Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Waliziona” Ahadi

“Waliziona” Ahadi

“Hawakupata utimizo wa zile ahadi, bali waliziona kwa mbali.”—EBR. 11:13.

1. Uwezo wetu wa kuwazia mambo ambayo hatujawahi kuyaona unaweza kutunufaishaje? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

UWEZO wetu wa kuwazia mambo ambayo hatujawahi kuyaona ni zawadi kutoka kwa Mungu. Unatusaidia kupanga mambo kwa hekima na kutazamia mambo mazuri ya wakati ujao. Yehova anaweza kujua matukio ya wakati ujao, na mara nyingi anatuambia mapema kupitia Maandiko kile kitakachotokea. Tunaweza kuwazia akilini mambo yatakayotokea. Kwa kweli, uwezo wetu wa kuwazia vitu visivyoonekana unatusaidia kuwa na imani.—2 Kor. 4:18.

2, 3. (a) Kwa nini ni muhimu kuzingatia msingi wa mambo tunayowazia? (b) Tutachunguza maswali gani katika makala hii?

2 Wakati mwingine watu huwazia mambo yasiyo na msingi. Kwa mfano, ikiwa msichana mdogo anajiwazia amepanda kipepeo, hilo ni jambo lisilo halisi. Lakini Hana alikuwa na msingi wa kuwazia jinsi mambo yatakavyokuwa atakapompeleka Samweli akatumikie kwenye maskani. Mawazo yake yalitegemea jambo aliloazimia kufanya, na hilo lilimsaidia kukazia fikira lengo lake. (1 Sam. 1:22) Tunapowazia ahadi za Mungu, tunafikiria mambo ambayo tuna uhakika yatatokea.—2 Pet. 1:19-21.

3 Bila shaka, watu wengi waaminifu walioishi zamani waliwazia mambo ambayo Mungu aliahidi. Walinufaikaje kwa kuwazia baraka za wakati ujao? Nasi tunanufaikaje kwa kufikiria mambo mazuri ambayo Mungu ameahidi kuwafanyia wanadamu watiifu?

WALIIMARISHWA KWA KUWAZIA TUMAINI LAO

4. Abeli alikuwa na msingi gani wa kuwazia mambo ya wakati ujao?

4 Je, Abeli, mwanadamu wa kwanza mwaminifu, aliwazia ahadi yoyote ya Yehova? Hatuwezi kusema kwamba Abeli alijua mapema utimizo wa ahadi hii inayopatikana katika maneno ambayo Mungu alimwambia nyoka: “Nitaweka uadui kati yako na yule mwanamke na kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.” (Mwa. 3:14, 15) Hata hivyo, inaelekea Abeli alifikiria sana ahadi hiyo na alitambua kwamba mtu fulani ‘angetiwa jeraha kwenye kisigino,’ ili wanadamu warudishiwe ukamilifu waliokuwa nao Adamu na Hawa kabla ya kufanya dhambi. Haidhuru Abeli aliwazia jambo gani kuhusu wakati ujao, alikuwa na imani iliyotegemea ahadi ya Mungu, hivyo Yehova alikubali dhabihu yake.—Soma Mwanzo 4:3-5; Waebrania 11:4.

5. Kwa nini kuwazia wakati ujao kulimwimarisha Enoko?

5 Enoko mwaminifu alikuwa na imani, hata ingawa aliishi kati ya watu wasiomwogopa Mungu waliosema mambo ya kushtua kumhusu Mungu. Enoko aliongozwa na roho ya Mungu kutabiri kwamba Yehova angekuja “pamoja na watakatifu wake makumi ya maelfu, ili kufanya hukumu juu ya wote, na kuwathibitisha kuwa ni wenye hatia wote wasiomwogopa Mungu kuhusu matendo yao yote ya kutomwogopa Mungu ambayo walitenda kwa njia ya kutomwogopa Mungu, na kuhusu mambo yote ya kushtua ambayo watenda-dhambi wasiomwogopa Mungu walisema juu yake.” (Yuda 14, 15) Kwa kuwa alikuwa na imani, Enoko angeweza kuwazia ulimwengu usio na watu wasiomwogopa Mungu.—Soma Waebrania 11:5, 6.

