Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ishi Kupatana na Sala ya Mfano—Sehemu ya Pili

Ishi Kupatana na Sala ya Mfano—Sehemu ya Pili

“Baba yenu anajua ni vitu gani mnavyohitaji.”—MT. 6:8.

1-3. Kwa nini Lana alikuwa na uhakika kwamba Yehova anajua mahitaji yetu?

LANA hatasahau kamwe mambo yaliyotokea alipokuwa nchini Ujerumani mwaka 2012. Anahisi kwamba sala zake mbili zilijibiwa. Alitoa sala ya kwanza alipokuwa ndani ya treni akielekea uwanja wa ndege. Alimwomba Yehova amsaidie kutoa ushahidi. Alitoa sala ya pili baada ya kufika uwanja wa ndege na kujulishwa kwamba safari yake imeahirishwa hadi siku iliyofuata. Lana alimwomba Yehova amsaidie kwa kuwa hakuwa na pesa za kutosha wala mahali pa kulala.

2 Mara tu baada ya kumaliza sala yake ya pili, alimsikia kijana mmoja akimwambia, “Habari Lana, unafanya nini hapa?” Kijana huyo alikuwa mwanafunzi mwenzake wa zamani! Mama na nyanya yake walikuwa wamemsindikiza kwa kuwa alikuwa anaelekea Afrika Kusini. Lana alipowaeleza hali yake, Elke, mama ya kijana huyo alimkaribisha nyumbani kwake. Elke na mama yake walikuwa wakarimu sana, na walimuuliza Lana maswali mengi kuhusu imani yake na kazi yake ya upainia.

3 Baada ya kupata kiamsha kinywa asubuhi ya siku iliyofuata, Lana aliwajibu maswali mengine mengi kuhusu Biblia, na akawaomba anwani zao ili apange mtu fulani aendelee kujibu maswali yao. Lana alifika nyumbani salama salimini na anaendelea kufanya upainia wa kawaida. Anahisi kwamba “msikiaji wa sala” alijua mambo aliyohitaji, na alimsaidia.—Zab. 65:2.

4. Tutazungumzia mahitaji gani?

4 Inaweza kuwa rahisi kumwomba Yehova msaada tunapokabili tatizo fulani bila kutazamia, naye hufurahi kusikiliza maombi hayo ya watumishi wake waaminifu. (Zab. 34:15; Met. 15:8) Hata hivyo, tunapotafakari sala ya mfano, huenda tukaona kwamba kuna mahitaji mengine muhimu ambayo hatuyataji katika sala zetu. Katika makala hii tutazungumzia maombi manne ya mwisho. Tunapofanya hivyo, fikiria jinsi maombi matatu ya mwisho yanavyofunua mahitaji yetu ya kiroho, na pia jinsi tunavyoweza kuishi kupatana na ombi la nne linalohusu mkate wetu wa kila siku.—Soma Mathayo 6:11-13.

“UTUPE LEO MKATE WETU KWA AJILI YA SIKU HII”

5, 6. Kwa nini ni muhimu tuombe “mkate wetu” wa kila siku hata kama tuna chakula cha kutosha?

5 Ona kwamba Yesu hakutufundisha tuombe mkate “wangu” wa kila siku, bali mkate “wetu” wa kila siku. Victor, mwangalizi wa mzunguko barani Afrika, anaeleza hivi: “Mara nyingi ninamshukuru sana Yehova kwa kuwa mimi na mke wangu hatuhitaji kuhangaikia chakula au kodi ya nyumba. Kila siku ndugu zetu wanatutunza kwa upendo. Hata hivyo, ninasali kwamba wale wanaotusaidia wafanikiwe kushughulikia matatizo ya kiuchumi wanayokabili.”

6 Huenda tuna chakula cha kutosha, lakini ndugu zetu wengi ni maskini au wameathiriwa na majanga. Tunapaswa kusali kwa ajili yao na kutenda kupatana na sala hizo. Kwa mfano, ikiwa tuna vitu fulani tunaweza kuwasaidia waabudu wenzetu wenye uhitaji. Pia, tunaweza kuchangia kwa ukawaida kazi ya ulimwenguni pote, tukijua kwamba pesa hizo hutumiwa kwa hekima.—1 Yoh. 3:17.

