Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kumshinda Shetani!

Unaweza Kumshinda Shetani!

“Chukueni msimamo mkampinge [Shetani], mkiwa imara katika imani.”—1 PET. 5:9.

1. (a) Kwa nini tunapaswa kujitahidi kupambana na Shetani? (b) Tunajuaje kwamba inawezekana kumshinda Shetani?

SHETANI anapigana vita na watiwa-mafuta walio duniani na “kondoo wengine.” (Yoh. 10:16) Lengo lake ni kuwameza watumishi wengi wa Yehova kadiri iwezekanavyo katika muda mfupi uliobaki. (Soma Ufunuo 12:9, 12.) Je, tunaweza kumshinda Shetani? Ndiyo! Biblia inasema: “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.”—Yak. 4:7.

2, 3. (a) Kwa nini Shetani anataka watu waamini kwamba hayupo? (b) Unajuaje kwamba Shetani ni kiumbe halisi?

2 Watu wengi hawaamini kwamba Shetani ni kiumbe halisi. Kwa maoni yao, Shetani na mashetani ni wahusika wa kubuniwa kwenye vitabu vya hadithi, filamu za kutisha, na michezo ya video. Watu hao wanafikiri kwamba hakuna mtu mwenye akili anayeamini kuwa kuna roho waovu. Je, unafikiri Shetani na roho waovu wanakasirika wanapoona ulimwengu ukiwapuuza kwa kuwaona kuwa viumbe wa kuwazia tu? Haielekei kuwa wanakasirika. Isitoshe, ni rahisi sana kwa Shetani kupofusha akili za watu ambao hawaamini kwamba yupo. (2 Kor. 4:4) Shetani anatumia mawazo kama hayo kuwapotosha watu.

3 Watumishi wa Yehova si miongoni mwa watu wanaopotoshwa. Tunajua kwamba Ibilisi ni kiumbe halisi, kwa kuwa yeye ndiye aliyeongea na Hawa kupitia nyoka. (Mwa. 3:1-5) Alipokuwa akizungumza na Yehova, Shetani alitilia shaka nia ya Ayubu. (Ayu. 1:9-12) Shetani ndiye aliyejaribu kumshawishi Yesu. (Mt. 4:1-10) Pia, baada ya Ufalme wa Mungu kuanza kutawala mwaka wa 1914, Shetani ndiye aliyeanza “kupigana vita” na watiwa-mafuta walio duniani. (Ufu. 12:17) Bado vita hivyo vinaendelea kwa kuwa Shetani anataka kuvunja imani ya watiwa-mafuta walio duniani na pia ya kondoo wengine. Ili kushinda vita hivyo, tunapaswa kumpinga Shetani na kubaki imara katika imani. Makala hii inazungumzia njia tatu za kufanya hivyo.

EPUKA MAJIVUNO

4. Shetani ameonyeshaje kwamba ana majivuno?

4 Shetani si mnyenyekevu hata kidogo. Kiumbe huyo wa roho alionyesha majivuno na kimbelembele kwa kuthubutu kupinga enzi kuu ya Yehova, na kuwafanya watu wamwabudu yeye badala ya kumwabudu Mungu. Kwa hiyo, njia moja ya kumpinga Shetani ni kuepuka majivuno na kusitawisha unyenyekevu. (Soma 1 Petro 5:5.) Lakini majivuno ni nini? Je, ni vibaya kujivunia mambo ambayo sisi au watu wengine wametimiza?

5, 6. (a) Je, ni vibaya kujivunia mambo ambayo sisi au watu wengine wametimiza? Fafanua. (b) Kwa nini ni hatari kuwa na majivuno? Na kuna mifano gani ya Kimaandiko inayoonyesha jambo hilo?

5 Kulingana na kamusi moja, kujivunia ni “hali ya kujistahi na kujiheshimu,” na “hisia ya kuridhika unayopata kwa sababu wewe au watu wako wa karibu wanamiliki au wametimiza jambo fulani zuri.” Si vibaya kuhisi hivyo. Mtume Paulo aliwaambia hivi Wathesalonike: “Sisi wenyewe tunajivunia ninyi kati ya makutaniko ya Mungu kwa sababu ya uvumilivu wenu na imani katika mateso yenu yote na dhiki mnazovumilia.” (2 The. 1:4) Hivyo, si vibaya kufurahia mambo ambayo wengine wamefanya au kujivunia kwa kadiri fulani mambo tuliyotimiza. Mathalani, hatuhitaji kuionea aibu familia yetu, utamaduni wetu, au mahali tulipozaliwa.—Mdo. 21:39.

