Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mnahitaji Kuwa na Uvumilivu”

“Mnahitaji Kuwa na Uvumilivu”

BAADA ya Anita * kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, mume wake alimpinga vikali. Anita anasema hivi: “Alinikataza kwenda kwenye mikutano na alinizuia hata kutaja jina la Mungu.” Anaongezea, “Kutaja tu jina Yehova kulimkasirisha sana mume wangu.”

Haikuwa rahisi kwake kuwafundisha watoto wake kumhusu Yehova. “Ibada ya Yehova ilipigwa marufuku nyumbani kwangu mwenyewe. Sikuwa na uhuru wa kuwafundisha watoto wangu, au kwenda nao mikutanoni.”

Kama kisa cha Anita kinavyoonyesha, upinzani kutoka kwa watu wa familia unaweza kujaribu uaminifu wa Mkristo. Inaweza kuwa hivyo pia afya ya Mkristo inapodhoofika, mtoto au mwenzi wa ndoa anapokufa, au mshiriki wa karibu wa familia anapomwacha Yehova. Hivyo basi, ni nini kinachoweza kumsaidia Mkristo aendelee kuwa mwaminifu kwa Yehova?

Majaribu kama hayo yanapotokea, unaweza kufanya nini? Mtume Paulo alisema: “Mnahitaji kuwa na uvumilivu.” (Ebr. 10:36) Ni nini kinachoweza kukusaidia uvumilie?

MWOMBE YEHOVA AKUSAIDIE

Njia moja kuu inayotusaidia tupate nguvu za kuvumilia majaribu ni kusali kwa Mungu. Fikiria mfano mmoja. Familia ya Ana ilipatwa na msiba siku ya Jumatatu mchana. Mume wake ambaye aliishi naye kwa miaka 30, alikufa ghafla. “Hakurudi nyumbani kutoka kazini,” anasema Ana, “na alikuwa na umri wa miaka 52 tu.”

Ana alikabilianaje na hali hiyo? Alirudi tena kazini, na jambo hilo lilimsaidia kwa sababu kazi yake ilimfanya awe na shughuli nyingi sana. Hata hivyo, kazi hiyo haikumwondolea huzuni aliyokuwa nayo. Anaeleza hivi: “Nilimmiminia Yehova moyo wangu na kumwomba anisaidie kukabiliana na huzuni yangu.” Je, Yehova alijibu sala zake? Anasadiki kabisa kuwa Yehova alifanya hivyo. Anasema: “Amani ambayo ni Mungu tu anaweza kuitoa ilituliza nafsi yangu na kulinda akili yangu. Sina shaka kwamba Yehova atamfufua mume wangu.”—Flp. 4:6, 7.

“Msikiaji wa sala” ameahidi kuwapa watumishi wake chochote wanachohitaji ili waendelee kuwa waaminifu kwake. (Zab. 65:2) Je, hukubali kwamba ahadi hiyo inaimarisha imani? Je, ahadi hiyo haikuhakikishii kwamba wewe pia unaweza kuvumilia?

MIKUTANO YA KIKRISTO —CHANZO CHA MSAADA

Yehova anawategemeza watu wake kupitia kutaniko la Kikristo. Kwa mfano, kutaniko la Thesalonike lilipopata mateso makali, Paulo aliwasihi Wakristo hao ‘waendelee kufarijiana na kujengana, kama vile walivyokuwa wakifanya.’ (1 The. 2:14; 5:11) Wakristo wa Thesalonike waliweza kuvumilia majaribu ya imani kwa sababu walipendana na kusaidiana. Uaminifu wao ni mfano mzuri kwetu na unaonyesha jambo linaloweza kutusaidia tuvumilie.

Kuwa na urafiki wa karibu na washiriki wa kutaniko kutatusaidia tufanye “mambo ambayo ni ya kujengana.” (Rom. 14:19) Jambo hilo ni muhimu hasa wakati wa matatizo. Paulo alipata taabu nyingi, na Yehova alimpa nguvu za kuvumilia. Nyakati nyingine, Mungu alimtia moyo Paulo kupitia waumini wenzake. Kwa mfano, Paulo alipowatumia salamu washiriki wa kutaniko la Kolosai, alisema hivi kuwahusu: “Hawa ndio wamekuwa msaada wenye kunitia nguvu.” (Kol. 4:10, 11) Kwa kweli, upendo wao kwa Paulo uliwasukuma wamfariji na kumtia nguvu alipokuwa na matatizo. Inawezekana wewe pia umetiwa moyo na kutegemezwa na washiriki wa kutaniko lako.