6. Inaelekea Noa aliendelea kutafakari nini baada ya Gharika?

6 Noa aliokoka Gharika kwa sababu ya imani yake. (Ebr. 11:7) Baada ya Gharika, imani ilimchochea kutoa dhabihu. (Mwa. 8:20) Kama Abeli, Noa aliamini kwamba mwishowe wanadamu wangewekwa huru kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo. Noa aliendelea kuwa na imani na tumaini hata baada ya Gharika, wakati ambapo Nimrodi alimpinga Yehova. (Mwa. 10:8-12) Inaelekea alitiwa moyo sana alipofikiria wakati ambapo wanadamu watawekwa huru kutokana na utawala mbaya, dhambi tuliyorithi, na kifo. Sisi pia tunaweza kuwazia wakati huo mzuri ulio karibu sana!—Rom. 6:23.

WALIWAZIA UTIMIZO WA AHADI

7. Abrahamu, Isaka, na Yakobo waliwazia mambo gani ya wakati ujao?

7 Abrahamu, Isaka, na Yakobo wangeweza kuwazia wakati ujao ulio bora kwa sababu Mungu aliwaahidi kwamba kupitia uzao wao, mataifa yote ya dunia yatapata baraka. (Mwa. 22:18; 26:4; 28:14) Wazao wa wazee hao wa ukoo wangekuwa wengi na wangeishi katika Nchi ya Ahadi waliyopewa na Mungu. (Mwa. 15:5-7) Kwa imani, wanaume hao waliomwogopa Mungu wangeweza kuwazia wazao wao wakimiliki Nchi ya Ahadi. Kwa hiyo, tangu wanadamu walipopoteza ukamilifu, Yehova amewahakikishia watumishi wake waaminifu kwamba atawarudishia baraka zilizopotezwa na Adamu.

8. Ni nini kilichomsaidia Abrahamu kuwa na imani thabiti?

8 Inaelekea kwamba uwezo wa Abrahamu wa kuwazia ahadi za Mungu ulimwezesha kutenda kwa imani yenye nguvu. Maandiko yanaonyesha kwamba ingawa Abrahamu na watumishi wengine waaminifu wa Mungu “hawakupata utimizo wa zile ahadi” maishani mwao, “waliziona kwa mbali na kuzikaribisha.” (Soma Waebrania 11:8-13.) Abrahamu alikuwa na uthibitisho wa kutosha kuwa tumaini lake ni halisi hivi kwamba ni kama aliona mambo ambayo hakuwahi kuyaona!

9. Abrahamu alinufaikaje kwa kuamini ahadi za Mungu?

9 Imani ya Abrahamu katika ahadi za Mungu iliimarisha azimio lake la kufanya mapenzi ya Mungu. Kwa imani, aliondoka Uru na hakuwa mkaaji wa kudumu katika jiji lolote la Kanaani. Kama jiji la Uru, majiji hayo hayakuwa na misingi imara kwa sababu yaliongozwa na watawala wasiomwogopa Mungu. (Yos. 24:2) Katika miaka iliyobaki ya maisha yake, Abrahamu “alikuwa akingojea jiji lililo na misingi ya kweli, ambalo mjenzi na mtengenezaji wa jiji hilo ni Mungu.” (Ebr. 11:10) Alijiwazia akiwa mkaaji wa kudumu chini ya utawala wa Yehova. Abeli, Enoko, Noa, Abrahamu, na wengine waliamini kwamba kutakuwa na ufufuo na walitazamia kuishi duniani wakati ujao chini ya Ufalme wa Mungu, “jiji lililo na misingi ya kweli.” Kutafakari baraka hizo kuliimarisha imani yao katika Yehova.—Soma Waebrania 11:15, 16.

