Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Aliwapenda Watu

Aliwapenda Watu

“Vitu nilivyopenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.”—MET. 8:31.

1, 2. Yesu alithibitishaje kwamba anawapenda sana wanadamu?

MWANA mzaliwa wa kwanza wa Mungu ameonyesha kikamili zaidi hekima isiyo na kifani ya Yehova. Aliitwa hekima na alikuwa “stadi wa kazi” kando ya Baba yake. Wazia shangwe ambayo Yesu alikuwa nayo Baba yake “alipozitayarisha mbingu” na “alipoiweka misingi ya dunia!” Ingawa alifurahia vitu hivyo, Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu aliwapenda zaidi “wana wa binadamu.” (Met. 8:22-31) Naam, tangu mwanzo, Yesu anawapenda na kuwajali sana wanadamu.

2 Baadaye, Yesu alithibitisha upendo na ushikamanifu wake kwa Baba yake, na kuonyesha kwamba anawapenda sana “wana wa binadamu,” kwa ‘kujiondolea mwenyewe hali yake’ na kuwa kama wanadamu. Alifanya hivyo ili kutoa nafsi yake kuwa “fidia badala ya wengi.” (Flp. 2:5-8; Mt. 20:28) Kwa kweli, anawapenda sana wanadamu! Alipokuwa duniani, Yesu alitumia nguvu alizopewa na Mungu kufanya miujiza iliyofunua jinsi anavyowapenda sana wanadamu. Miujiza hiyo ilionyesha mambo mazuri yatakayotendeka duniani kote hivi karibuni.

3. Tutachunguza nini?

3 Pia, alipokuwa duniani, Yesu ‘alitangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.’ (Luka 4:43) Yesu alijua kwamba Ufalme huo utalitakasa jina la Baba yake na kuleta suluhisho la kudumu la matatizo yote ya wanadamu. Haishangazi kwamba katika huduma yake yote, Yesu aliwahangaikia sana wanadamu. Kwa nini tuvutiwe na jambo hilo? Kwa sababu mambo tunayojifunza yataimarisha uhakika wetu na tumaini letu la wakati ujao. Acheni tuchunguze miujiza minne ya Yesu.

“NINATAKA, TAKASIKA”

4. Mambo yalikuwaje Yesu alipokutana na mtu mwenye ukoma?

4 Yesu alikuwa akihubiri katika eneo la Galilaya. Akiwa katika mojawapo ya majiji ya Galilaya, alikutana na mtu mwenye ugonjwa mbaya sana, yaani, ukoma. (Marko 1:39, 40) Mtu huyo aliathiriwa sana na ugonjwa huo hivi kwamba Luka, ambaye alikuwa tabibu, alisema mwanaume huyo alikuwa ‘amejaa ukoma.’ (Luka 5:12) “Alipomwona Yesu akajiangusha kifudifudi akamwomba, akisema: ‘Bwana, ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.’” Bila shaka, mwanaume huyo alijua kwamba Yesu anaweza kumponya, ila hakuwa na uhakika ikiwa Yesu alitaka kufanya hivyo. Yesu angeitikiaje ombi lake? Yesu alifikiria nini alipomwona mtu huyo ambaye huenda mwonekano wake ulibadilika kabisa kwa sababu ya ugonjwa? Je, angemtendea kama Mafarisayo ambao waliwadharau watu wenye ukoma? Ungekuwa wewe ungefanya nini?

5. Ni nini kilichomchochea Yesu kumponya mtu mwenye ukoma?

5 Inaonekana mtu huyo alipuuza Sheria ya Musa iliyomtaka apaze sauti hivi: “Si safi, si safi!” Lakini Yesu hakukazia fikira jambo hilo. Badala yake, alimhangaikia mtu huyo na alitaka kumsaidia. (Law. 13:43-46) Hatujui kikamili Yesu alikuwa akiwaza nini akilini, lakini tunajua kilichokuwa moyoni mwake. Alichochewa na huruma kufanya jambo la ajabu sana. Alinyoosha mkono wake, akamgusa mwenye ukoma, halafu akasema hivi kwa sauti yenye hisia: “Ninataka. Takasika.” Kisha “ukoma ukamtoka.” (Luka 5:13) Kwa kweli, nguvu za Yehova zilikuwa hapo ili Yesu afanye muujiza huo na kuonyesha jinsi anavyowapenda wanadamu.—Luka 5:17.

