Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uhusiano Wako na Yehova Ni Halisi Kadiri Gani?

Uhusiano Wako na Yehova Ni Halisi Kadiri Gani?

“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” —YAK. 4:8.

1. Kwa nini tunapaswa kusitawisha uhusiano wenye nguvu pamoja na Yehova?

JE, WEWE ni Shahidi wa Yehova aliyejiweka wakfu na kubatizwa? Ikiwa ndivyo, basi una kitu chenye thamani sana, yaani, uhusiano wa karibu na Mungu. Hata hivyo, ulimwengu wa Shetani na hali yetu ya kutokamilika inahatarisha uhusiano huo. Wakristo wote wanakabili hatari hiyo. Kwa hiyo, tunapaswa kujitahidi kadiri tuwezavyo kusitawisha uhusiano wenye nguvu pamoja na Yehova.

2. (a) Uhusiano ni nini? (Tazama maelezo ya chini.) (b) Tunawezaje kuimarisha uhusiano wetu na Yehova?

2 Uhusiano wako na Yehova ni halisi kadiri gani? Je, ungependa kuuimarisha zaidi? Andiko la Yakobo 4:8 linatueleza jinsi tunavyoweza kufanya hivyo. Linasema, “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” Ona kwamba jambo hilo linahusisha pande mbili. * Tunapochukua hatua ili kumkaribia Mungu, yeye pia anatukaribia. Tunapoendelea kufanya hivyo, uhusiano wetu na Yehova unaimarika na kuwa halisi zaidi. Hilo linatufanya tuwe na uhakika kama Yesu aliyesema: “Yule aliyenituma ni halisi, . . . Mimi ninamjua.” (Yoh. 7:28, 29) Hata hivyo, tunaweza kuchukua hatua gani ili kumkaribia Yehova?

Unaweza kuwasilianaje na Mungu? (Tazama fungu la 3)

3. Tunawasilianaje na Yehova?

3 Ili kumkaribia Yehova, ni muhimu sana kuwasiliana naye kwa ukawaida. Unaweza kuwasilianaje na Mungu? Fikiria hili, unawasilianaje na rafiki yako anayeishi mbali? Huenda mnaandikiana ujumbe na kuzungumza kupitia simu mara kwa mara. Unazungumza na Yehova unaposali kwake kwa ukawaida. (Soma Zaburi 142:2.) Unamsikiliza Yehova unaposoma Neno Lake na kulitafakari kwa ukawaida. (Soma Isaya 30:20, 21.) Acheni tuone jinsi mawasiliano hayo yanavyoimarisha uhusiano wetu na Yehova na kuufanya uwe halisi zaidi.

MSIKILIZE YEHOVA KWA KUJIFUNZA BIBLIA

4, 5. Yehova anatumiaje Neno lake, Biblia, kuwasiliana nawe? Toa mfano.

4 Bila shaka, unakubali kwamba kwa ujumla Biblia ni ujumbe wa Mungu kwa wanadamu. Lakini je, Biblia inaeleza jinsi wewe binafsi unavyoweza kumkaribia Yehova? Bila shaka. Jinsi gani? Unaposoma na kujifunza Biblia kwa ukawaida, fikiria jinsi unavyohisi kuhusu yale unayosoma na jinsi unavyoweza kuyatumia maishani; unapofanya hivyo, unamruhusu Yehova azungumze nawe kupitia Neno lake. Hilo linafanya umkaribie zaidi.—Ebr. 4:12; Yak. 1:23-25.

5 Kwa mfano, soma na utafakari maneno haya ya Yesu, “acheni kujiwekea hazina duniani.” Ikiwa tayari unatanguliza masilahi ya Ufalme, basi unahisi ni kana kwamba Yehova anakupongeza. Kwa upande mwingine, ikiwa unahisi unahitaji kufanya marekebisho ili utangulize masilahi ya Ufalme, basi Yehova anakusaidia kujua unachoweza kufanya ili umkaribie zaidi.—Mt. 6:19, 20.

6, 7. (a) Kujifunza Biblia kuna matokeo gani katika uhusiano wetu na Yehova? (b) Tunapaswa kuwa na lengo gani tunapojifunza Biblia?

6 Kujifunza Maandiko kunatusaidia kuboresha hali yetu ya kiroho. Pia, kunatusaidia kuthamini zaidi njia za Yehova na kutufanya tumpende zaidi. Tunapozidi kumpenda Yehova, yeye pia anazidi kutupenda na hilo linaimarisha uhusiano wetu pamoja naye.—Soma 1 Wakorintho 8:3.