10. Sara alinufaikaje kwa kuwazia wakati ujao?

10 Mfikirie Sara, mke wa Abrahamu. Alipokuwa na umri wa miaka 90, akiwa hana mtoto, maoni yanayofaa kuhusu wakati ujao yalimwezesha kutenda kwa imani. Hivyo, aliwazia wazao wake wakifurahia baraka ambazo Yehova aliahidi. (Ebr. 11:11, 12) Kwa nini alikuwa na matarajio hayo? Yehova alikuwa amemwambia mume wake hivi: “Nitambariki yeye na pia nitakupa mwana kupitia yeye; nami nitambariki Sara naye atakuwa mataifa; wafalme wa vikundi vya watu watatoka kwake.” (Mwa. 17:16) Baada ya Isaka kuzaliwa, Sara alikuwa na sababu nzuri ya kuwazia utimizo wa ahadi nyingine ambazo Mungu alimwahidi Abrahamu. Sisi pia tuna zawadi ya pekee sana, yaani, uwezo wa kuwazia mambo ambayo Mungu ameahidi, na tuna uhakika yatatimia!

ALIKAZA MACHO KWENYE THAWABU

11, 12. Musa alisitawishaje upendo kwa Yehova?

11 Musa alikuwa na imani na alimpenda sana Yehova. Alipokuwa kijana, akiishi pamoja na familia ya mfalme wa Misri, Musa angeweza kusitawisha kwa urahisi tamaa ya kupata mamlaka na utajiri. Hata hivyo, ni wazi kwamba wazazi wake walimfundisha kumhusu Yehova na kusudi Lake la kuwakomboa Waebrania kutoka utumwani na kuwapa Nchi ya Ahadi. (Mwa. 13:14, 15; Kut. 2:5-10) Ikiwa mara nyingi Musa alifikiria baraka ambazo Mungu aliwaahidi watu wake, unafikiri ni nini kilisitawi moyoni mwake—kupenda umashuhuri au kumpenda Yehova?

12 Maandiko yanatuambia: “Kwa imani Musa, alipokuwa mtu mzima, alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao, akachagua kutendewa vibaya pamoja na watu wa Mungu badala ya kufurahia dhambi kwa muda, kwa sababu aliona shutuma ya Kristo kuwa ni utajiri mkubwa kuliko hazina za Misri; kwa maana alikaza macho kwenye malipo ya thawabu.”—Ebr. 11:24-26.

13. Musa alinufaikaje kwa kutafakari kwa kina ahadi za Mungu?

13 Musa alipotafakari kwa kina mambo ambayo Yehova aliwaahidi Waisraeli, imani yake na upendo wake kwa Mungu uliimarika. Kama wanadamu wengine waliomwogopa Mungu, huenda aliwazia wakati ambapo Yehova ataondoa kifo. (Ayu. 14:14, 15; Ebr. 11:17-19) Haishangazi kwamba Musa alichochewa kumpenda Mungu ambaye aliwahurumia Waebrania na wanadamu wote. Musa alikuwa na imani na alimpenda Yehova katika maisha yake yote. (Kum. 6:4, 5) Hata Farao alipotishia kumuua, imani yake, kumpenda Mungu, na kuwazia wakati ujao kulimwimarisha kukabiliana na vitisho hivyo kwa ujasiri.—Kut. 10:28, 29.

WAZIA MAMBO HALISI YA UFALME

14. Watu huwazia mambo gani yasiyo halisi?

14 Watu wengi wana mawazo yasiyo halisi kuhusu wakati ujao. Kwa mfano, wana vitu vichache lakini wana ndoto za kuwa matajiri wakubwa na kuishi bila wasiwasi, ingawa maisha ya mwanadamu yamejaa “taabu na mambo yenye kuumiza.” (Zab. 90:10) Wanajiwazia wakiishi bila mahangaiko chini ya serikali za wanadamu, wakati Biblia inasema kwamba Ufalme wa Mungu ndiyo suluhisho pekee la matatizo ya wanadamu. (Dan. 2:44) Watu wengi wanahisi kwamba Mungu hatauharibu mfumo huu mwovu, lakini Biblia inaeleza jambo tofauti kabisa. (Sef. 1:18; 1 Yoh. 2:15-17) Matumaini ya watu hao wanaopuuza kusudi la Yehova kuhusu wakati ujao ni ndoto za mchana.

Hebu jiwazie ukiwa katika ulimwengu mpya! (Tazama fungu la 15)

15. (a) Wakristo wananufaikaje kwa kuwazia tumaini lao? (b) Unatazamia jambo gani Mungu atakapotimiza ahadi zake?