7. Yesu alitumia mfano gani ili kukazia ushauri wake, “msihangaike kamwe juu ya kesho”?

7 Inaelekea Yesu alikuwa akizungumzia mahitaji yetu ya msingi alipokuwa akifundisha kuhusu kuomba mkate wa kila siku. Alionyesha namna ambavyo Mungu huyavisha maua ya porini, kisha akasema hivi: “Je, yeye hataona ni afadhali zaidi awavike, ninyi wenye imani kidogo? Kwa hiyo msihangaike kamwe na kusema, . . . ‘Tutavaa nini?’” Akamalizia kwa kurudia ushauri huu muhimu: “Msihangaike kamwe juu ya kesho.” (Mt. 6:30-34) Jambo hilo linaonyesha kwamba tunapaswa kuridhika na mahitaji yetu ya kila siku badala ya kufuatilia vitu vya kimwili. Mahitaji hayo huenda yakatia ndani mahali pa kuishi, kazi itakayotusaidia kuiruzuku familia yetu, na hekima ya kufanya uamuzi mzuri kuhusiana na afya. Hata hivyo, mbali na kumwomba Yehova atutimizie mahitaji yetu ya kimwili, tunapaswa kusali pia kuhusu mahitaji yetu ya kiroho ambayo ni muhimu hata zaidi.

8. Maneno ya Yesu kuhusu mkate wetu wa kila siku yanapaswa kutukumbusha nini? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 25.)

8 Maneno ya Yesu kuhusu mkate wetu wa kila siku yanapaswa kutukumbusha uhitaji wetu wa chakula cha kiroho. “Mwanadamu ataishi,” akasema Bwana wetu, “si kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mt. 4:4) Hivyo, sikuzote tunapaswa kumwomba Yehova aendelee kutulisha chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa.

“UTUSAMEHE MADENI YETU”

9. Kwa nini dhambi zetu ni kama “madeni”?

9 Kwa nini Yesu alitumia neno “madeni,” ilhali wakati mwingine alitumia neno “dhambi”? (Mt. 6:12; Luka 11:4) Zaidi ya miaka 60 iliyopita, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilifafanua kwamba tunapotenda dhambi, ni kana kwamba tunadaiwa na Yehova. Tuna wajibu wa kumpenda na kumtii Yehova. Kwa hiyo, tunapomtendea dhambi Mungu, tunakuwa tumeshindwa kutimiza wajibu wetu. Yehova akitaka, anaweza kuondoa amani yake na kuvunja urafiki wetu pamoja naye. Gazeti hilo liliongeza hivi: “Kutenda dhambi humaanisha kwamba hatumpendi Mungu.”—1 Yoh. 5:3.

10. Yehova anatusamehe kwa msingi gani, na tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu jambo hilo?

10 Tunamshukuru sana Yehova kwa kutupatia njia ya pekee ya kusamehe dhambi zetu, yaani, dhabihu ya fidia ya Yesu. Ingawa fidia hiyo ilitolewa karibu miaka 2,000 iliyopita, tunapaswa kuithamini sana kana kwamba ni zawadi tuliyopewa leo. Hiyo ni zawadi “yenye thamani sana,” kwa kuwa hakuna mwanadamu angeweza kulipa fidia tunayohitaji ili tuwekwe huru kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo. (Soma Zaburi 49:7-9; 1 Petro 1:18, 19.) Pia, maneno “dhambi zetu,” na si “dhambi zangu,” yanapaswa kutukumbusha kwamba sisi sote tunahitaji zawadi hiyo ya fidia. Ni wazi kwamba Yehova anataka tufikirie si tu hali yetu ya kiroho, bali pia hali ya kiroho ya wengine, kutia ndani wale ambao wametukosea. Kwa kawaida makosa hayo huwa madogo, na yanatupatia nafasi ya kuonyesha kwamba tunawapenda kikweli ndugu zetu, na tuko tayari kuwasamehe, kama vile ambavyo Mungu hutusamehe kwa hiari.—Kol. 3:13.