7 Hata hivyo, ili tumkaribie Yehova, tunapaswa kujifunza tukiwa na lengo linalofaa. Andiko la Yohana 17:3 linasema hivi: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” Tunaweza kujifunza mambo mengi mapya na yenye kupendeza tunaposoma Biblia, lakini lengo letu kuu linapaswa kuwa kumjua Yehova vizuri ili awe halisi zaidi kwetu.—Soma Kutoka 33:13; Zab. 25:4.

8. (a) Mtu anaweza kuhisije kuhusu jinsi Yehova alivyomtendea Mfalme Azaria? (b) Ikiwa tunamjua Yehova, tutahisije kuhusu mambo anayofanya?

8 Tukimjua vizuri Yehova, hatutavunjika moyo ikiwa hatuelewi kikamili kwa nini alitenda kwa njia fulani katika baadhi ya masimulizi ya Biblia. Kwa mfano, unahisije kuhusu jinsi Yehova alivyomtendea Mfalme Azaria wa Yuda? (2 Fal. 15:1-5) Ingawa “watu walikuwa bado wanatoa dhabihu na kufukiza moshi wa dhabihu katika mahali pa juu,” Azaria ‘aliendelea kufanya yaliyokuwa manyoofu machoni pa Yehova.’ Hata hivyo, “Yehova akamletea mfalme pigo, naye akaendelea kuwa mwenye ukoma mpaka siku ya kufa kwake.” Kwa nini? Simulizi hilo halitaji sababu. Je, jambo hilo linapaswa kutuvunja moyo au kutufanya tuhisi kwamba Yehova alimwadhibu Azaria bila sababu? Hapana. Ikiwa tunajua vizuri njia za Yehova, tunaelewa kwamba siku zote yeye hutoa nidhamu kwa “kwa kiwango kinachofaa.” (Yer. 30:11) Ujuzi huo unatuhakikishia kwamba hata kama hatuelewi kwa nini Yehova alimwadhibu Azaria, hukumu Yake ilikuwa ya uadilifu.

9. Ni mambo gani yanayotusaidia kuelewa kwa nini Yehova alimpiga Azaria kwa ukoma?

9 Hata hivyo, katika kisa cha Mfalme Azaria, Maandiko mengine yanatoa habari zaidi. Yanaonyesha kwamba Mfalme Azaria, aliitwa pia Mfalme Uzia. (2 Fal. 15:7, 32) Andiko la 2 Mambo ya Nyakati 26:3-5, 16-21, linaonyesha kwamba ingawa Uzia alifanya yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova, baada ya muda “moyo wake ukawa na majivuno hata kufikia hatua ya kusababisha uharibifu.” Kwa kimbelembele, alitaka kufanya jambo ambalo ni makuhani tu waliruhusiwa kufanya. Makuhani 81 walimfuata wakiwa na kusudi la kumrekebisha. Uzia aliitikiaje? Alitenda kwa kiburi. “Akawa na ghadhabu” dhidi ya makuhani. Basi haishangazi kwamba Yehova alimpiga kwa ukoma!

10. Kwa nini si lazima tupate ufafanuzi wa kila jambo ambalo Yehova anafanya? Na tunaweza kufanya nini ili tuwe na uhakika zaidi katika njia za Yehova za uadilifu?

10 Tunajifunza nini? Vipi ikiwa hakuna habari za kutosha zinazoweza kutusaidia kuelewa kikamili simulizi fulani la Biblia? Je, utatilia shaka uadilifu wa Mungu? Au utakuwa na uhakika kwamba siku zote Yehova hufanya yaliyo sawa, na kwamba ana haki ya kuweka viwango vya mambo yanayofaa na mambo yasiyofaa? (Kum. 32:4) Tunapozidi kumjua Yehova, tutampenda sana na kuthamini njia zake hivi kwamba hatutahitaji kupata ufafanuzi wa kila jambo analofanya. Uwe na uhakika kwamba unaweza kusitawisha upendo na uthamini kama huo kumwelekea Yehova kadiri unavyoendelea kujifunza na kutafakari Neno lake, Biblia, analotumia kuwasiliana nasi. (Zab. 77:12, 13) Jambo hilo litaimarisha uhusiano wako na Yehova na kuufanya uwe halisi zaidi.

ZUNGUMZA NA YEHOVA KUPITIA SALA

11-13. Tunajuaje kwamba Yehova husikiliza sala? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 19.)

11 Tunaposali, tunamkaribia Yehova. Tunamsifu, tunamshukuru, na kuomba mwongozo wake. (Zab. 32:8) Lakini ikiwa unataka uhusiano wako na Yehova uwe halisi, unapaswa kusadiki kabisa kwamba anasikiliza sala.