6 Kwa upande mwingine, majivuno yanaweza kuvuruga uhusiano wetu na wengine, na kuvunja urafiki wetu na Yehova. Badala ya kukubali ushauri kwa unyenyekevu, majivuno yanaweza kutufanya tukatae kushauriwa. (Zab. 141:5) Majivuno yanafafanuliwa kuwa “hisia za kujiona kuwa mtu wa maana sana,” au “mtazamo wa kiburi unaoonyeshwa na watu wanaoamini kwamba wao ni bora kuliko wengine.” Yehova anachukia kiburi. (Amo. 6:8) Lakini Shetani anafurahi sana wanadamu wanapojivuna kwa kiburi, kwa sababu yeye mwenyewe ana kiburi. Pasipo shaka, Shetani alishangilia sana watu kama Nimrodi, Farao, Absalomu, na wengine wengi walipojivuna kwa kiburi. (Mwa. 10:8, 9; Kut. 5:1, 2; 2 Sam. 15:4-6) Kiburi kilisababisha Kaini afanye dhambi. Mungu alimshauri Kaini lakini kwa kiburi alikataa kurekebishwa. Alikataa kwa ukaidi kutii onyo la Yehova, hivyo akamuua ndugu yake.—Mwa. 4:6-8.

7, 8. (a) Ubaguzi wa rangi ni nini, na unahusianaje na majivuno? (b) Fafanua jinsi majivuno yanavyoweza kuvuruga amani ya kutaniko.

7 Leo, watu huonyesha majivuno katika njia mbalimbali zisizofaa. Nyakati fulani majivuno huambatana na ubaguzi wa rangi. Kamusi moja inasema kwamba ubaguzi wa rangi ni “chuki au uadui dhidi ya watu wa rangi tofauti,” na “imani ya kwamba watu wa jamii nyingine wana sifa na uwezo tofauti, na kwamba kiasili jamii fulani ni bora zaidi au ni duni kuliko nyingine.” Ubaguzi wa rangi umesababisha ghasia, vita, au hata mauaji ya halaiki.

8 Bila shaka, mambo hayo hayapaswi kutendeka katika kutaniko la Kikristo. Mabishano kati ya waamini wenzetu, ambayo nyakati fulani huchochewa na majivuno, yanaweza kuwa makubwa kiasi cha kushindwa kudhibitiwa. Hali hiyo iliwapata Wakristo fulani katika karne ya kwanza, ndiyo sababu Yakobo aliwauliza hivi: “Vita vinatoka chanzo gani na mapigano yanatoka chanzo gani katikati yenu?” (Yak. 4:1) Hisia kali za chuki na kujiona kuwa bora kuliko wengine zinaweza kuathiri maneno na matendo yetu, na hivyo kuwaumiza wengine. (Met. 12:18) Kwa kweli, majivuno yanaweza kuvuruga amani ya kutaniko.

9. Biblia inatusaidiaje kushinda ubaguzi wa rangi na kuepuka majivuno? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 14.)

9 Ikiwa tuna mwelekeo wa kujiona kuwa bora kuliko wengine, tunahitaji kukumbuka kwamba “kila mtu mwenye kiburi moyoni ni chukizo kwa Yehova.” (Met. 16:5) Pia, ni vizuri tuchunguze maoni yetu kuhusu watu wa rangi, taifa, au utamaduni tofauti na wetu. Ikiwa tuna hisia za ubaguzi wa rangi au uzalendo, tutakuwa tunapuuza ukweli wa kwamba Mungu “alifanya kutoka kwa mtu mmoja kila taifa la watu.” (Mdo. 17:26) Kwa njia fulani, kuna jamii moja tu ya wanadamu kwa sababu wote tumetoka kwa mzazi wetu wa kwanza, Adamu. Hivyo, ni upumbavu kufikiri kwamba kiasili watu wa jamii fulani ni bora zaidi au ni duni kuliko watu wa jamii nyingine. Maoni kama hayo yatamsaidia Shetani kutimiza lengo lake la kuvuruga amani na umoja wa Kikristo. (Yoh. 13:35) Ili tumshinde Shetani, ni lazima tuepuke majivuno.—Met. 16:18.