Ili Mungu akusamehe, unapaswa kuwa tayari kuwasamehe wengine (Tazama fungu la 11)

11. Kwa nini ni muhimu kuwa tayari kuwasamehe wengine?

11 Inasikitisha kwamba kwa sababu ya kutokamilika, huenda nyakati nyingine tukawawekea kinyongo wale waliotukosea. (Law. 19:18) Tukianza kuongea na wengine kuhusu jambo hilo, huenda baadhi yao wakatuunga mkono, na hivyo kusababisha mgawanyiko kutanikoni. Tukiruhusu hali hiyo iendelee, tutakuwa tunaonyesha wazi kwamba hatuthamini rehema za Mungu na zawadi ya fidia. Tusipokuwa na utayari wa kusamehe, Baba yetu hatatusamehe dhambi zetu kwa msingi wa dhabihu ya Mwana wake. (Mt. 18:35) Yesu alifafanua jambo hilo mara tu alipomaliza sala yake ya mfano. (Soma Mathayo 6:14, 15.) Mwishowe, ili tunufaike na msamaha wa Mungu, ni lazima tujitahidi kuepuka mazoea ya kufanya dhambi nzito. Tamaa yetu ya kuepuka mazoea ya kufanya dhambi ndiyo msingi wa ombi linalofuata.—1 Yoh. 3:4, 6.

“USITUINGIZE KATIKA JARIBU”

12, 13. (a) Ni nini kilichotokea muda mfupi baada ya Yesu kubatizwa? (b) Kwa nini hatupaswi kuwalaumu wengine ikiwa tumekubali kushawishika? (c) Yesu alitimiza nini kwa kuwa mwaminifu mpaka kifo?

12 Kufikiria kile kilichomtokea Yesu muda mfupi baada ya kubatizwa, kunaweza kutusaidia tuelewe umuhimu wa ombi hili: “Usituingize katika jaribu.” Yesu aliongozwa na roho ya Mungu kuingia nyikani. Kwa nini? “Ili kujaribiwa na Ibilisi.” (Mt. 4:1; 6:13) Je, tushangazwe na jambo hilo? Hapana. Inafaa tuelewe sababu kuu iliyomfanya Mungu amtume Mwana wake duniani. Yesu alitumwa duniani ili kutatua suala lililozushwa wakati Adamu na Hawa walipoikataa enzi kuu ya Mungu. Maswali yaliyozushwa yalihitaji wakati ili kujibiwa. Kwa mfano, je, kulikuwa na tatizo kuhusiana na jinsi Mungu alivyomuumba mwanadamu? Je, mwanadamu mkamilifu angeweza kuunga mkono enzi kuu ya Mungu licha ya kushawishiwa na “yule mwovu”? Na je, mwanadamu ana uwezo wa kujitawala, kama Shetani alivyodai? (Mwa. 3:4, 5) Bila shaka, wakati ulihitajika ili kujibu maswali hayo. Isitoshe, kujibiwa kwa maswali hayo kungewaonyesha wazi viumbe wote wenye akili kwamba utawala wa Yehova ndio bora zaidi.

13 Yehova ni mtakatifu, hivyo hamjaribu yeyote kwa mambo maovu. Badala yake, Ibilisi ndiye “Mjaribu.” (Mt. 4:3) Ibilisi anaweza kutujaribu katika njia mbalimbali. Hata hivyo, kila mmoja wetu ana uhuru wa kuchagua kukubali au kupinga kishawishi. (Soma Yakobo 1:13-15.) Yesu alipokuwa akishawishiwa na Shetani, alipinga mara moja kila kishawishi kwa kunukuu Neno la Mungu. Hivyo, Yesu aliitetea enzi kuu ya Mungu. Lakini Shetani hakukata tamaa. Alisubiri “mpaka wakati mwingine unaofaa.” (Luka 4:13) Yesu aliendelea kumpinga Shetani na kumtii Mungu akiwa Mtawala wake. Alitetea uadilifu wa enzi kuu ya Yehova na kuthibitisha kwamba mwanadamu mkamilifu anaweza kuwa mwaminifu hata anapokabili jaribu kali sana. Hata hivyo, Shetani anajaribu kuwanasa wafuasi wa Yesu, kutia ndani wewe.