MSAADA KUTOKA KWA WAZEE WA KUTANIKO

Mungu ametupatia msaada mwingine katika kutaniko la Kikristo, yaani, wazee. Wanaume hao wa kiroho wanaweza kuwa “kama mahali pa kujificha kutokana na upepo na mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua, kama vijito vya maji katika nchi isiyo na maji, kama kivuli cha mwamba mzito katika nchi iliyochoka.” (Isa. 32:2) Tunafarijika sana kujua kwamba ndugu hao wako tayari kutusaidia. Je, umewahi kusaidiwa na wazee wakati wa shida? Wanaweza kukutia moyo na kukusaidia ili uendelee kuvumilia.

Bila shaka, wazee hawafanyi miujiza. Ni wanadamu wasio wakamilifu, ‘wenye udhaifu uleule kama sisi.’ (Mdo. 14:15) Lakini dua wanazotoa kwa niaba yetu zinaweza kutusaidia sana. (Yak. 5:14, 15) Ndugu fulani nchini Italia ambaye kwa miaka mingi amevumilia ugonjwa unaodhoofisha mifupa anasema hivi: “Nimeweza kuvumilia kwa sababu ndugu hao wamenitembelea mara nyingi na kuonyesha kwamba wananipenda sana.” Je, unafaidika kikamili kutokana na msaada huo kutoka kwa Yehova, yaani, wazee?

UWE NA RATIBA NZURI YA MAMBO YA KIROHO

Kuna mambo mengine tunayoweza kufanya ili tuendelee kuvumilia. Jambo moja ni kuwa na ratiba nzuri ya mambo ya kiroho. Fikiria mfano wa John, mwenye umri wa miaka 39, ambaye aligunduliwa kuwa ana kansa isiyojulikana sana. Anasema: “Nilihisi kwamba haikuwa haki kwa kuwa bado nilikuwa kijana sana.” Wakati huo, mwana wake alikuwa na umri wa miaka mitatu tu. John anaeleza, “Hilo lilimaanisha kwamba mke wangu alihitaji kunitunza mimi na mtoto wetu, na kunisaidia kila mara nilipohitaji kumwona daktari.” Matibabu ya kemikali yalimchosha sana John na kumfanya ahisi kichefuchefu. Si hayo tu. Baba yake John aliugua ugonjwa usio na tiba na alihitaji kutunzwa.

John na familia yake walikabilianaje na hali hiyo? Anaeleza hivi: “Licha ya uchovu mwingi, nilihakikisha kwamba familia yangu ilikuwa na ratiba nzuri ya mambo ya kiroho. Tulihudhuria mikutano yote, tulishiriki katika huduma kila juma, na tulifanya ibada ya familia kwa ukawaida hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo.” Kwa kweli, John alitambua kuwa siri ya kuvumilia tatizo lolote lile ni kudumisha hali nzuri ya kiroho. John anawashauri nini wale wanaokabili majaribu mbalimbali? Anasema hivi: “Baada ya ule mshtuko wa mwanzoni kwisha, nguvu na upendo wa Yehova utakuondolea wasiwasi. Yehova atakupa nguvu, kama alivyonipa mimi.”

Bila shaka, kwa msaada wa Yehova tunaweza kuvumilia majaribu makali au hali nyingine ngumu zinazoweza kutupata sasa au wakati ujao. Acheni tusali kwa Yehova, tusitawishe urafiki wa karibu na waumini wenzetu kutanikoni, tutafute msaada wa wazee, na tudumishe ratiba nzuri ya mambo ya kiroho. Tukifanya hivyo, tutakuwa tukitenda kupatana na maneno ya Paulo: “Mnahitaji kuwa na uvumilivu.”

^ fu. 2 Baadhi ya majina yamebadilishwa.