Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunaweza Kuwa Safi Kiadili

Tunaweza Kuwa Safi Kiadili

“Safisheni mikono yenu, . . . na takaseni mioyo yenu.” —YAK. 4:8.

1. Ulimwengu unaonaje usafi wa kiadili?

TUNAISHI katika ulimwengu usiopenda usafi wa kiadili. Katika nchi nyingi, watu huona kufanya ngono nje ya ndoa na ushoga kuwa mambo ya kawaida. Sinema, vitabu, nyimbo, na matangazo yamejaa mambo hayo. (Zab. 12:8) Uasherati umeenea sana hivi kwamba huenda ukajiuliza, ‘Je, kweli inawezekana kuendelea kuwa safi kiadili?’ Tunaweza kujibu hivi kwa uhakika: Ndiyo, kwa msaada wa Yehova, Wakristo wa kweli wanaweza kuendelea kuwa safi kiadili.—Soma 1 Wathesalonike 4:3-5.

2, 3. (a) Kwa nini ni muhimu tupinge tamaa mbaya? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Kwanza, tunapaswa kutambua kwamba ili tuishi maisha safi kiadili, ni lazima tupinge tamaa zisizofaa. Lakini kwa sababu sisi si wakamilifu, tunaweza kuvutiwa na ukosefu wa maadili kama ambavyo samaki huvutiwa na chambo katika ndoano. Tukianza kuwa na mawazo mapotovu, ni lazima tuyaondoe mara moja. Tusipofanya hivyo, tamaa zilizopotoka zinaweza kuwa na nguvu sana hivi kwamba tunaweza kufanya dhambi nafasi ikijitokeza. Ni kama tu Biblia inavyosema: “Tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi.”—Soma Yakobo 1:14, 15.

3 Tunaona uzito wa jambo hilo tunapofikiria jinsi tamaa za muda mfupi zinavyoweza kutuongoza tufanye dhambi nzito. Lakini inatia moyo sana kujua kwamba tukiondoa tamaa mbaya mioyoni mwetu, tutaepuka uasherati na madhara yake. (Gal. 5:16) Acheni tuchunguze mambo matatu yanayoweza kutusaidia tushinde tamaa mbaya: uhusiano wetu na Yehova, ushauri wa Neno lake, na msaada kutoka kwa Wakristo wakomavu.

‘MKARIBIE MUNGU’

4. Kwa nini ni muhimu kumkaribia Yehova?

4 Biblia inawahimiza hivi wale wanaotaka kumkaribia Mungu: “Safisheni mikono yenu, . . . na takaseni mioyo yenu.” (Yak. 4:8) Ikiwa tunathamini urafiki wetu na Yehova, tutajitahidi kumpendeza katika kila sehemu ya maisha yetu, kutia ndani mawazo yetu. Tunaonyesha tunatamani kuwa “safi moyoni” kwa kukazia fikira mambo yaliyo safi kiadili, mema, na yanayostahili sifa. (Zab. 24:3, 4; 51:6; Flp. 4:8) Yehova anaelewa hali yetu ya kutokamilika. Anajua tuna mwelekeo wa kutamani mambo yasiyofaa. Hata hivyo, tunatambua kwamba tunamhuzunisha tunapoendelea kufikiria mambo yasiyofaa badala ya kufanya juu chini kuyaondoa mawazo hayo. (Mwa. 6:5, 6) Kutafakari jambo hilo kunatufanya tuazimie hata zaidi kufikiria mambo safi kiadili.

5, 6. Sala inaweza kutusaidiaje kushinda tamaa zisizofaa?