15 Kwa upande mwingine, Wakristo tunaimarishwa kwa kuwazia tumaini letu, iwe ni kuishi mbinguni au duniani. Je, unaweza kujiwazia ukifurahia mambo ambayo Yehova ameahidi? Bila shaka unafurahi sana unapotafakari mambo utakayofanya Mungu atakapokuwa akitimiza ahadi zake. Labda unajiwazia ukiishi duniani milele. Fikiria jinsi utakavyoshirikiana na wengine kuigeuza dunia kuwa paradiso. Una majirani wanaompenda Yehova kama wewe. Una afya nzuri, nguvu, na mtazamo mzuri. Maisha ni mazuri kwa sababu wale wanaosimamia kazi ya kuigeuza dunia kuwa paradiso wanakujali kikweli. Unafurahia kutumia vipawa na ujuzi wako kwa sababu kila jambo unalofanya linawanufaisha wengine na linampendeza Mungu. Kwa mfano, unawasaidia watu waliofufuliwa kumjua Yehova. (Yoh. 17:3; Mdo. 24:15) Mambo hayo si ndoto. Kuwazia mambo hayo yenye kupendeza kunategemea kweli za Kimaandiko zinazohusu wakati ujao.—Isa. 11:9; 25:8; 33:24; 35:5-7; 65:22.

KWA NINI TUZUNGUMZIE TUMAINI LETU?

16, 17. Tunanufaikaje kwa kuzungumzia tumaini letu?

16 Tumaini letu linakuwa halisi zaidi tunapozungumza na Wakristo wenzetu kuhusu jambo tunalotazamia kufanya Yehova atakapotimiza ahadi zake. Ingawa hakuna anayejua kikamili hali zake zitakuwaje katika ulimwengu mpya, kuzungumzia mambo tunayotazamia kutatutia moyo na kuonyesha kwamba tunaamini kuwa ahadi za Mungu ni halisi. Mtume Paulo alipowatembelea ndugu huko Roma, walifurahia sana “ubadilishanaji wa kitia-moyo,” na hivyo ndivyo ilivyo kwetu katika nyakati hizi zenye misukosuko.—Rom. 1:11, 12.

17 Kuwazia wakati ujao kunaweza pia kutusaidia kudhibiti mawazo yasiyofaa kuhusu hali ngumu tunazokabili. Huenda mtume Petro alihangaikia jambo hilo alipomwambia Yesu hivi: “Tazama! Tumeacha vitu vyote na kukufuata wewe; kwa kweli kutakuwa na nini kwa ajili yetu?” Ili kumsaidia Petro na wote waliokuwepo kuwazia wakati ujao, Yesu alijibu: “Kwa kweli ninawaambia ninyi, katika uumbaji-mpya Mwana wa binadamu atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu, ninyi ambao mmenifuata mtaketi pia juu ya viti vya ufalme kumi na viwili, mkiyahukumu yale makabila kumi na mawili ya Israeli. Na kila mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au baba au mama au watoto au mashamba kwa ajili ya jina langu atapokea mara nyingi zaidi naye atarithi uzima wa milele.” (Mt. 19:27-29) Hivyo, Petro na wanafunzi wengine wangeweza kutafakari majukumu yao katika serikali ambayo ingetawala dunia yote na kuwaletea wanadamu watiifu baraka tele.

18. Tunanufaikaje kwa kufikiria utimizo wa ahadi za Mungu?

18 Sikuzote watumishi wa Yehova walio duniani wamenufaika kwa kufikiria kuhusu utimizo wa ahadi za Mungu. Abeli alijua mambo ya kutosha kuhusu ahadi za Mungu, hivyo angeweza kuwazia wakati ujao ulio bora, kuwa na imani, na kuwa na tumaini hakika. Abrahamu alikuwa na imani thabiti kwa sababu aliwazia utimizo wa unabii wa Mungu kuhusu “uzao.” (Mwa. 3:15) Musa “alikaza macho kwenye malipo ya thawabu,” hivyo alitenda kwa imani na alimpenda sana Yehova. (Ebr. 11:26) Imani yetu kwa Mungu na upendo wetu kwake utaongezeka sana tunapotumia uwezo wetu kuwazia utimizo wa ahadi za Yehova. Katika makala inayofuata tutazungumzia jinsi tunavyoweza kutumia vizuri uwezo huo.