6. Yesu aliwaponya watu jinsi gani, na hilo linaonyesha nini?

6 Nguvu za Mungu zilimwezesha Yesu Kristo kufanya miujiza mingi yenye kustaajabisha. Zaidi ya kuponya ukoma, aliponya kila aina ya ugonjwa na kila aina ya udhaifu. Maandiko yanasema hivi: “Umati wakashangaa walipoona mabubu wakisema na viwete wakitembea na vipofu wakiona.” (Mt. 15:31) Ili kufanya hivyo, Yesu hakuhitaji kutumia viungo vya bandia. Aliponya viungo au sehemu za mwili zilizoathirika! Tena aliwaponya watu papo hapo, na wakati mwingine aliwaponya wale waliokuwa mbali naye. (Yoh. 4:46-54) Miujiza hiyo inaonyesha nini? Inaonyesha kwamba Yesu, ambaye sasa ni Mfalme anayetawala mbinguni, ana uwezo na anatamani sana kuondoa magonjwa milele. Kujifunza jinsi Yesu alivyowatendea watu kunatuhakikishia kwamba katika ulimwengu mpya, unabii huu utatimia: “Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini.” (Zab. 72:13) Naam, Yesu atawaondolea wanadamu matatizo yote kwa sababu anatamani kufanya hivyo.

“SIMAMA, CHUKUA KITANDA CHAKO, UTEMBEE”

7, 8. Eleza matukio yaliyopelekea Yesu akutane na mgonjwa katika dimbwi la Bethzatha.

7 Miezi kadhaa imepita tangu Yesu alipokutana na mtu mwenye ukoma huko Galilaya. Sasa ametoka Galilaya na kuelekea Yudea kuhubiri na kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu. Bila shaka, maelfu ya watu walisikia ujumbe wa Yesu na kuvutiwa sana na sifa zake. Aliazimia kuwatangazia maskini habari njema, kutangaza uhuru kwa mateka, na kufunga majeraha ya waliovunjika moyo.—Isa. 61:1, 2; Luka 4:18-21.

8 Kisha, mwezi wa Nisani ukawadia. Yesu akasafiri kwenda Yerusalemu ili kusherehekea Pasaka, kama Baba yake alivyokuwa ameagiza. Jiji hilo lilikuwa na shamrashamra nyingi kwa kuwa watu walikuwa wakiwasili kwa ajili ya sherehe hiyo takatifu. Kaskazini ya hekalu kulikuwa na dimbwi la Bethzatha, na huko Yesu alikutana na mgonjwa.

9, 10. (a) Kwa nini watu walienda kwenye dimbwi la Bethzatha? (b) Yesu alifanya nini katika dimbwi hilo, na hilo linatufundisha nini? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 8.)

9 Watu wengi wagonjwa na wenye udhaifu walikusanyika Bethzatha. Kwa nini? Kwa sababu fulani isiyojulikana, waliamini kwamba ikiwa mgonjwa ataingia ndani ya dimbwi hilo maji yanapotibuliwa, atapona kimuujiza. Hebu wazia hali iliyokuwepo! Kulikuwa na watu wengi ambao wamekata tamaa, wenye mahangaiko, na wasio na tumaini. Lakini kwa nini Yesu alienda mahali hapo licha ya kwamba alikuwa mkamilifu na hakuwa na tatizo lolote? Kwa sababu aliwasikitikia watu, alienda hapo na kukutana na mtu ambaye alikuwa mgonjwa kwa muda mrefu hata kabla ya Yesu kuja duniani.—Soma Yohana 5:5-9.