EPUKA KUUPENDA ULIMWENGU NA VITU VYA KIMWILI

10, 11. (a) Kwa nini huenda ikawa rahisi kuanza kuupenda ulimwengu? (b) Huenda Dema alionyeshaje kwamba anaupenda ulimwengu?

10 Shetani ni “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yoh. 12:31; 1 Yoh. 5:19) Kwa hiyo, mambo mengi ambayo hutendeka katika ulimwengu huu hayapatani na viwango vya Biblia. Bila shaka, si kila kitu katika ulimwengu huu ni kibaya. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba Shetani anatumia ulimwengu wake kuchochea tamaa zetu ili tufanye dhambi, au tuupende ulimwengu na kupuuza ibada yetu kwa Yehova.—Soma 1 Yohana 2:15, 16.

11 Baadhi ya Wakristo wa karne ya kwanza waliupenda ulimwengu. Kwa mfano, Paulo aliandika hivi: “Dema ameniacha kwa sababu aliupenda mfumo wa mambo wa sasa.” (2 Tim. 4:10) Biblia haitaji jambo hususa ambalo Dema alilipenda katika ulimwengu, lililomfanya amwache Paulo. Huenda Dema alianza kupenda zaidi vitu vya kimwili kuliko mambo ya kiroho. Ikiwa ndivyo, basi alikosa baraka nyingi za kiroho! Je, ulimwengu ungeweza kumpa kitu chochote kinachozidi baraka ambazo Yehova angempa kwa kuandamana na Paulo?—Met. 10:22.

12. Tunawezaje kushawishiwa na “nguvu za udanganyifu wa utajiri”?

12 Jambo kama hilo linaweza kutupata sisi pia. Kwa kawaida, tunatamani kuandaa mahitaji yetu ya kimwili na ya familia yetu. (1 Tim. 5:8) Tunajua kwamba Yehova anataka tufurahie maisha, kwa kuwa alipowaumba Adamu na Hawa aliwaandalia mazingira yenye kuvutia sana. (Mwa. 2:9) Lakini Shetani anaweza kutushawishi kwa kutumia “nguvu za udanganyifu wa utajiri.” (Mt. 13:22) Watu wengi wanafikiri kwamba pesa na mali zitawafanya wawe na furaha au wafanikiwe. Mawazo hayo ni uwongo mtupu, na yanaweza kutufanya tupoteze kitu chenye thamani zaidi, yaani, urafiki wetu na Yehova. Yesu aliwaonya hivi wafuasi wake: “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamchukia mmoja na kumpenda yule mwingine, ama atashikamana na mmoja na kumdharau yule mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.” (Mt. 6:24) Ikiwa tunatumikia tu Utajiri, basi tutakuwa tumeacha kumtumikia Yehova, na hivyo ndivyo Shetani anataka tufanye! Tusiruhusu kamwe pesa au vitu vya kimwili viharibu urafiki wetu na Yehova. Ili kumshinda Shetani, tunapaswa kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu vitu vya kimwili.—Soma 1 Timotheo 6:6-10.

EPUKA UASHERATI

13. Ulimwengu huu una maoni gani yasiyofaa kuhusu ndoa?

13 Mtego mwingine wa ulimwengu wa Shetani ni uasherati. Leo, watu wengi wanaona kwamba kuwa mwaminifu kwa mwenzi wa ndoa, au hata kufunga ndoa, kumepitwa na wakati na kunawanyima uhuru. Kwa mfano, mwigizaji fulani maarufu wa kike alisema hivi: “Mtu hawezi kuwa na mwenzi mmoja tu wa ndoa. Sidhani kwamba kuna mtu yeyote ambaye ni mwaminifu au anataka kuwa mwaminifu kwa mwenzi wake.” Mwigizaji mwingine alisema: “Sidhani kwamba tumeumbwa ili tuwe na mwenzi mmoja tu katika maisha yetu yote.” Shetani anafurahi sana anapoona watu maarufu wakiidharau zawadi ya ndoa. Kwa kweli, Ibilisi haungi mkono hata kidogo mpango huo na wala hataki ufanikiwe. Hivyo, ili tumshinde Shetani, ni lazima tuheshimu mpango wa ndoa wa Mungu.

14, 15. Tunawezaje kuepuka uasherati?