5 Njia muhimu ya kuonyesha tunamtegemea kabisa Yehova ni kusali ili atusaidie kupambana na mawazo yasiyofaa. Tunapomkaribia Yehova katika sala, yeye pia anatukaribia. Anatupatia roho yake takatifu ili tuweze kupinga mawazo mapotovu na kuendelea kuwa safi kiadili. Hivyo, katika sala zetu tumweleze Yehova kuwa tunatamani sana kumpendeza kupitia mawazo yetu. (Zab. 19:14) Je, tunamwomba kwa unyenyekevu atuchunguze ili aone kama kuna “njia yoyote yenye kuumiza,” yaani, mwelekeo au tamaa zozote zisizofaa, ambazo zinaweza kutuchochea tufanye dhambi? (Zab. 139:23, 24) Je, tunamwomba Yehova atusaidie kudumisha uaminifu wetu tunapokabili kishawishi?—Mt. 6:13.

6 Malezi yetu au mwenendo wetu wa zamani unaweza kutufanya tupende mambo yanayomchukiza Yehova. Hata hivyo, Yehova anaweza kutusaidia tubadilike ili tuendelee kumtumikia kwa njia anayokubali. Mfalme Daudi alitambua jambo hilo. Baada ya kufanya uzinzi na Bath-sheba, Daudi alimsihi hivi Yehova: “Uumbe moyo safi ndani yangu, . . . na kuweka ndani yangu roho mpya, iliyo imara.” (Zab. 51:10, 12) Mwili wetu usio mkamilifu unaweza kuvutiwa kufanya dhambi, lakini Yehova anaweza kutuchochea tuwe na tamaa ya kumtii. Hata ikiwa tamaa zisizofaa zimetia mizizi na kutuzuia tusifikirie mambo safi kiadili, Yehova anaweza kutuongoza ili tutii sheria zake na kuishi kupatana nazo. Anaweza kutusaidia tusitawaliwe na mawazo yasiyofaa.—Zab. 119:133.

Tamaa mbaya ikianza kusitawi na kutia mizizi moyoni, tunahitaji kuing’oa mara moja (Tazama fungu la 6)

“IWENI WATENDAJI WA NENO”

7. Neno la Mungu linawezaje kutulinda kutokana na mawazo yasiyofaa?

7 Yehova anaweza kujibu maombi yetu kupitia Neno lake, Biblia. Hekima iliyo katika Neno la Mungu “kwanza kabisa ni safi kiadili.” (Yak. 3:17) Kusoma Biblia kila siku na kutafakari yale tunayosoma kunaweza kulinda akili zetu zisifikirie mambo yasiyofaa. (Zab. 19:7, 11; 119:9, 11) Pia, Biblia ina mifano na ushauri unaoweza kutusaidia kuepuka tamaa mbaya.

8, 9. (a) Ni nini kilichomfanya kijana fulani afanye uasherati na mwanamke mwenye ukosefu wa maadili? (b) Tunawezaje kutii onyo lililo kwenye Methali sura ya 7?

8 Andiko la Methali 5:8, linasema hivi: “Itenge njia yako mbali naye [mwanamke mwenye ukosefu wa maadili]; wala usiukaribie mlango wa nyumba yake.” Hatari ya kupuuza onyo hilo inaonyeshwa kwenye Methali sura ya 7, ambapo tunasoma kuhusu mwanaume kijana anayepita karibu na nyumba ya mwanamke mwenye ukosefu wa maadili giza linapoanza kuingia. Akiwa barabarani, anafuatwa na mwanamke ambaye amevaa kama kahaba. Mwanamke huyo anamshika na kumbusu. Maneno yake yenye ushawishi yanaamsha tamaa ambayo anaona hawezi kuipinga. Mwishowe wanafanya uasherati. Ni wazi kwamba kijana huyo hakuwa amepanga kufanya uasherati. Hana uzoefu na uwezo wa kufanya uamuzi mzuri. Hata hivyo, atalazimika kukabiliana na matokeo mabaya ya matendo yake. Laiti angemwepuka kabisa mwanamke huyo!—Met. 7:6-27.

