengine? (Ona sanduku “ Jinsi ya Kuwazoeza Wengine.”)

7 Mweleze yule unayemzoeza sababu za Kimaandiko za kufanya jambo analoombwa afanye. Unapofanya hivyo, unamfundisha kufanya mambo kwa kutegemea kanuni za Biblia. Kwa mfano, wazia unamwomba ndugu ahakikishe kwamba eneo la kuingia Jumba la Ufalme ni safi na halihatarishi usalama. Unaweza kutumia andiko la Tito 2:10 na kueleza jinsi ambavyo kazi hiyo ‘italipamba fundisho la Mwokozi wetu, Mungu.’ Pia, mchochee ndugu afikirie jinsi kazi hiyo itakavyowanufaisha wale waliozeeka kutanikoni. Mazungumzo kama hayo yatamchochea kufikiria zaidi jinsi ambavyo ndugu na dada wanafaidika kutokana na kazi yake, badala ya kufanya tu kulingana na anavyoagizwa. Atapata shangwe anapoona jinsi utumishi wake unavyowanufaisha ndugu na dada kutanikoni.

8 Zaidi ya hayo, usisahau kumpongeza ndugu unayemzoeza anapojitahidi kutumia mapendekezo yako. Kwa nini ni muhimu kafanya hivyo? Pongezi za kutoka moyoni ni kama maji katika mmea—zitamchochea kufanya maendeleo.—Linganisha na Mathayo 3:17.

CHANGAMOTO

9. (a) Baadhi ya wazee wanakabili changamoto gani katika nchi tajiri? (b) Kwa nini vijana fulani hawajawahi kutanguliza utumishi wao kwa Mungu?

9 Katika nchi tajiri, huenda wazee wakakabili changamoto fulani: wanawezaje kuwachochea vijana waliobatizwa wenye umri wa miaka 20 au 30 na kitu hivi kushiriki katika utendaji wa kutaniko? Tuliwauliza wazee kutoka nchi 20 za Magharibi kwa nini vijana wengi wanasita kukubali mapendeleo kutanikoni. Wengi wao walisema kwamba baadhi ya vijana hawakutiwa moyo kujiwekea malengo ya kiroho walipokuwa wadogo. Katika visa fulani, vijana ambao walikuwa na mwelekeo wa kujiwekea malengo ya kiroho walichochewa na wazazi wao kujiwekea malengo ya kimwili! Hivyo, vijana hao hawajawahi kutanguliza utumishi wao kwa Mungu.—Mt. 10:24.

10, 11. (a) Mzee anaweza kumsaidiaje ndugu ambaye hajihusishi sana na utendaji wa kutaniko abadili mtazamo wake? (b) Mzee anaweza kutumia kanuni gani za Kimaandiko, na kwa nini? (Tazama maelezo ya chini.)

10 Ikionekana kwamba ndugu hapendi kujihusisha sana na utendaji wa kutaniko, jitihada nyingi na subira zinahitajika ili kubadili mtazamo wake, hata hivyo inawezekana kuubadili. Kama vile mtunza bustani anavyojitahidi kunyoosha shina la mmea kadiri unavyokua,ndivyo  unavyoweza kumsaidia hatua kwa hatua ndugu anayesita kukubali mapendeleo abadili mtazamo wake. Jinsi gani?

11 Sitawisha urafiki wa karibu pamoja naye. Mfanye ahisi kwamba anahitajika kutanikoni. Kisha, baada ya muda, zungumzia naye Maandiko yatakayomsaidia  kufikiria wakfu wake kwa Yehova. (Mhu. 5:4; Isa. 6:8; Mt. 6:24, 33; Luka 9:57-62; 1 Kor. 15:58; 2 Kor. 5:15; 13:5) Unaweza kumuuliza hivi, ‘Ulimwahidi nini Yehova ulipojiweka wakfu kwake?’ Jaribu kuchochea moyo wake kwa kumuuliza hivi, ‘Unafikiri Yehova alihisije ulipobatizwa?’ (Met. 27:11) ‘Unafikiri Shetani alihisije?’ (1 Pet. 5:8) Maandiko yaliyochaguliwa vizuri yanaweza kumchochea sana ndugu huyo.—Soma Waebrania 4:12. *

MNAOZOEZWA, IWENI WAAMINIFU

12, 13. (a) Elisha alikuwa na mtazamo gani alipokuwa akizoezwa? (b) Yehova alimthawabishaje Elisha kwa uaminifu wake?

12 Vijana, kutaniko linahitaji msaada wenu! Mnapaswa kuwa na mtazamo gani ili mfanikiwe katika utumishi wenu? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze matukio fulani ya wakati uliopita kumhusu Elisha.

13 Karibu miaka 3,000 hivi iliyopita, nabii Eliya alimwomba kijana Elisha awe msaidizi wake. Elisha alikubali mara moja mwaliko huo na kumhudumia Eliya kwa uaminifu akifanya kazi za hali ya chini. (2 Fal. 3:11) Baada ya kuzoezwa kwa miaka sita, Elisha alitambua kwamba kazi ya Eliya katika Israeli ilikaribia kwisha. Wakati huo, Eliya alimwambia Elisha asiendelee kufuatana naye, lakini mara tatu Elisha alimwambia Eliya hivi: “Sitakuacha.” Aliazimia kuandamana na Eliya kwa muda mrefu iwezekanavyo. Yehova alimthawabisha Elisha kwa sababu ya uaminifu na ushikamanifu wake; alishuhudia Eliya akichukuliwa katika dhoruba ya upepo.—2 Fal. 2:1-12.