12 Watu wengine wanaamini kwamba sala inawasaidia watu kisaikolojia tu. Wanadai kuwa mtu huhisi kwamba sala yake imejibiwa kwa sababu ameeleza mawazo yake, ametambua tatizo lake, na kujitahidi kutafuta suluhisho. Ni kweli kwamba sala inaweza kutusaidia katika njia hizo. Hata hivyo, tunajuaje kwamba kwa kweli Yehova anasikiliza sala zetu za kutoka moyoni?

13 Fikiria hili: Kabla ya kuja duniani, Yesu alijionea moja kwa moja jinsi Yehova alivyojibu sala za watumishi Wake. Hivyo, wakati wa huduma yake hapa duniani, Yesu aliwasiliana na Yehova na kumweleza hisia zake kupitia sala. Wakati mwingine alisali usiku kucha. Je, Yesu angefanya hivyo ikiwa alijua kwamba baba yake hasikilizi sala? (Luka 6:12; 22:40-46) Je, angewafundisha wanafunzi wake wasali ikiwa alijua kwamba sala inawasaidia watu kisaikolojia tu? Kwa kweli, Yesu alijua kwamba sala ni njia halisi ya kuwasiliana na Yehova. Wakati fulani alisema hivi: “Baba, ninakushukuru kwamba umenisikia. Kweli, nilijua kwamba sikuzote wewe hunisikia.” Sisi pia tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ni “msikiaji wa sala.”—Yoh. 11:41, 42; Zab. 65:2.

14, 15. (a) Tunanufaikaje kwa kutaja mambo hususa tunaposali? (b) Sala zilimsaidiaje Kathy kuimarisha uhusiano wake na Yehova?

14 Ukitaja mambo hususa unaposali, utaona wazi jinsi Yehova anavyojibu sala, hata katika njia isiyo ya moja kwa moja. Yehova atakuwa halisi zaidi kwako unapoona akijibu sala zako. Isitoshe, kadiri unavyomweleza Yehova hisia zako za ndani kabisa, ndivyo anavyozidi kukukaribia.

15 Mfikirie dada anayeitwa Kathy. * Ingawa alishiriki kwa ukawaida katika huduma, hakufurahia kuhubiri. Anasema hivi: “Sikupenda kwenda utumishi wa shambani. Sikupenda hata kidogo. Nilipostaafu, mzee mmoja wa kutaniko alisema kwamba ninaweza kuwa painia wa kawaida, hata akanipa fomu ya upainia. Niliamua kufanya upainia, lakini nilianza pia kusali kila siku nikimwomba Yehova anisaidie kuupenda utumishi wa shambani.” Je, Yehova alijibu sala zake? Kathy anasema hivi: “Nimekuwa painia kwa miaka mitatu sasa. Nimeboresha hatua kwa hatua ustadi wangu wa kutoa ushahidi kwa sababu ya kutumia muda mwingi katika huduma na kushirikiana na dada wengine. Sasa ninafurahia kuhubiri—ninapenda sana kwenda utumishi wa shambani. Jambo muhimu zaidi ni kwamba sasa nina uhusiano wa karibu sana na Yehova kuliko mwanzoni.” Kwa hakika, sala zilifanya uhusiano kati ya Kathy na Yehova uwe halisi.

TIMIZA SEHEMU YAKO

16, 17. (a) Tunapaswa kufanya nini ili uhusiano wetu na Yehova uwe halisi na uendelee kukua? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

16 Sikuzote tunapaswa kuendelea kusitawisha uhusiano wa karibu na Yehova. Ikiwa tunataka Mungu atukaribie, tunapaswa kuchukua hatua ya kumkaribia. Hivyo, katika hali yoyote ile, acheni tuendelee kuwasiliana na Yehova kwa ukawaida kwa kujifunza Biblia na kusali. Tukifanya hivyo, uhusiano wetu na Yehova utazidi kukua na hatimaye tutafanikiwa kukabiliana na hali ngumu.

Sikuzote tunapaswa kuendelea kusitawisha uhusiano wa karibu na Yehova (Tazama fungu la 16 na 17)

17 Hata hivyo, huenda mambo yakawa magumu tunapoona matatizo yetu yanaendelea licha ya kusali kwa bidii. Katika nyakati kama hizo, imani yetu kwa Yehova inaweza kuyumba-yumba. Tunaweza kuanza kutilia shaka ikiwa kwa kweli Yehova anasikiliza sala zetu au ana uhusiano wa karibu pamoja nasi. Tunawezaje kukabiliana na hali hizo tukiwa na uhakika kwamba uhusiano wetu na Yehova ni halisi? Makala inayofuata itazungumzia jambo hilo.

^ fu. 2 Uhusiano umefafanuliwa kuwa jinsi ambavyo watu wawili wanatendeana na kuonyeshana hisia. Hivyo, wote wawili wanahusika.

^ fu. 15 Jina limebadilishwa.