10 Wazia huzuni aliyokuwa nayo mtu huyo Yesu alipomuuliza ikiwa anataka kuponywa. Alijibu mara moja. Alitaka kuponywa, lakini hakujua afanye nini kwa kuwa hakukuwa na mtu wa kumwingiza kwenye dimbwi. Yesu akamwambia afanye jambo lililoonekana kuwa haliwezekani, yaani, achukue kitanda chake na kutembea. Kwa sababu ya maneno ya Yesu, mtu huyo akachukua kitanda chake na kuanza kutembea. Hicho ni kionjo kizuri ajabu cha mambo ambayo Yesu atafanya katika ulimwengu mpya! Pia, muujiza huo unaonyesha kwamba Yesu ana huruma. Aliwatafuta waliohitaji msaada. Mfano wake unapaswa kutuchochea tuendelee kuwatafuta watu ambao wamekata tamaa kwa sababu ya mambo mabaya yanayoendelea ulimwenguni.

“NI NANI ALIYEYAGUSA MAVAZI YANGU YA NJE?”

11. Andiko la Marko 5:25-34 linaonyeshaje kwamba Yesu aliwahurumia wagonjwa?

11 Soma Marko 5:25-34. Mwanamke mmoja aliugua ugonjwa wenye kuaibisha kwa miaka 12. Ugonjwa huo uliathiri kila sehemu ya maisha yake, kutia ndani ibada. “Alikuwa ameumizwa sana na matabibu wengi na alikuwa ametumia mali zake zote,” lakini hali yake ilizidi kuwa mbaya. Siku moja, mwanamke huyo alifikiria njia tofauti ya matibabu. Alienda katika eneo ambalo Yesu alikuwepo. Akaingia katikati ya umati na kugusa vazi la nje la Yesu. (Law. 15:19, 25) Yesu alitambua kwamba nguvu zilimtoka, hivyo akauliza ni nani aliyemgusa. “Akiogopa na kutetemeka,” mwanamke huyo “akaanguka chini mbele yake, akamwambia kweli yote.” Yesu alijua kwamba Baba yake, Yehova, ndiye aliyemponya mwanamke huyo, hivyo alimtendea kwa fadhili, na kumwambia: “Binti yangu, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani, na uwe na afya njema kutokana na ugonjwa wako wenye kuhuzunisha.”

Miujiza ya Yesu inaonyesha wazi kwamba anatujali sana na anahangaikia matatizo yetu (Tazama fungu la 11 na 12)

12. (a) Kutokana na yale ambayo tayari tumejifunza, unaweza kumfafanuaje Yesu? (b) Yesu alituwekea mfano gani?

12 Yesu ni mwenye fadhili sana! Anawajali na kuwahurumia sana wagonjwa. Shetani anataka kutuhakikishia kwamba hatupendwi wala hatuna thamani. Hata hivyo, miujiza ya Yesu inaonyesha wazi kwamba anatujali sana na anahangaikia matatizo yetu. Naam, yeye ni Mfalme na Kuhani Mkuu mwenye huruma kwelikweli! (Ebr. 4:15) Inaweza kuwa vigumu kuelewa hisia za wale wanaougua magonjwa ya kudumu, hasa ikiwa hatujawahi kupata magonjwa kama hayo. Hata hivyo, Yesu aliwahurumia wagonjwa licha ya kwamba hakuwahi kuugua. Acheni tufanye yote tuwezayo ili kuiga mfano wake.—1 Pet. 3:8.

“YESU AKATOKWA NA MACHOZI”

13. Ufufuo wa Lazaro unafunua nini kuhusu utu wa Yesu?

13 Yesu aliguswa sana na maumivu ya wengine. ‘Aliugua na kutaabika’ alipoona watu wakihuzunika kwa sababu ya kifo cha rafiki yake, Lazaro. Alihisi hivyo hata ingawa alijua kwamba angemfufua Lazaro baada ya muda mfupi. (Soma Yohana 11:33-36.) Yesu hakuona aibu kuonyesha hisia zake za ndani. Watu waliokuwepo waliona jinsi alivyompenda Lazaro na familia yake. Yesu alionyesha huruma kwa kutumia nguvu alizopewa na Mungu kumfufua Lazaro.—Yoh. 11:43, 44.