9 Je, inawezekana nyakati nyingine tunafanya uamuzi usiofaa kama kijana huyo, labda kwa kujiruhusu kuwa katika hali hatari zinazoweza kuamsha tamaa mbaya? Kwa mfano, nyakati za usiku, vituo vya televisheni vinaweza kuonyesha vipindi vyenye mambo mapotovu. Vipi ikiwa tunabadili-badili vituo vya televisheni wakati huo? Au labda tunaweza kubonyeza viunganishi kwenye Intaneti ambavyo hatujui vitatupeleka wapi, au kutembelea vituo vya maongezi na tovuti zenye mialiko ya kutazama ponografia au huduma nyingine zinazohusiana na mambo ya ngono. Je, si ni kweli kwamba katika hali hizo huenda tukakutana na mambo yanayoweza kuamsha tamaa zisizofaa na kudhoofisha azimio letu la kuendelea kuwa safi kiadili?

10. Kwa nini ni hatari kuwachezea wengine kimapenzi? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 13.)

10 Pia, Biblia inatushauri kuhusu jinsi tunavyopaswa kuwatendea watu wa jinsia tofauti. (Soma 1 Timotheo 5:2.) Ni wazi kwamba ushauri huo unakataza kabisa kuwachezea wengine kimapenzi. Huenda wengine wakafikiri kuwa si vibaya kuwaonyesha wengine hisia za kimapenzi kupitia ishara za mwili na kutazamana ilimradi hawagusani. Lakini kuwachezea wengine kimapenzi, au kukubali kuchezewa kimapenzi, kunaweza kuamsha mawazo yasiyofaa yanayoweza kumwongoza mtu kufanya uasherati. Iliwahi kutokea, na inaweza kutokea tena.

11. Yosefu aliweka mfano gani mzuri?

11 Yosefu alitenda kwa hekima kuhusiana na jambo hilo. Mke wa Potifa alipojaribu kumshawishi, Yosefu alikataa. Lakini mwanamke huyo hakukata tamaa. Siku baada ya siku alimshawishi awe pamoja naye. (Mwa. 39:7, 8, 10) Kulingana na msomi mmoja wa Biblia ni kama mke wa Potifa alikuwa akisema hivi: “‘Acha tuwe pamoja peke yetu kwa muda mfupi tu,’ akitumaini kuwa [Yosefu] ataanza kumtamani.” Hata hivyo, Yosefu aliazimia kutomruhusu mwanamke huyo amshawishi. Alikataa kuchezewa kimapenzi, na hakumchezea kimapenzi mwanamke huyo. Kwa hiyo, hakuruhusu tamaa zozote mbaya zitie mizizi moyoni mwake. Alipolazimishwa kufanya ngono, Yosefu alichukua hatua mara moja. “Akaliacha vazi lake mkononi mwake, akakimbia na kwenda nje.”—Mwa. 39:12.

12. Tunajuaje kwamba mambo tunayotazama yanaweza kuathiri moyo wetu?

12 Isitoshe, Biblia inatuonya kuhusu hatari ya kuruhusu macho yetu yapotoshe moyo wetu. Jicho linalotangatanga linaweza kuamsha au kuchochea tamaa mbaya za ngono. Yesu alionya kuwa “kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mt. 5:28) Kumbuka kilichotokea katika kisa cha Mfalme Daudi. “Kutoka juu ya dari [Daudi] akamwona mwanamke akioga.” (2 Sam. 11:2) Alishindwa kutazama pembeni na kuanza kufikiria mambo mengine. Jambo hilo lilimfanya amtamani mke wa mtu mwingine na kufanya naye uzinzi.

13. Kwa nini tunapaswa ‘kufanya agano na macho yetu,’ na tunawezaje kufanya hivyo?

13 Ili kuepuka kuwazawaza mambo machafu, tunahitaji ‘kufanya agano na macho yetu,’ kama alivyofanya Ayubu mwaminifu. (Ayu. 31:1, 7, 9) Tunapaswa kuazimia kudhibiti macho yetu na kutoyaruhusu yamtazame mtu mwingine kwa kutamani kufanya naye ngono. Pia, hatupaswi kuruhusu macho yetu yatazame picha za ngono, iwe katika kompyuta, bango la matangazo, jalada la gazeti, au sehemu nyingine yoyote.