14. Tunapaswa kufanya nini ili tusiingie katika kishawishi?

14 Kwa kuwa maswali yaliyozuka kuhusu enzi kuu ya Mungu bado yanahitaji kujibiwa, Yehova amemruhusu Mjaribu atumie ulimwengu wake kutushawishi. Yehova hatuingizi katika majaribu. Badala yake, ana uhakika kwamba tunaweza kuwa waaminifu na anataka kutusaidia. Hata hivyo, kwa kuwa Yehova anaheshimu uhuru wetu wa kuchagua, anaturuhusu tujiamulie wenyewe ikiwa tunataka kuwa waaminifu au la. Tunapaswa kufanya mambo mawili: kuwa macho kiroho na kudumu katika sala. Yehova anajibuje sala zetu?

Endelea kuwa mtu wa kiroho na mwenye bidii katika huduma (Tazama fungu la 15)

15, 16. (a) Tunapaswa kupinga vishawishi gani? (b) Ni nani anayepaswa kulaumiwa tukikubali kushawishika?

15 Yehova hutupatia roho yake takatifu ili kutuimarisha na kutusaidia tushinde vishawishi. Pia, Mungu anatuonya kupitia Neno lake na kutaniko kuhusu hali ambazo ni lazima tuziepuke, kama vile kutumia wakati, pesa, na nguvu nyingi katika mambo yasiyo ya lazima. Espen na Janne wanaishi katika nchi tajiri barani Ulaya. Kwa miaka mingi, walitumikia wakiwa mapainia wa kawaida katika eneo lililokuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme nchini mwao. Walilazimika kuacha upainia walipopata mtoto wa kwanza, na sasa wana watoto wawili. Espen anasema hivi: “Tunasali kwa Yehova mara kwa mara ili tusiingie katika kishawishi, kwa kuwa sasa hatuwezi kutumia muda mwingi katika utendaji wa kitheokrasi kama ilivyokuwa zamani. Tunamwomba Yehova atusaidie tuendelee kuwa watu wa kiroho na wenye bidii katika huduma.”

16 Kishawishi kingine ambacho kimewanasa watu wengi sana katika siku za karibuni ni kutazama ponografia. Hatupaswi kumlaumu Shetani ikiwa tumeshawishika kutazama ponografia. Kwa nini? Kwa sababu Shetani na ulimwengu wake hauwezi kutulazimisha tufanye jambo lolote lisilofaa. Baadhi ya watu hutazama ponografia kwa sababu wameruhusu akili yao itafakari mambo yasiyofaa. Hata hivyo, tunaweza kupinga kishawishi hicho, kama vile ambavyo maelfu ya ndugu na dada zetu wamefanya.—1 Kor. 10:12, 13.

“UTUKOMBOE KUTOKANA NA YULE MWOVU”

17. (a) Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaishi kupatana na ombi letu: “Utukomboe kutokana na yule mwovu”? (b) Tutapata faraja gani hivi karibuni?

17 Ili tuishi kupatana na ombi letu: “Utukomboe kutokana na yule mwovu,” ni lazima tujitahidi sikuzote kutokuwa ‘sehemu ya ulimwengu wa Shetani.’ Hatupaswi ‘kuupenda ulimwengu wa Shetani au vitu vilivyo katika ulimwengu.’ (Yoh. 15:19; 1 Yoh. 2:15-17) Tutafarijika sana Yehova atakapojibu ombi letu kwa kumharibu Shetani na ulimwengu wake mwovu! Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba Shetani alipofukuzwa mbinguni, alijua kuwa muda wake ni mfupi. Kwa kuwa ana ghadhabu kubwa, anafanya yote anayoweza ili avunje uaminifu wetu. Kwa hiyo, ni lazima tuendelee kuomba tukombolewe kutokana na mwovu huyo.—Ufu. 12:12, 17.

18. Tunapaswa kufanya nini ili tuokoke ulimwengu wa Shetani utakapoharibiwa?

18 Je, unatamani kuishi katika ulimwengu mpya? Basi endelea kusali Ufalme wa Mungu uje ili kulitakasa jina la Mungu na kufanya mapenzi yake yatendeke duniani. Mtegemee Yehova ili akutunze kiroho na kimwili. Naam, azimia kuishi kupatana na sala ya mfano.