14, 15. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anatamani sana kuondoa mateso ya wanadamu? (b) Maneno “makaburi ya ukumbusho” yanatufundisha nini?

14 Biblia inasema kwamba Yesu ni “mwakilisho sawasawa wa utu” wa Muumba. (Ebr. 1:3) Hivyo, miujiza ya Yesu inatuthibitishia kwamba yeye na Baba yake wanatamani kuondoa magonjwa na kifo. Hivi karibuni, watawafufua watu wengi zaidi ili waishi tena. Yesu alisema, ‘Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho . . . watatoka.’—Yoh. 5:28, 29.

15 Yesu alitumia maneno “makaburi ya ukumbusho,” kwa sababu kumbukumbu ya Mungu inahusika. Mungu Mweza-Yote, aliyeumba vitu vyote, anaweza kukumbuka kila jambo kuwahusu wapendwa wetu waliokufa, kutia ndani sifa zao. (Isa. 40:26) Hata hivyo, si kwamba tu anaweza kukumbuka, bali yeye na Mwana wake wanataka kufanya hivyo. Ufufuo wa Lazaro na masimulizi mengine ya ufufuo yaliyoandikwa kwenye Biblia, yanaonyesha kile kitakachotendeka katika ulimwengu mpya.

MIUJIZA YA YESU INATUFUNDISHA NINI?

16. Wanaoendelea kuwa waaminifu watapata nafasi ya kufanya nini?

16 Tukiendelea kuwa waaminifu, tunaweza kushuhudia muujiza mkubwa zaidi kuwahi kutokea, yaani, kuokoka dhiki kuu. Mara tu baada ya Har–Magedoni, kutakuwa na miujiza mingi zaidi, na wanadamu watarudishiwa afya nzuri. (Isa. 33:24; 35:5, 6; Ufu. 21:4) Hebu wazia ukiwaona watu wakitupa miwani, mikongojo, magongo, viti vya magurudumu, vifaa vya kuwasaidia kusikia, na kadhalika! Yehova atakuwa na sababu nzuri ya kuwarudishia wanadamu afya nzuri. Wale watakaookoka Har–Magedoni watakuwa na kazi ya kufanya. Wataigeuza sayari yetu, ambayo ni zawadi kutoka kwa Mungu, kuwa paradiso.—Zab. 115:16.

17, 18. (a) Kwa nini Yesu alifanya miujiza? (b) Kwa nini unapaswa kufanya yote uwezayo ili uwepo katika ulimwengu mpya?

17 Miujiza ya Yesu inawafariji wale wa “umati mkubwa” na kuimarisha tumaini lao la kuponywa magonjwa yote wakati ujao. (Ufu. 7:9) Inaonyesha jinsi Mwana mzaliwa wa kwanza wa Mungu anavyowajali na kuwapenda sana wanadamu. (Yoh. 10:11; 15:12, 13) Huruma ya Yesu inaonyesha vizuri jinsi Yehova anavyomjali kila mmoja wetu.—Yoh. 5:19.

18 Wanadamu wanaugua, wanateseka, na kufa. (Rom. 8:22) Tunahitaji ulimwengu mpya wa Mungu, ambapo sote tutakuwa na afya bora kama Mungu alivyoahidi. Andiko la Malaki 4:2 linatuhakikishia kwamba wale watakaoponywa ‘watatoka nje na kuukanyaga udongo kama ndama waliononeshwa,’ watafurahi na kusisimuka kwa sababu ya kuondolewa kwa madhara ya kutokamilika. Acheni tumshukuru Mungu na kuonyesha imani katika ahadi zake kwa kufanya yote tuwezayo ili tustahili kuwepo katika ulimwengu mpya. Inafariji sana kujua kwamba miujiza ambayo Yesu alifanya alipokuwa duniani inaonyesha kuwa hivi karibuni, chini ya utawala wake wa Kimasihi, wanadamu watafurahia kitulizo cha kudumu!