14. Tunapaswa kufanya nini ili tuendelee kuwa safi kiadili?

14 Ikiwa kuna jambo lolote kati ya yale ambayo yametajwa unalohitaji kufanyia kazi ili ushinde tamaa mbaya, chukua hatua mara moja. Tii kwa hiari ushauri wa Neno la Mungu ambao unaweza kukusaidia uepuke kufanya dhambi, na hivyo uendelee kuwa safi kiadili.—Soma Yakobo 1:21-25.

‘WAITE WAZEE’

15. Ikiwa tunapambana na tamaa mbaya, kwa nini ni muhimu kutafuta msaada kutoka kwa Wakristo wenzetu?

15 Wakristo wenzetu wanaweza pia kutusaidia kupambana na tamaa mbaya za ngono. Bila shaka, si rahisi kuzungumza na wengine kuhusu matatizo kama hayo, lakini ni muhimu sana kufanya hivyo. (Met. 18:1; Ebr. 3:12, 13) Kuzungumzia udhaifu wetu na Mkristo mkomavu kiroho kunaweza kutusaidia kutambua marekebisho tunayohitaji kufanya. Jambo hilo linaweza kutusaidia tufanye mabadiliko yanayohitajika ili tubaki katika upendo wa Yehova.

16, 17. (a) Wazee wanaweza kuwasaidiaje wale wanaopambana na tamaa mbaya? Toa mfano. (b) Kwa nini wale wenye mazoea ya kutazama ponografia wanapaswa kutafuta msaada haraka?

16 Wazee Wakristo hasa ndio wanaostahili kutusaidia. (Soma Yakobo 5:13-15.) Kijana fulani nchini Brazili alipambana na tamaa mbaya kwa miaka mingi. Anaeleza: “Nilijua kuwa mawazo yangu yalimchukiza Yehova, lakini niliona aibu kuwaeleza wengine hisia zangu.” Jambo zuri ni kwamba mzee aliyemjali katika kutaniko lake alimfuata na kumtia moyo atafute msaada. Kijana huyo anakumbuka hivi: “Nilishangaa sana jinsi wazee walivyonitendea, walielewa hali yangu na walikuwa wenye fadhili sana kuliko nilivyofikiri. Walinisikiliza kwa makini nilipowaeleza matatizo yangu. Walitumia Biblia kunihakikishia kuwa Yehova ananipenda, na walisali pamoja nami. Hilo lilifanya iwe rahisi kwangu kukubali ushauri wa Biblia walionipa.” Baada ya kufanya maendeleo ya kiroho, anasema hivi: “Sasa ninatambua umuhimu wa kutafuta msaada badala ya kubeba mizigo peke yetu.”

17 Ni muhimu sana kutafuta msaada ikiwa tamaa mbaya zinatokana na mazoea ya kutazama ponografia. Kadiri mtu anavyochelewa kuomba msaada, ndivyo kunavyokuwa na uwezekano mkubwa wa tamaa mbaya ‘kutunga mimba na kuzaa dhambi’ inayoweza kuwaumiza wengine na kuliletea suto jina la Yehova. Tamaa ya kumfurahisha Yehova na kubaki katika kutaniko la Kikristo imewachochea watumishi wengi wa Yehova wakubali msaada wanaopewa kwa upendo.—Yak. 1:15; Zab. 141:5; Ebr. 12:5, 6.

AZIMIA KUENDELEA KUWA SAFI KIADILI!

18. Umeazimia kufanya nini?

18 Maadili ya ulimwengu wa Shetani yanapozidi kuporomoka, Yehova anajivunia kuwa na watumishi wanaojitahidi sana kufikiria mambo safi na kushika viwango vyake vya juu vya maadili. Hivyo basi, acheni kila mmoja wetu aazimie kumkaribia Yehova na kukubali mwongozo anaotoa kupitia Neno lake na kutaniko la Kikristo. Tukiendelea kuwa safi kiadili tutaridhika na kuwa na amani ya akili. (Zab. 119:5, 6) Wakati ujao, baada ya Shetani kuondolewa, tutapata nafasi ya kuishi milele katika ulimwengu ulio safi kiadili.