14. (a) Wale wanaozoezwa wanawezaje kumwiga Elisha? (b) Kwa nini wanaozoezwa wanapaswa kuwa waaminifu?

14 Unawezaje kumwiga Elisha? Kubali migawo bila kusita, hata ikiwa ni ya hali ya chini. Mwone anayekuzoeza kuwa rafiki, na umweleze jinsi unavyothamini jitihada zake za kukuzoeza. Ukifanya hivyo, ni kana kwamba utakuwa ukimwambia: “Sitakuacha.” Zaidi ya yote, timiza kwa uaminifu mgawo wowote unaopewa. Kwa nini ni muhimu kufanya hivyo? Ukiwa mwaminifu na mwenye kutegemeka, wazee watakuwa na uhakika kwamba Yehova anataka ukabidhiwe majukumu zaidi kutanikoni.—Zab. 101:6; soma 2 Timotheo 2:2.

WAHESHIMU WANAOKUZOEZA

15, 16. (a) Elisha alionyeshaje kwamba alimheshimu yule aliyemzoeza? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 9.) (b) Kwa nini manabii wengine walimtumaini Elisha?

15 Simulizi la Elisha linaonyesha pia jinsi ndugu wanavyoweza kuwaheshimu wazee wenye uzoefu. Baada ya Eliya na Elisha kukutana na kundi la manabii huko Yeriko, walielekea kwenye Mto Yordani. Wakiwa hapo, “Eliya akachukua vazi lake rasmi, akalifunga, akapiga maji, nayo mwishowe yakagawanyika.” Baada ya kuvuka, waliendelea ‘kuzungumza huku wakitembea.’ Bila shaka, Elisha hakufikiri kwamba sasa anajua kila kitu. Alisikiliza kwa makini kila jambo ambalo Eliya alisema na kujifunza kutoka kwake. Kisha Eliya akachukuliwa na dhoruba ya upepo. Baadaye, Elisha alipofika kwenye Mto Yordani, aliyapiga maji kwa kutumia vazi la Eliya na kusema: “Yuko wapi Yehova Mungu wa Eliya?” Kwa mara nyingine, maji yakagawanyika.—2 Fal. 2:8-14.

16 Je, umetambua kwamba muujiza wa kwanza wa Elisha ulikuwa sawa kabisa na muujiza wa mwisho wa Eliya? Jambo hilo linatufundisha nini? Elisha hakuhisi kwamba alihitaji kufanya mambo kwa njia tofauti na ile iliyotumiwa na Eliya kwa sababu tu sasa yeye ndiye aliyekuwa na mamlaka. Badala yake, alimheshimu yule aliyemzoeza, yaani Eliya, kwa kuendeleza njia aliyotumia katika kutimiza huduma yake. Jambo hilo lilifanya manabii wenzake wamtumaini. (2 Fal. 2:15) Hata hivyo, katika miaka 60 ya huduma ya Elisha akiwa nabii, Yehova alimwezesha kufanya miujiza mingi zaidi kuliko Eliya. Wale wanaozoezwa wanajifunza nini?

17. (a) Wale wanaozoezwa wanawezaje kuiga mtazamo wa Elisha? (b) Yehova anaweza kuwatumiaje ndugu wanaozoezwa ambao ni waaminifu?

17 Usifikiri kwamba baada tu ya kukabidhiwa majukumu kutanikoni, basi unapaswa kubadili kila kitu, yaani, kufanya mambo kwa njia tofauti kabisa na yalivyokuwa yakifanywa mwanzoni. Mabadiliko hayafanywi kwa sababu tu unatamani kubadili mambo, badala yake hufanywa ikitegemea uhitaji wa kutaniko na mwongozo tunaopata kutoka katika tengenezo la Yehova. Elisha alifanya manabii wenzake wamtumaini na alimheshimu Eliya kwa kuendelea kutumia njia ambazo alitumia. Vivyo hivyo, ndugu na dada watakutumaini na utaonyesha unawaheshimu wazee wenye uzoefu kwa kuendelea kutumia njia zao zinazotegemea Biblia. (Soma 1 Wakorintho 4:17.) Hata hivyo, unapozidi kupata uzoefu, bila shaka utashiriki kufanya mabadiliko yatakayolisaidia kutaniko kwenda sambamba na tengenezo la Yehova. Kwa kweli, kama ilivyokuwa katika kisa cha Elisha, baada ya muda Yehova anaweza kukutumia kufanya kazi kubwa zaidi kuliko wale waliokuzoeza.—Yoh. 14:12.

18. Kwa nini ni muhimu sana kuwazoeza ndugu sasa?

18 Tunatumaini kwamba makala hii na ile iliyotangulia zitawachochea wazee wengi zaidi watenge wakati wa kuwazoeza wengine. Pia, tunatumaini kwamba ndugu wanaozoezwa watakubali kwa moyo mkunjufu mazoezi hayo na kuyatumia kwa hekima kuwatunza kondoo wa Yehova. Kufanya hivyo kutayaimarisha makutaniko ulimwenguni pote na kumsaidia kila mmoja wetu aendelee kuwa mwaminifu wakati wa matukio makubwa yaliyo mbele yetu.

^ fu. 5 Ikiwa kijana Mkristo amekomaa kiroho, ni mnyenyekevu, na anatimiza matakwa ya Kimaandiko, wazee wanaweza kumpendekeza kuwa mtumishi wa huduma hata kama hajafikia umri wa miaka 20.—1 Tim. 3:8-10, 12; tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1989, ukurasa wa 29.