14 Iwe tumefunga ndoa au la, tunapaswa kuepuka kabisa uasherati. Je, ni rahisi kufanya hivyo? Hapana! Kwa mfano, ikiwa wewe ni kijana, labda umewasikia wanafunzi wenzako wakijisifu kwa kufanya ngono ovyoovyo au kutumiana ujumbe mchafu wa ngono, jambo ambalo mahali pengine huonwa kuwa sawa na kusambaza ponografia ya watoto. Biblia inasema hivi: “Yeye aliye na mazoea ya kufanya uasherati anautendea dhambi mwili wake mwenyewe.” (1 Kor. 6:18) Watu wengi wanateseka na kufa kutokana na kuenea kwa magonjwa ya zinaa. Pia, vijana wengi waseja ambao wamepoteza ubikira wao wanasema kwamba wanajutia mambo waliyofanya. Matokeo ya uasherati ni tofauti kabisa na mambo yanayoonyeshwa katika vyombo vya habari ambavyo vinajaribu kutufanya tuamini kwamba kuvunja sheria za Mungu hakuna madhara. Maoni hayo huwafanya watu wanaswe na “nguvu za udanganyifu za dhambi.”—Ebr. 3:13.

15 Unapaswa kufanya nini unapokabili kishawishi cha kufanya uasherati? Tambua udhaifu wako. (Rom. 7:22, 23) Mwombe Mungu akupe nguvu. (Flp. 4:6, 7, 13) Epuka hali zinazoweza kukuongoza kwenye upotovu wa maadili. (Met. 22:3) Kishawishi kinapotokea, kipinge bila kukawia.—Mwa. 39:12.

16. Yesu alijibuje aliposhawishiwa na Shetani, na hilo linatufundisha nini?

16 Yesu alituwekea mfano bora sana katika kupinga vishawishi. Hakupumbazwa na ahadi za Shetani, wala hakutumia muda wake kufikiria faida na hasara za ahadi hizo. Badala yake, alijibu hivi mara moja: “Imeandikwa.” (Soma Mathayo 4:4-10.) Yesu alilijua Neno la Mungu, na hilo lilimsaidia kuchukua hatua mara moja kwa kutumia maandiko kupinga kishawishi. Ili tumshinde Shetani, ni lazima tuepuke uasherati.—1 Kor. 6:9, 10.

MSHINDE SHETANI KWA KUENDELEA KUVUMILIA

17, 18. (a) Shetani ana silaha gani nyingine, na kwa nini hilo halitushangazi? (b) Shetani atapatwa na nini, na hilo linakuchocheaje uendelee kuvumilia?

17 Majivuno, kupenda vitu vya kimwili, na uasherati ni baadhi tu ya silaha za Shetani. Ana silaha nyingine nyingi. Kwa mfano, Wakristo fulani wanapingwa na washiriki wa familia zao, wanadhihakiwa na wanafunzi wenzao, au serikali imewazuia kuhubiri. Hatushangai tunapopatwa na hali hizo ngumu, kwa sababu Yesu aliwaonya hivi wafuasi wake: “Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu; lakini yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”—Mt. 10:22.

Shetani ataharibiwa kabisa (Tazama fungu la 18)

18 Tunawezaje kumshinda Shetani? Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Kwa kuvumilia mtajipatia nafsi zenu.” (Luka 21:19) Mwanadamu hawezi kufanya jambo lolote linaloweza kutusababishia madhara ya kudumu. Hakuna anayeweza kuharibu urafiki wetu na Yehova isipokuwa sisi wenyewe tumruhusu afanye hivyo. (Rom. 8:38, 39) Hata watumishi wa Yehova wanapokufa haimaanishi kwamba Shetani ameshinda, kwa kuwa Yehova atahakikisha kwamba wanafufuliwa! (Yoh. 5:28, 29) Kwa upande mwingine, Shetani hana tumaini lolote. Baada ya kuharibiwa kwa watu wasiomwogopa Mungu, Shetani atafungwa ndani ya abiso kwa miaka 1,000. (Ufu. 20:1-3) Mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Yesu, Shetani “atafunguliwa kutoka katika gereza lake” kwa muda mfupi ili ajaribu kuwapotosha wanadamu wakamilifu kwa mara ya mwisho. Baada ya hapo, Ibilisi ataharibiwa. (Ufu. 20:7-10) Shetani anajua kabisa kwamba ataharibiwa, lakini sivyo ilivyo kwako! Chukua msimamo umpinge Shetani, ukiwa imara katika imani. Unaweza kumshinda Shetani!